Jumatano, Julai 22
Nitalisamehe kosa lao, nami sitaikumbuka tena dhambi yao.—Yer. 31:34.
Nabii Yeremia anamnukuu Yehova akisema maneno yanayopatikana katika andiko la leo. Mtume Paulo alitumia msemo unaofanana aliporejelea maneno hayo, alisema hivi: “Sitazikumbuka tena dhambi zao.” (Ebr. 8:12) Hilo linamaanisha nini hasa? Katika Biblia, neno “kukumbuka” sikuzote halirejelei kukumbuka au kufikiria jambo fulani lililotokea zamani. Badala yake, linaweza kuhusisha kuchukua hatua fulani. Mhalifu aliyekuwa ametundikwa kwenye mti kando ya Yesu alimwambia hivi: “Yesu, unikumbuke utakapoingia katika Ufalme wako.” (Luka 23:42, 43) Hakuwa tu akimwomba Yesu amfikirie wakati huo. Jibu la Yesu lilionyesha kwamba angechukua hatua ya kumfufua mhalifu huyo. Hivyo, Yehova anaposema kwamba hakumbuki tena dhambi zetu, anamaanisha kuwa hatachukua hatua dhidi yetu. Hatatuadhibu wakati ujao kwa sababu ya dhambi ambazo tayari ametusamehe. w25.02 10-11 ¶14-15
Alhamisi, Julai 23
Kumjua Aliye Mtakatifu Zaidi ni uelewaji.—Met. 9:10.
Naam, uelewaji wa kweli unatokana na kujua sifa za Yehova, kusudi lake, na mambo ambayo anapenda na anayochukia. Jiulize hivi, ‘Kulingana na mambo ambayo ninajua kumhusu Yehova, ni uamuzi gani utakaomfurahisha?’ (Efe. 5:17) Ili kumfurahisha Yehova, nyakati nyingine ni lazima tufanye jambo ambalo watu tulio karibu nao hawatafurahia. Kwa mfano, huenda wazazi wenye nia nzuri wakasisitiza kwamba binti yao aliye mtu mzima afunge ndoa na mwanamume ambaye ana mali nyingi—au ambaye atatoa kiasi kikubwa cha mahari—ingawa mtu huyo ni dhaifu kiroho. Ni kweli kwamba wangependa binti yao atunzwe kimwili, lakini ni nani atakayemsaidia aendelee kukua kiroho? Yehova anaonaje jambo hilo? Tunapata jibu kwenye Mathayo 6:33. Hapo, Wakristo wanahimizwa kuendelea “kuutafuta kwanza Ufalme.” Ingawa tunawaheshimu wazazi wetu na watu katika jamii yetu, hangaiko letu kuu ni kumfurahisha Yehova. w25.01 17 ¶9-10
Ijumaa, Julai 24
Lakini Bwana alisimama karibu nami na kunitia nguvu.—2 Tim. 4:17.
Leo, tunahitaji msaada wa Yehova ili tuendelee kuhubiri kwa bidii licha ya upinzani. (Ufu. 12:17) Kwa nini unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atakutegemeza? Fikiria sala ya Yesu inayopatikana kwenye Yohana sura ya 17. Yesu alimwomba Yehova awalinde mitume wake na Yehova alijibu sala hiyo. Kitabu cha Matendo kinaonyesha jinsi ambavyo Yehova aliwasaidia mitume kuhubiri kwa bidii licha ya mateso. Katika sala yake, Yesu alimwomba pia Yehova awalinde wale watakaoamini mambo ambayo mitume wangehubiri. Kutia ndani wewe. Yehova bado anaendelea kujibu sala ya Yesu. Na atakusaidia, kama alivyowasaidia mitume. (Yoh. 17:11, 15, 20) Hata ikiwa kazi ya kuhubiri habari njema itazidi kuwa ngumu kadiri mwisho unavyokaribia, tutapata msaada wowote tunaouhitaji.—Luka 21:12-15. w25.03 18 ¶13-14