Alhamisi, Aprili 9
Naye aliwatetea wakosaji.—Isa. 53:12.
Yehova alimwomba Abrahamu amtoe dhabihu Isaka, mwana wake. Bila shaka jambo hilo lilimtaabisha sana Abrahamu. Hata hivyo, alijitayarisha ili kulitimiza. Lakini Abrahamu alipokaribia kumuua Isaka, Mungu alimzuia. Mfano huo unawafundisha ukweli muhimu watu wote wenye imani, yaani, Yehova angekuwa tayari kumtoa Mwana wake mpendwa kuwa dhabihu. Yehova anawapenda sana wanadamu. (Mwa. 22:1-18) Karne nyingi baadaye, Yehova alipowapa Waisraeli Sheria, aliwaagiza watoe dhabihu za wanyama ili kufunika dhambi zao. (Law. 4:27-29; 17:11) Dhabihu hizo zilionyesha kwamba Yehova angeandaa dhabihu kubwa zaidi, ambayo ingewakomboa kikamili wanadamu kutoka katika dhambi. Manabii wa Mungu waliongozwa na roho ili kufafanua kwamba uzao ulioahidiwa, ambaye alikuwa Mwana wa pekee wa Mungu, angeteseka na kuuawa ili kuwakomboa wanadamu—kutia ndani wewe—kutoka katika dhambi na kifo!—Isa. 53:1-12. w24.08 4 ¶7-8
Ijumaa, Aprili 10
Jinsi ninavyoipenda sana sheria yako! Ninaitafakari mchana kutwa.—Zab. 119:97.
Unaposoma Biblia, jitahidi kutafuta njia za kutumia mambo unayosoma. Unaposoma sehemu fulani ya Neno la Mungu, jiulize hivi, ‘Ninawezaje kutumia habari hii sasa au wakati ujao?’ Kwa mfano, tuseme katika usomaji wako wa Biblia unasoma 1 Wathesalonike 5:17, 18. Baada ya kusoma mistari hiyo miwili, unaweza kutua na kufikiria unasali mara ngapi, na sala zako ni zenye kina kadiri gani. Pia, unaweza kutafakari kuhusu mambo ya kumshukuru Yehova. Na huenda unaamua kwamba utamshukuru Yehova kwa mambo matatu hususa. Ukitumia hata dakika chache kukaza fikira kwa njia hiyo, kwa kadiri fulani utakuwa msikiaji na mtendaji wa Neno la Mungu. Fikiria jinsi utakavyonufaika kwa kurudia hatua hizo kila siku unaposoma sehemu nyingine za Biblia! Naam, utakuwa mtendaji mzuri zaidi wa Neno la Mungu. w24.09 4-5 ¶9-10
Jumamosi, Aprili 11
Jihadharini, msije mkapoteza mambo ambayo tumefanya kazi ili kuyatokeza, bali mpate thawabu kamili.—2 Yoh. 8.
Yehova alituumba tukiwa na uwezo wa pekee. Ingawa tunafurahia kupokea, tunapata furaha kubwa zaidi tunapotoa. Tunahisi vizuri tunapoweza kuwasaidia waabudu wenzetu. Na tunakuwa na furaha wanapotushukuru. Hata hivyo, iwe mpokeaji anatushukuru au la, tunaweza kufurahi kwamba tulifanya jambo linalofaa. Usisahau kamwe kwamba chochote unachotoa, ‘Yehova anaweza kukupa vingi zaidi.’ (2 Nya. 25:9) Sikuzote Yehova hutupatia vitu vingi zaidi kuliko tunavyotoa! Na hakuna shangwe kubwa zaidi kuliko kuthawabishwa na Yehova mwenyewe. Basi, acheni tuazimie kuendelea kumwiga Baba yetu wa mbinguni mwenye ukarimu. w24.09 31 ¶20-21