Alhamisi, Februari 19
Watiini wale wanaoongoza kati yenu.—Ebr. 13:17.
Wanapopokea mwongozo, wazee wa kutaniko wanahitaji kuusoma kwa makini na kisha kufanya yote wawezayo kuufuata. Wazee wa kutaniko wanapokea mwongozo wa jinsi ya kutimiza sehemu mbalimbali za mikutano, jinsi ya kutoa sala kwa niaba ya kutaniko, na pia jinsi ya kuwatunza kondoo wa Kristo. Wazee wa kutaniko wanaofuata mwongozo wa tengenezo wanawasaidia wale walio chini ya utunzaji wao wahisi wanapendwa na wako salama. Tunapopokea mwongozo kutoka kwa wazee wa kutaniko, tunapaswa kuufuata kwa hiari. Tunapofanya hivyo, inakuwa rahisi kwa wale wanaoongoza kufanya kazi yao. Biblia inatutia moyo tuwanyenyekee na kuwatii wale wanaoongoza. (Ebr. 13:7, 17) Wakati mwingine jambo hilo linaweza kuwa changamoto. Kwa nini? Kwa sababu wazee wa kutaniko si wakamilifu. Hata hivyo, ikiwa tutakazia fikira sifa zao mbaya badala ya sifa zao nzuri, tutakuwa tukiwasaidia maadui wetu. Katika njia gani? Tutaacha kulitumaini tengenezo la Mungu. w24.04 10 ¶11-12
Ijumaa, Februari 20
Atawatenganisha watu mmoja kutoka kwa mwenzake.—Mt. 25:32.
Je, watu wote watakaokufa wakati wa matukio ya dhiki kuu wataangamizwa milele bila kuwa na tumaini la ufufuo? Maandiko yanaonyesha wazi kwamba wale wanaompinga Yehova moja kwa moja na ambao yeye na majeshi yake watawaangamiza katika Har–Magedoni hawatafufuliwa. (2 The. 1:6-10) Lakini vipi kuhusu watu wengine, kwa mfano, wale ambao huenda watakufa kwa sababu ya magonjwa au uzee, au kutokana na aksidenti, au wale watakaouawa na wanadamu wengine? (Mhu. 9:11; Zek. 14:13) Je, inawezekana kwamba baadhi ya watu hao watakuwa miongoni mwa watu “wasio waadilifu” ambao watafufuliwa katika dunia mpya? (Mdo. 24:15) Hatujui. Lakini tunajua mambo kadhaa kuhusu matukio ya wakati ujao. Kwa mfano, tunajua kwamba wakati wa Har–Magedoni watu watahukumiwa kwa kutegemea jinsi walivyowatendea ndugu za Kristo. (Mt. 25:40) Na wale watakaohukumiwa kuwa kondoo watakuwa wameonyesha kwamba wanawaunga mkono watiwa-mafuta na Kristo.—Ufu. 12:17. w24.05 10-11 ¶9-11
Jumamosi, Februari 21
Yehova yuko hai! Mwamba wangu na asifiwe! Mungu wa wokovu wangu na akwezwe.—Zab. 18:46.
Biblia inafafanua siku zetu kuwa “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Tim. 3:1) Watu wa Yehova wanakabiliana na changamoto ambazo kila mtu anakabili katika mfumo huu wa mambo, lakini pia wanakabiliana na upinzani na mateso. Ni nini kinachotusaidia kuendelea kumwabudu Yehova licha ya matatizo hayo? Jambo moja kuu ni kwamba tunajua Yehova ndiye “Mungu aliye hai.” (Yer. 10:10; 2 Tim. 1:12) Yehova ni Mtu halisi anayetutegemeza wakati wa majaribu na anatafuta fursa za kutusaidia. (2 Nya. 16:9; Zab. 23:4) Kumwona Yehova kuwa Mungu aliye hai kunaweza kutusaidia kukabiliana na jaribu lolote tunalopata kwa mafanikio. w24.06 20 ¶1-2