Alhamisi, Februari 12
Mahangaiko yaliponilemea, ulinifariji na kunibembeleza.—Zab. 94:19.
Unaweza kufanya nini ikiwa una shaka kuhusu thamani yako? Soma mistari ya Biblia ambayo inakuhakikishia thamani yako kwa Yehova na uitafakari. Ikiwa umeshindwa kufikia lengo fulani au umevunjika moyo kwa sababu huwezi kufanya mengi kama wengine, usijihukumu vikali. Yehova ana matarajio yaliyosawazika. (Zab. 103:13, 14) Ikiwa ulitendewa kwa njia isiyofaa wakati uliopita, usijilaumu kwa sababu ya mambo ambayo mtu huyo alikutendea. Hukustahili kutendewa hivyo! Kumbuka kwamba waliotenda mabaya ndio watatoa hesabu mbele za Yehova, si waliotendewa mabaya. (1 Pet. 3:12) Kamwe usitilie shaka kwamba Yehova anaweza kukutumia ili uwasaidie watu wengine. Amekupa pendeleo la kuwa mfanyakazi mwenzi unaposhiriki katika huduma ya Kikristo. (1 Kor. 3:9) Inaelekea mambo uliyopitia maishani yamekusaidia uwaonyeshe wengine hisia mwenzi na utambue jinsi ambavyo huenda wanahisi. Unaweza kufanya mengi ili kuwasaidia. w24.10 7-8 ¶6-7
Ijumaa, Februari 13
Je, Mungu hatawatendea haki watu wake waliochaguliwa ambao wanamlilia mchana na usiku, huku akiwaonyesha subira? Ninawaambia, atawatendea haki upesi.—Luka 18:7, 8.
Yehova anataka tutendewe vizuri na anatambua tunapotendewa isivyo haki. Biblia inasema kwamba “Yehova anapenda haki.” (Zab. 37:28) Yesu anatuhakikishia kwamba kwa wakati unaofaa, Yehova ‘atatutendea haki upesi.’ Na hivi karibuni, ataondoa madhara yote yanayosababisha tuteseke na kuondoa aina zote za ukosefu wa haki. (Zab. 72:1, 2) Tunapoendelea kusubiri wakati ambao uadilifu utakuwepo duniani kote, Yehova anatusaidia kukabiliana na ukosefu wa haki. (2 Pet. 3:13) Anatufundisha jinsi ya kuepuka kufanya jambo lisilo la hekima tunapotendewa kwa njia isiyo ya haki. Kupitia Mwana wake, Yehova anatupatia mfano mkamilifu wa jinsi tunavyoweza kushughulikia ukosefu wa haki. Na anatupatia ushauri hususa ambao tunaweza kutumia tunapotendewa isivyo haki. w24.11 2-3 ¶3-4
Jumamosi, Februari 14
Wapeni chakula.—Mt. 14:16.
Ombi la Yesu la kulisha umati lilikuwa tatizo kwa sababu kulikuwa na wanaume 5,000 hivi. Na ukijumlisha wanawake na watoto, huenda kulikuwa na watu 15,000 waliohitaji kulishwa. (Mt. 14:21) Andrea akasema hivi: “Hapa kuna mvulana mdogo aliye na mikate mitano ya shayiri na samaki wawili wadogo. Je, hivi vitawatosha watu wengi hivi?” (Yoh. 6:9) Mikate ya shayiri ilikuwa chakula ambacho watu walikula kwa ukawaida, na huenda samaki hao wadogo walikuwa wamewekwa chumvi na kukaushwa. Hata hivyo, chakula ambacho mvulana huyo alikuwa nacho hakingetosha kuwalisha watu wengi hivyo—au je, kingetosha? Yesu alitaka kuuonyesha ukarimu umati huo wa watu, hivyo aliwaagiza wote waketi katika vikundi kwenye nyasi. (Marko 6:39, 40; Yoh. 6:11-13) Tunasoma kwamba Yesu alitoa shukrani kwa Baba yake kwa ajili ya mikate na samaki hao. Ilifaa kabisa kumshukuru Mungu, ambaye kihalisi ndiye Chanzo cha chakula. Hicho ni kikumbusho kizuri kwetu cha kufuata mfano wa Yesu wa kusali kabla ya kula. Kisha, Yesu akaagiza chakula kigawanywe, na watu wakala na kushiba. w24.12 2-3 ¶3-4