Alhamisi, Machi 28
Nawe utarudi mavumbini.—Mwa. 3:19.
Bila shaka, hatungependa kufanya kosa ambalo Adamu na Hawa walifanya. Tunaweza kuepuka matokeo hayo mabaya ikiwa tutaendelea kujifunza kumhusu Yehova, kuthamini sifa zake, na kujitahidi kuelewa njia yake ya kufikiri. Tunapofanya hivyo, bila shaka tutaimarisha upendo wetu kwa Yehova. Mfikirie Abrahamu. Alimpenda sana Yehova. Hata ilipokuwa vigumu kwake kuelewa maamuzi ambayo Yehova alifanya, Abrahamu hakuasi. Badala yake, alijitahidi kumjua Yehova vizuri zaidi. Kwa mfano, aliposikia kuhusu uamuzi wa Yehova wa kuangamiza Sodoma na Gomora, mwanzoni Abrahamu aliogopa kwamba “Mwamuzi wa dunia yote” angefagilia mbali waadilifu pamoja na waovu. Abrahamu aliona hilo kuwa jambo lisilowezekana, basi kwa unyenyekevu alimuuliza Yehova maswali kadhaa. Yehova alimjibu kwa subira. Mwishowe, Abrahamu alitambua kwamba Yehova anachunguza moyo wa kila mwanadamu na kwamba hawaadhibu kamwe watu wasio na hatia pamoja na wenye hatia.—Mwa. 18:20-32. w22.08 28 ¶9-10
Ijumaa, Machi 29
Mtu anayeaminika hutunza siri.—Met. 11:13.
Mwaka wa 455 K.W.K., baada ya Gavana Nehemia kujenga upya kuta za Yerusalemu, alitafuta wanaume wanaotegemeka ambao wangetunza jiji hilo. Kati ya watu wengine, Nehemia alimchagua Hanani, awe mkuu wa Ngome. Biblia inamfafanua Hanani kuwa “mwanamume mwaminifu zaidi [ambaye] alimwogopa Mungu wa kweli kuliko watu wengine wengi.” (Neh. 7:2) Kumpenda Yehova na kuogopa kufanya jambo ambalo litamkasirisha, kulimchochea Hanani achukue kwa uzito mgawo wowote aliopewa. Sifa hizo zitatusaidia sisi pia tuwe wenye kutegemeka katika utumishi wa Mungu. Fikiria mfano wa Tikiko, mwandamani aliyetumainika wa mtume Paulo. Paulo alimtegemea Tikiko na alimfafanua kuwa “mhudumu mwaminifu.” (Efe. 6:21, 22) Paulo alikuwa na uhakika kwamba Tikiko angepeleka barua kwa akina ndugu huko Efeso na Kolosai na pia angewatia moyo na kuwafariji. Tikiko anatukumbusha kuhusu wanaume waaminifu wanaotegemeka ambao leo wanatutunza kiroho.—Kol. 4:7-9. w22.09 9-10 ¶5-6
Jumamosi, Machi 30
Upendo hufunika dhambi nyingi.—1 Pet. 4:8.
Yosefu alikabili majaribu makali yaliyodumu kwa miaka 13 hivi. Yosefu angeweza kutilia shaka ikiwa kweli Yehova anampenda. Na huenda alijiuliza ikiwa Yehova alikuwa amemwacha wakati alipohitaji msaada. Lakini Yosefu hakuweka kinyongo. Badala yake, alitunza akili zake kwa kuendelea kuwa mtulivu. Alipopata nafasi ya kulipiza kisasi dhidi ya ndugu zake, alijizuia kufanya hivyo na akawaonyesha upendo na kuwasamehe. (Mwa. 45:4, 5) Yosefu alitenda hivyo kwa sababu alifikiria mambo kwa njia nzuri. Badala ya kukazia fikira matatizo yake, aliona mambo kwa njia pana—alitambua kusudi la Yehova. (Mwa. 50:19-21) Tunapata somo gani? Unapotendewa kwa njia isiyofaa, usiwe na uchungu kumwelekea Yehova au kujiuliza ikiwa amekuacha. Badala yake, tafakari kuhusu jinsi anavyokusaidia kuvumilia jaribu hilo. Isitoshe, wengine wanapokutendea kwa njia isiyofaa, jitahidi kufunika udhaifu wao kwa upendo. w22.11 21 ¶4