Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • es22 kur. 47-57
  • Mei

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mei
  • Kuyachunguza Maandiko Kila Siku—2022
  • Jumapili, Mei 1
  • Jumatatu, Mei 2
  • Jumanne, Mei 3
  • Jumatano, Mei 4
  • Alhamisi, Mei 5
  • Ijumaa, Mei 6
  • Jumamosi, Mei 7
  • Jumapili, Mei 8
  • Jumatatu, Mei 9
  • Jumanne, Mei 10
  • Jumatano, Mei 11
  • Alhamisi, Mei 12
  • Ijumaa, Mei 13
  • Jumamosi, Mei 14
  • Jumapili, Mei 15
  • Jumatatu, Mei 16
  • Jumanne, Mei 17
  • Jumatano, Mei 18
  • Alhamisi, Mei 19
  • Ijumaa, Mei 20
  • Jumamosi, Mei 21
  • Jumapili, Mei 22
  • Jumatatu, Mei 23
  • Jumanne, Mei 24
  • Jumatano, Mei 25
  • Alhamisi, Mei 26
  • Ijumaa, Mei 27
  • Jumamosi, Mei 28
  • Jumapili, Mei 29
  • Jumatatu, Mei 30
  • Jumanne, Mei 31
Kuyachunguza Maandiko Kila Siku—2022
es22 kur. 47-57

Mei

Jumapili, Mei 1

Akaendelea kuwatii.​—Luka 2:51.

Mwanzoni mwa maisha yake akiwa mwanadamu, Yesu alichagua kujitiisha kwa wazazi wake. Kamwe hakupinga mwongozo wa wazazi wake, akifikiri kwamba yeye alijua mambo mengi kuliko wao. Bila shaka, Yesu alichukua jukumu lake akiwa mwana wa kwanza. Hapana shaka kwamba alijifunza kwa bidii kutoka kwa baba yake wa kambo jinsi ya kufanya kazi ambayo ingemsaidia kuitegemeza familia yao. Inaelekea wazazi wa Yesu walimweleza kuhusu alivyozaliwa kimuujiza na mambo ambayo wajumbe wa Mungu walisema kumhusu. (Luka 2:8-19, 25-38) Yesu hakuridhika tu na mambo aliyoelezwa; bali alijifunza pia Maandiko kibinafsi. Tunajuaje kwamba Yesu alikuwa mwanafunzi mzuri wa Neno la Mungu? Kwa sababu alipokuwa angali mvulana, walimu huko Yerusalemu ‘walishangazwa na majibu yake na uwezo wake wa kuelewa.’ (Luka 2:46, 47) Akiwa na umri wa miaka 12 tu, tayari Yesu alikuwa amejithibitishia kwamba Yehova alikuwa Baba yake.​—Luka 2:42, 43, 49. w20.10 29-30 ¶13-14

Jumatatu, Mei 2

Kristo amefufuliwa kutoka kwa wafu.​—1 Kor. 15:12.

Imani katika ufufuo wa Yesu ndio msingi wa tumaini letu la Kikristo. Mwanzoni mwa mazungumzo yake kuhusu ufufuo, Paulo alitaja mambo matatu ya kweli. Nayo ni (1) “Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu.” (2) “Alizikwa.” (3) “Alifufuliwa siku ya tatu kulingana na Maandiko.” (1 Kor. 15:3, 4) Kufa kwa Yesu, kuzikwa, na kufufuliwa kwake kunamaanisha nini kwetu? Nabii Isaya alitabiri kwamba Masihi ‘angeondolewa katika nchi ya walio hai’ na ‘angepewa kaburi pamoja na waovu.’ Hata hivyo, mengi zaidi yalihusika. Isaya aliongeza kwamba Masihi ‘angebeba dhambi ya watu wengi.’ Yesu alifanya hivyo alipotoa uhai wake kuwa fidia. (Isa. 53:8, 9, 12; Mt. 20:28; Rom. 5:8) Hivyo kufa, kuzikwa, na kufufuliwa kwa Yesu kunatupatia msingi imara wa tumaini letu la kuwekwa huru kutokana na dhambi na kifo na kuungana tena na wapendwa wetu waliokufa. w20.12 2-3 ¶4-6; 5 ¶11

Jumanne, Mei 3

Mimi kati ya watu wote, nina sababu za kuwa na uhakika katika mwili. Mtu yeyote akifikiri ana sababu za kuwa na uhakika katika mwili, mimi ninazo zaidi.​—Flp. 3:4.

Mtume Paulo alihubiri mara kwa mara katika masinagogi ya Wayahudi. Kwa mfano, ‘kwa sabato tatu alijadiliana na Wayahudi akitumia Maandiko’ katika sinagogi moja huko Thesalonike. (Mdo. 17:1, 2) Inaelekea Paulo alijihisi huru akiwa katika sinagogi. Alilelewa na wazazi Wayahudi. (Mdo. 26:4, 5) Paulo aliwafahamu vizuri Wayahudi, hivyo angeweza kuwahubiria akiwa na uhakika. (Flp. 3:5) Baada ya watu waliomtesa Paulo kumlazimisha aondoke Thesalonike na kisha Beroya, aliwasili Athene. Kwa mara nyingine tena, “akaanza kujadiliana katika sinagogi pamoja na Wayahudi na watu wengine waliomwabudu Mungu.” (Mdo. 17:17) Hata hivyo, alipokuwa akihubiri sokoni, Paulo alikutana na wasikilizaji tofauti. Miongoni mwa wasikilizaji wake kulikuwa na wanafalsafa na watu wengine wa mataifa ambao waliuona ujumbe wa Paulo kuwa ‘fundisho jipya.’ Walimwambia hivi: “Unaanzisha mambo yaliyo mageni masikioni mwetu.”—Mdo. 17:18-20. w20.04 9 ¶5-6

Jumatano, Mei 4

Ninapotaka kufanya yaliyo sawa, yaliyo mabaya yapo pamoja nami.​—Rom. 7:21.

Usijihukumu vikali ikiwa unapambana na udhaifu fulani. Kumbuka kwamba hatuwezi kuwa na msimamo wa uadilifu mbele za Mungu kwa jitihada zetu wenyewe. Sote tunahitaji fadhili zisizostahiliwa za Mungu kupitia dhabihu ya fidia. (Efe. 1:7; 1 Yoh. 4:10) Na tunaweza kuwaendea ndugu na dada zetu ambao ni familia yetu ya kiroho ili tutiwe moyo! Wanaweza kutusikiliza tunapohitaji mtu wa kuzungumza naye na kutufariji kwa maneno yanayoweza kutuchangamsha moyo. (Met. 12:25; 1 The. 5:14) Joy, dada kutoka nchini Nigeria ambaye amepambana na hisia za kuvunjika moyo anasema hivi: “Ningekuwa wapi bila ndugu na dada zangu? Ndugu na dada zangu ni uthibitisho kwamba Yehova anajibu sala zangu. Hata nimejifunza kutoka kwao jinsi ya kuwatia moyo wengine ambao wamevunjika moyo.” Hata hivyo, tunahitaji kukumbuka kwamba si nyakati zote ndugu na dada zetu watajua ni wakati gani tunahitaji kitia-moyo. Hivyo, huenda tukahitaji kuchukua hatua ya kwanza kwa kumfikia Mkristo mkomavu na kumweleza kwamba tunahitaji msaada. w20.12 23-24 ¶7-8

Alhamisi, Mei 5

Nimewaita rafiki.​—Yoh. 15:15.

Kwa kawaida, hatua ya kwanza ya kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na mtu ni kutumia wakati pamoja naye. Kadiri mnavyozungumza pamoja na kushiriki mawazo na hisia zenu, ndivyo mnavyozidi kuwa marafiki. Hata hivyo, tunakabili changamoto mbalimbali inapohusu kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na Yesu. Changamoto mojawapo ni kwamba hatujawahi kukutana na Yesu ana kwa ana. Wakristo wengi wa karne ya kwanza walikabili changamoto hiyo pia. Ingawa hivyo, mtume Petro alisema hivi: “Mnampenda ingawa hamkumwona kamwe. Ijapokuwa hammwoni sasa, bado mnaonyesha imani katika yeye.” (1 Pet. 1:8) Hivyo, inawezekana kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na Yesu hata ingawa hatujawahi kukutana naye kibinafsi. Pia, hatuwezi kuzungumza na Yesu. Tunaposali, tunamweleza Yehova mawazo yetu. Ni kweli kwamba tunasali katika jina la Yesu, lakini hatuzungumzi na Yesu. Isitoshe, Yesu hataki tusali kwake. Kwa nini? Kwa sababu sala ni tendo la ibada, na ni Yehova peke yake anayepaswa kuabudiwa. (Mt. 4:10) Licha ya hilo, tunaweza kumwonyesha Yesu upendo wetu. w20.04 20 ¶1-3

Ijumaa, Mei 6

[Mungu] atawafanya muwe imara, atawatia nguvu.​—1 Pet. 5:10.

Wakimbiaji katika mashindano huko Ugiriki walihitaji kushinda changamoto, kama vile kuhisi uchovu na maumivu. Lakini walihitaji hasa kutegemea mazoezi na nguvu zao wenyewe. Sisi ni kama wakimbiaji hao katika maana ya kwamba tunapata mazoezi ya jinsi ya kukimbia katika shindano letu. Lakini tuna msaada ambao wakimbiaji halisi hawana. Tunaweza kupata nguvu zisizo na kikomo kutoka kwa Yehova. Yehova anatuahidi kwamba ikiwa tutamtegemea, atatuzoeza na kututia nguvu! Mtume Paulo alilazimika kukabiliana na changamoto nyingi. Mbali na kutukanwa na kuteswa, nyakati nyingine Paulo alijihisi akiwa dhaifu na alihitaji kukabiliana na hali ambayo aliitaja kuwa “mwiba katika mwili.” (2 Kor. 12:7) Lakini badala ya kuona changamoto hizo kuwa sababu ya kukata tamaa, aliziona kuwa fursa ya kumtegemea Yehova. (2 Kor.12:9, 10) Kwa kuwa Paulo alisitawisha mtazamo huo, Yehova alimsaidia kukabiliana na matatizo yake yote. w20.04 29 ¶13-14

Jumamosi, Mei 7

Hakuna mtu anayeweza kuja kwangu isipokuwa Baba . . . amvute.​—Yoh. 6:44.

Tuna hazina isiyoonekana ya ‘kufanya kazi pamoja’ na Yehova, Yesu, na malaika. (2 Kor. 6:1) Tunafanya kazi pamoja nao wakati wowote tunaposhiriki katika huduma. Paulo alisema hivi kujihusu na kuwahusu wale wanaoshiriki kazi hiyo: “Sisi ni wafanyakazi wenzi wa Mungu.” (1 Kor. 3:9) Tunaposhiriki katika huduma ya Kikristo, sisi pia ni wafanyakazi wenzi wa Yesu. Kumbuka kwamba baada ya Yesu kuwaamuru wafuasi wake ‘wakafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote,’ aliwaambia hivi: “Mimi nipo pamoja nanyi.” (Mt. 28:19, 20) Na vipi kuhusu malaika? Tunashukuru sana kwamba malaika wanatuongoza tunapoendelea kutangaza “habari njema ya milele . . . kwa wale wanaokaa duniani”! (Ufu. 14:6) Tunatimiza nini kwa sababu ya utegemezo huo tunaopata kutoka mbinguni? Tunapoendelea kupanda mbegu za ujumbe wa Ufalme, baadhi ya mbegu hizo huanguka kwenye mioyo mizuri na kukua. (Mt. 13:18, 23) Ni nani anayesababisha mbegu hizo za kweli zikue na kuzaa matunda? Yesu anaeleza jibu kwenye andiko la leo. w20.05 30 ¶14-15

Jumapili, Mei 8

Acheni kufinyangwa na mfumo huu wa mambo.​—Rom. 12:2.

Leo, mamilioni ya familia zimetenganishwa na talaka. Hata familia zinazoishi kwenye nyumba moja huenda zisiwe na uhusiano wa karibu. Mshauri fulani wa familia anasema hivi: “Baba, mama, na watoto hawana mawasiliano mazuri na wanatumia muda mwingi kwenye kompyuta, tablet, simu za mkononi au michezo ya video. Ingawa watu hao wa familia wanaishi katika nyumba moja, hawajuani vizuri.” Tusingependa kufinyangwa na ulimwengu huu usio na upendo. Badala yake, tunahitaji kusitawisha upendo mwororo, si kuelekea watu wetu wa familia tu, bali pia wale ambao ni ndugu zetu katika imani. (Rom. 12:10) Upendo mwororo ni nini? Ni maneno ambayo kihususa yanayofafanua urafiki wa karibu ulio miongoni mwa watu wa familia. Tunapaswa kusitawisha aina hiyo ya upendo kuelekea familia yetu ya kiroho, yaani, ndugu na dada zetu Wakristo. Tunapowaonyesha wengine upendo mwororo, tunasaidia kudumisha umoja ambao ni sehemu muhimu ya ibada ya kweli.​—Mika 2:12. w21.01 20 ¶1-2

Jumatatu, Mei 9

Unganisha moyo wangu ili niliogope jina lako.​—Zab. 86:11.

Timu yenye umoja ina uwezekano mkubwa zaidi wa kushinda kuliko timu iliyo na wachezaji ambao hawana umoja. Moyo wako unaweza kuwa kama timu yenye mafanikio, ikiwa mawazo, tamaa, na hisia zako zimeungana ili kumtumikia Yehova. Kumbuka kwamba Shetani angependa kuugawanya moyo wako. Anataka mawazo, tamaa, na hisia zako zipingane na viwango vya Yehova. Hata hivyo, ili umtumikie Yehova unahitaji kuwa na moyo kamili. (Mt. 22:36-38) Kamwe usimruhusu Shetani augawanye moyo wako! Sali kwa Yehova kama Daudi alivyofanya aliposali: “Unganisha moyo wangu ili niliogope jina lako.” Azimia kuishi kulingana na sala hiyo. Azimia kila siku kuonyesha kwamba unaliheshimu sana jina takatifu la Yehova kupitia maamuzi unayofanya, iwe ni makubwa au madogo. Kwa kufanya hivyo, ukiwa Shahidi wa Yehova, utalitukuza jina la Yehova. (Met. 27:11) Na sisi sote tutaweza kusema hivi kama nabii Mika: “Sisi tutatembea katika jina la Yehova Mungu wetu milele na milele.”​—Mika 4:5. w20.06 13 ¶17-18

Jumanne, Mei 10

Naye atatoka kwa hasira kali ili kuwaangamiza na kuwaua wengi.​—Dan. 11:44.

Shambulizi hilo la mfalme wa kaskazini akishirikiana pamoja na serikali nyingine za ulimwengu, litamkasirisha Mweza-Yote na vita vya Har–Magedoni vitaanza. (Ufu. 16:14, 16) Wakati huo, mfalme wa kaskazini pamoja na mataifa mengine yanayofanyiza Gogu wa Magogu, atafikia mwisho wake, na “hakuna atakayemsaidia.” (Dan. 11:45) Mstari unaofuata katika unabii huo wa Danieli unatupatia habari zaidi kuhusu jinsi mfalme wa kaskazini na wale wanaomuunga mkono watakavyofikia mwisho wao na jinsi tutakavyookolewa. (Dan. 12:1) Mstari huo unamaanisha nini? Mikaeli ni jina lingine la Mfalme wetu anayetawala, Kristo Yesu. Amekuwa ‘akisimama kwa ajili’ ya watu wa Mungu tangu mwaka wa 1914 wakati ambapo Ufalme wake ulisimamishwa mbinguni. Hivi karibuni, “atasimama,” au atawaangamiza maadui wake katika vita vya Har–Magedoni. Vita hivyo ndivyo vitakavyohitimisha kipindi cha wakati ambacho Danieli alikiita “wakati wa taabu” ambao haujawahi kamwe kutokea katika historia.​—Ufu. 6:2; 7:14. w20.05 15-16 ¶15-17

Jumatano, Mei 11

Yosefu akapelekwa Misri.​—Mwa. 39:1.

Alipokuwa mtumwa na baadaye mfungwa, Yosefu hakuwa na uhuru wa kwenda mahali popote alipotaka na mambo ambayo angeweza kufanya yalidhibitiwa. Ni nini kilichomsaidia kuwa na usawaziko? Badala ya kukazia fikira mambo ambayo hangeweza kutimiza, alifanya kwa bidii kazi aliyokuwa amepewa. Yosefu aliendelea kumwona Yehova kuwa Mtu muhimu zaidi maishani mwake. Kwa sababu hiyo, Yehova alibariki kila kitu ambacho Yosefu alifanya. (Mwa. 39:21-23) Simulizi la Yosefu linatukumbusha kwamba ulimwenguni kuna ukatili na kwamba watu watatutendea isivyo haki. Hata mwamini mwenzetu anaweza kutuumiza. Lakini ikiwa tutamwona Yehova kuwa Mwamba au Kimbilio letu, hatutavunjika moyo au kuacha kumtumikia. (Zab. 62:6, 7; 1 Pet. 5:10) Kumbuka pia kwamba huenda Yosefu alikuwa na umri wa miaka 17 hivi, Yehova alipoanza kushughulika naye kwa njia ya pekee. Ni wazi kwamba Yehova anawatumaini watumishi wake vijana. Leo, vijana wengi ni kama Yosefu. Wao pia wana imani katika Yehova. Baadhi yao wamefungwa gerezani isivyo haki kwa sababu wameendelea kuwa washikamanifu kwa Mungu.​—Zab. 110:3. w20.12 16 ¶3; 17 ¶5, 7

Alhamisi, Mei 12

Wakawaita mitume, wakawapiga viboko, na kuwaagiza waache kusema kwa msingi wa jina la Yesu.​—Mdo. 5:40.

Mtume Petro na Yohana waliliona kuwa jambo la heshima kuteswa kwa sababu ya kuwa wafuasi wa Yesu na kuwaambia wengine kuhusu mafundisho yake. (Mdo. 4:18-21; 5:27-29, 41, 42) Wanafunzi hao hawakuwa na sababu yoyote ya kuaibika. Mwishowe, Wakristo hao wanyenyekevu wa karne ya kwanza waliwatendea wanadamu mambo mengi mema kuliko yaliyotendwa na wapinzani wao. Kwa mfano, vitabu vilivyoongozwa na roho ya Mungu vilivyoandikwa na baadhi ya Wakristo hao, bado vinaendelea kuwasaidia na kuwapa tumaini mamilioni ya watu. Na Ufalme waliotangaza unatawala sasa mbinguni na hivi karibuni utawatawala wanadamu wote. (Mt. 24:14) Kinyume cha hilo, serikali ya kisiasa yenye nguvu ambayo iliwatesa Wakristo hao ilianguka na kubaki historia, ilhali wanafunzi hao washikamanifu sasa ni wafalme mbinguni. Wapinzani wao wamekufa; na ikiwa watafufuliwa, watakuwa raia wa Ufalme ambao ulitangazwa na Wakristo hao ambao waliwachukia.​—Ufu. 5:10. w20.07 15 ¶4

Ijumaa, Mei 13

[Abrahamu] alikuwa akingojea jiji lililo na misingi ya kweli, ambalo mbuni na mjenzi wake ni Mungu.​—Ebr. 11:10.

Abrahamu alikuwa na imani yenye nguvu katika ahadi za Mungu, hivi kwamba ni kana kwamba alikuwa akimwona Mtiwa-Mafuta au Masihi ambaye angekuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Kwa sababu hiyo, Yesu aliweza kuwaambia hivi Wayahudi katika siku zake: “Baba yenu Abrahamu alishangilia sana tazamio la kuona siku yangu, naye aliiona na kushangilia.” (Yoh. 8:56) Ni wazi kwamba Abrahamu alijua kuwa wazao wake wangefanyiza Ufalme ambao ungesimamishwa na Yehova, naye alikuwa tayari kumngojea Yehova atimize ahadi hiyo. Abrahamu alionyeshaje kwamba alikuwa akingojea Ufalme, au “jiji,” ambalo mbuni wake ni Mungu? Kwanza, Abrahamu hakuwa raia wa ufalme wowote hapa dunia. Alikuwa akihama-hama kutoka eneo moja kwenda lingine, hakuwa na eneo la kudumu la kuishi na hakumuunga mkono mfalme yeyote wa kibinadamu. Kwa kuongezea, Abrahamu hakuamua kuanzisha ufalme wake mwenyewe. Badala yake aliendelea kumtii Yehova, akimngojea atimize ahadi Yake. Kwa kufanya hivyo, Abrahamu alionyesha imani ya pekee katika Yehova. w20.08 3 ¶4-5

Jumamosi, Mei 14

Yule ambaye amekufa ameondolewa hatia ya dhambi yake.​—Rom. 6:7.

Yehova anaahidi kwamba hakuna mtu atakayeishi chini ya utawala wa Kristo atakayesema: “Mimi ni mgonjwa.” (Isa. 33:24) Hivyo, wale watakaofufuliwa kutoka kwa wafu wataumbwa upya wakiwa na miili yenye afya. Hata hivyo, hawatakuwa wakamilifu hapohapo baada ya ufufuo. Kwa kuwa huenda hilo lingefanya wapendwa wao wasiwatambue. Inaonekana kwamba wanadamu wote watafikia ukamilifu hatua kwa hatua wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo. Ni mwishoni tu mwa ile miaka elfu moja ndipo Yesu atakapomrudishia Baba yake Ufalme. Kisha, Ufalme utakuwa umekamilisha kazi yake kikamili, kutia ndani kuwafanya wanadamu kuwa wakamilifu. (1 Kor. 15:24-28; Ufu. 20:1-3) Wazia hali itakavyokuwa kukutana tena na wapendwa wako. Je, shangwe utakayohisi itakufanya ucheke au ulie? Je, utamwimbia Yehova nyimbo za sifa kwa sauti? Jambo moja ni hakika: utahisi upendo mkubwa kwa Baba yako anayekujali na mwana wake asiye na ubinafsi, kwa sababu ya zawadi ya pekee ya ufufuo. w20.08 16-17 ¶9-10

Jumapili, Mei 15

Kila mmoja ana zawadi yake mwenyewe kutoka kwa Mungu, mmoja kwa njia hii, mwingine kwa njia ile.​—1 Kor. 7:7.

Mtume Paulo aliwatia moyo Wakristo wafikirie ikiwa wangeweza kumtumikia Yehova wakiwa waseja. (1 Kor. 7:8, 9) Kwa hakika, Paulo hakuwadharau Wakristo waseja. Isitoshe, alimchagua kijana Timotheo, ndugu mseja, kushughulikia migawo mizito. (Flp. 2:19-22) Hivyo, ni wazi kwamba lingekuwa kosa kufikiri kuwa ndugu ana sifa za kustahili au hana kwa msingi tu wa kwamba amefunga ndoa au la. (1 Kor. 7:32-35, 38) Yesu na Paulo hawakufundisha kwamba ni lazima kwa Mkristo kufunga ndoa ama kubaki mseja. Hivyo, tunaweza kusema nini kuhusu ndoa na useja? Mnara wa Mlinzi wa Oktoba 1, 2012, ulieleza jambo hilo kwa njia nzuri uliposema: “Kwa kweli, useja na ndoa unaweza kuonwa kuwa zawadi kutoka kwa Mungu. . . . Yehova hauoni [useja] kuwa chanzo cha aibu na huzuni.” Tukiwa na hilo akilini, tunahitaji kuheshimu sehemu ya ndugu na dada waseja kutanikoni. w20.08 28 ¶8-9

Jumatatu, Mei 16

Kuhusu siku hiyo na saa hiyo, hakuna mtu anayejua, . . . ila Baba tu.​—Mt. 24:36.

Katika baadhi ya nchi, watu huitikia kwa njia nzuri wanaposikia habari njema. Wamekuwa wakisubiri kwa hamu habari hizo! Katika nchi nyingine, watu hawapendezwi na habari za Mungu au Biblia. Kwa kawaida watu huitikiaje katika eneo lako? Haidhuru watu wanaitikiaje, Yehova anatarajia tuendelee kuhubiri hadi atakaposema kazi hiyo imekamilika. Tayari Yehova amepanga wakati ambapo kazi ya kuhubiri itakamilika, na ndipo “ule mwisho utakapokuja.” (Mt. 24:14) Yesu alitabiri kuhusu matukio na hali ambazo zingekuwepo katika siku za mwisho na ambazo zingewakengeusha wafuasi wake na kuwafanya waache kukazia fikira kazi ya kuhubiri. Aliwahimiza wafuasi wake ‘waendelee kukesha.’ (Mt. 24:42) Leo, tunakabiliana na mambo yanayofanana na yale yaliyowazuia watu wa siku za Noa kukazia fikira onyo lililotolewa na Noa. (Mt. 24:37-39; 2 Pet. 2:5) Hivyo, tungependa kukazia fikira kazi ambayo Yehova ametupatia tufanye. w20.09 8 ¶1-2, 4

Jumanne, Mei 17

Wale wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.​—2 Tim. 3:12.

Shetani ana “hasira kali,” na tutakuwa tukijidanganya ikiwa tutafikiri kwamba kwa njia fulani tunaweza kuepuka ghadhabu yake. (Ufu. 12:12) Hivi karibuni, utimilifu wa kila mmoja wetu utajaribiwa. Muda si mrefu, ulimwengu utakumbwa na “dhiki kuu ambayo haijawahi kutokea tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa.” (Mt. 24:21) Wakati huo, huenda watu wa familia wakatusaliti na kazi yetu ikapigwa marufuku. (Mt. 10:35, 36) Kama Mfalme Asa, je, kila mmoja wetu atamtumaini Yehova ili kupata msaada na ulinzi? (2 Nya. 14:11) Yehova amekuwa akituandaa kiroho kwa ajili ya mambo yatakayotokea wakati ujao. Anamwongoza “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” anayetuandalia chakula cha kiroho chenye lishe kwa wakati unaofaa, kinachotusaidia kuendelea kuwa imara tunapomwabudu Mungu. Lakini ni lazima tufanye sehemu yetu ili tujenge imani thabiti katika Yehova.​—Ebr. 10:38, 39. w20.09 18 ¶16-18

Jumatano, Mei 18

Moyo wa mfalme ni kama vijito vya maji mkononi mwa Yehova. Yeye huuelekeza mahali popote anapopenda.​—Met. 21:1.

Yehova anaweza kuitumia roho yake takatifu yenye nguvu kuwafanya watu wenye mamlaka watende kulingana na mapenzi yake, ikiwa hilo linapatana na kusudi lake. Wanadamu wanaweza kuchimba mfereji ili kuyafanya maji ya kijito yaelekee mahali wanakotaka. Vivyo hivyo, Yehova anaweza kuitumia roho yake kuelekeza mawazo ya watawala yapatane na kusudi lake. Jambo hilo linapotokea, watu wenye mamlaka huchochewa kufanya maamuzi yatakayowanufaisha watu wa Mungu. (Linganisha Ezra 7:21, 25, 26.) Tunaweza kufanya nini? Tunaweza kusali “kwa ajili ya . . . wafalme na wote wenye mamlaka” pindi wanapohitaji kufanya maamuzi ambayo yanaweza kuathiri maisha na huduma yetu ya Kikristo. (1 Tim. 2:1, 2, maelezo ya chini; Neh. 1:11) Kama Wakristo wa karne ya kwanza walivyofanya, sisi pia tunasali kwa bidii kwa Mungu kwa ajili ya ndugu na dada zetu ambao wako gerezani.​—Mdo. 12:5; Ebr. 13:3. w20.11 15 ¶13-14

Alhamisi, Mei 19

Mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza.​—Mt. 28:19.

Ikiwa wewe ndiye uliyejifunza na mwanafunzi mpya wa Biblia, unasisimuka sana unapomwona akibatizwa! (1 The. 2:19, 20) Wanafunzi wapya waliobatizwa ni ‘barua nzuri zinazowapendekeza’ wale waliojifunza nao na pia kutaniko zima. (2 Kor. 3:1-3) Inapendeza kuona kwamba katika kipindi cha miaka minne, kwa wastani mafunzo ya Biblia 10,000,000 hivi yameripotiwa kila mwezi ulimwenguni pote. Katika kipindi hichohicho, kwa wastani wanafunzi zaidi ya 280,000 walibatizwa kila mwaka na kuwa Mashahidi wa Yehova na wanafunzi wapya wa Kristo. Tunaweza kuwasaidiaje wengi zaidi kati ya mamilioni hayo ya wanafunzi wa Biblia wafikie hatua ya ubatizo? Maadamu Yehova anaonyesha subira kwa kuwapa watu wakati na fursa ya kuwa wanafunzi wa Kristo, tungependa kufanya yote tunayoweza kuwasaidia wafanye maendeleo na kubatizwa haraka iwezekanavyo. Wakati uliobaki ni mfupi sana!​—1 Kor. 7:29a; 1 Pet. 4:7. w20.10 6 ¶1-2

Ijumaa, Mei 20

Mungu huwapinga wenye majivuno, lakini huwapa wanyenyekevu.​—Yak. 4:6.

Mfalme Sauli hakumtii Yehova. Na nabii Samweli alipomwambia kuhusu kosa lake, Sauli hakukubali kwamba amekosea. Badala yake, alijaribu kujitetea kwa kupunguza uzito wa kosa lake la kutotii na kuwatupia wengine lawama. (1 Sam. 15:13-24) Mapema, Sauli alikuwa ameonyesha mtazamo kama huo. (1 Sam. 13:10-14) Inasikitisha kwamba Sauli aliruhusu moyo wake uwe na kiburi. Hakurekebisha njia yake ya kufikiri, hivyo Yehova alimkaripia na kumkataa. Ili tujifunze kutokana na mfano wa Sauli, ni vema tukajiuliza maswali haya: ‘Ninaposoma shauri kutoka katika Neno la Mungu, je, ninatafuta visingizio vya kutotumia shauri hilo? Je, ninapunguza uzito wa kosa ninalofanya? Je, ninamtupia lawama mtu mwingine?’ Ikiwa jibu letu ni ndiyo kwa swali lolote kati ya hayo, ni lazima turekebishe njia yetu ya kufikiri na mtazamo wetu. La sivyo, moyo wetu unaweza kuwa na kiburi sana hivi kwamba Yehova atakataa tusiwe rafiki zake. w20.11 20 ¶4-5

Jumamosi, Mei 21

Mkumbuke Muumba wako Mkuu katika siku za ujana wako, kabla hazijaja siku za taabu wala haijafika miaka utakaposema: “Siifurahii.”—Mhu. 12:1.

Enyi vijana, chagueni ni nani mtakayemtumikia. Mnahitaji kujithibitishia wenyewe Yehova ni nani, kusudi lake linahusisha nini, na jinsi mapenzi yake yanavyohusiana na maisha yenu. (Rom. 12:2) Kisha, mtaweza kufanya uamuzi muhimu zaidi maishani mwenu, yaani, uamuzi wa kumtumikia Yehova. (Yos. 24:15) Ikiwa utadumisha ratiba ya kusoma na kujifunza Biblia kwa ukawaida, upendo wako kwa Yehova utaendelea kukua na imani yako kumwelekea itakuwa imara zaidi. Chagua kutanguliza mapenzi ya Yehova maishani mwako. Ulimwengu wa Shetani unatuahidi kwamba ikiwa tukitumia vipawa vyetu kujinufaisha tutakuwa na furaha. Lakini ukweli ni kwamba, wale wanaokazia fikira malengo ya kimwili wanajichoma wenyewe “kila mahali kwa maumivu mengi.” (1 Tim. 6:9, 10) Kwa upande mwingine, ikiwa utamsikiliza Yehova na kuchagua kutanguliza mapenzi yake, utafanikiwa maishani ‘nawe utatenda kwa hekima.’​—Yos. 1:8. w20.10 30-31 ¶17-18

Jumapili, Mei 22

Ni lazima . . . nitangaze habari njema ya Ufalme wa Mungu . . . , kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.​—Luka 4:43.

Katika karne ya kwanza, ujumbe ambao Yesu alihubiri uliwapa wanadamu wote tumaini. Aliwaamuru wafuasi wake waendeleze kazi aliyokuwa ameanzisha, yaani, kutoa ushahidi “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Bila shaka, wasingeweza kufanya kazi hiyo kwa nguvu zao wenyewe. Wangehitaji roho takatifu, yaani, “msaidizi” ambaye Yesu alikuwa amewaahidi. (Yoh. 14:26; Zek. 4:6) Wafuasi wa Yesu walipokea roho takatifu siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. Kwa msaada wa roho hiyo mara moja walianza kuhubiri, na kwa muda mfupi, maelfu ya watu walikubali habari njema. (Mdo. 2:41; 4:4) Upinzani ulipotokea, wanafunzi hawakushindwa na woga bali walimwomba Mungu ili awasaidie. Walisali hivi: “[Wawezeshe] watumwa wako waendelee kutangaza neno lako kwa ujasiri wote.” Kisha walijazwa roho takatifu na kuendelea “kutangaza neno la Mungu kwa ujasiri.”​—Mdo. 4:18-20, 29, 31. w20.10 21 ¶4-5

Jumatatu, Mei 23

Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu kulingana na Maandiko; na . . . alifufuliwa.​—1 Kor. 15:3, 4.

Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova alimfufua Yesu? Kulikuwa na watu wengi waliomwona Yesu baada ya kufufuliwa nao walitoa ushahidi kwamba alikuwa amefufuliwa. (1 Kor. 15:5-7) Shahidi wa kwanza kutajwa katika orodha ya mtume Paulo alikuwa mtume Petro (Kefa). Kikundi cha wanafunzi kilithibitisha kwamba Petro alimwona Yesu aliyefufuliwa. (Luka 24:33, 34) Pia, ‘wale mitume 12’ walimwona Yesu baada ya kufufuliwa. Kisha Kristo “aliwatokea ndugu zaidi ya 500 kwa wakati mmoja,” huenda ni huko Galilaya kwenye tukio lenye shangwe linalotajwa kwenye Mathayo 28:16-20. Pia, Yesu “alimtokea Yakobo,” ambaye inaelekea alikuwa ndugu nusu ya Yesu, na ambaye awali hakuamini kwamba Yesu alikuwa Masihi. (Yoh. 7:5) Baada ya kumwona Yesu aliyefufuliwa, Yakobo aliamini. Inapendeza kwamba karibu mwaka wa 55 W.K., Paulo alipoandika barua hiyo, watu wengi walioshuhudia ufufuo wa Yesu walikuwa hai, hivyo mtu yeyote ambaye alikuwa na shaka angeweza kuwauliza mashahidi hao wenye kutegemeka. w20.12 3 ¶5, 7-8

Jumanne, Mei 24

Yehova atamtegemeza kwenye kitanda chake cha ugonjwa.​—Zab. 41:3.

Tunapokuwa wagonjwa na hasa ikiwa tunapambana na ugonjwa wa kudumu, huenda ikawa vigumu kwetu kuwa na maoni yanayofaa kuhusu hali yetu. Hivyo mwombe Yehova msaada. Ingawa hatuponyi kimuujiza kwa sasa, anatufariji na anaweza kutupatia nguvu tunazohitaji ili kuvumilia. (Zab. 94:19) Kwa mfano, huenda akawachochea Wakristo wenzetu watusaidie tunapohitaji msaada wa kufanya kazi fulani za nyumbani. Anaweza kuwachochea ndugu zetu wasali pamoja nasi. Au anaweza kutukumbusha mawazo yenye kufariji yanayopatikana katika Neno lake, kama vile tumaini zuri la uhai mkamilifu usio na magonjwa wala maumivu katika ulimwengu mpya unaokuja. (Rom. 15:4) Hata hivyo, huenda tukahisi kwamba hatuwezi kufanya mengi katika huduma. Dada anayeitwa Laurel alilazimika kulala ndani ya mashine ya chuma iliyomsaidia kupumua kwa miaka 37! Laurel alikabiliana na kansa, upasuaji mbalimbali mkubwa, na magonjwa ya kudumu ya ngozi. Lakini hayo hayakumnyamazisha. Aliwatolea ushahidi wauguzi na wahudumu wengine wa afya ambao walifika nyumbani kwake na aliwasaidia angalau watu 17 kupata ujuzi sahihi wa Biblia! w20.12 24 ¶9; 25 ¶12

Jumatano, Mei 25

Yehova yuko upande wangu; sitaogopa. Mwanadamu atanifanya nini?​—Zab. 118:6.

Mtume Paulo alihitaji msaada. Karibu mwaka wa 56 W.K., umati ulimkokota nje ya hekalu huko Yerusalemu na kujaribu kumuua. Siku iliyofuata maadui wa Paulo walikuwa karibu kumrarua-rarua alipokuwa mbele ya Sanhedrini. (Mdo. 21:30-32; 22:30; 23:6-10) Wakati huo, huenda Paulo alijiuliza, ‘Nitaweza kuvumilia hali hii hadi lini?’ Paulo alipata msaada gani? Usiku uliofuata, “Bwana,” yaani, Yesu, alisimama kando yake na kumwambia: “Jipe moyo! Kwa maana kama vile ambavyo umekuwa ukitoa ushahidi kamili kunihusu katika Yerusalemu, ndivyo utakavyotoa ushahidi huko Roma pia.” (Mdo. 23:11) Alitiwa moyo kwa wakati unaofaa! Yesu alimpongeza Paulo kwa ushahidi ambao alikuwa ametoa huko Yerusalemu. Na aliahidi kwamba Paulo atafika salama Roma, ambako pia angetoa ushahidi. Baada ya kupata uhakikisho huo, lazima Paulo alihisi akiwa salama kama mtoto aliyebebwa mikononi mwa baba yake. w20.11 12 ¶1, 3; 13 ¶4

Alhamisi, Mei 26

Tuna tumaini hilo . . . , likiwa hakika na imara.​—Ebr. 6:19.

Tumaini letu la Ufalme ni “kama nanga ya nafsi,” inayotusaidia kuendelea kuwa imara licha ya changamoto tunazokabiliana nazo au mawazo yenye kuhangaisha. Tafakari kuhusu ahadi za Yehova za wakati ujao ambapo hatutakuwa na mawazo yenye kuhangaisha. (Isa. 65:17) Jiwazie ukiwa katika ulimwengu mpya wenye amani ambamo hali zenye kusababisha mkazo hazitakuwapo tena. (Mika 4:4) Pia, unaweza kuimarisha tumaini lako kadiri unavyowaeleza wengine kuhusu tumaini hilo. Fanya yote uwezayo katika kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Ukifanya hivyo, unaweza “kuwa na uhakikisho kamili wa tumaini mpaka mwisho.” (Ebr. 6:11) Kadiri mfumo huu wa mambo unavyofikia mwisho wake, tutakabili changamoto nyingi hata zaidi zinazoweza kutuletea mawazo yenye kuhangaisha. Tutafaulu kukabiliana na changamoto hizo na kuendelea kuwa watulivu, si kwa nguvu zetu wenyewe, bali kwa kumtumaini Yehova. Acheni tuonyeshe kwa matendo yetu kwamba tuna imani katika ahadi hii ya Yehova: “Mtakuwa na nguvu mkiendelea kuwa watulivu na kuwa na tumaini.”​—Isa. 30:15. w21.01 7 ¶17-18

Ijumaa, Mei 27

Yehova ni mwenye upendo mwororo sana.​—Yak. 5:11.

Ona kwamba andiko la Yakobo 5:11 linahusianisha upendo mwororo wa Yehova na sifa nyingine inayotufanya tumkaribie, yaani, rehema yake. (Kut. 34:6) Njia moja ambayo Yehova anatuonyesha rehema ni kwa kutusamehe makosa tunayofanya. (Zab. 51:1) Katika Biblia, sifa ya rehema inahusisha mengi zaidi ya kusamehe. Rehema ni hisia yenye nguvu inayotoka ndani kabisa ya moyo wa mtu anapomwona mtu mwingine akitaabika, naye anachochewa kujitahidi kumsaidia mtu huyo. Yehova anaifafanua tamaa yake yenye kina ya kutusaidia kuwa ni yenye nguvu zaidi kuliko hisia ambazo mama anazo kwa mtoto wake. (Isa. 49:15) Tunapotaabika, rehema ya Yehova inamchochea atusaidie. (Zab. 37:39; 1 Kor. 10:13) Tunaweza kuwaonyesha rehema ndugu na dada zetu kwa kuwasamehe na kutoweka kinyongo wanapotukosea. (Efe. 4:32) Lakini njia nyingine muhimu tunayoweza kuonyesha rehema ni kwa kuwategemeza ndugu na dada zetu wanapopitia hali ngumu maishani. Hivyo, tutakuwa tukimwiga Yehova ambaye ni mfano bora zaidi wa kuonyesha upendo mwororo.​—Efe. 5:1. w21.01 21 ¶5

Jumamosi, Mei 28

Kristo . . . [aliwaachia] ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu.​—1 Pet. 2:21.

Kichwa cha familia anahitaji kuwa na usawaziko. Hapaswi kuhangaikia kupita kiasi kazi yake ya kimwili hivi kwamba ashindwe kuiandalia familia yake mahitaji yao ya kiroho na ya kihisia kwa njia nzuri na kuwazoeza. Yehova hutuzoeza na kututia nidhamu kwa sababu anataka kutusaidia. (Ebr. 12:7-9) Kama Baba yake, Yesu huwazoeza kwa upendo wale walio chini ya mamlaka yake. (Yoh. 15:14, 15) Yuko thabiti lakini ni mwenye fadhili. (Mt. 20:24-28) Anaelewa kwamba sisi si wakamilifu na tuna mwelekeo wa kukosea. (Mt. 26:41) Kichwa cha familia anayemwiga Yehova na Yesu anakumbuka kwamba mke na watoto wake hawajakamilika. ‘Hamkasirikii kwa uchungu’ mke wake na watoto. (Kol. 3:19) Badala yake, anatumia kanuni ambayo inapatikana katika andiko la Wagalatia 6:1 na kujitahidi kuwarekebisha “kwa roho ya upole,” akikumbuka kwamba yeye pia si mkamilifu. Kama Yesu, anatambua kwamba njia bora ya kuwafundisha ni kupitia kielelezo chake kizuri. w21.02 6-7 ¶16-18

Jumapili, Mei 29

Kila kitu kinachopumua​—na kimsifu Yah.​—Zab. 150:6.

Kupitia fidia, Yehova alinunua uhai wa kila mtu kutanikoni, na wa wanadamu wengine wote ambao watamwamini Yesu. (Marko 10:45; Mdo. 20:28; 1 Kor. 15:21, 22) Hivyo, ni jambo linalofaa kwamba alimweka rasmi Yesu, ambaye alitoa uhai wake kuwa fidia, awe kichwa cha kutaniko. Akiwa kichwa chetu, Yesu ana mamlaka ya kuweka sheria zinazoongoza mwenendo wa mtu mmoja-mmoja kwenye familia na katika kutaniko lote, na pia kuhakikisha kwamba zinafuatwa. (Gal. 6:2) Lakini Yesu anafanya mengi zaidi ya kuweka tu sheria. Anamlisha na kumtunza kila mmoja wetu. (Efe. 5:29) Akina dada wanaonyesha kwamba wanamheshimu Kristo kwa kufuata mwongozo wanaopewa na wanaume ambao amewaweka rasmi ili wawatunze. Akina ndugu wanaonyesha kwamba wanaelewa mpango wa ukichwa kwa kuwaheshimu na kuwastahi akina dada. Wote kutanikoni wanapoelewa na kuheshimu kanuni ya ukichwa, kutaniko linakuwa na amani. Na jambo muhimu hata zaidi ni kwamba tunamletea sifa Yehova, Baba yetu wa mbinguni anayetupenda. w21.02 18-19 ¶14-17

Jumatatu, Mei 30

Daudi akamuuliza Yehova.​—1 Sam. 30:8.

Pindi fulani Daudi na wanaume wake walipokuwa katika eneo la Wafilisti wakimkimbia Sauli, waliacha familia zao na kwenda kupigana vita. Wanaume hao walipokuwa wameondoka, maadui walivamia nyumba zao na kuteka familia zao. Daudi angeweza kufikia mkataa kwamba kwa kuwa alikuwa shujaa wa vita mwenye uzoefu, angeweza kupanga kirahisi mkakati wa kuwakomboa mateka. Badala ya kufanya hivyo, Daudi alitafuta mwongozo kutoka kwa Yehova. Daudi alimuuliza hivi Yehova: “Je, nilifuatie kundi hili la wavamizi?” Yehova alimwambia Daudi alipaswa kufanya hivyo na akamhakikishia kwamba angefanikiwa. (1 Sam. 30:7-10) Unaweza kujifunza nini kutokana na kisa hicho? Tafuta ushauri kabla ya kufanya maamuzi. Enyi vijana, waulizeni wazazi wenu. Mnaweza pia kupata ushauri mzuri kwa kuzungumza na mzee wa kutaniko mwenye uzoefu. Yehova anawatumaini wanaume hao waliowekwa rasmi, nawe unaweza kufanya vivyo hivyo pia. Yehova anawaona kuwa “zawadi” kwa kutaniko. (Efe. 4:8) Utanufaika kwa kuiga imani yao na kwa kusikiliza mapendekezo yenye hekima wanayokupa. w21.03 4-5 ¶10-11

Jumanne, Mei 31

[Hakuna kitakachoweza] kututenga na upendo wa Mungu.​—Rom. 8:38, 39.

Yesu alisema kwamba ikiwa hatutumii mambo tunayojifunza, tunakuwa kama mwanamume aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga. Anafanya kazi kwa bidii, lakini jitihada zake ni za bure. Kwa nini? Kwa sababu dhoruba na mafuriko yakipiga nyumba yake, itaporomoka. (Mt. 7:24-27) Vivyo hivyo, ikiwa hatutatumia mambo tunayojifunza, tutakuwa tumefanya kazi ya bure. Imani yetu inapojaribiwa kwa sababu ya majaribu au mateso, haitakuwa imara vya kutosha. Kwa upande mwingine, tunapojifunza na kutumia mambo hayo, tunafanya maamuzi mazuri zaidi, tunakuwa na amani zaidi, na tunasitawisha imani yenye nguvu zaidi. (Isa. 48:17, 18) Ili kudumisha utimilifu wetu wakati wa jaribu, tunahitaji kumtegemea Yehova kupitia sala na kudumisha ratiba nzuri ya kujifunza. Na ni lazima sikuzote tukumbuke kwamba moja kati ya mambo muhimu zaidi tunayoweza kufanya, ni kumletea Yehova utukufu. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba kamwe Yehova hatatuacha na kwamba hakuna kitu chochote ambacho mtu anaweza kufanya ili kuvunja kifungo cha upendo wake kwetu.​—Ebr. 13:5, 6. w21.03 15 ¶6; 18 ¶20

    Maktaba Kwenye Mtandao (1950-2022)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2022 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki