Jumatano, Machi 27
[Tafuta] kwanza Ufalme.—Mt. 6:33.
Wanafunzi walihuzunika sana Yesu alipokufa. Hawakuwa tu wamempoteza rafiki yao mpendwa, bali pia walihisi kana kwamba wamepoteza tumaini. (Luka 24:17-21) Hata hivyo, Yesu alipowatokea, alitumia muda ili kuwasaidia waelewe jukumu lake katika kutimizwa kwa unabii wa Biblia. Pia, aliwapatia kazi muhimu. (Luka 24:26, 27, 45-48) Kufikia wakati ambapo Yesu alirudi mbinguni, huzuni ya wanafunzi ilikuwa imegeuka na kuwa shangwe kubwa. Kujua kwamba Bwana wao alikuwa hai na tayari kuwasaidia watimize jukumu lao jipya, kuliwaletea furaha. Shangwe yao iliwachochea kumsifu Yehova bila kuacha. (Luka 24:52, 53; Mdo. 5:42) Ili kuwaiga wanafunzi wa Yesu tunahitaji kutanguliza Ufalme wa Mungu maishani mwetu. Ingawa tunahitaji uvumilivu ili tuendelee kumtumikia Yehova, anaahidi kwamba atatubariki sana ikiwa tutafanya hivyo.—Met. 10:22. w23.01 30-31 ¶15-16
Usomaji wa Biblia wa Ukumbusho: (Matukio ya mchana: Nisani 16) Marko 16:2-8
Alhamisi, Machi 28
Nawe utarudi mavumbini.—Mwa. 3:19.
Bila shaka, hatungependa kufanya kosa ambalo Adamu na Hawa walifanya. Tunaweza kuepuka matokeo hayo mabaya ikiwa tutaendelea kujifunza kumhusu Yehova, kuthamini sifa zake, na kujitahidi kuelewa njia yake ya kufikiri. Tunapofanya hivyo, bila shaka tutaimarisha upendo wetu kwa Yehova. Mfikirie Abrahamu. Alimpenda sana Yehova. Hata ilipokuwa vigumu kwake kuelewa maamuzi ambayo Yehova alifanya, Abrahamu hakuasi. Badala yake, alijitahidi kumjua Yehova vizuri zaidi. Kwa mfano, aliposikia kuhusu uamuzi wa Yehova wa kuangamiza Sodoma na Gomora, mwanzoni Abrahamu aliogopa kwamba “Mwamuzi wa dunia yote” angefagilia mbali waadilifu pamoja na waovu. Abrahamu aliona hilo kuwa jambo lisilowezekana, basi kwa unyenyekevu alimuuliza Yehova maswali kadhaa. Yehova alimjibu kwa subira. Mwishowe, Abrahamu alitambua kwamba Yehova anachunguza moyo wa kila mwanadamu na kwamba hawaadhibu kamwe watu wasio na hatia pamoja na wenye hatia.—Mwa. 18:20-32. w22.08 28 ¶9-10
Ijumaa, Machi 29
Mtu anayeaminika hutunza siri.—Met. 11:13.
Mwaka wa 455 K.W.K., baada ya Gavana Nehemia kujenga upya kuta za Yerusalemu, alitafuta wanaume wanaotegemeka ambao wangetunza jiji hilo. Kati ya watu wengine, Nehemia alimchagua Hanani, awe mkuu wa Ngome. Biblia inamfafanua Hanani kuwa “mwanamume mwaminifu zaidi [ambaye] alimwogopa Mungu wa kweli kuliko watu wengine wengi.” (Neh. 7:2) Kumpenda Yehova na kuogopa kufanya jambo ambalo litamkasirisha, kulimchochea Hanani achukue kwa uzito mgawo wowote aliopewa. Sifa hizo zitatusaidia sisi pia tuwe wenye kutegemeka katika utumishi wa Mungu. Fikiria mfano wa Tikiko, mwandamani aliyetumainika wa mtume Paulo. Paulo alimtegemea Tikiko na alimfafanua kuwa “mhudumu mwaminifu.” (Efe. 6:21, 22) Paulo alikuwa na uhakika kwamba Tikiko angepeleka barua kwa akina ndugu huko Efeso na Kolosai na pia angewatia moyo na kuwafariji. Tikiko anatukumbusha kuhusu wanaume waaminifu wanaotegemeka ambao leo wanatutunza kiroho.—Kol. 4:7-9. w22.09 9-10 ¶5-6