Jumapili, Mei 10
Je, kuna yeyote anayeweza kuwazuia hawa . . . wasibatizwe kwa maji?—Mdo. 10:47.
Ni nini kilichomsaidia Kornelio kubatizwa? Tunasoma kwamba “[alimwogopa] Mungu, yeye pamoja na watu wote wa nyumba yake.” Na Kornelio aliomba dua sikuzote kwa Mungu. (Mdo. 10:2) Petro alipomtangazia Kornelio habari njema, yeye na familia yake walimkubali Kristo, na wakabatizwa bila kukawia. (Mdo. 10:47, 48) Bila shaka, Kornelio alikuwa tayari kufanya mabadiliko yoyote yaliyohitajika ili yeye na familia yake waweze kumwabudu Yehova. (Yos. 24:15; Mdo. 10:24, 33) Kama Sauli, Kornelio angeweza kuruhusu cheo chake kimzuie kuwa Mkristo. Lakini hakuruhusu jambo hilo limzuie. Je, utahitaji kufanya mabadiliko makubwa maishani mwako ili ustahili kubatizwa? Ikiwa ndivyo, Yehova atakuwa Msaidizi wako. Atabariki azimio lako la kumtumikia kulingana na kanuni za Biblia. w25.03 5 ¶12-13
Jumatatu, Mei 11
Kataa hadithi za uwongo zisizo na heshima.—1 Tim. 4:7.
Ukisikia habari za uwongo kuhusu tengenezo la Yehova au ndugu wanaoongoza, kumbuka jinsi maadui wa Mungu walivyomtendea Yesu na wanafunzi wa karne ya kwanza. Leo, watu wa Yehova wanateswa na kusingiziwa mambo ya uwongo kama tu Biblia ilivyotabiri. (Mt. 5:11, 12) Hatutaamini habari za uwongo ikiwa tutatambua chanzo cha habari hizo na kuchukua hatua za kujilinda haraka iwezekanavyo. Tunapaswa kuchukua hatua gani? Kataa habari za uwongo. Mtume Paulo alitupatia maagizo yaliyo wazi ya mambo ya kufanya tunaposikia habari za uwongo. Paulo alimwambia Timotheo kwamba ‘awaamuru watu fulani wasisikilize hadithi za uwongo’ na ‘wakatae hadithi za uwongo zisizo na heshima.’ (1 Tim. 1:3, 4) Tunakataa habari za uwongo kwa sababu tunajua chanzo cha habari hizo. Hivyo, tunasikiliza tu “maneno yenye manufaa” ya kweli.—2 Tim. 1:13. w24.04 11 ¶16; 13 ¶17
Jumanne, Mei 12
Kwa maneno laini na maneno ya kusifusifu wao huishawishi mioyo ya wasiotambua.—Rom. 16:18.
Endelea kushirikiana kwa umoja na wale ambao ni washikamanifu kwa Yehova. Mungu anataka tumwabudu kwa umoja. Tutaendelea kuwa na umoja ikiwa tutashikamana na kweli. Yeyote anayeeneza habari zinazopingana na ile kweli anasababisha migawanyiko kutanikoni, hivyo Mungu anatuonya ‘tujiepushe nao.’ La sivyo, sisi pia tunaweza kupeperushwa mbali na kweli. (Rom. 16:17) Tunapoitambua kweli na kushikamana nayo kabisa, tutaendelea kuwa karibu na Yehova na kuimarisha imani yetu. (Efe. 4:15, 16) Tutalindwa dhidi ya mafundisho ya uwongo na propaganda za Shetani, na tutaendelea kuwa salama chini ya utunzaji wa Yehova wakati wa dhiki kuu. Endeleeni kushikamana sana na ukweli, “na Mungu wa amani atakuwa pamoja nanyi.”—Flp. 4:8, 9. w24.07 13 ¶16-17