Biblia Katika Lugha ya Maisha ya Kila Siku
“IKIWA wewe waamini kwamba Biblia ndiyo Neno la Mungu kwa wanadamu, hiyo yamaanisha kwamba Mungu anawasiliana nasi. . . . Ikiwa dini yako huathiri maisha yako yote, basi lugha [ya Biblia] lazima iwe ya maisha ya kila siku.” Ndivyo alivyoandika msomi Alan Duthie katika kitabu chake Bible Translations: And How to Choose Between Them.
Wapendao Neno la Mungu hukubaliana na hilo kwa moyo wote. Wao huamini kwa dhati kwamba “andiko lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu.” (2 Timotheo 3:16) Kwa vyovyote Biblia si kitabu chenye maneno baridi ya kidini yasiyofaa wakati huu. Hiyo ni “hai na hukazia nguvu,” ikitoa masuluhisho halisi kwa matatizo ya maisha ya kila siku. (Waebrania 4:12) Lakini ili kitabu hicho kitakatifu kiweze kueleweka na kutumiwa na wasomaji wacho, lazima kiwe katika lugha ya maisha ya kila siku. Kwa vyovyote, lile lenye kuitwa isivyofaa, Agano Jipya, halikuandikwa katika Kigiriki bora kilichotumiwa na wanafalsafa kama vile Plato, bali kiliandikwa katika Kigiriki cha kawaida, cha kila siku kilichoitwa Kikoine. Ndiyo, Biblia iliandikwa ili iweze kusomwa na kueleweka na watu wa kawaida.
Kwa kusudi hili, tafsiri kadhaa za kisasa zimetokezwa katika miaka ya juzijuzi katika lugha mbalimbali. Mara nyingi matokeo yamekuwa yenye manufaa sana. Maandiko yamefanywa yaeleweke zaidi kwa watu wote kwa ujumla. Hata hivyo, nyingi za tafsiri hizi mpya zina upungufu mkubwa sana, kwani zakosa upatano na usahihi usio na upendeleo. Kwa kielelezo, baadhi yazo huelekea kuficha mafundisho ya wazi ya Biblia juu ya hali ya wafu, nafsi ya kibinadamu ilivyo, na jina la Mungu wa kweli.
Kwa hiyo, wapendao Neno la Mungu wanakaribisha kutolewa kwa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Kiswahili. Mashahidi wa Yehova walitangaza kutolewa kwa tafsiri hii ya siku ya kisasa kwenye Mkusanyiko wa Wilaya wa 1996. Pasipo kuvutwa na imani za kidini, hiyo huonyesha usahihi usio na kifani katika ufasiri wayo, ikiwezesha uelewevu wa Biblia wenye kina ambao hapo awali haukupatikana kwa wale ambao hawakuzijua lugha za kale. Lakini, huenda ukataka kujua, aliyetokeza tafsiri hii yenye kutokeza ni nani?
Watafsiri Waliomtukuza Mungu
Ingawa huenda ikawa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ni mpya kwa wale wasemao Kiswahili, kwa kweli imekuwapo tangu 1950. Wakati huo ilitolewa katika lugha ya Kiingereza na Watch Tower Bible and Tract Society—Sosaiti ya Biblia ya kimataifa yenye historia ndefu ya kuchapisha Biblia. Kichwa cha tafsiri hii mpya—ambacho chatofautiana sana na mgawanyo wa kidesturi wa Biblia katika agano “la kale” na “jipya”—ndicho mojawapo tu ya zile njia nyingi ambazo imethibitika kuwa ya kipekee. Mnara wa Mlinzi la Kiingereza la Septemba 15, 1950, lilisema hivi: “Wanaume wafanyizao halmashauri ya utafsiri wameeleza tamaa yao . . . ya kubaki bila kujulikana, na hawataki kimahususi majina yao yatangazwe wakiwa wangali hai wala baada ya kifo. Kusudi la hiyo tafsiri ni kulikweza jina la Mungu wa kweli, aliye hai.”
Biblia ya New World Translation of the Holy Scriptures, ambayo ni chapa yenye buku moja la Biblia nzima, ilitolewa katika 1961. Na ingawa majina ya watafsiri wayo yangali hayajafunuliwa hadi leo, hakuwezi kuwa na shaka kuhusu makusudio yao au kuhusu kina cha ujitoaji wao. Dibaji ya chapa ya 1984 ilitaarifu hivi: “Kutafsiri Maandiko Matakatifu kwamaanisha kufasiri katika lugha nyingine mawazo na maneno ya Yehova Mungu . . . Watafsiri wa kitabu hiki, wamhofuo na kumpenda Mtungaji wa Kimungu wa Maandiko Matakatifu, wahisi daraka la pekee Kwake la kuwasilisha mawazo na majulisho yake kwa usahili iwezekanavyo.”
Yajapokuwa makusudio mazuri bila shaka, je, washiriki wa halmashauri hiyo walikuwa na sifa za ustahili za kufanya kazi hiyo? Wasomi fulani wasioridhika walijadili kwamba pasipo kufunuliwa kwa majina ya watafsiri na ustahili wao wa kielimu, bila kukawia, tafsiri hiyo yapaswa kuachiwa mbali, kuwa kazi iliyofanywa na watu wasio stadi. Lakini si wasomi wote ambao wamechukua msimamo huo usioonyesha kiasi. Alan S. Duthie aandika hivi: “Tukijua ni nani walio watafsiri au wachapishaji wa tafsiri ya Biblia fulani, je, hilo hutusaidia tuamue kama tafsiri hiyo ni nzuri au mbaya? Si moja kwa moja. Hakuna njia ya badala ya kuchunguza sifa za kila tafsiri yenyewe.”a
Maelfu ya wasomaji wamefanya hivyo hasa. Hadi sasa nakala zaidi ya 84,400,000 za Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika lugha 27 zimechapwa ulimwenguni pote. Wasomaji wayo wamegundua nini?
Tafsiri Inayotakasa Jina la Mungu
Kwenye Mathayo 6:9, Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kusali hivi: “Baba yetu uliye katika mbingu, jina lako na litakaswe.” Hata hivyo, katika tafsiri zilizo nyingi, Mungu ni mtu asiye na jina, atambulishwaye tu kwa jina la cheo “Mungu” au “Bwana.” Hata hivyo hali haikuwa hivyo mwanzoni. Mungu alitambulishwa kwa wazi karibu mara 7,000 katika Maandiko ya Kiebrania ya awali kwa jina la kibinafsi “Yehova.” (Kutoka 3:15; Zaburi 83:18) Katika miaka ya baadaye hofu za kishirikina ziliwafanya Wayahudi wakome kulitumia jina la kimungu. Baada ya kifo cha mitume wa Yesu, maoni hayo ya kishirikina yaliathiri kutaniko la Kikristo. (Linganisha Matendo 20:29, 30; 1 Timotheo 4:1.) Wenye kunakili sehemu za Kigiriki za Maandiko walianza kuweka mahali pa jina la kibinafsi la Mungu, Yehova, maneno ya Kigiriki Kyʹri·os na The·osʹ, yanayomaanisha “Bwana” na “Mungu.”
Kwa furaha, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya imechukua ile hatua yenye ujasiri ya kurudisha jina Yehova kwenye Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo (“Agano Jipya”), jina hilo linaonekana mara 237. Kurudisha huko hakutegemei vile watafsiri watakavyo, bali wategemea usomi timamu, wenye uangalifu. Kwa kielelezo, Luka 4:18 hunukuu maneno ya Isaya 61:1. Katika maandishi ya Kiebrania ya awali, jina Yehova lilionekana katika mstari huo wa Isaya.b Kwa kufaa basi, katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, Luka 4:18 limetafsiriwa hivi: “Roho ya Yehova iko juu yangu, kwa sababu alinitia mafuta kutangaza habari njema kwa walio maskini.”
Fasiri hizo husaidia pia wasomaji watofautishe Yehova Mungu na Mwana wake mzaliwa-pekee, Yesu Kristo. Mathalani, tafsiri zilizo nyingi hufasiri Mathayo 22:44 hivi: “Bwana alimwambia Bwana wangu.” Lakini ni nani asemaye na anasema na nani? Kwa kweli, mstari huo ni nukuu kutoka Zaburi 110:1, ambalo, katika maandishi ya Kiebrania ya awali, lina jina la kimungu. Kwa hiyo Tafsiri ya Ulimwengu Mpya hufasiri mstari huo hivi: “Yehova alimwambia Bwana wangu: ‘Keti kwenye mkono wangu wa kuume mpaka niwekapo maadui wako chini ya miguu yako.’” Kufahamu ile tofauti ambayo Maandiko huonyesha kati ya Yehova Mungu na Mwana wake si jambo la kitaalamu. (Marko 13:32; Yohana 8:17, 18; 14:28) Ni jambo la maana kwa habari ya wokovu wa mtu. Lasema Matendo 2:21: “Kila mtu aitiaye jina la Yehova ataokolewa.”
Usahihi na Uwazi
Kuna sehemu nyinginezo zenye kutokeza za Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Yale maandishi-awali ya Kigiriki yaliyosahihishwa sana ya Westcott na Hort yalichaguliwa kuwa msingi mkuu wa tafsiri hiyo. Uangalifu mwingi ulikaziwa ili kufasiri Kigiriki cha awali kwa usahihi na kwa maneno yote mojamoja iwezekanavyo katika lugha ya kisasa iliyo sahili. Kufanya hivyo kulihifadhi ladha na udhahiri mwingi wa maandishi ya Biblia ya awali na pia ulifungulia njia uelewevu mwingi sana.
Kwa kielelezo, chukua lile andiko la Waroma 13:1, ambalo katika hilo mtume Paulo aliwasihi sana Wakristo wawe “katika ujitiisho kwa mamlaka zilizo kubwa,” au kwa serikali za kilimwengu. Watafsiri wengi huendelea kusema kwamba serikali hizo ‘zimeamriwa na Mungu’ au ‘zimewekwa na Mungu.’ (Union Version ya Kiswahili; Habari Njema ya Watu Wote) Watawala fulani wametumia fasiri hizo ili kutetea udhalimu wao. Lakini kwa ukawaida wayo wa kutafsiri maneno yote mojamoja na usahihi, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya hufasiri mstari huo kwa kusema, “mamlaka zilizopo zimesimama zikiwa zimewekwa na Mungu katika mahali pa vyeo vyazo vyenye kuhusu.”c Sasa yaweza kuonwa kwamba ingawa Mungu hachagui kibinafsi watawala walimwengu, yeye huwaruhusu wanadamu hao kuchukua vyeo vya mamlaka vyenye kuhusiana—lakini sikuzote vikiwa chini yake mwenyewe.
Tafsiri ya Ulimwengu Mpya hujitahidi pia kuwasilisha hali mbalimbali za vitenzi vya Kigiriki. Katika lugha nyingi za kisasa, vitenzi vinaainishwa kiuambishi ili kuwasilisha wakati wa kutendeka kwa kitenzi—yaani, wakati uliopita, wakati uliopo, au wakati ujao. Katika Kigiriki vitenzi huonyesha pia ni aina gani ya kitendo kinachohusika—kama ni cha muda tu, kama kimekamilishwa, au kama ni chenye kuendelea. Fikiria maneno ya Yesu kwenye Mathayo 6:33. Kitenzi cha Kigiriki kimaanishacho “kutafuta” huwasilisha wazo la kitendo chenye kuendelea. Hivyo maana kamili ya maneno ya Yesu inaonyeshwa katika fasiri hii: “Basi, fulizeni kutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, na vitu vingine vyote hivi mtaongezewa.” Vivyo hivyo, Mathayo 7:7 inafasiriwa hivi: “Fulizeni kuomba, nanyi mtapewa; fulizeni kutafuta sana, nanyi mtapata; fulizeni kubisha hodi, nanyi mtafunguliwa.”—Ona pia Waroma 1:32; 6:2; Wagalatia 5:15.
Tafsiri ya Ulimwengu Mpya hujitahidi sana kuwa yenye upatano na bila kubadilikabadilika katika kufasiri kwayo maneno makuu. Mathalani, neno la Kigiriki psy·kheʹ, limetafsiriwa “nafsi” kila mahali linapotukia. Likiwa tokeo, wasomaji waweza kuona upesi kwamba, kinyume cha nadharia za kidini, nafsi haina hali ya kutoweza kufa. Yaweza kuangamia, kufa.—Mathayo 2:20; Marko 3:4; Luka 6:9; 17:33.
Kufanya Neno la Mungu Lipatikane Ulimwenguni Pote
Kutolewa kwa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Kiswahili ni mwanzo tu. Mipango imefanywa ya kuitafsiri Biblia nzima hatimaye. Lakini, je, wasomaji waweza kuwa na uhakika kwamba tafsiri ya Kiswahili itakuwa na usahihi na upatano uleule wa tafsiri ya Kiingereza?
Bila shaka, ndiyo. Hiyo ni kwa sababu kazi ya kutafsiri imesimamiwa kwa ukaribu na Watch Tower Society. Kwa hekima, iliamuliwa kwamba utafsiri wa Biblia katika lugha za kigeni ungefanywa vyema zaidi kwa jitihada ya timu. Hivyo timu za utafsiri wa Biblia zilianzishwa katika nchi kadhaa kotekote ulimwenguni. Idara iitwayo Utumishi wa Utafsiri ilianzishwa katika makao makuu ya Watch Tower Society, huko Brooklyn, New York, ili ishughulikie mahitaji ya timu hizo, ijibu maswali, na kuhakikisha mwafaka wa chapa za lugha tofauti za Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Watch Tower Society imesitawisha pia chombo chenye mafaa sana, yaani, mfumo wa kompyuta ili kuwasaidia watafsiri wa Biblia. Waweza kuwa na uhakika huu: Bado kazi ya kutafsiri yataka jitihada nyingi za wanadamu. Lakini kompyuta imesahilisha sana ule mradi mkubwa uliowekwa mbele ya timu za utafsiri wa Biblia, ambao ni kufasiri Tafsiri ya Ulimwengu Mpya kwa usahihi na upatano uleule wa tafsiri ya Kiingereza ya awali. Miongoni mwa mambo mengine, mfumo wa kompyuta huonyesha jinsi kila neno la Kiebrania na la Kigiriki linavyofasiriwa katika chapa ya Kiingereza—msaada mkubwa kwa watafsiri katika kuteua maneno visawe vya kilugha.
Mafanikio ya mipango hiyo yaweza kuonwa kwa urahisi kwa kuyaangalia matokeo tu. Twakuhimiza uichunguze Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Waweza kujipatia nakala kutoka kwa wachapishaji wa gazeti hili. Utafurahia pia sehemu zayo nyingi za pekee: herufi za chapa zilizo wazi, zenye kusomeka vizuri; vichwa vya kila ukurasa, vinavyokusaidia upate upesi zaidi mistari unayoijua; ramani zenye mambo mengi; na habari za nyongeza zenye kusisimua. La maana zaidi ni kwamba, waweza kuisoma Biblia hii ukiwa na uhakika kwamba hiyo huwasilisha kwa usahihi maneno yenyewe ya Mungu katika lugha ya maisha ya kila siku.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa kupendeza, jalada la Chapa Yenye Marejezo (1971) ya New American Standard Bible vilevile lilitaarifu hivi: “Hatukutumia jina la msomi yeyote la kurejezewa ama kupendekezwa kwa sababu ni itikadi yetu kwamba Neno la Mungu lapaswa likadiriwe kwa msingi wa ustahili walo lenyewe.”
b Ni kweli kwamba tafsiri ya Septuagint ya Kigiriki ilikuwa msingi wa manukuu ya Maandiko ya Kiebrania katika lile lenye kuitwa isivyofaa, Agano Jipya. Kwa kuwa nakala za baadaye za Septuagint hazina jina la kimungu, wasomi wengi hujadili kwamba jina hilo halipaswi vilevile kutiwa ndani katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Hata hivyo, nakala zilizoko za zamani zaidi za Septuagint zina hilo jina Yehova—katika namna yalo ya Kiebrania cha awali. Hilo lategemeza kwa nguvu kule kurudishwa kwa jina Yehova katika Maandiko ya Kigiriki.
c Ona A Manual Greek Lexicon of the New Testament, ya G. Abbot-Smith, na A Greek-English Lexicon ya Liddell na Scott. Kulingana na vyanzo hivyo na vinginevyo vyenye kutegemeka, neno la Kigiriki humaanisha kihalisi “kusimama kwa utaratibu, kupanga katika mahali fulani.”
[Picha katika ukurasa wa 24]
Sehemu za Tafsiri ya Ulimwengu Mpya:
Uangalifu mwingi ulikaziwa ili kufasiri Kigiriki cha awali kwa usahihi na kwa maneno yote mojamoja iwezekanavyo katika lugha ya kisasa, iliyo sahili
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 24]
Kwa hisani ya Director and University Librarian, The John Rylands University of Manchester
Herufi za chapa zilizo rahisi kusoma hufanya kusoma kupendeze
Vichwa vya kila ukurasa hufanya iwe rahisi kupata upesi zaidi mistari ya Biblia unayoijua
Ramani zenye mambo mengi husaidia wasomaji waongeze uelewevu wao wa jiografia ya Biblia
[Picha katika ukurasa wa 23]
Waandikaji wa Biblia kama vile mtume Paulo waliandika katika lugha ya maisha ya kila siku
[Picha katika ukurasa wa 26]
Uwazi wa “Tafsiri ya Ulimwengu Mpya” ni wa manufaa sana katika huduma ya Kikristo