Maana ya Mithali
Kwa Nini Kuomba Sana Mabusu ya Mchukiaji?
MWANAMUME mwenye hekima aliyevuviwa kimungu alionelea hivi: “Majeraha yatiwayo na mpendwa ni ya uaminifu, lakini mabusu ya mchukiaji ni mambo yapasayo kuombwa sana.” (Mithali 27:6, NW) Maneno hayo yapasa kuelewekaje?
Mtu akupendaye atatia jeraha la kitamathali juu yako kwa njia ya uaminifu. Huenda akakushauri kwa upendo katika moyo wake na kwa matumaini ya kukufanyia wema. Si lazima wewe umwombe sana rafiki wa kweli msaada wa jinsi hiyo wala hata karipio wakati ulihitajipo. Nawe ni mwenye hekima kama nini ukikubali kwa neema shauri lihitajiwalo, uchambuzi wenye kujenga, au karipio ambalo lahitajiwa kabisa!
Hata hivyo, ikiwa wewe wataka mtu fulani akuchukiaye akutendee jambo lenye fadhili, ni lazima umwombe sana. Kwa nini? Kwa sababu ni jambo la kiasili kwamba chuki yake haingempa mbetuko wa kukupiga wewe mabusu. Bali, angekuwa na mbetuko wa kukutenda kwa njia ya ukatili. Fadhili yoyote iwezekanayo akuonyeshe wewe ingepatikana kutoka kwake kwa shida sana na kwa wewe kumwomba sana tu.
Wa kupendeza katika habari hii ni mmoja wa mifano ya Yesu Kristo. Wakati mmoja yeye alisema juu ya mjane aliyepata haki kutoka kwa hakimu asiyekuwa na hofu ya Mungu wala staha kwa binadamu. Mjane huyo alifauluje? Hakimu alihakikisha kwamba mwanamke huyo alipata kitulizo alichostahili kwa sababu tu mwanamke aliendelea kumwomba sana. Yesu alitumia kielezi hicho kukazia wanafunzi wake uhitaji wa ‘kuomba sikuzote, wala wasikate tamaa.’—Luka 18:1-8.
Ni Jinsi Gani Waadilifu Huwa Wengi
Waovu Watowekapo?
Mithali 28:28, NW, yataarifu hivi: “Waovu wainukapo, mtu hujificha; lakini watowekapo, waadilifu huwa wengi.” Hiyo huthibitikaje kuwa kweli?
Huenda waovu ‘wakainuka’ katika mamlaka, labda wakiwa watawala wakatili. Wakati kama huo, mtu mwadilifu hujificha. Huenda akafanya hivyo kwa sababu ya kuwa na hofu juu ya uonevu wao. Na mbona isiwe hivyo? Ni kweli kwamba “mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.”—Mhubiri 8:9.
Hata hivyo, waovu waangamiapo, watu waadilifu “huwa wengi.” Jinsi gani? Kwa wazi katika jambo la kwamba wakati huo waadilifu hutoka mafichoni na kuonekana peupe. Hivyo wao husitawi na kuonekana ni kama wameongezeka hesabu kwa sababu hawana tena uhitaji wa kujificha. Ikitukia kwamba wanyoofu watawale wakati huo, wao wangeadhibu watenda makosa na kuendeleza mwenendo wa uadilifu. Hilo pia lingeweza kuwa na tokeo la kupunguza hesabu ya watu wasio waadilifu na kuwazidisha waadilifu.—Linganisha Mithali 28:12; 29:2.
Karibuni wale walio wanyoofu wataona waovu wakitoweka duniani katika “siku ya kasirani ya Yehova” inayokaribia kasi. Kwa hiyo, tafuta uadilifu na usikivu kulingana na viwango vya kimungu, na huenda wewe ukahifadhiwa uingie katika ulimwengu mpya wa Mungu, ambamo kwa kweli waadilifu watakuwa wengi.—Sefania 2:2, 3; 2 Petro 3:11-13, NW.