Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • cf sura 6 kur. 65-76
  • “Alijifunza Kutii”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Alijifunza Kutii”
  • ‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mambo Yaliyomchochea Yesu Kutii
  • “Hakufanya Dhambi”
  • “Sikuzote Mimi Hufanya Mambo Yanayompendeza”
  • Thawabu za Kuwa Watiifu Kama Kristo
  • “Watoto, Watiini Wazazi Wenu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Yehova Anathamini Utii Wako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Jifunze Utii kwa Kukubali Nidhamu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Utii Je, Ni Somo Muhimu Utotoni?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
Pata Habari Zaidi
‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
cf sura 6 kur. 65-76

SURA YA SITA

“Alijifunza Kutii”

1, 2. Kwa nini baba mwenye upendo anafurahi anapomwona mwana wake akimtii, na hisia zake zinaonyeshaje hisia za Yehova?

BABA anasimama dirishani na kumtazama mwana wake akicheza na rafiki zake. Mpira wao unadunda na kwenda barabarani. Mvulana huyo anautazama mpira huo na anatamani kwenda kuuchukua. Rafiki yake mmoja anamhimiza akimbie kwenda barabarani ili auchukue. Hata hivyo, mvulana huyo anatikisa kichwa chake na kusema: “Siruhusiwi kufanya hivyo.” Baba yake anafurahi.

2 Kwa nini baba huyo amefurahi? Kwa sababu alimwambia mwana wake asiende barabarani akiwa peke yake. Mvulana huyo anapotii, ingawa hajui kwamba baba yake anamtazama, baba yake anajua kwamba mwana wake anajifunza kutii na hivyo atakuwa salama. Baba huyo anahisi kama Baba yetu wa mbinguni, Yehova anavyohisi. Mungu anajua kwamba ili tuendelee kuwa waaminifu na kuwa na wakati ujao mzuri ambao ametuahidi, ni lazima tujifunze kumtegemea na kumtii. (Methali 3:5, 6) Ndiyo sababu alimtumia mwalimu bora zaidi kati ya walimu wote wa kibinadamu ili atusaidie kujifunza kuhusu hilo.

3, 4. Ni katika njia gani Yesu “alijifunza kutii” na “kufanywa kuwa mkamilifu”? Toa mfano.

3 Biblia inasema jambo fulani lenye kushangaza kumhusu Yesu: “Ingawa alikuwa mwana, alijifunza kutii kutokana na mateso yaliyompata. Na baada ya kufanywa kuwa mkamilifu, akawa na daraka la wokovu wa milele kwa ajili ya wote wanaomtii.” (Waebrania 5:8, 9) Mwana huyo alikuwa ameishi mbinguni kwa miaka mingi. Alimwona Shetani na malaika wenzake wakiasi, lakini Mwana huyo mzaliwa wa kwanza hakuwaunga mkono. Unabii ulioongozwa na roho ulisema hivi kumhusu: “Sikuwa mwasi.” (Isaya 50:5) Ikiwa Yesu alimtii Baba yake sikuzote, maneno “alijifunza kutii” yalimhusuje? Kiumbe huyo mkamilifu angefanywa “kuwa mkamilifu” jinsi gani?

4 Fikiria mfano huu. Askari ana upanga wa chuma. Ingawa haujatumiwa vitani, umetengenezwa vizuri. Hata hivyo, anabadilisha upanga huo na kutumia mwingine uliotengenezwa kwa chuma kigumu zaidi. Upanga huo wa pili tayari umetumiwa sana vitani. Je, hilo si jambo la hekima? Vivyo hivyo, Yesu alimtii Baba yake kikamili kabla ya kuja duniani. Lakini baada ya kukaa hapa duniani, utii wake ukawa tofauti kabisa. Ulijaribiwa, uliimarishwa, na kuthibitishwa kwa majaribu ambayo Yesu hangekabili akiwa mbinguni.

5. Kwa nini Yesu alihitaji kuonyesha utii, nasi tutachunguza nini katika sura hii?

5 Utii ulikuwa sifa muhimu ambayo Yesu alihitaji alipokuja duniani. Akiwa “Adamu wa mwisho,” Yesu alikuja kufanya kile ambacho mzazi wetu wa kwanza alishindwa kufanya, yaani, kuendelea kuwa mtiifu kwa Yehova Mungu, hata chini ya jaribu. (1 Wakorintho 15:45) Hata hivyo, utii wa Yesu haukuwa wa kulazimishwa. Yesu alitii kwa akili, moyo, na nafsi yake yote. Naye alifanya hivyo kwa shangwe. Kufanya mapenzi ya Baba yake lilikuwa jambo muhimu kwake kuliko kula! (Yohana 4:34) Ni nini kitakachotusaidia kuiga utii wa Yesu? Kwanza acheni tuchunguze mambo yaliyomchochea kutii. Kuchochewa na mambo hayo kutatusaidia kupinga vishawishi na kufanya mapenzi ya Mungu. Kisha, tutazungumzia baadhi ya baraka tutakazopata kwa kuonyesha utii kama wa Kristo.

Mambo Yaliyomchochea Yesu Kutii

6, 7. Ni mambo gani yaliyomchochea Yesu kutii?

6 Utii wa Yesu ulitokana na mambo yaliyokuwa moyoni mwake. Kama tulivyoona katika Sura ya 3, Kristo alikuwa mnyenyekevu moyoni. Kiburi hufanya watu wachukie kutii, lakini unyenyekevu unatusaidia kumtii Yehova kwa hiari. (Kutoka 5:1, 2; 1 Petro 5:5, 6) Isitoshe, utii wa Yesu ulitokana na yale aliyopenda na pia, yale aliyochukia.

7 Zaidi ya yote, Yesu alimpenda Yehova, Baba yake wa mbinguni. Katika Sura ya 13, upendo huo utazungumziwa kwa undani zaidi. Upendo huo ulimchochea Yesu kumwogopa Mungu. Alimpenda na kumheshimu sana Yehova, Baba yake, hivi kwamba aliogopa kumkasirisha. Kumwogopa Mungu ni sababu moja iliyofanya sala za Yesu zisikilizwe vizuri. (Waebrania 5:7) Pia, kumwogopa Yehova ni jambo moja linaloonekana wazi katika utawala wa Yesu akiwa Mfalme wa Kimasihi.​—Isaya 11:3.

Ndugu wawili wamesimama mbele ya bango linalotangaza sinema yenye jeuri. Ndugu mmoja amekunja uso na mwingine ameinua mkono na kugeukia upande mwingine.

Je, burudani unayochagua inaonyesha kwamba unachukia lililo baya?

8, 9. Kama ilivyotabiriwa, Yesu alihisije kuhusu uadilifu na uovu, naye alionyeshaje hisia hizo?

8 Kumpenda Yehova kunatia ndani kuchukia mambo ambayo anachukia. Kwa mfano, ona unabii huu unaomhusu Mfalme wa Kimasihi: “Ulipenda uadilifu na kuchukia uovu. Ndiyo sababu Mungu, Mungu wako, amekutia mafuta kwa mafuta ya kushangilia kuliko wenzako.” (Zaburi 45:7) Wale wanaotajwa kuwa ‘wenzake’ na Yesu ni wale wafalme wengine katika ukoo wa Mfalme Daudi. Yesu alipotiwa mafuta, alikuwa na sababu ya kushangilia zaidi kuliko wale wafalme wengine. Kwa nini? Kwa sababu thawabu yake ni kubwa kuliko yao, na faida za ufalme wake ni nyingi kuliko zile za falme zao. Anapewa thawabu kwa sababu kupenda uadilifu na kuchukia uovu kulimchochea amtii Mungu katika mambo yote.

9 Yesu alionyeshaje hisia zake kuhusu uadilifu na uovu? Kwa mfano, Yesu alihisije wafuasi wake walipotii maagizo yake katika kazi ya kuhubiri na hivyo kupata baraka? Alijawa na shangwe. (Luka 10:1, 17, 21) Na watu wa Yerusalemu walipokosa kutii tena na tena, na kukataa jitihada zake zenye upendo za kuwasaidia, Yesu alihisije? Alilia kwa sababu ya uasi wa jiji hilo. (Luka 19:41, 42) Yesu alipendezwa sana na mwenendo mzuri na kuchukizwa na mwenendo mbaya.

10. Tunahitaji kusitawisha hisia gani kuhusu matendo ya uadilifu na matendo mabaya, na ni nini kitakachotusaidia kufanya hivyo?

10 Kutafakari kuhusu hisia za Yesu kunatusaidia kuchunguza nia yetu ya kumtii Yehova. Ingawa sisi si wakamilifu, tunaweza kujizoeza kupenda mema kutoka moyoni na kuchukia kabisa mwenendo mbaya. Tunahitaji kusali kwa Yehova, na kumwomba atusaidie kusitawisha hisia kama zake na za Mwana wake. (Zaburi 51:10) Wakati huohuo, tunapaswa kuepuka mambo yanayoweza kudhoofisha hisia zetu kuhusu mema na mabaya. Ili tufanikiwe kufanya hivyo tunapaswa kuchagua burudani na marafiki kwa uangalifu. (Methali 13:20; Wafilipi 4:8) Tukichochewa na mambo yaliyomchochea Kristo, hatutamtii Yehova kidesturi tu. Tutatenda mema kwa sababu tunapenda kufanya hivyo. Tutaepuka kutenda mabaya, si kwa sababu tunaogopa kugunduliwa, bali kwa sababu tunachukia mwenendo huo.

“Hakufanya Dhambi”

11, 12. (a) Yesu alikabili hali gani mapema katika huduma yake? (b) Shetani alianza kumshawishi Yesu jinsi gani, naye alitumia njia gani za ujanja?

11 Mapema katika huduma yake, Yesu alijaribiwa kuhusiana na kuchukia dhambi. Baada ya kubatizwa, alikaa nyikani kwa siku 40 mchana na usiku bila chakula. Mwishoni mwa kipindi hicho, Shetani alikuja kumshawishi. Ona jinsi Ibilisi alivyotumia ujanja.​—Mathayo 4:1-11.

12 Shetani alianza kwa kusema: “Ikiwa wewe ni mwana wa Mungu, yaambie mawe haya yawe mikate.” (Mathayo 4:3) Yesu alihisije baada ya kufunga kwa muda mrefu? Biblia inasema wazi: ‘Alihisi njaa.’ (Mathayo 4:2) Kwa hiyo, Shetani alitumia tamaa ya asili ya kutaka kula, na inaonekana alingoja kimakusudi mpaka Yesu alipokuwa dhaifu kimwili. Fikiria pia maneno haya ambayo Shetani alitumia kumdhihaki: “Ikiwa wewe ni mwana wa Mungu.” Shetani alijua kwamba Yesu ni “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote.” (Wakolosai 1:15) Hata hivyo, Yesu hakumruhusu Shetani amchochee kuasi. Yesu alijua kwamba si mapenzi ya Mungu atumie nguvu zake kwa sababu za ubinafsi. Alikataa kufanya hivyo, akionyesha kwamba anamtegemea Yehova kwa unyenyekevu ili amtegemeze na kumwongoza.​—Mathayo 4:4.

13-15. (a) Shetani alimshawishi Yesu katika njia gani nyingine mbili, na Yesu alitendaje? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba Yesu alihitaji kuwa macho sikuzote dhidi ya Shetani?

13 Katika kishawishi cha pili, Shetani alimpeleka Yesu juu ya mnara wa hekalu. Shetani alilitumia Neno la Mungu vibaya na kwa ujanja, akimshawishi Yesu afanye tamasha la kujionyesha kwa kujirusha chini kutoka kwenye mnara huo ili malaika wamwokoe. Ikiwa umati uliokuwa hekaluni ungeona muujiza huo, je, baada ya kisa hicho kuna mtu yeyote ambaye angejaribu kutilia shaka kwamba Yesu ni Masihi aliyeahidiwa? Na ikiwa umati ungemkubali Yesu kuwa Masihi kwa sababu ya muujiza huo, je, Yesu hangekuwa ameepuka matatizo mengi? Huenda. Lakini Yesu alijua kwamba Yehova alitaka Masihi afanye kazi yake kwa unyenyekevu, bali si kuwashawishi watu wamwamini kwa kufanya tamasha kubwa. (Isaya 42:1, 2) Kwa mara nyingine tena, Yesu alikataa kumwasi Yehova. Hakushawishiwa na mtego wa umashuhuri.

14 Vipi kuhusu mtego wa mamlaka? Katika kishawishi chake cha tatu, Shetani aliahidi kumpa Yesu falme zote za ulimwengu ikiwa tu Yesu angefanya tendo moja la kumwabudu. Je, Yesu alitua na kufikiria kuhusu ahadi hiyo ya Shetani? Hapana. Alimjibu: “Nenda zako, Shetani!” Kisha akaongeza: “Kwa maana imeandikwa, ‘Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.’” (Mathayo 4:10) Hakuna jambo ambalo lingeweza kumshawishi Yesu aabudu mungu mwingine. Hakuna ahadi yoyote ya kupata mamlaka au uwezo katika ulimwengu huu ambayo ingeweza kumshawishi afanye tendo lolote la uasi.

15 Je, Shetani alikubali kushindwa? Aliondoka alipofukuzwa na Yesu. Hata hivyo, Injili ya Luka inasema kwamba Ibilisi ‘alimwacha mpaka wakati mwingine unaofaa.’ (Luka 4:13) Bila shaka, Shetani angepata nafasi nyingine za kumjaribu na kumshawishi Yesu, hadi mwisho wa maisha yake hapa duniani. Biblia inatuambia kwamba Yesu ‘alijaribiwa katika mambo yote.’ (Waebrania 4:15) Kwa hiyo, Yesu alihitaji kuwa macho sikuzote; nasi tunapaswa kufanya vivyo hivyo.

16. Shetani anatumia njia gani kuwashawishi watumishi wa Mungu leo, nasi tunawezaje kupinga hila zake?

16 Shetani anaendelea kuwashawishi watumishi wa Mungu hata leo. Inasikitisha kwamba kutokamilika kwetu kunafanya iwe rahisi kushambuliwa. Kwa ujanja, Shetani anatumia mwelekeo wetu wa kuwa na ubinafsi, kiburi, na tamaa ya mamlaka. Akitumia mtego wa kufuatia vitu vya kimwili, Shetani anaweza hata kutumia mambo yote hayo kwa wakati mmoja! Ni muhimu kujichunguza kwa unyoofu mara kwa mara. Tunapaswa kutafakari maneno ya 1 Yohana 2:15-17. Tunapofanya hivyo, tunaweza kujiuliza ikiwa tamaa za kimwili za mfumo huu wa mambo, tamaa ya mali, na tamaa ya kuwapendeza wengine imedhoofisha kwa kiasi fulani upendo wetu kwa Baba yetu wa mbinguni. Tunahitaji kukumbuka kwamba ulimwengu huu utaangamizwa, na pia mtawala wake, Shetani. Na tukatae kabisa hila zake za kutushawishi tutumbukie katika dhambi! Acheni tuchochewe na Bwana wetu, kwa maana “hakufanya dhambi.”​—1 Petro 2:22.

“Sikuzote Mimi Hufanya Mambo Yanayompendeza”

17. Yesu alihisije kuhusu kumtii Baba yake, lakini huenda wengine wakadai nini?

17 Kutii kunatia ndani mengi zaidi kuliko kuepuka dhambi; Kristo alitimiza amri zote za Baba yake. Alisema hivi: “Sikuzote mimi hufanya mambo yanayompendeza.” (Yohana 8:29) Utii huo ulimletea Yesu shangwe nyingi. Bila shaka, wengine wanaweza kudai kwamba haikuwa vigumu kwa Yesu kutii. Huenda wakafikiri kwamba alipaswa kumtii Yehova tu, ambaye ni mkamilifu, ilhali sisi tunalazimika kuwatii wanadamu wasio wakamilifu walio na mamlaka. Hata hivyo, ukweli ni kwamba, Yesu alikuwa mtiifu kwa wanadamu wasio wakamilifu waliokuwa na mamlaka.

18. Yesu aliweka mfano gani kuhusu utii alipokuwa kijana?

18 Alipokuwa akikua, Yesu alikuwa chini ya mamlaka ya Yosefu na Maria, wazazi wake wa kibinadamu ambao hawakuwa wakamilifu. Inawezekana kwamba angeweza kuona makosa ya wazazi wake hata kuliko watoto wengine. Je, aliasi na kuvuka mipaka iliyowekwa na Mungu kwa ajili ya watoto na kuanza kuwaambia jinsi ya kusimamia familia? Ona jinsi andiko la Luka 2:51 linavyosema kumhusu Yesu, alipokuwa na umri wa miaka 12: “Akaendelea kuwatii.” Kwa kutii, aliwawekea mfano mzuri vijana Wakristo, ambao wanawatii wazazi wao na kuwapa heshima wanayostahili.​—Waefeso 6:1, 2.

19, 20. (a) Yesu alikabili hali gani zisizo za kawaida zilizofanya isiwe rahisi kuwatii wanadamu wasio wakamilifu? (b) Kwa nini Wakristo wa kweli leo wanapaswa kuwatii wale wanaoongoza miongoni mwao?

19 Inapohusu kuwatii wanadamu wasio wakamilifu, Yesu alikabili hali fulani ngumu ambazo Wakristo wa kweli leo hawatakabili kamwe. Fikiria hali zisizo za kawaida ambazo zilikuwapo nyakati alizoishi. Kwa muda mrefu, Yehova alikuwa ameukubali mfumo wa mambo wa dini ya Kiyahudi pamoja na hekalu lake huko Yerusalemu na ukuhani wake. Hata hivyo, baada ya muda mfupi, mfumo huo ungeondolewa mbali na mahali pake pangechukuliwa na mpango wa kutaniko la Kikristo. (Mathayo 23:33-38) Hata hivyo, viongozi wengi wa dini walikuwa wakifundisha uwongo uliotokana na falsafa ya Kigiriki. Ufisadi ulikuwa umeenea sana hekaluni hivi kwamba Yesu aliliita “pango la wanyang’anyi.” (Marko 11:17) Je, Yesu alikataa kwenda hekaluni na kwenye masinagogi? Hapana! Bado Yehova alikuwa akitumia mipango hiyo. Mpaka wakati Mungu alipochukua hatua na kufanya mabadiliko, Yesu aliendelea kutii kwa kwenda katika sinagogi na kuhudhuria sherehe hekaluni.​—Luka 4:16; Yohana 5:1.

20 Ikiwa Yesu alikuwa mtiifu chini ya hali hizo, bila shaka Wakristo wa kweli wanapaswa kuwa watiifu hata zaidi leo! Tunaishi katika hali tofauti kabisa, katika enzi zilizotabiriwa zamani sana ambapo ibada safi ingerudishwa. Mungu anatuhakikishia kwamba hatamruhusu Shetani awapotoshe watu wake waliorudishwa. (Isaya 2:1, 2; 54:17) Ni kweli kwamba katika kutaniko la Kikristo tunakabiliana na dhambi na watu ambao si wakamilifu. Lakini, je, tunapaswa kuyatumia makosa ya wengine kuwa kisingizio cha kutomtii Yehova, labda kwa kutohudhuria mikutano ya Kikristo au kuwachambua wazee? Hatupaswi kufanya hivyo! Badala yake, tunawaunga mkono kwa moyo wote wale wanaoongoza kutanikoni. Tunatii kwa kuhudhuria mikutano na makusanyiko ya Kikristo na kutumia mashauri ya Kimaandiko tunayopata katika pindi hizo.​—Waebrania 10:24, 25; 13:17.

Ndugu na dada wakizungumza nje ya Jumba la Ufalme huku wakiwa na furaha.

Tunamtii Yehova tunapotumia mambo tunayojifunza katika mikutano ya Kikristo

21. Yesu alifanya nini wanadamu walipomshawishi asimtii Mungu, naye alituwekea mfano gani?

21 Yesu hakuwaruhusu watu au hata rafiki zake wenye nia njema, wamzuie kumtii Yehova. Kwa mfano, mtume Petro alijaribu kumsadikisha Bwana wake kwamba haikuwa lazima ateseke na kufa. Ingawa Petro hakuwa na nia mbaya alipomshauri Yesu ajitendee kwa fadhili, Yesu alikataa kabisa shauri hilo lisilofaa. (Mathayo 16:21-23) Leo, wafuasi wa Yesu hukabiliana na watu wa ukoo ambao, ingawa hawana nia mbaya, wanaweza kujaribu kuwashawishi wasitii sheria na kanuni za Mungu. Kama ilivyokuwa kwa wafuasi wa Yesu wa karne ya kwanza, msimamo wetu ni kwamba “lazima tumtii Mungu kuwa mtawala badala ya wanadamu.”​—Matendo 5:29.

Thawabu za Kuwa Watiifu Kama Kristo

22. Yesu alijibu swali gani, na jinsi gani?

22 Yesu alipokaribia kufa, utii wake ulijaribiwa zaidi. Katika siku hiyo ngumu na yenye majonzi “alijifunza kutii” kikamili. Alifanya mapenzi ya Baba yake, si mapenzi yake. (Luka 22:42) Kwa kufanya hivyo, alituwekea mfano mzuri wa utimilifu. (1 Timotheo 3:16) Alijibu swali lililotokezwa miaka mingi iliyopita: Je, mwanadamu mkamilifu anaweza kuendelea kumtii Yehova anapojaribiwa? Adamu na Hawa walishindwa kumtii Mungu. Kisha Yesu akaja, na kupitia maisha na kifo chake akajibu swali hilo. Yule aliye mkuu zaidi kati ya viumbe wote wa Yehova alitii hata wakati ambapo utii ulifanya ateseke sana na hata kufa.

23-25. (a) Kuna uhusiano gani kati ya utii na utimilifu? Toa mfano. (b) Sura inayofuata itazungumzia nini?

23 Utimilifu, au kujitoa kwa Yehova kwa moyo wote, unaonyeshwa kupitia utii. Kwa kuwa Yesu alitii, aliendelea kuwa mtimilifu na hivyo akawanufaisha wanadamu wote. (Waroma 5:19) Yehova alimthawabisha Yesu kwa njia kubwa sana. Tukimtii Bwana wetu, Kristo, Yehova atatuthawabisha pia. Kumtii Kristo kunatuwezesha kupata “wokovu wa milele.”​—Waebrania 5:9.

24 Isitoshe, utimilifu wenyewe ni thawabu. Methali 10:9 inasema: “Anayetembea kwa utimilifu atatembea kwa usalama.” Kila tendo la utii ni muhimu. Fikiria kuhusu hili: Tunaweza kumlinganisha mtu ambaye ni mwaminifu kwa Yehova na jengo kubwa maridadi lililojengwa kwa matofali imara. Kila wakati mtu anapomtii Yehova mtu huyo anaongeza tofali lingine kwenye ukuta wa jengo hilo. Mtu anaweza kufikiri kwamba tofali moja halina umuhimu, lakini kila tofali lina sehemu yake na kazi yake. Na matofali mengi yanapounganishwa pamoja, jengo lenye thamani hata zaidi linatokezwa. Matendo ya utii yanapowekwa pamoja, siku baada ya siku na mwaka baada ya mwaka, tunajenga nyumba yenye kupendeza ya utimilifu wetu.

25 Utii wa muda mrefu unatukumbusha sifa nyingine, yaani, uvumilivu. Sifa hiyo ya Yesu itazungumziwa katika sura inayofuata.

Unawezaje Kumfuata Yesu?

  • Baadhi ya amri za Kristo ni zipi, tunawezaje kuzitii, nasi tutapata baraka gani kwa kuzitii?​—Yohana 15:8-19.

  • Mwanzoni, watu wa ukoo wa Yesu walikuwa na maoni gani kuhusu huduma yake, na tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi alivyoshughulika nao?​—Marko 3:21, 31-35.

  • Kwa nini hatupaswi kuogopa kwamba tukimtii Yehova tutakosa furaha maishani?​—Luka 11:27, 28.

  • Tunaweza kujifunza nini kutokana na utayari wa Yesu wa kutii sheria ambayo haikuwa lazima aitii?​—Mathayo 17:24-27.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki