SURA YA PILI
“Njia na Kweli na Uzima”
“Uwe mfuasi wangu”
1, 2. Kwa nini tunahitaji msaada ili kumfikia Yehova, na Yesu Kristo ametuandalia msaada gani?
JE, UMEWAHI kupotea? Huenda ukafikiria kuhusu siku ambayo ulipotea ulipokuwa ukienda kumtembelea rafiki yako au mtu wa ukoo. Ukiwa katika barabara usiyoijua, je, ulisimama na kumwomba mtu fulani akuonyeshe njia? Ungehisije ikiwa mtu mwenye fadhili, badala tu ya kukuonyesha njia, angekuambia: “Nifuate, nitakupeleka mpaka huko”! Ungefurahi sana, sivyo?
2 Tunaweza kusema kwamba Yesu Kristo anatufanyia jambo kama hilo. Tunahitaji msaada ili kumfikia Mungu. Kwa sababu ya dhambi waliyorithi na kutokamilika, wanadamu wamepotea, “wametenganishwa na uzima ambao ni wa Mungu.” (Waefeso 4:17, 18) Tunahitaji msaada ili kumjua Mungu na kupata kibali chake. Yesu, Kielelezo chetu, ambaye ni mwenye fadhili, hatushauri tu na kutuelekeza, bali anafanya mengi zaidi. Kama tulivyoona katika Sura ya 1, Yesu anatualika, akisema: ‘Njoo uwe mfuasi wangu.’ (Marko 10:21) Isitoshe, anatupatia sababu inayotuchochea kuukubali mwaliko huo. Pindi moja Yesu alisema: “Mimi ndiye njia na kweli na uzima. Hakuna mtu anayekuja kwa Baba bila kupitia kwangu.” (Yohana 14:6) Acheni tuzungumzie, kwa nini haiwezekani kumfikia Baba isipokuwa kupitia Mwana tu. Kisha, kwa kutegemea sababu hizo tutaona jinsi ambavyo Yesu ndiye “njia na kweli na uzima.”
Jukumu Muhimu Katika Kusudi la Yehova
3. Kwa nini tunaweza kumfikia Mungu kupitia Yesu tu?
3 Kwanza kabisa, tunaweza kumfikia Mungu kupitia Yesu tu kwa sababu Yehova ameona inafaa kumpa Mwana wake jukumu la pekee.a Baba amemtumia kwa njia kubwa zaidi kutimiza mambo yote aliyokusudia. (2 Wakorintho 1:20; Wakolosai 1:18-20) Ili kuelewa jukumu la pekee la Mwana huyo, tunahitaji kujikumbusha mambo yaliyotukia katika bustani ya Edeni, ambako wenzi wa kwanza wa ndoa walijiunga na Shetani kumwasi Yehova.—Mwanzo 2:16, 17; 3:1-6.
4. Uasi uliotokea katika Edeni ulitokeza suala gani, naye Yehova aliamua kufanya nini ili kujibu suala hilo?
4 Uasi uliotokea katika Edeni ulitokeza suala lililohusisha viumbe wote wa Mungu: Je, yule anayeitwa Yehova ni mtakatifu, mwema, mwadilifu, na mwenye upendo katika njia zake zote? Ili kujibu suala hilo muhimu, Yehova aliamua kumtuma duniani mwana wake mkamilifu wa kiroho. Mwana huyo alikuwa na mgawo muhimu sana. Alipaswa kufa ili kulitakasa jina la Baba yake na kuwa fidia ya kuwaokoa wanadamu. Kwa kuendelea kuwa mwaminifu mpaka kifo, mwana huyo aliyechaguliwa angefungua njia ya kuondoa matatizo yote yaliyosababishwa na uasi wa Shetani. (Waebrania 2:14, 15; 1 Yohana 3:8) Lakini Yehova alikuwa na mamilioni ya wana wa roho walio wakamilifu. (Danieli 7:9, 10) Alimchagua nani kati yao atimize mgawo huo muhimu sana? Yehova alimchagua “Mwana wake mzaliwa pekee,” ambaye baadaye alijulikana kama Yesu Kristo.—Yohana 3:16.
5, 6. Yehova alionyesha jinsi gani kwamba anamwamini Mwana wake, na msingi wa imani hiyo ulikuwa nini?
5 Je, tunapaswa kushangazwa na uamuzi wa Yehova? Hapana! Baba alimwamini kabisa Mwana wake mzaliwa pekee. Karne nyingi kabla ya Mwana wake kuja hapa duniani, Yehova alitabiri kwamba Mwana huyo angeendelea kuwa mshikamanifu licha ya mateso ambayo angekabili. (Isaya 53:3-7, 10-12; Matendo 8:32-35) Fikiria maana ya jambo hilo. Kama viumbe wengine wote wenye akili, Mwana huyo alikuwa na uhuru wa kuchagua, naye angeweza kujiamulia mwenyewe jambo la kufanya. Hata hivyo, Yehova alimwamini sana hivi kwamba angeweza kutabiri uaminifu wa Mwana wake. Kwa nini alimwamini Yesu? Kwa sababu anamjua. Yehova anamjua vizuri Mwana wake na anajua kwamba Mwana wake anataka sana kumpendeza. (Yohana 8:29; 14:31) Mwana huyo anampenda Baba yake, naye Yehova anampenda Mwana Wake. (Yohana 3:35) Upendo kati ya Baba na Mwana unawafanya wawe na kifungo cha muungano na kutumainiana kabisa.—Wakolosai 3:14.
6 Kwa kuwa Mwana ana jukumu la pekee sana, naye Baba anamwamini sana, na wana upendo unaowaunganisha, basi haishangazi kwamba ni Yesu tu ndiye njia ya kumfikia Mungu. Hata hivyo, kuna sababu nyingine inayoonyesha kwa nini Mwana tu ndiye anayeweza kutuongoza kwa Baba.
Ni Mwana Tu Anayemjua Baba Vizuri
7, 8. Kwa nini Yesu hakukosea aliposema kwamba hakuna anayemjua Baba “isipokuwa Mwana”?
7 Ili kumfikia Yehova, ni lazima tutimize matakwa fulani. (Zaburi 15:1-5) Ni nani mwingine isipokuwa Mwana, anayejua vizuri zaidi jinsi ya kutimiza matakwa ya Mungu na kupata kibali Chake? Yesu alisema: “Baba yangu amenikabidhi vitu vyote, na hakuna mtu anayemjua Mwana kikamili isipokuwa Baba; wala hakuna anayemjua Baba kikamili isipokuwa Mwana, na yeyote ambaye Mwana anapenda kumfunulia.” (Mathayo 11:27) Acheni tuone kwa nini Yesu hakukosea wala kutia chumvi aliposema kwamba hakuna anayemjua Baba vizuri “isipokuwa Mwana.”
8 Kwa kuwa yeye ndiye “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote,” Mwana huyo ana uhusiano wa pekee pamoja na Yehova. (Wakolosai 1:15) Fikiria uhusiano huo wa karibu sana uliositawi kati ya Baba na Mwana kwa miaka mingi ambayo walikuwa peke yao, tangu mwanzo wa uumbaji mpaka viumbe wengine wa roho walipoumbwa! (Yohana 1:3; Wakolosai 1:16, 17) Fikiria pia pendeleo la pekee ambalo Mwana huyo alipata alipokuwa pamoja na Baba yake, akijifunza kutoka kwa Baba yake na kuelewa mapenzi yake, viwango, na njia zake. Kwa kweli, kusema kwamba Yesu anamjua Baba vizuri kuliko mtu mwingine yeyote, si kutia chumvi. Bila shaka, uhusiano huo wa karibu ulimwezesha Yesu kueleza mambo mengi kumhusu Baba yake kwa njia ambazo hakuna mtu mwingine angeweza.
9, 10. (a) Ni katika njia gani Yesu alitusaidia kumfahamu Baba yake? (b) Tunapaswa kufanya nini ili tupate kibali cha Yehova?
9 Mafundisho ya Yesu yalionyesha kwamba alijua kabisa maoni na hisia za Yehova na mambo anayotaka waabudu Wake wafanye.b Yesu alitusaidia tumjue Baba yake katika njia nyingine ya pekee. Yesu alisema: “Yeyote ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.” (Yohana 14:9) Yesu alimwiga Baba yake kikamili katika kila jambo alilosema na kutenda. Kwa hiyo, tunaposoma kumhusu Yesu katika Biblia, iwe tunasoma maneno yenye kuchochea na yenye kuvutia aliyotumia alipokuwa akifundisha, au jinsi alivyochochewa na huruma kuwaponya wengine na kutokwa na machozi, tunaweza kumwazia Yehova mwenyewe akisema na kutenda mambo hayohayo. (Mathayo 7:28, 29; Marko 1:40-42; Yohana 11:32-36) Maneno na matendo ya Mwana yanaonyesha kikamili njia na mapenzi ya Baba. (Yohana 5:19; 8:28; 12:49, 50) Kwa hiyo, ili tupate kibali cha Yehova, tunapaswa kutii mafundisho ya Yesu na kufuata mfano wake.—Yohana 14:23.
10 Kwa kuwa Yesu anamjua Yehova vizuri na anamwiga kikamili, haishangazi kwamba Yehova ameamua Mwana awe njia ya kumfikia Baba. Baada ya kuzungumzia kwa nini tunaweza kumfikia Yehova kupitia Yesu tu, acheni sasa tuzungumzie maana ya maneno haya ya Yesu: “Mimi ndiye njia na kweli na uzima. Hakuna mtu anayekuja kwa Baba bila kupitia kwangu.”—Yohana 14:6.
“Mimi Ndiye Njia”
11. (a) Kwa nini tunaweza kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu kupitia Yesu tu? (b) Andiko la Yohana 14:6 linakazia jinsi gani cheo cha pekee cha Yesu? (Ona maelezo ya chini.)
11 Tayari tumejifunza kwamba hatuwezi kumfikia Mungu isipokuwa kupitia Yesu. Fikiria jinsi sisi tunavyohusika. Yesu ndiye “njia” katika maana ya kwamba ni kupitia yeye tu tunaweza kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu. Kwa nini? Kwa kuwa alikuwa mwaminifu mpaka kifo, Yesu alitoa uhai wake uwe dhabihu ya fidia. (Mathayo 20:28) Bila fidia hiyo, hatuwezi kumfikia Mungu. Dhambi inawazuia wanadamu wasimfikie Mungu, kwa kuwa Yehova ni mtakatifu naye hawezi kukubali dhambi. (Isaya 6:3; 59:2) Lakini dhabihu ya Yesu iliondolea mbali kizuizi hicho; ilifunika dhambi, au kutupatanisha na Mungu. (Waebrania 10:12; 1 Yohana 1:7) Tukiukubali mpango huo wa Mungu kupitia Kristo na kuuamini, tunaweza kupata kibali cha Yehova. Hakuna njia nyingine ya ‘kupatanishwa na Mungu.’c—Waroma 5:6-11.
12. Yesu “ndiye njia” katika maana gani?
12 Yesu “ndiye njia” ya kumfikia Mungu katika sala. Ni kupitia Yesu tu tunaweza kumfikia Yehova katika sala tukiwa na uhakika kwamba maombi yetu ya kutoka moyoni yatasikiwa vizuri. (1 Yohana 5:13, 14) Yesu mwenyewe alisema: “Mkimwomba Baba jambo lolote, atawapa katika jina langu. . . . Ombeni nanyi mtapewa, ili shangwe yenu iwe kamili.” (Yohana 16:23, 24) Kwa hiyo, kupitia jina la Yesu, tunaweza kumfikia Yehova katika sala na kumwita “Baba yetu.” (Mathayo 6:9) Yesu “ndiye njia” katika maana nyingine—kupitia mfano wake. Kama ilivyotajwa hapo awali, Yesu alimwiga Baba yake kikamili. Hivyo, mfano wa Yesu unaonyesha jinsi tunavyoweza kuishi kwa njia itakayompendeza Yehova. Basi ili kumfikia Yehova, ni lazima tutembee katika hatua za Yesu.—1 Petro 2:21.
“Mimi Ndiye . . . Kweli”
13, 14. (a) Yesu alisema kweli kwa njia gani? (b) Ili Yesu awe “kweli” alipaswa kufanya nini, na kwa nini?
13 Nyakati zote, Yesu alisema kweli kuhusu neno la kinabii la Baba yake. (Yohana 8:40, 45, 46) Udanganyifu haukupatikana kinywani mwa Yesu. (1 Petro 2:22) Hata wale waliompinga walikubali kwamba alifundisha “njia ya Mungu kupatana na kweli.” (Marko 12:13, 14) Hata hivyo, Yesu aliposema “Mimi ndiye . . . kweli,” hakumaanisha tu kwamba alisema kweli alipozungumza, alipohubiri, na kufundisha, bali, Yesu alifundisha kweli katika njia nyingine pia.
14 Kumbuka kwamba miaka mingi kabla ya Yesu kuja duniani, Yehova alitumia roho yake kuwaongoza waandikaji wa Biblia waandike unabii mwingi kumhusu Masihi, au Kristo. Unabii huo ulitabiri mambo mbalimbali kuhusu maisha, huduma, na kifo chake. Isitoshe, Sheria ya Musa ilitia ndani unabii ambao Masihi angetimiza. (Waebrania 10:1) Je, Yesu angeendelea kuwa mwaminifu mpaka kifo, na hivyo kutimiza mambo yote yaliyotabiriwa kumhusu? Kufanya hivyo kungethibitisha kwamba Yehova ni Mungu wa unabii wa kweli. Yesu ndiye aliyekuwa na jukumu hilo zito. Kupitia maisha yake, yaani, kila neno alilosema na kila jambo alilofanya, Yesu alionyesha kwamba mambo yaliyotabiriwa kumhusu yalikuwa kweli. (2 Wakorintho 1:20) Kwa hiyo, Yesu alikuwa “kweli.” Tunaweza kusema kwamba Neno la Yehova la kinabii lilithibitika kuwa kweli Yesu alipokuja duniani.—Yohana 1:17; Wakolosai 2:16, 17.
“Mimi Ndiye . . . Uzima”
15. Inamaanisha nini kumwamini Mwana, na kufanya hivyo kutatuwezesha kupata nini?
15 Yesu ndiye “uzima,” kwa kuwa ni kupitia yeye tu tunaweza kupata uzima, “uzima ulio wa kweli.” (1 Timotheo 6:19) Biblia inasema: “Yule anayemwamini Mwana ana uzima wa milele; yule asiyemtii Mwana hataona uzima, bali ghadhabu ya Mungu hukaa juu yake.” (Yohana 3:36) Inamaanisha nini kumwamini Mwana wa Mungu? Inamaanisha kuamini kwamba hatuwezi kupata uzima bila yeye. Pia, inamaanisha kuonyesha imani yetu kwa matendo, kuendelea kujifunza kutoka kwa Yesu, na kufanya yote tuwezayo kufuata mafundisho yake na mfano wake. (Yakobo 2:26) Hivyo, kumwamini Mwana wa Mungu kunatuwezesha kupata uzima wa milele. “Kundi dogo” la Wakristo waliotiwa mafuta litapata uhai wa kiroho usioweza kufa mbinguni, nao “umati mkubwa” wa “kondoo wengine” utapata uhai mkamilifu wa kibinadamu katika paradiso duniani.—Luka 12:32; 23:43; Ufunuo 7:9-17; Yohana 10:16.
16, 17. (a) Yesu atakuwa “uzima” jinsi gani hata kwa wale ambao tayari wamekufa? (b) Tunaweza kuwa na uhakika gani?
16 Namna gani wale ambao tayari wamekufa? Yesu ni “uzima” kwao pia. Muda mfupi kabla ya kumfufua rafiki yake, Lazaro, Yesu alimwambia hivi Martha, dada ya Lazaro: “Mimi ndiye ufufuo na uzima. Yule anayeniamini, hata akifa, ataishi tena.” (Yohana 11:25) Yehova amempa Mwana wake uwezo wa kufufua kwa kumpa “funguo za kifo na za Kaburi.” (Ufunuo 1:17, 18) Yesu aliyetukuzwa atatumia funguo hizo kufungua malango ya kaburi na hivyo kuwaachilia wote walio humo.—Yohana 5:28, 29.
17 “Mimi ndiye njia na kweli na uzima.” Kupitia maneno hayo, Yesu alionyesha kusudi la maisha na huduma yake duniani. Maneno hayo ni muhimu sana kwetu leo. Kumbuka kwamba baada ya kusema maneno hayo, Yesu alisema hivi: “Hakuna mtu anayekuja kwa Baba bila kupitia kwangu.” (Yohana 14:6) Maneno ya Yesu ni ya kweli leo kama tu yalivyokuwa alipoyasema. Hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba tukimfuata Yesu, kamwe hatutapotea. Ni yeye tu anayeweza kutuonyesha njia ya kumfikia “Baba.”
Utafanya Nini?
18. Kuwa wafuasi wa kweli wa Yesu kunatia ndani nini?
18 Kwa kuwa Yesu ana jukumu la pekee na anamjua Baba vizuri kuliko mtu mwingine yeyote, tuna sababu nzuri ya kumfuata Mwana huyo. Kama tulivyoona katika sura iliyotangulia, kuwa wafuasi wa kweli wa Yesu kunatia ndani matendo, si maneno au hisia tu. Kumfuata Kristo hutia ndani kuishi kulingana na mafundisho na mfano wake. (Yohana 13:15) Kitabu hiki kinaweza kukusaidia kufanya hivyo.
19, 20. Kitabu hiki kina habari gani zinazoweza kukusaidia kumfuata Kristo?
19 Katika sura zinazofuata, tutachunguza kwa makini maisha na huduma ya Yesu. Sura hizo zimegawanywa katika sehemu tatu. Kwanza, tutazungumzia sifa na njia zake. Kisha, tutachunguza jinsi alivyohubiri na kufundisha kwa bidii. Halafu, tutaona jinsi alivyoonyesha upendo. Kuanzia Sura ya 3, kuna sanduku la kufundisha lenye kichwa: “Unawezaje Kumfuata Yesu?” Maandiko na maswali yaliyo katika sanduku hilo yamekusudiwa kutusaidia kutafakari jinsi tunavyoweza kumwiga Yesu katika neno na tendo.
20 Yehova Mungu ametuandalia msaada ili tusipotee, au kutenganishwa naye kwa sababu ya dhambi tuliyorithi. Ingawa ilimgharimu sana, Yehova alionyesha upendo wake alipomtuma Mwana wake atuonyeshe njia ya kuwa na uhusiano mzuri pamoja Naye. (1 Yohana 4:9, 10) Upendo huo mkubwa na ukuchochee kuupokea na kuukubali mwaliko wa Yesu: “Njoo uwe mfuasi wangu.”—Yohana 1:43.
a Jukumu la Mwana ni la pekee sana hivi kwamba Biblia inampa majina mbalimbali ya kinabii na ya cheo.—Ona sanduku “Baadhi ya Majina ya Cheo ya Yesu Kristo.”
b Kwa mfano, ona maneno ya Yesu yaliyo katika Mathayo 10:29-31; 18:12-14, 21-35; 22:36-40.
c Kwenye Yohana 14:6, maneno “mimi ndiye” yanakazia cheo cha pekee cha Yesu, kwamba yeye ndiye njia. Tunaweza kumfikia Baba kupitia kwake tu.