Jumatano, Juni 3
Chakula kigumu ni cha watu wakomavu.—Ebr. 5:14.
Mafundisho ya msingi yanatia ndani toba, imani, ubatizo, na ufufuo. (Ebr. 6:1, 2) Hayo ni baadhi ya mafundisho ya msingi ambayo Wakristo wote huamini. Ndiyo sababu mtume Petro alizungumzia mafundisho hayo ya msingi alipouhubiria umati wa watu katika siku ya Pentekoste. (Mdo. 2:32-35, 38) Ni lazima tukubali mafundisho hayo ya msingi ili tuwe wanafunzi wa Kristo. Kwa mfano, Paulo alionya kwamba yeyote anayekataa fundisho la ufufuo anakataa imani yote ya Kikristo. (1 Kor. 15:12-14) Hata hivyo, hatupaswi kuridhika tu na mafundisho ya msingi ya kweli. Tofauti na fundisho hilo la msingi, chakula kigumu cha kiroho kinahusisha sheria na pia kanuni za Yehova, ambazo zinatusaidia kuelewa njia yake ya kufikiri. Ili tunufaike na chakula hicho kigumu cha kiroho, ni lazima tujifunze kwa makini Neno la Mungu, tulitafakari, na kutumia mambo tunayojifunza. Tunapofanya hivyo, tunajizoeza kufanya maamuzi yanayomfurahisha Yehova. w24.04 5 ¶12-13
Alhamisi, Juni 4
Watu wa Ninawi watasimama katika hukumu.—Mt. 12:41.
Mungu alimkumbusha Yona kwamba Waninawi hao “hawajui kutofautisha jema na baya.” (Yona 1:1, 2; 3:10; 4:9-11) Baadaye, Yesu alitumia mfano huo kufundisha kuhusu haki na rehema ya Yehova. Waninawi “watasimama katika hukumu” gani? Yesu alifundisha kuhusu “ufufuo wa hukumu” wa wakati ujao. (Yoh. 5:29) Alikuwa akirejelea Utawala wake wa Miaka Elfu Moja, kipindi ambacho “waadilifu na wasio waadilifu” watafufuliwa. (Mdo. 24:15) Kwa wasio waadilifu, huo utakuwa “ufufuo wa hukumu.” Yaani, Yehova na Yesu watachunguza na kuchanganua tabia zao na jinsi wanavyoitikia mafundisho yanayotoka kwa Yehova. Ikiwa Mninawi aliyefufuliwa atakataa kujiunga na ibada ya kweli, Yehova hatamruhusu aendelee kuishi. (Isa. 65:20) Lakini wale wote watakaochagua kumwabudu Yehova kwa uaminifu, watapata hukumu nzuri. Watakuwa na tumaini la kuishi milele!—Dan. 12:2. w24.05 5 ¶13-14
Ijumaa, Juni 5
Mwana wa binadamu alikuja kutafuta na kuokoa kilichopotea.—Luka 19:10.
Yesu alitupatia mfano halisi na mkamilifu wa rehema za Baba yake. (Yoh. 14:9) Kwa maneno na matendo, alionyesha kwamba Baba yake mwenye huruma na rehema, anawapenda watu na anataka kumsaidia kila mmoja wao ashinde pambano dhidi ya dhambi. Yesu aliwasaidia watu wenye dhambi watamani kubadili njia zao na kumfuata. (Luka 5:27, 28) Yesu alijua mambo ambayo yangempata. Aliwaeleza wafuasi wake zaidi ya mara moja kwamba angesalitiwa na kuuawa kwenye mti wa mateso. (Mt. 17:22; 20:18, 19) Alijua kwamba dhabihu yake ingeondoa dhambi ya ulimwengu. Pia, Yesu alifundisha kwamba baada ya kutoa uhai wake, ‘angewavuta watu wa namna zote’ kwake. (Yoh. 12:32) Wanadamu wenye dhambi wangeweza kumfurahisha Yehova kwa kumkubali Yesu kuwa Bwana wao na kwa kufuata hatua zake. Ikiwa wangefanya hivyo, mwishowe ‘wangewekwa huru kutoka katika dhambi.’ (Rom. 6:14, 18, 22; Yoh. 8:32) Hivyo, Yesu alikuwa jasiri, na kwa hiari alikuwa tayari kukabili kifo chenye maumivu makali.—Yoh. 10:17, 18. w24.08 5 ¶11-12