Wewe Umedanganywa?
Kwa kuwa Yesu ana jina, je! Baba yake asiwe na jina?
MAMILIONI mengi ya watu kote kote ulimwenguni wana mashaka sana leo juu ya dini. Lakini huenda wakashangaa kujua kwamba Mungu mwenyewe anachukizwa na dini zilizo nyingi. Sababu moja kati ya sababu nyingi zinazofanya achukizwe ni kwamba zile zenye kuitwa dini za Kikristo ati zimefanya moja la madanganyo yaliyo makubwa zaidi katika historia, Udanganyifu huo unahusiana na kufunulia watu habari fulani ya msingi—kuwajulisha habari zinazohusu Mungu ni nani.
Watu walio wengi katika makanisa ya Jumuiya ya Wakristo wanamjua Muumba kuwa anaitwa “Mungu,” “Bwana,” “Mwenyezi” au neno jingine linalofanana na hayo. Lakini je! Aliye Juu Zaidi hana jina? Kabla ya kuwakomboa Waisraeli katika utumwa huko Misri, Mungu huyo mwenye uwezo wote alijulisha kwamba alikusudia kufanya ‘jina lake litangazwe katika dunia yote.’ (Kutoka 9:16) Kwa hiyo ni hakika kwamba yeye ana jina. Na bila shaka si Mungu asiye na jina ambaye kuwapo kwake kulitokeza tamasha ya ajabu sana huko kwenye Mlima Sinai (ulioonyeshwa katika jalada la gazeti hili), akafanya mlima uteteme, wakati zile Amri Kumi zilipokuwa zikitolewa kupitia nabii Musa. Kati ya mambo mengine, wakati huo Waisraeli waliambiwa: “Usilitaje bure jina la [Yehova] Mungu wako.” (Kutoka 19:16—20:18) Je! amri ya namna hiyo ingaliweza kutolewa na Mungu fulani asiye na jina?
Wenye kujiita Wakristo wanapaswa kulijua hilo Jina la Kimungu. Ni kweli kwamba wanalitumia jina la Mwana wa Mungu. Lakini kama kweli wanalitamka jina la kibinafsi la Baba, ni mara chache sana wanapofanya hivyo. Lakini, Yesu Kristo alipokuwa duniani alimwambia Baba yake wa kimbingu katika sala hivi: “Nami naliwajulisha [wafuasi wangu] jina lako, tena nitawajulisha hilo.”—Yohana 17:26.
Ni wazi kutokana na yaliyotangulia kusemwa na kutokana na Sala ya Kielelezo ya Yesu kwamba ni kweli Mungu ana jina. Yesu hata alifundisha wafuasi wake kusali kwamba jina la Baba wa kimbingu “litakaswe,” au lichukuliwe kuwa takatifu! (Mathayo 6:9, NW) Basi, kwa sababu gani halitumiwi katika makanisa ya Jumuiya ya Wakristo? Na ni kwa sababu gani jina hilo linakosekana katika tafsiri zilizo nyingi za kisasa za Biblia?
[Picha katika ukurasa wa 3]
BABA
ALIYE JUU ZAIDI
MWENYEZI
BWANA
MUNGU