Jumatano, Januari 21
Kwa nini unakawia? Simama, ubatizwe.—Mdo. 22:16.
Je,unampenda Yehova Mungu, ambaye amekupatia kila zawadi njema, kutia ndani uhai? Je, ungependa kumwonyesha upendo wako? Njia bora ya kufanya hivyo ni kujiweka wakfu kwake na kuonyesha wakfu wako kupitia ubatizo. Unapofanya hivyo, unakuwa sehemu ya familia ya Yehova. Matokeo ni kwamba Yehova, Baba na Rafiki yako, atakuongoza na kukutunza kwa sababu wewe ni mali yake. (Zab. 73:24; Isa. 43:1, 2) Pia, kujiweka wakfu na kubatizwa kunakupatia tumaini la kufurahia uzima wa milele. (1 Pet. 3:21) Je, kuna jambo linalokufanya usite kubatizwa? Ikiwa ndivyo, hauko peke yako. Mamilioni ya watu waliokutangulia, walihitaji kufanya mabadiliko katika mwenendo wao na njia yao ya kufikiri ili wastahili kubatizwa. Sasa wanamtumikia Yehova kwa bidii na shangwe. w25.03 2 ¶1-2
Alhamisi, Januari 22
Maana wewe hutoa msamaha wa kweli.—Zab. 130:4.
Katika Biblia, mara nyingi dhambi hulinganishwa na mizigo mizito. Mfalme Daudi alieleza hivi kuhusu dhambi zake: “Dhambi zangu zimetanda juu ya kichwa changu; kama mzigo mzito, ni nzito sana siwezi kuzibeba.” (Zab. 38:4) Lakini Yehova husamehe dhambi za wakosaji wanaotubu. (Zab. 25:18; 32:5) Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “kusamehe” kimsingi linamaanisha “kuinua” au “kubeba.” Kwa njia ya mfano, huenda tukamwazia Yehova akiwa mwanamume mwenye nguvu ambaye anainua mzigo wa dhambi kutoka kwenye mabega yetu na kuuondoa. Mfano mwingine unaonyesha jinsi Yehova anavyopeleka dhambi zetu mbali sana na sisi. Zaburi 103:12 inatuambia hivi: “Kama mashariki ilivyo mbali sana na magharibi, ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali sana na sisi.” Mashariki iko mbali sana na magharibi. Pande hizo mbili haziwezi kukutana kamwe. Kwa maneno mengine, Yehova anapeleka dhambi zetu mbali sana kuliko tunavyoweza kuwazia. Hilo linatuhakikishia kwamba Yehova anatusamehe kikamili! w25.02 9 ¶5-6
Ijumaa, Januari 23
Unapotoa zawadi za rehema, usipige tarumbeta mbele yako.—Mt. 6:2.
Baada ya Yesu kurudi mbinguni, Mtume Petro alimponya mwanamume aliyekuwa kilema tangu kuzaliwa kwake. (Mdo. 1:8, 9; 3:2, 6-8) Umati mkubwa wa watu uliona muujiza huo na kumzunguka Petro. (Mdo. 3:11) Je, Petro angefurahia kupokea utukufu pindi hiyo, ukizingatia kwamba alilelewa katika jamii ambayo ilikazia fikira sana vyeo na umashuhuri? Hapana, kwa unyenyekevu Petro hakuelekeza sifa kwake, bali kwa Yehova na Yesu ambao wanastahili. Alisema hivi: “Kupitia jina [la Yesu], na kwa imani yetu katika jina lake, mtu huyu mnayemwona na kumfahamu amefanywa awe mwenye nguvu.” (Mdo. 3:12-16) Tunaweza kuiga mfano wa Petro kwa kusitawisha unyenyekevu. Tunafanya mambo kwa ajili ya wengine kwa sababu tunampenda Yehova na tunawapenda watu, na si kwa sababu tunapenda kusifiwa. Tutaonyesha kwamba sisi ni wanyenyekevu, ikiwa kwa furaha tunamtumikia Yehova na ndugu zetu kadiri tuwezavyo, iwe wengine wanaona jitihada zetu au la.—Mt. 6:1-4. w25.03 10-11 ¶11-12