Jumatatu, Juni 27
Iweni na upendo mwororo kwa mtu na mwenzake.—Rom. 12:10.
Biblia ina masimulizi ya watu wasio wakamilifu ambao walionyesha upendo mwororo. Fikiria mfano wa Yonathani na Daudi. Biblia inasema hivi: “Yonathani na Daudi wakashikamana na kuwa marafiki wa karibu sana, na Yonathani akaanza kumpenda kama alivyojipenda mwenyewe.” (1 Sam. 18:1) Daudi alikuwa ametiwa mafuta ili amrithi Mfalme Sauli. Baada ya hapo, Sauli alianza kumwonea wivu Daudi, na alijaribu kumuua. Lakini Yonathani, mwana wa Sauli, hakujiunga na baba yake alipokuwa akijaribu kumuua Daudi. Yonathani na Daudi waliweka ahadi kwamba wataendelea kuwa marafiki sikuzote na kutegemezana. (1 Sam. 20:42) Upendo mwororo uliokuwa kati ya Yonathani na Daudi ni wenye kustaajabisha hata zaidi tunapofikiria baadhi ya mambo ambayo yangeweza kuwazuia kuwa marafiki. Kwa mfano, Yonathani alimzidi umri Daudi kwa miaka 30 hivi. Yonathani angeweza kufikiri kwamba hawezi kuwa na urafiki wa karibu na mtu mwenye umri mdogo sana na asiye na uzoefu maishani. Hata hivyo, Yonathani hakumwona au kumtendea Daudi kama mtu aliye duni machoni pake. w21.01 21-22 ¶6-7
Jumanne, Juni 28
Oneni yote kuwa shangwe, ndugu zangu, mnapopata majaribu mbalimbali.—Yak. 1:2.
Yesu aliwaahidi wafuasi wake kwamba wangekuwa na furaha ya kweli. Pia, aliwaonya wale wanaompenda kwamba wangekabili majaribu. (Mt. 10:22, 23; Luka 6:20-23) Tunapata shangwe kwa kuwa wanafunzi wa Kristo. Lakini tunahisije kuhusu uwezekano wa kwamba tutapingwa na washiriki wa familia yetu, tutateswa na serikali, au kushinikizwa kufanya mambo mabaya na wafanyakazi au wanafunzi wenzetu? Inaeleweka kwamba tunapofikiria kuhusu mambo hayo tunaweza kupatwa na mahangaiko. Kwa kawaida, watu hawayaoni mateso kuwa sababu ya kuwa na shangwe. Lakini hivyo ndivyo Neno la Mungu linavyotuambia. Kwa mfano, mwanafunzi Yakobo aliandika kwamba badala ya kulemewa, tunapaswa kuona yote kuwa shangwe tunapopata majaribu. (Yak. 1:2, 12) Na Yesu alisema kwamba tunapaswa kuwa na furaha hata tunapoteswa. (Mt. 5:11) Yehova alimwongoza Yakobo awaandikie Wakristo ili kuwapa ushauri unaofaa, ambao ungewasaidia waendelee kuwa na shangwe hata walipokabili majaribu. w21.02 26 ¶1-2; 27 ¶5
Jumatano, Juni 29
Jiepushe na maneno matupu yanayochafua mambo matakatifu.—1 Tim. 6:20.
Baadhi ya Wakristo walioishi kipindi kimoja na Timotheo hawakuthamini pendeleo lao la kuwa wafanyakazi wenzi pamoja na Mungu. Walitia ndani Dema, Figelo, Hermogene, Himenayo, Aleksanda, na Fileto. (1 Tim. 1:19, 20; 2 Tim. 1:15; 2:16-18; 4:10) Mwanzoni, watu hao wote walikuwa imara kiroho, lakini waliacha kuyaona mambo waliyokabidhiwa kuwa yenye thamani. Shetani anajaribu jinsi gani kutufanya tuache kuthamini hazina ambazo Yehova ametukabidhi? Fikiria baadhi ya mbinu za Shetani. Anatumia burudani na vyombo vya habari kuendeleza viwango, njia ya kufikiri, na tabia ambazo anaamini kwamba zinaweza kutufanya tulegeze msimamo wetu inapohusu kweli za Biblia. Anajaribu kututisha kupitia watu wanaotushinikiza au kututesa ili tuache kuhubiri. Anajaribu kutushawishi tusikilize “‘ujuzi’ wa uwongo” wa waasi-imani ili tuiache kweli. Tusipokuwa waangalifu, hatua kwa hatua tunaweza kuiacha kweli.—1 Tim. 6:21. w20.09 27 ¶6-8