Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • es22 kur. 57-67
  • Juni

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Juni
  • Kuyachunguza Maandiko Kila Siku—2022
  • Jumatano, Juni 1
  • Alhamisi, Juni 2
  • Ijumaa, Juni 3
  • Jumamosi, Juni 4
  • Jumapili, Juni 5
  • Jumatatu, Juni 6
  • Jumanne, Juni 7
  • Jumatano, Juni 8
  • Alhamisi, Juni 9
  • Ijumaa, Juni 10
  • Jumamosi, Juni 11
  • Jumapili, Juni 12
  • Jumatatu, Juni 13
  • Jumanne, Juni 14
  • Jumatano, Juni 15
  • Alhamisi, Juni 16
  • Ijumaa, Juni 17
  • Jumamosi, Juni 18
  • Jumapili, Juni 19
  • Jumatatu, Juni 20
  • Jumanne, Juni 21
  • Jumatano, Juni 22
  • Alhamisi, Juni 23
  • Ijumaa, Juni 24
  • Jumamosi, Juni 25
  • Jumapili, Juni 26
  • Jumatatu, Juni 27
  • Jumanne, Juni 28
  • Jumatano, Juni 29
  • Alhamisi, Juni 30
Kuyachunguza Maandiko Kila Siku—2022
es22 kur. 57-67

Juni

Jumatano, Juni 1

Tulijitahidi kuwapa habari njema ya Mungu na hata uhai wetu wenyewe.—1 The. 2:8.

Ni lazima mwalimu apendezwe kibinafsi na mwanafunzi wake. Amwone kuwa ndugu au dada yake mtarajiwa wa kiroho. Si rahisi kwao kuwaacha marafiki zao ulimwenguni na kufanya mabadiliko yanayohitajika ili kumtumikia Yehova. Walimu wa Biblia wenye matokeo huwatambulisha wanafunzi wao kwa wengine kutanikoni, wanaoweza kuwasaidia wamkaribie Yehova zaidi. Kisha, wanafunzi wanaweza kufurahia kushirikiana na watu wa Mungu ambao wanaweza kuwasaidia kiroho na kihisia. Tungependa kila mwanafunzi ahisi kwamba yeye ni sehemu ya kutaniko na ya familia yetu ya kiroho. Tunataka avutiwe na undugu wetu wa Kikristo wenye upendo mchangamfu. Kisha, itakuwa rahisi zaidi kwake kuacha kushirikiana kwa ukaribu na watu ambao hawamsaidii kumpenda Yehova. (Met. 13:20) Ikiwa rafiki zake wa awali wataacha kushirikiana naye, atajua kwamba anaweza kupata marafiki wa kweli katika tengenezo la Yehova.​—Marko 10:29, 30; 1 Pet. 4:4. w20.10 17 ¶10-11

Alhamisi, Juni 2

Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.​—Mt. 28:18.

Ikiwa tunataka kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova, ni lazima tuwe rafiki za Yesu. Kwa nini? Fikiria sababu hizi mbili. Kwanza, Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Baba mwenyewe anawapenda ninyi, kwa sababu mmenipenda.” (Yoh. 16:27) Pia, alisema hivi: “Hakuna mtu anayekuja kwa Baba bila kupitia kwangu.” (Yoh. 14:6) Kujaribu kuwa rafiki ya Yehova bila kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na Yesu ni kama kujaribu kuingia katika jengo fulani bila kupitia mlangoni. Yesu alitumia mfano kama huo alipojifafanua mwenyewe kuwa “mlango wa kondoo.” (Yoh. 10:7) Sababu ya pili ni kwamba Yesu aliiga kikamilifu sifa za Baba yake. Aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Yeyote ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.” (Yoh. 14:9) Hivyo, njia moja muhimu ya kumjua Yehova ni kujifunza kuhusu maisha ya Yesu. Kadiri tunavyojifunza kumhusu Yesu, ndivyo tutakavyozidi kumpenda. Na kadiri urafiki wetu pamoja naye unavyozidi kusitawi, ndivyo tutakavyozidi kumpenda Baba yake pia. w20.04 21-22 ¶5-6

Ijumaa, Juni 3

Ninapendezwa na udhaifu, . . . kwa maana ninapokuwa dhaifu, ndipo ninapokuwa na nguvu.​—2 Kor. 12:10.

Je, wewe ni mgonjwa kitandani au unatumia kiti cha magurudumu? Je, miguu yako ni dhaifu au uwezo wako wa kuona umepungua? Ikiwa ndivyo, je, unaweza kukimbia pamoja na wale ambao ni vijana na wenye afya? Ndiyo, unaweza! Ndugu na dada wengi wenye umri mkubwa na wenye matatizo ya afya wanakimbia katika barabara ya uzima. Hawawezi kufanya hivyo kwa nguvu zao wenyewe. Badala yake, wanategemea nguvu kutoka kwa Yehova wanaposikiliza mikutano ya Kikristo kupitia simu au kupitia Intaneti. Pia, wanashiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi kwa kuwahubiria madaktari, wauguzi, na watu wa ukoo. Usiruhusu kamwe matatizo yako ya afya yakufanye uvunjike moyo na kuamini kwamba wewe ni dhaifu na huwezi kukimbia kwenye barabara ya uzima. Yehova anakupenda kwa sababu ya imani uliyo nayo kwake na uvumilivu wako wa miaka mingi. Unahitaji msaada wake sasa kuliko wakati mwingine wowote, naye hatakuacha kamwe. (Zab. 9:10) Badala yake, atazidi kukukaribia hata zaidi. w20.04 29 ¶16-17

Jumamosi, Juni 4

Lakini ninafanya mambo yote kwa ajili ya habari njema, ili niishiriki pamoja na wengine.​—1 Kor. 9:23.

Unaweza kuzungumzia mambo gani na mtu wa dini? Jaribu kutafuta mambo mnayokubaliana. Huenda akawa anamwabudu Mungu mmoja, huenda anamtambua Yesu kuwa Mwokozi wa wanadamu, au huenda anaamini kwamba tunaishi katika nyakati zenye uovu ambazo zitakoma hivi karibuni. Kwa kutegemea mambo mnayokubaliana, wasilisha ujumbe wa Biblia kwa njia itakayomvutia. Kumbuka kwamba huenda watu wasiamini kila kitu ambacho dini zao hufundisha. Hivyo, hata baada ya kutambua dini ya mtu, jitahidi kujua mambo ambayo yeye binafsi anaamini. Ndugu mmoja mmishonari amejionea kwamba baadhi ya watu wanaosema kwamba wanaamini Utatu, kihalisi hawaamini kwamba Baba, Mwana, na roho takatifu ni Mungu mmoja. Anasema hivi: “Kujua jambo hilo kunafanya iwe rahisi zaidi kupata mambo tunayokubaliana na mtu huyo.” Hivyo, jitahidi kujua mambo ambayo watu wanaamini hasa. Kisha, kama mtume Paulo, unaweza kuwa “mambo yote kwa watu wa namna zote.”​—1 Kor. 9:19-22. w20.04 10 ¶9-10

Jumapili, Juni 5

Wakati huo watu wako wataponyoka, kila mtu atakayepatikana ameandikwa katika kile kitabu.​—Dan. 12:1.

Tunaweza kuutarajia wakati ujao tukiwa na uhakika kwa sababu Danieli na Yohana wanatuhakikishia kwamba wale wanaomtumikia Yehova na Yesu, wataokoka wakati huo wa taabu usioweza kulinganishwa na chochote. Danieli anasema kwamba watu watakaookoka ni wale ambao majina yao yatakuwa ‘yameandikwa katika kile kitabu.’ Tunaweza kufanya nini ili majina yetu yaandikwe katika kitabu hicho? Ni lazima tuthibitishe waziwazi kwamba tuna imani katika Yesu, Mwanakondoo wa Mungu. (Yoh. 1:29) Tunahitaji kujiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa. (1 Pet. 3:21) Na ni lazima tuunge mkono Ufalme wa Mungu kwa kufanya yote tuwezayo ili kuwasaidia wengine wajifunze kumhusu Yehova. Sasa ndio wakati wa kumtumaini Yehova hata zaidi na pia tengenezo lake la watu wanaomtumikia kwa ushikamanifu. Sasa ndio wakati wa kuunga mkono Ufalme wa Mungu. Ikiwa tutafanya hivyo, tutaokolewa wakati mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini watakapoharibiwa na Ufalme wa Mungu. w20.05 16 ¶18-19

Jumatatu, Juni 6

Ee Yehova, jina lako linadumu milele.​—Zab. 135:13.

Adamu na Hawa walijua jina la Yehova, na vilevile walijua kweli muhimu kumhusu Yule anayeitwa kwa jina hilo. Walimjua kuwa Muumba wao, yule aliyewapa uhai, makao maridadi ya Paradiso, na mwenzi mkamilifu. (Mwa. 1:26-28; 2:18) Hata hivyo, je, wangeendelea kutumia akili yao kamilifu kutafakari mambo yote ambayo Yehova alikuwa amefanya kwa ajili yao? Je, wangeendelea kumpenda na kumshukuru Yule aliyewakilishwa na jina hilo? Majibu ya maswali hayo yalikuwa wazi adui ya Mungu alipowajaribu. Akizungumza kupitia nyoka, Shetani alimuuliza Hawa swali hili: “Je, ni kweli kwamba Mungu alisema msile matunda ya kila mti wa bustani?” (Mwa. 2:16, 17; 3:1) Swali hilo lilikuwa na uwongo uliojificha uliokuwa kama sumu isiyoonekana. Lakini jambo ambalo Mungu alikuwa amesema ni kwamba wangeweza kula matunda ya kila mti, isipokuwa mti mmoja. (Mwa. 2:9) Shetani alifanya ionekane kwamba Mungu hakuwa mkarimu. Huenda Hawa alijiuliza, ‘Je, Mungu ananinyima jambo fulani zuri?’ w20.06 3-4 ¶8-9

Jumanne, Juni 7

Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari.​—Kol. 3:13.

Baadhi ya watumishi wa Yehova wameumizwa kihisia na waamini wenzao. Mtume Paulo alitambua kwamba nyakati fulani huenda tukawa na ‘sababu halali ya kulalamika juu ya’ ndugu au dada. Huenda hata tumetendewa isivyo haki. Tusipokuwa waangalifu, tunaweza kuwa na kinyongo. Hatimaye, hisia za uchungu zinaweza kumfanya mtu aache kushirikiana na watu wa Yehova. Pablo, ndugu kutoka Amerika Kusini alishtakiwa kwa uwongo kwamba amefanya kosa fulani, na kwa sababu hiyo akapoteza pendeleo la utumishi kutanikoni. Alitendaje? Pablo anasema hivi: “Nilikasirika, na hatua kwa hatua nikaacha kushirikiana na kutaniko.” Au dhamiri yenye hatia inaweza kumhangaisha sana mtu ambaye alivunja sheria ya Mungu wakati uliopita, na kumfanya ajihisi kwamba hastahili upendo wa Mungu. Hata kama alitubu na kuonyeshwa rehema, huenda akahisi kwamba sasa hafai tena kuwa miongoni mwa watu wa Mungu. Unahisije kuhusu ndugu na dada wanaokabili hali kama ambazo tumetoka tu kuzungumzia? w20.06 19 ¶6-7

Jumatano, Juni 8

Mtu mwerevu huona hatari na kujificha.​—Met. 22:3.

Ni lazima tujifunze kutambua hali zinazoweza kutudhuru na kisha tuziepuke. (Ebr. 5:14) Kwa mfano, tunahitaji kutumia hekima tunapochagua burudani na tafrija tutakazoshiriki. Mara nyingi, vipindi vya televisheni na sinema zinaonyesha upotovu wa maadili. Mwenendo huo unamchukiza Mungu na bila shaka unaleta madhara. Hivyo, tunaepuka burudani zinazoweza kudhoofisha upendo wetu kwa Mungu hatua kwa hatua. (Efe. 5:5, 6) Ni lazima sisi pia tutambue hatari inayotokana na maneno ya uwongo yanayosambazwa na waasi-imani, wanapojaribu kufanya tutilie shaka ndugu zetu na tengenezo la Yehova. (1 Tim. 4:1, 7; 2 Tim. 2:16) Habari kama hizo zinaweza kudhoofisha imani yetu. Ni lazima tuepuke kupotoshwa na propaganda hizo. Kwa nini? Kwa sababu habari kama hizo zinaenezwa na “watu waliopotoka kiakili na wasiojua kweli.” Lengo lao ni kuanzisha ‘mabishano na kushindana.’ (1 Tim. 6:4, 5) Wanataka tuamini uchongezi wao na tusitawishe shaka zenye uovu kuhusu ndugu zetu. w20.09 29 ¶13, 15

Alhamisi, Juni 9

[Tafuta], si faida [yako] mwenyewe, bali faida ya yule mtu mwingine.​—1 Kor. 10:24.

Mume na mke wanapaswa kupendana na kuheshimiana. (Efe. 5:33) Biblia inatufundisha tukazie fikira zaidi kutoa badala ya kupokea. (Mdo. 20:35) Ni sifa gani itakayowasaidia wenzi wa ndoa wapendane na kuheshimiana? Jibu ni unyenyekevu. Sifa ya unyenyekevu imewasaidia wenzi wengi Wakristo wawe na furaha nyingi zaidi katika ndoa zao. Kwa mfano, mume anayeitwa Steven anasema hivi: “Ikiwa ninyi ni kama timu, mtashirikiana pamoja, hasa matatizo yanapotokea. Badala ya kujiuliza ‘mimi nitafaidikaje?’ utajiuliza ‘sisi tutafaidikaje?’” Stephanie, mke wake, anahisi vivyo hivyo. Anasema hivi: “Hakuna anayependa kuishi na mtu wanayezozana naye. Tunapokosa kuelewana, tunajitahidi kujua chanzo cha tatizo. Kisha tunasali, tunafanya utafiti, na kuzungumzia jinsi ya kulisuluhisha. Tunashambulia tatizo, hatushambuliani.” Waume na wake huwa na furaha zaidi wanapoepuka kujifikiria zaidi wao wenyewe kuliko ilivyo lazima. w20.07 3-4 ¶5-6

Ijumaa, Juni 10

Nilikuwa nikifanya maendeleo makubwa katika dini ya Kiyahudi kuliko watu wengi wa umri wangu.​—Gal. 1:14.

Usitegemee nguvu au uwezo wako mwenyewe unapomtumikia Yehova. Mtume Paulo alikuwa msomi—alikuwa amefundishwa na Gamalieli, mmoja wa viongozi wa Kiyahudi aliyeheshimika katika siku zake. (Mdo. 5:34; 22:3) Wakati fulani, Paulo alikuwa na ushawishi mkubwa katika jamii ya Kiyahudi. (Mdo. 26:4) Lakini Paulo hakujitegemea mwenyewe. Kwa hiari, Paulo aliacha mambo yaliyomfanya awe mashuhuri kulingana na viwango vya ulimwengu. (Flp. 3:8) Paulo alipitia hali nyingi ngumu kwa sababu ya kuwa mfuasi wa Kristo. Alichukiwa na watu wa taifa lake mwenyewe. (Mdo. 23:12-14) Na raia wenzake wa Roma walimpiga na kumfunga gerezani. (Mdo. 16:19-24, 37) Zaidi ya hayo, Paulo alisikitishwa sana na mapungufu yake. (Rom. 7:21-25) Lakini badala ya kuruhusu wapinzani wake au mapungufu yake yamdhoofishe, ‘alipendezwa na udhaifu.’ Kwa nini? Kwa sababu alipokuwa dhaifu ndipo alipoona nguvu za Mungu zikitenda kazi maishani mwake.​—2 Kor. 4:7; 12:10. w20.07 16 ¶7-8

Jumamosi, Juni 11

Yeyote anayeniamini . . . atafanya kazi kubwa kuliko hizi.​—Yoh. 14:12.

Leo, tunahitaji kukazia sana fikira kazi ya kuhubiri habari njema za Ufalme. Yesu alitabiri kwamba kazi hiyo ingefanywa kwa kiwango kikubwa zaidi na kuendelea kwa muda mrefu baada ya kifo chake. Baada ya kufufuliwa, Yesu alifanya muujiza na kuwasaidia baadhi ya wanafunzi wake kuvua samaki wengi. Alitumia fursa hiyo kukazia kwamba mgawo wao wa kuwa wavuvi wa watu ulikuwa muhimu kuliko kazi nyingine yoyote. (Yoh. 21:15-17) Muda mfupi kabla ya kwenda mbinguni, Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwamba kazi ya kutoa ushahidi ingeenea hadi nje ya mipaka ya Israeli. (Mdo. 1:6-8) Miaka mingi baadaye, Yesu alimpa mtume Yohana maono ili kumwonyesha mambo ambayo yangetukia katika “siku ya Bwana.” Katika maono hayo, Yohana aliona ni tukio hili lenye kustaajabisha: Chini ya mwongozo wa malaika, “habari njema ya milele” ilikuwa ikihubiriwa “kwa kila taifa na kabila na lugha na watu.” (Ufu. 1:10; 14:6) Ni wazi kuwa leo mapenzi ya Yehova ni kwamba anataka tushiriki katika kazi hii kubwa ya kutoa ushahidi mpaka itakapokamilika. w20.09 9 ¶5

Jumapili, Juni 12

Kwa imani, Abrahamu alipojaribiwa, ni kana kwamba alimtoa Isaka.​—Ebr. 11:17.

Maisha ya familia ya Abrahamu yalikuwa magumu. Sara, mke wake mpendwa, hakuweza kupata watoto. Kwa miaka mingi walihitaji kukabiliana na hali hiyo yenye kuumiza. Mwishowe, Sara akamchukua Hagari, mtumishi wake, na kumpa Abrahamu ili awazalie Abrahamu na Sara watoto. Lakini Hagari alipopata mimba ya Ishmaeli, alianza kumdharau Sara. Hali ilikuwa mbaya sana hivi kwamba Sara alimfukuza Hagari. (Mwa. 16:1-6) Hatimaye Sara alipata mimba na kumzalia Abrahamu mwana ambaye alimwita Isaka. Abrahamu aliwapenda wana wake wote wawili, Ishmaeli na Isaka. Lakini kwa sababu Ishmaeli alimtendea kwa njia mbaya Isaka, Abrahamu alilazimika kuwafukuza Ishmaeli na Hagari. (Mwa. 21:9-14) Baadaye, Yehova alimwomba Abrahamu amtoe Isaka kuwa dhabihu. (Mwa. 22:1, 2; Ebr. 11:17-19) Katika pindi hizo zote, Abrahamu alihitaji kuwa na uhakika kwamba mwishowe Yehova angetimiza ahadi yake kuhusu wana wake. w20.08 4 ¶9-10

Jumatatu, Juni 13

[Vaa] utu mpya ulioumbwa kupatana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.​—Efe. 4:24.

Wazia shangwe ambayo wale watakaofufuliwa watahisi watakapouvua utu wao wa zamani na kuishi kulingana na viwango vya uadilifu vya Mungu. Wale wanaofanya mabadiliko hayo watapata ufufuo wa uzima. Kwa upande mwingine, wale watakaomwasi Mungu hawataruhusiwa kuvuruga amani ya Paradiso. (Isa. 65:20; Yoh. 5:28, 29) Chini ya utawala wa Ufalme, watu wote wa Mungu watajionea ukweli wa maneno ya Methali 10:22 inayosema: “Baraka ya Yehova ndiyo inayomtajirisha mtu, naye haichanganyi na maumivu.” Kwa msaada wa roho ya Yehova, watu wa Mungu watakuwa matajiri kiroho, yaani, watazidi kuwa kama Kristo, na hatua kwa hatua watafikia ukamilifu. (Yoh. 13:15-17; Efe. 4:23) Kila siku miili yao itazidi kuwa na nguvu zaidi na watazidi kuwa watu bora. Maisha hayo yatakuwa yenye shangwe sana!—Ayu. 33:25. w20.08 17 ¶11-12

Jumanne, Juni 14

Muwe na lengo la . . . kushughulika na mambo yenu wenyewe.​—1 The. 4:11.

Ni vema kukumbuka kwamba baadhi ya Wakristo waseja wamefanya uamuzi wa kibinafsi wa kuendelea kubaki wakiwa waseja. Wakristo wengine waseja wangependa kufunga ndoa, lakini ni kwa sababu tu hawajafanikiwa kumpata mtu anayewafaa. Ilhali wengine huenda wamepoteza wenzi wao katika kifo. Vyovyote vile, je, ingefaa kwa wale walio katika kutaniko kuwauliza Wakristo waseja kwa nini hawajafunga ndoa, au kujitolea kuwasaidia wapate mwenzi? Ikiwa hawajaomba msaada huo, ndugu au dada yetu mseja atahisije utakapompendekezea kwamba unataka kumsaidia apate mwenzi? (1 Tim. 5:13) Ndugu na dada zetu waseja watafurahi sana ikiwa tutapima thamani yao kwa msingi wa sifa zao nzuri na si kwa sababu wameoa au kuolewa au la. Badala ya kuwasikitikia, ni vema tukawathamini kwa sababu ya uaminifu wao. Matokeo ni kwamba ndugu na dada zetu waseja hawatahisi kamwe kuwa ni kana kwamba tunawaambia: ‘Hatuwahitaji ninyi.’ (1 Kor. 12:21) Badala yake, watajua kwamba tunawaheshimu na kuthamini sehemu yao katika kutaniko. w20.08 29 ¶10, 14

Jumatano, Juni 15

[Kristo] aliwatokea ndugu zaidi ya 500 kwa wakati mmoja.​—1 Kor. 15:6.

Baadaye, Yesu alimtokea mtume Paulo mwenyewe. (1 Kor. 15:8) Paulo (Sauli) alikuwa njiani kuelekea Damasko aliposikia sauti ya Yesu aliyefufuliwa na kumwona Yesu katika utukufu wake wa mbinguni. (Mdo. 9:3-5) Jambo ambalo Paulo alijionea liliongeza uthibitisho kwamba ufufuo wa Yesu haukuwa hadithi tu. (Mdo. 26:12-15) Ushahidi wa Paulo ungewavutia sana baadhi ya watu kwa sababu pindi fulani aliwatesa Wakristo. Mara tu aliposadiki kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa, Paulo alifanya kazi kwa bidii ili kuwasadikisha wengine kuhusu ukweli huo. Alivumilia kupigwa, kufungwa gerezani, na kuvunjikiwa na meli alipokuwa akihubiri ukweli kwamba Yesu alikufa lakini alikuwa hai tena. (1 Kor. 15:9-11; 2 Kor. 11:23-27) Paulo alikuwa na uhakika kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa kutoka kwa wafu hivi kwamba alikuwa tayari kufa ili kuitetea imani yake. Je, ushahidi huo kutoka kwa Wakristo wa mapema haukusadikishi kwamba Yesu alifufuliwa kutoka kwa wafu? Na je, hauimarishi imani yako katika ufufuo? w20.12 3 ¶8-10

Alhamisi, Juni 16

Mkimtafuta [Yehova], atawaruhusu mumpate.​—2 Nya. 15:2.

Tunaweza kujiuliza hivi: Je, ninahudhuria kwa ukawaida mikutano ya kutaniko? Tunapohudhuria mikutano inayoandaliwa na tengenezo la Yehova, tunapata burudisho la kweli la kiroho pamoja na ushirika unaojenga. (Mt. 11:28) Pia, tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, ninajifunza Biblia kwa ukawaida? ‘Ikiwa una familia, je, umetenga wakati wa kufanya ibada ya familia kila juma? Au ikiwa unaishi peke yako, je, unatenga wakati wa kujifunza kibinafsi kama tu ambavyo ungefanya ikiwa ungekuwa unaishi na familia? Pia, je, unashiriki kikamili kadiri iwezekanavyo katika kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi? Kwa nini tujiulize maswali hayo? Biblia inatuambia kwamba Yehova anachunguza mawazo na mambo yaliyo moyoni mwetu, sisi pia tunapaswa kufanya vivyohivyo. (2 Nya. 28:9) Ikiwa tunatambua kwamba tunahitaji kufanya mabadiliko fulani katika malengo yetu, mtazamo, au njia yetu ya kufikiri, tunapaswa kumwomba Yehova atusaidie kufanya mabadiliko hayo. Sasa ndiyo wakati wa kujitayarisha kwa ajili ya majaribu yaliyo mbele yetu. w20.09 19 ¶19-20

Ijumaa, Juni 17

Yeyote kati yenu asipoaga mali zake zote hawezi kuwa mwanafunzi wangu.​—Luka 14:33.

Yesu alitoa mfano ili kuonyesha gharama zinazohusika mtu anapotaka kuwa mwanafunzi wake. Alizungumza kuhusu mtu anayetaka kujenga mnara na kuhusu mfalme anayetaka kwenda kupigana vita. Yesu alisema kwamba yule anayetaka kujenga lazima ‘aketi kwanza na kuhesabu gharama’ ili akamilishe mnara huo na kwamba ni lazima mfalme ‘aketi kwanza na kufikiri’ ili kuona ikiwa wanajeshi wake wanaweza kutimiza kile wanachokusudia kufanya. (Luka 14:27-32) Vivyo hivyo, Yesu alijua kwamba mtu aliyetaka kuwa mwanafunzi wake, alipaswa kuchanganua kwa uangalifu sana kile kinachomaanishwa na kuwa mfuasi wake. Kwa sababu hiyo, tunahitaji kuwatia moyo wanafunzi wetu wa Biblia wajifunze nasi kila juma. Ukiwa mwalimu unahitaji kujitayarisha vizuri kwa ajili ya kila kipindi cha funzo. Huku ukimfikiria mwanafunzi wako, tafakari mapema jinsi utakavyofafanua habari hiyo kwa njia rahisi na iliyo wazi ili mwanafunzi wako aweze kuielewa na kuitumia kwa urahisi.​—Neh. 8:8; Met. 15:28a. w20.10 7 ¶5; 8 ¶7

Jumamosi, Juni 18

Basi, nendeni mkafanye wanafunzi . . . , na kuwafundisha kushika mambo yote niliyowaamuru.​—Mt. 28:19, 20.

Maagizo ya Yesu yako wazi. Ni lazima tuwafundishe watu mambo ambayo aliamuru. Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka jambo fulani muhimu. Yesu hakusema: ‘Wafundishe mambo yote niliyowaamuru.’ Badala yake, alisema: “Wafundishe kushika mambo yote niliyowaamuru.” Ili tufuate mwongozo huo hususa tunapomfundisha mwanafunzi wetu wa Biblia, hatutamfundisha tu, bali pia tutamwongoza. (Mdo. 8:31) “Kushika” amri fulani kunamaanisha kuitii. Tunapojifunza Biblia na wengine, tunawafundisha mambo ambayo Mungu anataka tufanye. Hata hivyo, ni lazima tufanye mengi zaidi. Ni lazima tuwafundishe wanafunzi wetu wa Biblia kutumia maishani mwao mambo wanayojifunza. (Yoh. 14:15; 1 Yoh. 2:3) Kupitia mfano wetu, tunaweza kuwaonyesha wanafunzi wetu jinsi ya kutumia kweli wanazojifunza katika Biblia wanapokuwa shuleni, kazini, au wakati wa tafrija. Tunapokuwa na wanafunzi wetu, tunaweza kusali kwa Yehova na kumwomba awaongoze kwa roho yake takatifu.​—Yoh. 16:13. w20.11 2-3 ¶3-5

Jumapili, Juni 19

“Si kwa jeshi, wala si kwa nguvu, bali kwa roho yangu,” asema Yehova wa majeshi.​—Zek. 4:6.

Wanafunzi wa Yesu walikabili changamoto. Kwa mfano, kulikuwa na nakala chache za Maandiko. Hawakuwa na machapisho ya kujifunzia kama tuliyo nayo leo. Na walihitaji kuwahubiria watu waliozungumza lugha nyingi tofauti. Licha ya changamoto hizo zote, wanafunzi hao wenye bidii walifanya jambo ambalo lilionekana kana kwamba haliwezekani—katika kipindi cha miaka thelathini hivi, walikuwa wamehubiri habari njema “katika uumbaji wote chini ya mbingu.” (Kol. 1:6, 23) Katika siku zetu, Yehova anaendelea kuwaongoza na kuwaimarisha watu wake. Bila shaka, kwa sehemu kubwa mwongozo unakuja kupitia Neno la Mungu lilioongozwa na roho. Katika Biblia tunasoma kuhusu huduma ya Yesu na amri yake kwamba wafuasi wake waendelee kufanya kazi aliyoianzisha. (Mt. 28:19, 20) Yehova hana ubaguzi; alitabiri kwamba habari njema zingehubiriwa “kwa kila taifa na kabila na lugha na watu.” (Ufu. 14:6, 7) Anataka ujumbe wa Ufalme uwafikie watu wote. w20.10 21 ¶6-8

Jumatatu, Juni 20

Kwa maana wewe huwaokoa walio wanyenyekevu, lakini macho yako hayapendezwi na wenye kiburi.​—2 Sam. 22:28.

Mfalme Daudi, alikuwa mwanamume aliyependezwa na “sheria ya Yehova.” (Zab. 1:1-3) Daudi alijua kwamba Yehova huwaokoa walio wanyenyekevu lakini huwapinga wenye kiburi. Hivyo, Daudi aliruhusu sheria ya Mungu irekebishe njia yake ya kufikiri. Aliandika hivi: “Nitamsifu Yehova, ambaye amenipa ushauri. Hata wakati wa usiku, mawazo yangu ya ndani kabisa hunirekebisha.” (Zab. 16:7) Ikiwa sisi ni wanyenyekevu tutaruhusu Neno la Mungu lirekebishe mawazo yetu mabaya kabla hayajatuongoza kufanya mambo mabaya. Neno la Mungu litakuwa kama sauti inayotuambia: “Hii ndiyo njia. Tembeeni ndani yake.” Itatuonya tutakapokuwa tumetoka kwenye njia, iwe tumeenda kushoto au kulia. (Isa. 30:21) Tukimsikiliza Yehova tutajinufaisha kwa njia mbalimbali. (Isa. 48:17) Kwa mfano, tutaepuka aibu ya kusahihishwa na mtu mwingine. Na tutamkaribia zaidi Yehova kwa sababu tunatambua kwamba anatutendea kama watoto wapendwa.​—Ebr. 12:7. w20.11 20 ¶6-7

Jumanne, Juni 21

Sasa waliposikia kuhusu ufufuo wa wafu, baadhi yao wakaanza kumdhihaki.​—Mdo. 17:32.

Mawazo kama hayo huenda yaliwaathiri baadhi ya watu huko Korintho. (1 Kor. 15:12) Pia, huenda wengine walifikiri ufufuo haukuwa halisi, kwamba kwa njia ya mfano ulimaanisha awali mtu alikuwa ‘mfu’ katika dhambi, lakini sasa amekuwa “hai” akiwa Mkristo. Haidhuru sababu yao, kukataa fundisho la ufufuo kulimaanisha imani yao ilikuwa ya bure. Ikiwa Mungu hakumfufua Yesu, fidia haikulipwa na watu wote walibaki katika dhambi. Hivyo, wale waliokataa fundisho la ufufuo hawakuwa na tumaini la kweli. (1 Kor. 15:13-19; Ebr. 9:12, 14) Mtume Paulo alikuwa amejithibitishia kibinafsi kwamba ‘Kristo alikuwa amefufuliwa kutoka kwa wafu.’ Ufufuo huo ulikuwa bora kuliko ule uliokuwa umefanywa awali, kwa sababu wale waliofufuliwa walikuja kufa tena. Paulo alisema kwamba Yesu alikuwa “matunda ya kwanza ya wale ambao wamelala usingizi katika kifo.” Alikuwa mtu wa kwanza kufufuliwa akiwa kiumbe wa roho, na wa kwanza kati ya wanadamu kwenda mbinguni.​—1 Kor. 15:20; Mdo. 26:23; 1 Pet. 3:18, 22. w20.12 5 ¶11-12

Jumatano, Juni 22

Walikuwa wakiwapa maagizo yaliyokuwa yameamuliwa na mitume na wazee.​—Mdo. 16:4.

Katika karne ya kwanza, baraza linaloongoza huko Yerusalemu lilifanya kazi kwa umoja ili kudumisha utaratibu na amani miongoni mwa watu wa Mungu. (Mdo. 2:42) Kwa mfano, suala la tohara lilipojitokeza mwaka wa 49 W.K. hivi, Baraza linaloongoza chini ya mwongozo wa roho takatifu lilizungumzia jambo hilo. Ikiwa kutaniko lingeendelea kuwa na mgawanyiko kuhusu jambo hilo, kazi ya kuhubiri ingeathirika. Ingawa walikuwa Wayahudi, mitume na wanaume wazee hawakuathiriwa na utamaduni wa Kiyahudi wala na wale waliokuwa wakiushikilia sana utamaduni huo. Badala yake, walichunguza Neno la Mungu na kutafuta mwongozo wa roho takatifu. (Mdo. 15:1, 2, 5-20, 28) Matokeo yakawaje? Yehova alibariki uamuzi wao, amani na umoja vikatawala, na kazi ya kuhubiri ikasonga mbele. (Mdo 15:30, 31; 16:5) Katika siku zetu, tengenezo la Yehova limewasaidia watu wake kudumisha utaratibu na amani miongoni mwao. w20.10 22-23 ¶11-12

Alhamisi, Juni 23

Mwanangu Sulemani [ndiye] ambaye Mungu amemchagua.​—1 Nya. 29:1.

Kwa sababu ya umri, afya, au hali nyingine, huenda tusiweze kupata mgawo au pendeleo fulani la kitheokrasi. Ikiwa tunapitia hali kama hiyo, tunaweza kujifunza kutokana na mfano wa Mfalme Daudi. Alipoambiwa kwamba hakuwa amechaguliwa kujenga hekalu la Mungu—jambo ambalo Daudi alitamani sana kufanya—alimuunga mkono kabisa yule ambaye Mungu alimchagua kutimiza mgawo huo. Daudi hata alichangia kwa ukarimu ili kufanikisha mradi huo. Huo ni mfano mzuri sana wa kuiga! (2 Sam. 7:12, 13; 1 Nya. 29:3-5) Kwa sababu ya matatizo ya afya, Hugues, ndugu kutoka nchini Ufaransa, aliacha kutumikia akiwa mzee wa kutaniko, na hangeweza kufanya hata kazi ndogo-ndogo za nyumbani. Anaandika hivi: “Mwanzoni nilijiona sifai na nilivunjika moyo sana. Lakini baada ya muda, niliona umuhimu wa kuikubali hali yangu, na nikaanza kupata shangwe kwa kumtumikia Yehova kulingana na hali yangu ya sasa. Kama Gideoni na wale wanaume mia tatu waliokuwa pamoja naye—ambao walikuwa wamechoka—nitaendelea kupambana!”—Amu. 8:4. w20.12 25 ¶14-15

Ijumaa, Juni 24

[Endeleeni] kupendana.​—1 Yoh. 4:7.

Katika simulizi lake kuhusu maisha ya Yesu, mtume Yohana anatumia maneno ya Kigiriki yanayotafsiriwa kuwa “upendo” na ‘-penda’ mara nyingi zaidi kuliko wale waandishi wengine watatu wa Injili kwa ujumla. Vitabu vyake vilivyoongozwa na roho ya Mungu vinafunua kwamba mambo yote ambayo Mkristo anafanya ni lazima yachochewe na upendo. (1 Yoh. 4:10, 11) Hata hivyo, ilichukua muda kwa Yohana kujifunza somo hilo. Yohana alipokuwa kijana, hakuonyesha upendo nyakati zote. Kwa mfano, pindi moja Yesu na wanafunzi wake walikuwa wakisafiri kwenda Yerusalemu kupitia Samaria. Watu wa kijiji fulani cha Samaria walikataa kuwaonyesha ukarimu. Yohana aliomba kuagiza moto ushuke kutoka mbinguni na kuwaangamiza wakazi wote wa kijiji hicho! (Luka 9:52-56) Pindi nyingine, Yohana na Yakobo, ndugu yake, walimwomba mama yao azungumze na Yesu ili awape nafasi za pekee kando yake katika Ufalme. Mitume wengine walipojua jambo ambalo Yakobo na Yohana walikuwa wamefanya, walikasirika sana! (Mt. 20:20, 21, 24) Hata hivyo, Yesu alimpenda Yohana licha ya mapungufu hayo yote.​—Yoh. 21:7. w21.01 8-9 ¶3-4

Jumamosi, Juni 25

Kristo hakujipendeza mwenyewe.​—Rom. 15:3.

Yehova anafanya maamuzi yanayowanufaisha wengine. Kwa mfano, aliamua kutokeza uhai, si kwa faida yake, bali alitaka kushiriki pamoja nasi shangwe ya kuishi. Hakuna ambaye angeweza kumlazimisha Yehova amtoe Mwana wake ili kufunika dhambi zetu. Kwa hiari, aliamua kutoa dhabihu hiyo kwa faida yetu. Yesu pia alifanya maamuzi ambayo lengo kuu lilikuwa ni kuwanufaisha wengine. Kwa mfano, aliamua kuahirisha kupumzika ili afundishe umati wa watu. (Marko 6:31-34) Kichwa kizuri cha familia anajua kwamba mojawapo ya mambo magumu zaidi ambayo ni lazima afanye, ni kufanya maamuzi ya hekima kwa ajili ya familia yake, na anachukua wajibu huo kwa uzito. Anajitahidi kuepuka kufanya maamuzi yasiyo na msingi mzuri au yanayotegemea tu hisia. Badala yake, anamruhusu Yehova amzoeze. (Met. 2:6, 7) Kwa njia hiyo, atafikiria kuwanufaisha wengine, na si kujinufaisha mwenyewe. (Flp. 2:4) Ikiwa mume anajitahidi kufuata kielelezo kilichowekwa na Yehova na Yesu, atakuwa kichwa kizuri cha familia. w21.02 7 ¶19-21

Jumapili, Juni 26

Asa alitenda yaliyokuwa mema na sawa machoni pa Yehova Mungu wake.​—2  Nya. 14:2.

Alipokuwa kijana, Mfalme Asa alikuwa mnyenyekevu na jasiri. Kwa mfano, aliporithi ufalme kutoka kwa Abiya, baba yake, alianzisha kampeni dhidi ya ibada ya sanamu. Pia, “aliwaambia watu wa Yuda wamtafute Yehova Mungu wa mababu zao na kushika Sheria na amri.” (2 Nya. 14:1-7) Na Zera Mwethiopia alipovamia Yuda akiwa na wanajeshi 1,000,000, kwa hekima Asa alimgeukia Yehova ili kuomba msaada, akisema: “Ee Yehova, haijalishi kwako ikiwa wale unaowasaidia ni wengi au hawana nguvu. Tusaidie, Ee Yehova Mungu wetu, kwa maana tunakutegemea wewe.” Maneno hayo mazuri sana yanaonyesha jinsi ambavyo Asa alikuwa na uhakika katika uwezo wa Yehova wa kumwokoa yeye na watu wake. Asa alimtumaini Baba yake wa mbinguni, na “Yehova akawashinda Waethiopia.” (2 Nya. 14:8-12) Bila shaka, utakubali kwamba kukabili jeshi lenye askari 1,000,000 ilikuwa changamoto kubwa—changamoto ambayo Asa alifanikiwa kuishinda. w21.03 5 ¶12-13

Jumatatu, Juni 27

Iweni na upendo mwororo kwa mtu na mwenzake.​—Rom. 12:10.

Biblia ina masimulizi ya watu wasio wakamilifu ambao walionyesha upendo mwororo. Fikiria mfano wa Yonathani na Daudi. Biblia inasema hivi: “Yonathani na Daudi wakashikamana na kuwa marafiki wa karibu sana, na Yonathani akaanza kumpenda kama alivyojipenda mwenyewe.” (1 Sam. 18:1) Daudi alikuwa ametiwa mafuta ili amrithi Mfalme Sauli. Baada ya hapo, Sauli alianza kumwonea wivu Daudi, na alijaribu kumuua. Lakini Yonathani, mwana wa Sauli, hakujiunga na baba yake alipokuwa akijaribu kumuua Daudi. Yonathani na Daudi waliweka ahadi kwamba wataendelea kuwa marafiki sikuzote na kutegemezana. (1 Sam. 20:42) Upendo mwororo uliokuwa kati ya Yonathani na Daudi ni wenye kustaajabisha hata zaidi tunapofikiria baadhi ya mambo ambayo yangeweza kuwazuia kuwa marafiki. Kwa mfano, Yonathani alimzidi umri Daudi kwa miaka 30 hivi. Yonathani angeweza kufikiri kwamba hawezi kuwa na urafiki wa karibu na mtu mwenye umri mdogo sana na asiye na uzoefu maishani. Hata hivyo, Yonathani hakumwona au kumtendea Daudi kama mtu aliye duni machoni pake. w21.01 21-22 ¶6-7

Jumanne, Juni 28

Oneni yote kuwa shangwe, ndugu zangu, mnapopata majaribu mbalimbali.​—Yak. 1:2.

Yesu aliwaahidi wafuasi wake kwamba wangekuwa na furaha ya kweli. Pia, aliwaonya wale wanaompenda kwamba wangekabili majaribu. (Mt. 10:22, 23; Luka 6:20-23) Tunapata shangwe kwa kuwa wanafunzi wa Kristo. Lakini tunahisije kuhusu uwezekano wa kwamba tutapingwa na washiriki wa familia yetu, tutateswa na serikali, au kushinikizwa kufanya mambo mabaya na wafanyakazi au wanafunzi wenzetu? Inaeleweka kwamba tunapofikiria kuhusu mambo hayo tunaweza kupatwa na mahangaiko. Kwa kawaida, watu hawayaoni mateso kuwa sababu ya kuwa na shangwe. Lakini hivyo ndivyo Neno la Mungu linavyotuambia. Kwa mfano, mwanafunzi Yakobo aliandika kwamba badala ya kulemewa, tunapaswa kuona yote kuwa shangwe tunapopata majaribu. (Yak. 1:2, 12) Na Yesu alisema kwamba tunapaswa kuwa na furaha hata tunapoteswa. (Mt. 5:11) Yehova alimwongoza Yakobo awaandikie Wakristo ili kuwapa ushauri unaofaa, ambao ungewasaidia waendelee kuwa na shangwe hata walipokabili majaribu. w21.02 26 ¶1-2; 27 ¶5

Jumatano, Juni 29

Jiepushe na maneno matupu yanayochafua mambo matakatifu.​—1 Tim. 6:20.

Baadhi ya Wakristo walioishi kipindi kimoja na Timotheo hawakuthamini pendeleo lao la kuwa wafanyakazi wenzi pamoja na Mungu. Walitia ndani Dema, Figelo, Hermogene, Himenayo, Aleksanda, na Fileto. (1 Tim. 1:19, 20; 2 Tim. 1:15; 2:16-18; 4:10) Mwanzoni, watu hao wote walikuwa imara kiroho, lakini waliacha kuyaona mambo waliyokabidhiwa kuwa yenye thamani. Shetani anajaribu jinsi gani kutufanya tuache kuthamini hazina ambazo Yehova ametukabidhi? Fikiria baadhi ya mbinu za Shetani. Anatumia burudani na vyombo vya habari kuendeleza viwango, njia ya kufikiri, na tabia ambazo anaamini kwamba zinaweza kutufanya tulegeze msimamo wetu inapohusu kweli za Biblia. Anajaribu kututisha kupitia watu wanaotushinikiza au kututesa ili tuache kuhubiri. Anajaribu kutushawishi tusikilize “‘ujuzi’ wa uwongo” wa waasi-imani ili tuiache kweli. Tusipokuwa waangalifu, hatua kwa hatua tunaweza kuiacha kweli.​—1 Tim. 6:21. w20.09 27 ¶6-8

Alhamisi, Juni 30

Yehova atasikia ombi langu la kutaka kibali; Yehova ataikubali sala yangu.​—Zab. 6:9.

Je, rafiki au mtu wa familia amekuumiza au kukusaliti? Ikiwa ndivyo, utanufaika kwa kuchunguza simulizi la Absalomu, mwana wa Mfalme Daudi. (2 Sam. 15:5-14, 31; 18:6-14) Ukiwa na simulizi hilo akilini, mweleze Yehova jinsi unavyohisi baada ya kutendewa kwa njia mbaya. (Zab. 6:6-8) Kisha, wazia jinsi Daudi alivyohisi mambo hayo yote yalipokuwa yakitokea. Alimpenda Absalomu na alimtumaini Ahithofeli. Hata hivyo, Absalomu na Ahithofeli, waliokuwa watu wake wa karibu walimsaliti. Walimhuzunisha sana na hata walijaribu kumuua. Daudi angeweza kuacha kuwaamini rafiki zake wengine, akifikiri kwamba wao pia wamejiunga na Absalomu. Angeweza kujifikiria mwenyewe tu na kutaka kuondoka nchini akiwa peke yake. Au labda angevunjika moyo na kukata tamaa. Badala yake, alisali kwa Yehova ili kupata msaada. Pia, aliwaomba rafiki zake wamsaidie. Na alitenda haraka kulingana na maamuzi aliyofanya. Aliendelea kumtumaini Yehova na kuwatumaini rafiki zake. w21.03 15 ¶7-8; 17 ¶10-11

    Maktaba Kwenye Mtandao (1950-2022)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2022 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki