Jumapili, Februari 22
Kijia cha waadilifu ni kama nuru nyangavu ya asubuhi Inayong’aa zaidi na zaidi mpaka mchana kamili.—Met. 4:18.
Tunapaswa kuendelea kulitumaini tengenezo la Yehova. Inapoonekana wazi kwamba kuna uhitaji wa kurekebisha uelewaji wetu wa kweli fulani ya Biblia au jinsi kazi ya Ufalme inavyofanywa, wale wanaoongoza hawasiti kufanya mabadiliko yanayohitajika. Wanafanya hivyo kwa sababu wanataka kumfurahisha Yehova kuliko jambo lingine lolote. Pia, wanafanya yote wanayoweza ili maamuzi yao yategemee Neno la Mungu, yaani, kiwango au kigezo ambacho ni lazima watu wote wa Yehova wakifuate. Mtume Paulo alisema hivi: “Endelea kushika kigezo cha maneno yenye manufaa.” (2 Tim. 1:13) “Kigezo cha maneno yenye manufaa” kinarejelea mafundisho ya Kikristo yanayopatikana katika Biblia. (Yoh. 17:17) Mafundisho hayo ndiyo msingi wa kila jambo tunaloamini. Tengenezo la Yehova limetufundisha kushikamana na kigezo hicho. Tukiendelea kufanya hivyo, tutabarikiwa. w24.07 11-12 ¶12-13
Jumatatu, Februari 23
Yehova . . . ni mwenye subira kwenu kwa sababu hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.—2 Pet. 3:9.
Kwa kuwa alikuwa ametubu na kusamehewa, mtume Petro angeweza kuwafundisha wengine kuhusu toba na msamaha. Muda fulani baada ya sherehe ya Pentekoste, Petro alitoa hotuba mbele ya umati wa Wayahudi wasioamini, akiwafafanulia kwamba walikuwa wamemuua Masihi. Hata hivyo, kwa upendo aliwahimiza hivi: “Kwa hiyo, tubuni na mgeuke ili dhambi zenu zifutwe, ili majira yenye kuburudisha yaje kutoka kwa Yehova mwenyewe.” (Mdo. 3:14, 15, 17, 19) Hivyo, Petro alionyesha kwamba toba inamchochea mtenda dhambi kugeuka—kubadili njia yake mbaya ya kufikiri na kutenda—na kufuatia njia mpya, ambayo inamfurahisha Yehova. Pia, mtume huyo alionyesha kwamba Yehova angefuta dhambi zao, au kuziondoa kabisa. Hilo ni tumaini zuri sana kwa Wakristo wanapotenda dhambi—hata dhambi nzito! w24.08 12 ¶14
Jumanne, Februari 24
Njia yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa.—Ebr. 13:5.
Ikiwa tuna imani yenye nguvu kwamba hivi karibuni Yehova atauharibu mfumo huu wa mambo, tutachochewa kuepuka kupenda mali. Watu “watatupa fedha yao barabarani” kwa sababu watatambua kwamba “fedha yao wala dhahabu yao haitaweza kuwaokoa katika siku ya ghadhabu ya Yehova.” (Eze. 7:19) Badala ya kukazia fikira kujikusanyia pesa nyingi iwezekanavyo, tunahitaji kufanya maamuzi yatakayotusaidia kuishi maisha rahisi na yenye usawaziko. Hilo linatia ndani kukataa kishawishi cha kuwa na madeni yasiyo ya lazima au kutumia muda mwingi sana kuhangaikia vitu vyetu vya kimwili. Pia, ni lazima tuwe waangalifu ili mali zetu zisiwe jambo muhimu zaidi maishani mwetu. (Mt. 6:19, 24) Huenda imani yetu ikajaribiwa inapohusu vitu vya kimwili na mambo mengine tunaposubiri mwisho wa mfumo huu wa mambo ufike. w24.09 11 ¶13-14