Jumapili, Septemba 8
Mchague uzima ili mwendelee kuishi, ninyi na wazao wenu.—Kum. 30:19.
Mengi zaidi yanahusika kuliko kuwaambia tu watoto wako mambo yanayofaa na yasiyofaa. Itafaa pia kuwasaidia wafikirie kuhusu maswali kama vile: ‘Kwa nini Biblia inakataza mambo fulani yanayoonekana kuwa yenye kuvutia? Ni nini kinachonisadikisha kwamba nitanufaika sikuzote ninapofuata viwango vya Biblia?’ (Isa. 48:17, 18) Mtoto anayetaka kubatizwa anapaswa kusaidiwa afikirie jambo lingine pia—anahisije kuhusu wajibu atakaohitaji kutimiza akiwa Mkristo? Kuna manufaa gani ya kuwa Mkristo? Atakabili changamoto zipi? Ni kwa njia gani manufaa atakayopata yatazidi changamoto atakazokabili? (Marko 10:29, 30) Hayo ni baadhi ya mambo ambayo mtu anaweza kukabili baada ya kubatizwa. Kwa hiyo, inafaa afikirie kwa uzito mambo hayo kabla ya kuchukua hatua hiyo muhimu. Watoto wanaposaidiwa kufikiria kwa uzito mambo hayo, kuna uwezekano mkubwa kwamba watasitawisha usadikisho wao wenyewe. Usadikisho kuhusu nini? Kwamba sikuzote viwango vya Biblia ni vyenye manufaa wanapovifuata. w17.12 21 ¶14-15
Jumatatu, Septemba 9
Huziita zote kwa majina.—Isa. 40:26.
Wengi miongoni mwenu mnakabiliana na matatizo makubwa ya afya. Wengine wanawatunza watu wao wa ukoo waliozeeka, ingawa umri wao pia umesonga. Na wengine wanapambana kuandalia familia zao, si vitu vya starehe, bali mahitaji ya lazima. Na tunajua kwamba wengi wanakabiliana na matatizo kadhaa kwa wakati uleule, si tatizo moja tu! Ikiwa Yehova anapendezwa kibinafsi na uumbaji wake usio na uhai, wazia jinsi anavyohisi kukuelekea wewe ambaye unamtumikia si kwa sababu unaongozwa na silika, bali kwa sababu unampenda! (Zab. 19:1, 3, 14) Baba yetu mpendwa anajua kila kitu kukuhusu. ‘Hata amehesabu nywele zote za kichwa chako.’ (Mt. 10:30) Na mtunga zaburi anatuhakikishia hivi: “Yehova anajua mambo wanayokabili watu wasio na lawama.” (Zab. 37:18) Naam, anajua majaribu yote unayokabili, naye anaweza kukupa nguvu ya kuvumilia kila moja ya majaribu hayo. w18.01 7 ¶1; 8 ¶4
Jumanne, Septemba 10
Tabitha, inuka!—Mdo. 9:40.
Ufufuo wa Tabitha uliofanywa na Petro ulikuwa wenye kusadikisha sana hivi kwamba “wengi wakamwamini Bwana.” Wote wangeweza kutoa ushahidi kumhusu Bwana na hasa kuhusu uwezo wa Yehova wa kuwafufua wafu. (Mdo. 9:36-42) Wengine pia walishuhudia ufufuo mwingine. Pindi moja, mtume Paulo alikuwa kwenye mkutano katika chumba cha juu katika jiji la Troa, ambalo kwa sasa ni kaskazini-magharibi mwa Uturuki. Paulo alizungumza hadi saa sita usiku. Kijana aliyeitwa Eutiko alikuwa ameketi dirishani akisikiliza. Lakini akasinzia na kuanguka chini kutoka ghorofa ya tatu. Huenda tabibu Luka ndiye aliyekuwa wa kwanza kufika chini na kumfanyia uchunguzi: Eutiko hakuwa amejeruhiwa tu au kupoteza fahamu—alikuwa amekufa! Paulo alipofika chini aliukumbatia mwili wa kijana huyo, kisha akatangaza hivi kwa furaha: ‘Yuko hai.’ Bila shaka tukio hilo liliwaimarisha sana wale waliolishuhudia! Walijua kabisa kwamba kijana huyo alikuwa amekufa na kwamba sasa alikuwa amefufuliwa, hivyo ‘walifarijiwa kupita kiasi.’—Mdo. 20:7-12. w17.12 5 ¶10-11