SURA YA 15
Yesu ‘Aimarisha Haki Duniani’
1, 2. Yesu alikasirika pindi gani, na kwa nini?
YESU alikuwa amekasirika sana, na alikuwa na sababu nzuri ya kufanya hivyo. Huenda ikawa vigumu kuwazia kwamba Yesu ambaye alikuwa mpole sana angeweza kukasirika. (Mathayo 21:5) Bila shaka, alijizuia kwa kuwa hasira yake ilikuwa yenye uadilifu.a Lakini ni nini kilichomkasirisha mwanamume huyo aliyependa amani? Alikasirishwa na ukosefu mkubwa wa haki.
2 Yesu alilipenda sana hekalu la Yerusalemu. Lilikuwa jengo pekee takatifu ulimwenguni pote lililowekwa wakfu kwa ajili ya ibada ya Baba yake wa mbinguni. Wayahudi walisafiri kutoka nchi nyingi za mbali ili kuabudu huko. Hata watu wa Mataifa waliomwogopa Mungu, walikuja katika ua wa hekalu uliotengwa kwa ajili yao. Lakini mapema katika huduma yake, Yesu aliingia hekaluni na kuona hali yenye kusikitisha sana. Hekalu lilikuwa kama soko badala ya kuwa nyumba ya ibada. Umati mkubwa wa wafanyabiashara na wale waliobadili pesa ulijaa hekaluni. Kwa nini huo ulikuwa ukosefu wa haki? Watu hao waliona hekalu la Mungu kuwa mahali pa kuwalaghai watu—hata kuwaibia. Jinsi gani?—Yohana 2:14.
3, 4. Ni ulaghai gani ulioendelea katika nyumba ya Yehova, na Yesu alichukua hatua gani kuukomesha?
3 Viongozi wa kidini walikuwa wameamua kwamba ni aina moja tu ya sarafu ingeweza kutumiwa kulipa kodi ya hekalu. Wageni walilazimika kubadili pesa zao ili kupata sarafu hizo. Kwa hiyo, wale waliobadili pesa walifanya kazi hiyo hekaluni, na walitoza malipo fulani kwa ajili ya kubadili pesa. Biashara ya kuuza wanyama ilileta faida kubwa pia. Wageni waliotaka kutoa dhabihu wangeweza kununua wanyama kutoka kwa mfanyabiashara yeyote jijini, lakini kulikuwa na uwezekano wa wakuu wa hekalu kukataa dhabihu hizo kwa kusema kwamba hazifai. Hata hivyo, walikubali mara moja wanyama wa dhabihu walionunuliwa hekaluni. Nyakati nyingine watu hao wasio na uwezo waliuziwa wanyama kwa bei ghali sana.b Biashara hiyo ilikuwa mbaya kuliko ulaghai. Huo ulikuwa wizi!
4 Yesu hakuweza kuvumilia ukosefu huo wa haki. Hiyo ilikuwa nyumba ya Baba yake! Alitengeneza mjeledi wa kamba akafukuza makundi ya ng’ombe na kondoo kutoka hekaluni. Kisha, akazipindua meza za waliobadili pesa. Hebu wazia, jinsi sarafu hizo zote zilivyotawanyika kwenye sakafu ya marumaru! Akawaamuru hivi kwa ukali waliokuwa wakiuza njiwa: “Ondoeni vitu hivi hapa!” (Yohana 2:15, 16) Inaonekana kwamba hakuna yeyote aliyethubutu kumpinga mwanamume huyo jasiri.
“Ondoeni vitu hivi hapa!”
Mwana Humwiga Baba
5-7. (a) Maisha ya Yesu kabla ya kuwa mwanadamu yaliboreshaje sifa yake ya haki, na mfano wake unatufundisha nini? (b) Yesu alishughulikiaje ukosefu wa haki ambao Shetani aliusababisha, na atafanyaje hivyo wakati ujao?
5 Bila shaka, wafanyabiashara hao walirudi hekaluni. Miaka mitatu hivi baadaye, Yesu aliwafukuza tena kutoka hekaluni. Wakati huu alimnukuu Yehova ambaye aliwakemea wale waliofanya nyumba Yake kuwa “pango la wanyang’anyi.” (Yeremia 7:11; Mathayo 21:13) Ndiyo, Yesu alipoona wafanyabiashara wenye pupa wakiwaibia watu na hekalu la Mungu likitiwa unajisi, alihisi kama Baba yake. Hilo halitushangazi kwa sababu Yesu alifundishwa na Baba yake wa mbinguni kwa mamilioni ya miaka. Hivyo, akawa na maoni kama ya Yehova kuhusu haki. Alionyesha kikweli jinsi ambavyo mwana anamwiga kabisa baba yake. Kwa hiyo, ikiwa tunataka kuelewa vizuri zaidi haki ya Yehova, tunahitaji kutafakari mfano wa Yesu Kristo.—Yohana 14:9, 10.
6 Mwana huyo mzaliwa pekee alikuwapo Shetani alipomsingizia Yehova Mungu kuwa mwongo na kutilia shaka uadilifu wa utawala Wake. Huo ulikuwa uchongezi mbaya sana! Mwana huyo pia alimsikia Shetani akidai baadaye kwamba hakuna mwanadamu anayeweza kumtumikia Yehova kwa sababu anampenda na bila ubinafsi. Kwa kweli, mashtaka hayo ya uwongo yalimuumiza Mwana huyo mwadilifu. Bila shaka, alifurahi sana alipojua kwamba angetimiza kazi muhimu sana ya kufutilia mbali mashtaka hayo ya uwongo! (2 Wakorintho 1:20) Angefanyaje hivyo?
7 Kama tulivyojifunza katika Sura ya 14, Yesu Kristo alijibu kikamili na kwa uhakika dai la Shetani ambalo lilitilia shaka uaminifu wa viumbe wa Yehova. Kwa kufanya hivyo, Yesu aliweka msingi wa kuliondolea suto jina takatifu la Mungu, Yehova—kutia ndani uwongo wa kwamba njia yake ya kutawala ina kasoro. Akiwa Wakili Mkuu wa Yehova, Yesu atahakikisha kwamba haki ya Yehova inatelekezwa ulimwenguni pote. (Matendo 5:31) Kupitia maisha yake duniani, Yesu alionyesha kwamba Mungu ana haki. Yehova alisema hivi kumhusu: “Nitaweka roho yangu juu yake, naye atayatangazia mataifa haki.” (Mathayo 12:18) Yesu alitimizaje maneno hayo?
Yesu Afafanua “Haki”
8-10. (a) Mapokeo ya viongozi wa dini ya Kiyahudi yaliwadharau wanawake na watu wasio Wayahudi jinsi gani? (b) Mapokeo yaliifanyaje sheria ya Yehova kuhusu Sabato iwe yenye kulemea?
8 Yesu aliipenda Sheria ya Yehova, naye aliishi kupatana nayo. Lakini viongozi wa kidini wa siku zake waliipotosha Sheria hiyo na kuitumia vibaya. Yesu aliwaambia hivi: “Ole wenu, waandishi na Mafarisayo wanafiki! . . . Mmepuuza mambo mazito zaidi ya Sheria, yaani, haki, rehema, na uaminifu.” (Mathayo 23:23) Ni wazi kabisa kwamba walimu hao wa Sheria ya Mungu hawakuwa wakifundisha waziwazi “haki” ni nini. Badala yake, walikuwa wakiipotosha haki ya Mungu. Jinsi gani? Fikiria mifano kadhaa.
9 Yehova aliwaagiza watu wake wajitenge na mataifa jirani ya kipagani. (1 Wafalme 11:1, 2) Hata hivyo, viongozi fulani washupavu wa kidini waliwatia watu moyo wawachukie watu wote wasio Wayahudi. Mishnah ilikuwa na sheria hii: “Ngo’mbe hawapaswi kuachwa kwenye hoteli ya watu wasio Wayahudi kwa sababu wanashukiwa kufanya ngono na wanyama.” Chuki yao kwa watu wote wasio Wayahudi ilikiuka haki na kusudi la Sheria ya Musa. (Mambo ya Walawi 19:34) Sheria nyingine zilizotungwa na wanadamu ziliwadharau wanawake. Mapokeo yalisema kwamba mke anapaswa kutembea nyuma ya mume wake wala si kando yake. Mwanamume hakuruhusiwa kuongea na mwanamke hadharani, hata iwe ni mke wake. Wanawake hawakuruhusiwa kutoa ushahidi mahakamani kama tu ilivyokuwa kwa watumwa. Hata kulikuwa na sala maalumu ambayo wanaume walitoa na kumshukuru Mungu kwamba hawakuwa wanawake.
10 Viongozi hao wa kidini walitunga sheria na maagizo mengi sana hivi kwamba ilikuwa vigumu kwa watu kuelewa Sheria ya Mungu. Kwa mfano, sheria ya Sabato ilikataza kazi isifanywe siku ya Sabato. Siku hiyo ilitengwa kwa ajili ya ibada na kupumzika. Lakini Mafarisayo waliifanya sheria hiyo iwe yenye kulemea. Walidai kwamba walikuwa na haki ya kuamua mambo hususa ambayo yangeonwa kuwa “kazi.” Walitaja shughuli 39 kuwa kazi, kama vile kuvuna au kuwinda. Mambo hayo yalizusha maswali mengi sana. Je, mtu aliyemwua kiroboto siku ya Sabato, alikuwa akiwinda? Je, mtu aliyevunja nafaka kidogo ili ale akitembea, alikuwa akivuna? Je, mtu aliyemponya mgonjwa, alikuwa akifanya kazi? Walitunga sheria nyingi ngumu ambazo zilijibu maswali hayo.
11, 12. Yesu alipingaje mapokeo yasiyo ya kimaandiko ya Mafarisayo?
11 Katika hali hizo, Yesu aliwasaidiaje watu kuelewa maana ya haki? Kwa ujasiri, Yesu aliwashutumu viongozi hao wa kidini kupitia mafundisho na maisha yake. Tuchunguze baadhi ya mafundisho yake. Alikemea waziwazi sheria zao nyingi zilizotungwa na wanadamu aliposema hivi: “Mnalibatilisha neno la Mungu kwa mapokeo yenu ambayo mlipewa.”—Marko 7:13.
12 Yesu alifundisha kwamba Mafarisayo hawakuelewa sheria ya Sabato—na hata hawakufahamu kusudi la sheria hiyo. Aliwaambia kwamba Masihi ni “Bwana wa Sabato” na hivyo alikuwa na haki ya kuwaponya watu siku ya Sabato. (Mathayo 12:8) Alikazia jambo hilo waziwazi kwa kuwaponya watu kimuujiza siku ya Sabato. (Luka 6:7-10) Uponyaji huo ulionyesha yale ambayo atafanya duniani pote wakati wa Utawala wake wa Miaka Elfu Moja. Miaka hiyo Elfu Moja itakuwa Sabato kuu, wakati ambapo hatimaye wanadamu wote waaminifu watapumzika baada ya kulemewa na dhambi na kifo kwa karne nyingi sana.
13. Ni sheria gani iliyoanza mwishoni mwa huduma ya Kristo duniani, na ilitofautianaje na Sheria ya Musa?
13 Yesu alionyesha wazi lililo haki kupitia sheria mpya, “sheria ya Kristo,” ambayo ilianza mwishoni mwa huduma yake duniani. (Wagalatia 6:2) Tofauti na Sheria ya Musa, sheria hii mpya ilitegemea hasa kanuni badala ya amri nyingi zilizoandikwa. Hata hivyo, ilitia ndani amri fulani za moja kwa moja. Yesu aliita mojawapo ya amri hizo “amri mpya.” Yesu aliwafundisha wafuasi wake wote wapendane kama alivyowapenda. (Yohana 13:34, 35) Ndiyo, wote wanaoishi kulingana na “sheria ya Kristo” wangekuwa na upendo huo wa kujidhabihu.
Mfano Halisi wa Haki
14, 15. Yesu alionyeshaje kwamba alitambua mipaka ya mamlaka yake, na kwa nini hilo linatia moyo?
14 Yesu hakuwafundisha watu kuhusu upendo tu. Aliishi kupatana na “sheria ya Kristo.” Alionyesha hilo kupitia maisha yake. Fikiria njia tatu ambazo mfano wa Yesu ulionyesha wazi lililo haki.
15 Kwanza, Yesu aliepuka kabisa ukosefu wa haki. Labda umeona kwamba mara nyingi watu wasio wakamilifu hutenda isivyo haki wanapokuwa na kiburi na kuvuka mipaka ya mamlaka yao. Yesu hakufanya hivyo. Pindi moja, mtu fulani alimfuata Yesu na kumwambia: “Mwalimu, mwambie ndugu yangu tugawane urithi.” Yesu alimjibuje? “Ni nani aliyeniweka niwe mwamuzi au mpatanishi kati yenu wawili?” (Luka 12:13, 14) Je, hilo si jambo lenye kustaajabisha? Uwezo wa Yesu wa kufikiri na kufanya maamuzi, na hata mamlaka aliyopewa na Mungu ilizidi mamlaka ya mtu yeyote duniani; lakini, alikataa kuingilia jambo hilo kwa sababu hakuwa amepewa mamlaka hususa ya kufanya hivyo. Sikuzote, Yesu amekuwa mnyenyekevu hata kabla ya kuwa mwanadamu. (Yuda 9) Kwa unyenyekevu, Yesu humtumaini Yehova aamue lililo haki na hilo linaonyesha kwamba ana sifa zinazovutia.
16, 17. (a) Yesu alionyeshaje haki alipohubiri habari njema za Ufalme wa Mungu? (b) Yesu alionyeshaje kwamba haki yake ilikuwa yenye rehema?
16 Pili, Yesu alionyesha haki alipohubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. Hakuwa na ubaguzi. Badala yake, alijitahidi sana kuwahubiria watu wa kila aina, hata iwe ni matajiri au maskini. Tofauti na Yesu, Mafarisayo waliwapuuza maskini na kuwaita kwa dharau ʽam-ha·ʼaʹrets, yaani, “watu wa ardhi.” Kwa ujasiri, Yesu alipinga ukosefu huo wa haki. Alipowafundisha watu habari njema, alipokula nao, alipowalisha, alipowaponya, au hata kuwafufua, aliunga mkono haki ya Mungu ambaye anataka “watu wa namna zote” waokolewe.c—1 Timotheo 2:4.
17 Tatu, Yesu alionyesha haki yenye rehema nyingi. Alijitahidi sana kuwasaidia watenda dhambi. (Mathayo 9:11-13) Alikuwa tayari kuwasaidia watu ambao hawangeweza kujilinda. Kwa mfano, Yesu hakuwa kama viongozi wa kidini ambao waliwatilia shaka watu wa Mataifa. Aliwasaidia na kuwafundisha baadhi yao kwa rehema, hata ingawa alitumwa hasa kwa Wayahudi. Alikubali kumponya kimuujiza mtumishi wa ofisa mmoja wa jeshi la Roma, na kusema: “Sijaona mtu yeyote katika Israeli mwenye imani kubwa kama hii.”—Mathayo 8:5-13.
18, 19. (a) Ni katika njia zipi Yesu aliwaheshimu wanawake? (b) Mfano wa Yesu unatusaidiaje kuona uhusiano uliopo kati ya ujasiri na haki?
18 Yesu hakuunga mkono maoni yaliyoenea kuhusu wanawake. Badala yake kwa ujasiri alitenda yaliyo haki. Wanawake Wasamaria walionwa kuwa wasio safi kama watu wa Mataifa. Hata hivyo, Yesu hakusita kumhubiria mwanamke Msamaria kwenye kisima cha Sikari. Kwa kweli, Yesu alijitambulisha waziwazi kwa mara ya kwanza kuwa Masihi aliyeahidiwa alipoongea na mwanamke huyo. (Yohana 4:6, 25, 26) Mafarisayo walisema kwamba wanawake hawakupaswa kufundishwa Sheria ya Mungu, lakini Yesu alitumia wakati mwingi na nguvu kuwafundisha wanawake. (Luka 10:38-42) Na ingawa mapokeo yalisema kwamba wanawake hawawezi kutoa ushahidi unaoaminika, Yesu aliwaheshimu wanawake kadhaa kwa kuwapa nafasi ya pekee ya kuwa watu wa kwanza kumwona baada ya kufufuliwa. Hata aliwatuma wakawaeleze wanafunzi wake ambao ni wanaume habari za tukio hilo muhimu sana!—Mathayo 28:1-10.
19 Yesu alionyesha mataifa maana ya haki. Mara nyingi, alihatarisha uhai wake kwa kufanya hivyo. Mfano wa Yesu unatusaidia kuona kwamba mtu anahitaji ujasiri ili kutetea haki ya kweli. Ndiyo sababu kwa kufaa aliitwa “Simba wa kabila la Yuda.” (Ufunuo 5:5) Kumbuka kwamba simba ni mfano unaofaa wa haki yenye ujasiri. Hivi karibuni, Yesu atatekeleza haki kwa njia kubwa zaidi, ataimarisha “haki duniani” kikamili zaidi.—Isaya 42:4.
Mfalme wa Kimasihi ‘Aimarisha Haki Duniani’
20, 21. Katika siku zetu, Mfalme wa Kimasihi ametekelezaje haki duniani pote na katika kutaniko la Kikristo?
20 Tangu alipowekwa kuwa Mfalme wa Kimasihi mwaka wa 1914, Yesu ametekeleza haki duniani. Jinsi gani? Amehakikisha kwamba unabii aliotoa kwenye Mathayo 24:14 unatimizwa. Wafuasi wa Yesu duniani wamewafundisha watu wa nchi zote kweli kuhusu Ufalme wa Yehova. Kama Yesu, wamehubiri bila ubaguzi na kwa njia ya haki, wakijitahidi kumpa kila mtu—vijana kwa wazee, matajiri kwa maskini, wanaume kwa wanawake—nafasi ya kumjua Yehova, Mungu wa haki.
21 Yesu, ambaye ni Kichwa cha kutaniko la Kikristo, anatekeleza haki kutanikoni pia. Kama ilivyotabiriwa, anatoa “wanaume kuwa zawadi,” yaani, wazee Wakristo walio waaminifu wanaoliongoza kutaniko. (Waefeso 4:8-12) Wanaume hao, wanafuata mfano wa Yesu Kristo katika kutekeleza haki wanapolichunga kundi la Mungu lenye thamani sana. Sikuzote wanakumbuka kwamba Yesu anataka kondoo wake watendewe kwa haki bila kujali cheo, umaarufu, au hali yao ya kiuchumi.
22. Yehova anahisije kuhusu ukosefu wa haki ulioenea ulimwenguni leo, na amemchagua Mwana wake achukue hatua gani?
22 Hata hivyo, hivi karibuni Yesu ataimarisha haki duniani kwa njia isiyo na kifani. Ukosefu wa haki umeenea sana katika ulimwengu huu wenye ufisadi. Kila mtoto anayekufa njaa, hufa kwa sababu ya ukosefu wa haki usiovumilika hasa tunapozingatia kwamba pesa nyingi sana na wakati hutumiwa kutengeneza silaha za vita na kutosheleza tamaa zenye ubinafsi za watu wanaopenda raha. Mamilioni ya watu wanaokufa bila sababu kila mwaka ni mojawapo tu ya mambo mengi yanayoonyesha ukosefu wa haki uliopo. Mambo hayo yote huchochea hasira ya Yehova ya uadilifu. Amemchagua Mwana wake apigane vita vya haki dhidi ya mfumo huu mwovu wa mambo na kukomesha kabisa ukosefu wote wa haki.—Ufunuo 16:14, 16; 19:11-15.
23. Baada ya Har–Magedoni, Kristo ataletaje haki kwa umilele wote?
23 Lakini ili kutekeleza haki Yehova anahitaji kufanya mengi zaidi kuliko kuwaangamiza tu waovu. Amemweka rasmi Mwana wake atawale akiwa “Mkuu wa Amani.” Baada ya vita ya Har–Magedoni, utawala wa Yesu utaleta amani duniani kote, naye atatawala “kupitia haki.” (Isaya 9:6, 7) Kisha, Yesu atafurahia kukomesha ukosefu wote wa haki ambao umesababisha mateso na maumivu mengi sana ulimwenguni. Atadumisha kwa uaminifu haki kamilifu ya Yehova kwa umilele wote. Basi, ni muhimu kwetu kujitahidi kuiga haki ya Yehova sasa. Tuone jinsi tunavyoweza kufanya hivyo.
a Kwa kuonyesha hasira kuelekea ukosefu wa haki, Yesu alimwiga Yehova, aliye “tayari kuonyesha ghadhabu yake” kuelekea uovu wote. (Nahumu 1:2) Kwa mfano, baada ya Yehova kuwaambia watu wake walioasi kwamba walikuwa wamefanya nyumba yake kuwa “pango la wanyang’anyi,” alisema hivi: “Hasira yangu na ghadhabu yangu zitamwagwa juu ya mahali hapa.”—Yeremia 7:11, 20.
b Mishnah inasema kwamba miaka kadhaa baadaye watu walilalamika kwa sababu njiwa waliuzwa kwa bei ghali sana hekaluni. Muda mfupi baadaye, bei ikapunguzwa kufikia asilimia 99! Ni nani waliopata faida kubwa kutokana na biashara hiyo yenye ufanisi? Wanahistoria fulani wanadokeza kwamba masoko ya hekaluni yalimilikiwa na ukoo wa Anasi, Kuhani Mkuu. Ukoo huo ulipata utajiri mkubwa sana kutokana na masoko hayo.—Yohana 18:13.
c Mafarisayo waliamini kwamba watu wa hali ya chini, ambao hawakujua Sheria, walikuwa watu “waliolaaniwa.” (Yohana 7:49) Walisema kwamba mtu hakupaswa kuwafundisha watu hao, kufanya biashara, kula, au kusali pamoja nao. Walisema mtu akimruhusu binti yake aolewe na mmoja wao lingekuwa jambo baya kuliko kumpeleka kwa wanyama wakali sana. Waliamini kwamba watu hao wa hali ya chini hawatafufuliwa.