Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w73 10/1 kur. 443-448
  • “Ukitumia kwa Halali Neno la Kweli”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Ukitumia kwa Halali Neno la Kweli”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MIFANO FULANI
  • EPUKA KUYAPOTOSHA MAANDIKO KUSUDI UHAKIKISHE JAMBO FULANI
  • MAANA YA MAANDIKO MARA NYINGI IMEFICHWA KATIKA HABARI INAYOZUNGUKA
  • KUTUMIA ANDIKO LA UNABII KWA HALALI
  • Je, Unalitumia Neno la Mungu Sawasawa?
    Huduma Yetu ya Ufalme—1996
  • Tumia kwa Ustadi “Upanga wa Roho”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Kutumia Maandiko Vizuri
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • ‘Tumia Sawasawa Neno la Mungu’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
w73 10/1 kur. 443-448

“Ukitumia kwa Halali Neno la Kweli”

“Jitahidi kujionyesha kuwa umekubaliwa na Mungu, mtenda kazi asiye na sababu ya kutahayari, ukitumia kwa halali neno la kweli.”​—2 Tim. 2:15.

1. Neno la Mungu linafananishwa na nini, na kwa hiyo imetupasa tuwe na nia gani tunapolitumia?

NENO la Mungu li hai na ni lenye uwezo katika maisha zetu. Kama upanga, linaweza kuigawanya nafsi na roho. (Ebr. 4:12) Linaingia katika akili zetu kwa sababu ya tunayofanya. Linapambanua kati ya tunavyoweza kuonekana kama nafsi iliyo hai, na namna tulivyo kweli kweli katika moyo wetu, katika nia yetu na katika roho yetu. Kwa maana Neno la Mungu linafananishwa na upanga, imetupasa tuhakikishe tunalitumia kwa ujuzi. Imetupasa tuwe wenye uangalifu kwamba hatukitumii chombo hicho cha kukatia kwa njia mbaya, lakini, kama vile Paulo alivyoonya, kwamba tukitumie “kwa halali.” Tunaposoma na kujifunza Neno la Mungu imetupasa tufanye hivyo kwa njia ambayo tutapata maana iliyo ya kweli na ufahamu mzuri wa ambayo linasema.

2. Haitupasi tuioneje Biblia, na kwa hiyo ni maulizo gani yangefaa tunaposoma sehemu fulani ya Maandiko?

2 Mara nyingi habari inayozunguka mstari tunaoweza kusoma itatusaidia kuufahamu na kuutumia inavyofaa. Imetupasa tukumbuke kwamba Biblia si mkusanyo wa mistari iliyotenganishwa, isiyolingana, iliyokusanywa pamoja kwa bahati, na inayofaa kutumiwa kwa njia yo yote kuhakikisha jambo tunaloweza kuona ni sawa. Bali, inatupasa tuupate ufahamu wote tunapolisoma Neno la Mungu. Imetupasa tujiulize nani anayesema, anasema kwa nani, juu ya jambo gani na kama andiko li juu ya habari ya namna yake peke yake. Hili ni la maana ikiwa ‘tutalitumia neno la kweli kwa halali.’

MIFANO FULANI

3. Ni habari gani ya msingi inayomsaidia mtu kuelewa 2 Timotheo 2:15 inavyofaa?

3 Kwa mfano, ebu na tuyaangalie maneno ya Paulo kwa Timotheo katika 2 Timotheo 2:15. Hapo anasema: “Jitahidi kujionyesha kuwa umekubaliwa na Mungu, mtenda kazi asiye na sababu ya kutahayari, ukitumia kwa halali neno la kweli.” Maneno haya aliandikiwa mtu aliyekuwa na msingi mzuri katika kweli ya Mungu na aliyekuwa anafanya mapenzi ya Mungu. Twajua hivi kwa sababu ya aliyoyaandika Paulo kwa Timotheo hapo mapema, kama yalivyoandikwa katika mwanzo wa barua hii. Kwa Timotheo, Paulo alisema: “Nikiikumbuka imani uliyo nayo isiyo na unafiki, ambayo ilikaa kwanza katika bibi yako Loisi, na katika mama yako Eunike, nami nasadiki wewe nawe unayo.” (2 Tim. 1:1, 2, 5) Katika maneno yake yaliyoandikwa katika 2 Timotheo 2:15, Paulo alikuwa akimwambia Timotheo namna ya kuwapa Wakristo maagizo, wale ambao walikuwa sehemu ya kundi la Mungu. Ijapokuwa ni kweli kwamba imempasa Mkristo alitumie neno la kweli sawasawa anapozungumza na wasioamini, Paulo hapa hakuwa akimwambia Timotheo namna ya kuwageuza wasioamini kwenye Ukristo. Hii ni wazi kutokana na ambayo Paulo alimwambia yeye juu ya kufundisha kwake: “Kama vile nilivyokusihi ukae Efeso, nilipokuwa nikisafiri kwenda Makedonia, ili uwakataze wengine wasifundishe elimu nyingine.” Hapa ni wazi kwamba wengine ndani ya kundi la Kikristo walikuwa wakifundisha mafundisho tofauti, hawakuwa ‘wakilitumia neno la kweli kwa halali.’ Vile vile Paulo alimwonya Timotheo hivi: “Mambo yale uliyoyasikia kwangu mbele ya mashahidi wengi, hayo uwakabidhi watu waaminifu watakaofaa kuwafundisha na wengine.” (1 Tim. 1:3; 4:16; 2 Tim. 2:2) Tena, mtajo wa kukabidhi habari yenye maana kwa watu waaminifu ambao wanaweza kufundisha wengine vile vile katika njia inayostahili unatoa ushuhuda zaidi kwamba Timotheo alikuwa akishughulika na wale waliokuwamo ndani ya kundi la Kikristo. Ilimpasa aitumie kweli kusudi awafaidi na kuwaongoza ndugu zake.

EPUKA KUYAPOTOSHA MAANDIKO KUSUDI UHAKIKISHE JAMBO FULANI

4. (a) Onyesha ni kwa kadiri gani viongozi wa dini wanafika katika kutumia Mathayo 10:28 vibaya. (b) Ukweli ni nini wa andiko hili kama linavyofungamana na nafsi ya mwanadamu?

4 Ni lazima tuepuke kutumia andiko vibaya kwa makusudi ili tuhakikishe jambo letu. Mara nyingi viongozi wa dini wa Kristendomu ni wenye hatia ya jambo ili hili. Chukua, kwa mfano, Mathayo 10:28. Hapo twasoma: “Msiwaogope wauuao mwili, wasiweze kuiua na [nafsi]; afadhali mwogopeni yule awezaye kuangamiza mwili na [nafsi] pia katika jehanum.” Viongozi wa dini wataitaja sehemu ya kwanza ya maneno ya Yesu kuhakikisha kwamba nafsi haiwezi kufa. Je! ndivyo Yesu alivyosema kwa kweli? Huenda ikaelekea kuwa hivyo, ukiachia kusoma katikati ya mstari. Lakini ukisoma sehemu iliyobaki ya mstari utaona kwamba Yesu aliuondoa uongo wa fundisho la kutokufa kwa nafsi waziwazi aliposema kwamba imempasa mtu amwogope yeye ambaye anaweza kuangamiza vyote nafsi na mwili katika jehanum. Kwa ‘kulitumia neno la kweli kwa halali’ maana ya kweli inatangulia.

5. (a) Wengine wanatafsiri 1 Petro 4:6 namna gani? (b) Nini iliyo maana ya kweli ya mstari huo, na ni uhakika gani zaidi wa Maandiko uwezao kutaja?

5 Inayolingana sana na fundisho la kutokufa kwa nafsi ni imani ya wengine ya kwamba roho ya mwanadamu ndiyo inayoendelea kuishi na yenyewe inatendewa sawasawa na mwanadamu mwenyewe. Petro wa Kwanza 4:6 anatajwa kuyategemeza maoni haya. Hapo twasoma: “Maana kwa ajili hiyo hata hao waliokufa walihubiriwa Injili, ili kwamba wahukumiwe katika mwili kama wahukumiwavyo wanadamu; bali wawe hai katika roho kama Mungu alivyo hai.” Wanaoamini katika maoni ya kwamba roho kama kitu chenye akili kinaokoka kifo cha mwili wanashikilia kauli ya kwamba hapa Petro alihakikisha hivyo alipoitaja Injili kama ikitangazwa kwa waliokufa. Ndivyo ilivyo? Ili ‘tulitumie neno la Mungu kwa halali,’ inatupasa tuliache lijisemee lenyewe. Je! Petro hapo alikuwa akiwataja watu waliokuwa wamekufa kwa kimwili? Kwa sababu waliokufa kwa kimwili “hawajui neno lo lote” (Mhu. 9:5), wafu hawa wanaotajwa na Petro ni kama wale waliosemwa na Yesu aliposema: “Waache wafu wazike wafu wao,” na wale waliotajwa na mtume Paulo alipoandika: “Nanyi mlikuwa wafu kwa sababu ya makosa na dhambi zenu.” Ye yote anayeishi ambaye ni mfu machoni pa Yehova anaweza kuwa hai katika maana ya kiroho kwa kulisikia neno la Mungu, kutubu na kumfuata Bwana Yesu. Tumaini kwa waliokufa kwa kweli ni ufufuo na halafu nafasi ya kuzisikia habari njema na kuhukumiwa.​—Mt. 8:22; Efe. 2:1.

6. (a) Ni maelezo gani yametolewa juu ya Isaya 14:12-16? (b) Nini yaliyo maelezo ya Maandiko? (c) Kwa hivyo nani Lusiferi wa Isaya 14:12-16, naye anaonyesha nia ya nani?

6 Watu wa Yehova, vile vile, imewapasa wawe waangalifu katika matumizi ya maandiko kusudi kwamba walitoe Neno la Mungu kwa njia ifaayo katika kuhubiri kwao na utendaji wa kufundisha. Kwa mfano, yachukue maneno yanayosemwa nyakati nyingine kwamba mojawapo la majina anayopewa Shetani Ibilisi ni Lusiferi. Huenda wengine wakaelekeza kwenye Isaya 14:12-16. Kulingana na Authorized Version (King James), mstari wa kumi na mbili unasema: “Lo! jinsi ulivyoanguka kutoka mbinguni, O Lusiferi, mwana wa asubuhi! jinsi ulivyotupwa chini, uliyeyalegeza mataifa!” Neno “Lusiferi” ni tafsiri ya neno la Kiebrania heh·lelʹ, “mwenye kung’aa.” Heh·lelʹ, kama linavyotumiwa hapa, si jina la mtu wala cheo, bali, ni neno linaloeleza cheo kitukufu kilichochukuliwa na nasaba ya Babeli ya wafalme katika ukoo wa Nebukadreza. Isingekuwa sawa kusema kwamba Shetani Ibilisi ndiye anayeitwa hapa Lusiferi kana kwamba lilikuwa mojawapo la majina yake. Neno hapa linaelekeza zaidi kwa mfalme wa Babeli, kwa maana, kulingana na mstari wa nne, huu ni “usemi wa mithali juu ya mfalme wa Babeli.” Vile vile, mistari ya kumi na tano na kumi na sita ya sura hii ya kumi na nne inasema kwamba huyu “mwenye kung’aa” (Lusiferi) atashushwa katika Sheol, ambalo ndilo kaburi la kawaida la mwanadamu, si makao ya Shetani Ibilisi. Zaidi ya hayo, ukweli ni kwamba wale wanaomwona huyu “mwenye kung’aa” akiwekwa katika hali hii wanasema: “Je! huyu ndiye mtu yule aliyekuwa akiifadhaisha dunia, yeye aliyekuwa akifanya falme zitikisike?” Shetani si mwanadamu bali kiumbe kisichoonekana cha kiroho. Hivyo, ijapokuwa mfalme wa Babeli alionyesha nia ya baba yake, Ibilisi, bado neno Lusiferi halikuwa jina alilopewa Shetani Ibilisi. Kwa ‘kulitumia kwa halali neno la kweli’ tunakuwa tayari kusema misemo iliyo safi ya Mungu kama ilivyoandikwa katika kurasa za Biblia.

7. (a) Kwa sababu gani Biblia haifanyiwi udhalimu kwa kutumia inavyofaa maandiko yaliyochaguliwa kuhakikisha mambo fulani ya pekee, na tuna mfano wa nani katika kufanya hivyo? (b) Onyesha namna ambavyo mtume Paulo angaliweza kuhakikisha kwa kuyataja Maandiko ya Kiebrania kwamba Kristo alipaswa ataabike na kuinuka kutoka kwa wafu?

7 Lakini, Neno la Mungu halifanyiwi udhalimu watumishi wake wanapotumia mistari iliyochaguliwa inavyofaa kutoka katika sehemu mbalimbali za Biblia ili kuhakikisha mambo ya mafundisho. Ijapokuwa ni kweli kwamba wapinzani wa Neno la Mungu nyakati nyingine wanadai kwamba Mashahidi wanatumia maandiko yaliyo mbali mbali katika Biblia kwa upotovu kuhakikisha mambo yao, sisi twajua vema kutokana na funzo la Biblia kwamba Yesu na mitume wake walitumia mistari iliyochaguliwa kwa kuhakikisha kweli fulani za msingi. Kwa mfano, Yesu, alipokuwa akijaribiwa jangwani mwishoni mwa siku zake arobaini za kufunga, alitaja sehemu mbalimbali za Neno la Mungu kuyakanusha maneno ya Ibilisi. (Mt. 4:3-10; Kum. 8:3; 6:13, 16; 5:9) Mtume Paulo vile vile alitumia njia hii kwa Wayahudi alipokuwa akifundisha katika sinagogi. Habari katika Matendo 17:2, 3, NW, inasema: “Kwa hiyo kulingana na desturi ya Paulo akaingia kwao, na kwa sabato tatu alihojiana nao katika Maandiko, akieleza na kuhakikisha kwa mitajo kwamba ilikuwa lazima Kristo ataabike na kuinuka kutoka kwa wafu, na kusema: ‘Huyu ndiye Kristo, Yesu huyu ambaye mimi nawahubiri juu yake.’”​—Tazama Zaburi 22:7, 8; Isaya 50:6; 53:3-5; Zaburi 16:8-10.

MAANA YA MAANDIKO MARA NYINGI IMEFICHWA KATIKA HABARI INAYOZUNGUKA

8. (a) Kwa sababu gani lazima matumizi mabaya ya Maandiko yaepukwe? (b) Onyesha iliyo maana ya kweli ya Mithali 10:7, na kwa sababu gani? (c) Ni maandiko gani ambayo ingekuwa hekima kutumia katika kuzungumza wasiostahili kufufuliwa ni akina nani?

8 Hata hivyo, maandiko yanapotumiwa vibaya kwa makusudi, huko ni kufanya udhalimu mzito kwa Maandiko. Hatutaki kuwa wenye hatia ya matumizi hayo mabaya hata katika mambo makubwa zaidi ama madogo zaidi. Kwa mfano, katika kusema na mtu juu ya ufufuo tunaweza tukasema kwa wazi sana kwamba waovu hawatafufuliwa. Huenda basi tukawasomea mstari huu wa Biblia: “Kuwakumbuka wenye haki huwa na baraka; bali jina la mtu mwovu litaoza.” (Mit. 10:7) Sasa, ni kweli kwamba wale ambao Yehova anaona ni waovu sana, wasiotiwa katika wanaosaidiwa na dhabihu ya ukombozi ya Kristo Yesu, hawatafufuliwa. Lakini, Mithali 10:7 haihakikishi uamuzi huu wa Yehova. Kwa sababu gani? Wakati wa kusoma habari inayozunguka ya sura hii katika Mithali, inaonekana kwamba umewekwa mfulizo wa mambo tofauti: mwana mwenye hekima na mwana mpumbavu, mtu mwenye bidii na mvivu, mwana mwenye busara na mwana mwenye kutenda kwa aibu. Lakini ufufuo wala jehanum haizungumzwi hapo. Kwa hiyo isingefaa kusema kwamba andiko hili linazungumza juu ya jambo hilo. Bali, jambo litakalosemwa ni kwamba jina au sifa ya watu waovu si kumbukumbu nzuri, bali ni yenye kuhuzunisha, inayovunda. Kuhakikisha kwamba wengine hawatafufuliwa, ingekuwa vizuri zaidi kutaja Maandiko yanayosema juu ya jehanum, mauti ya pili.​—Mt. 23:33; Ufu. 21:8; tazama vile vile Mathayo 25:46.

9. Kwa sababu gani kusisitizia kuiangalia habari inayozunguka ya andiko hakumzuii mtu asiieleze kweli?

9 Kuhakikisha huku kwa mambo kwa kusoma na kuona maana ya habari inayozunguka hakumzuii mtu kwa njia yo yote asiieleze kweli. Bali, kunatia nguvu maneno ya mtu yenye msingi wa Biblia, kwa maana inakuwa wazi kwa wepesi kwa anayefundishwa kwamba linalofundishwa ndilo ambalo kwa kweli Biblia inasema. Biblia ni Neno lililoongozwa na roho ya Mungu Mwenye Nguvu Zote, na kujua namna yeye anavyoona mambo, kwa usaidizi wa roho takatifu, ni kufaidika kutokana na hekima ya Muumba kama inavyoonyeshwa katika Neno lake lililoandikwa. Yehova alikusudia jambo fulani alipoweka andiko fulani katika Biblia. Yeye anajua kabisa tunachohitaji na kwa hiyo anatupa kile ambacho kinatusaidia kukua kwa kiroho katika ufahamu na katika ujuzi wake wa kweli.

10, 11. (a) Ni maana gani anayoweza mtu kwa wepesi kuipa 1 Yohana 4:18? (b) Habari inayozunguka inaonyesha nini juu ya maana iliyo ya kweli? (c) Hii inakubalianaje na Zaburi 139?

10 Katika ujamaa wetu na Yehova imetupasa tuwe kama watoto wake. Tukiwa hivyo, ni kwa kadiri gani tunavyoshukuru kwa upendo wake na uangalizi kwetu sisi? Je! sisi ‘tunalitumia kwa halali neno’ kwa habari ya linavyosema juu ya sala zetu za kipekee kwake na je! tunafahamu ambavyo Neno lake linatuambia juu ya namna yeye atakavyo tumwone? Wengi wameyasoma maneno ya 1 Yohana 4:18 kwa habari ya upendo mkamilifu nao wakafanya matumizi mabaya ya maneno hayo. Hapo Biblia inasema: “Katika pendo hamna hofu; lakini pendo lililo kamili huitupa nje hofu, kwa maana hofu ina adhabu; na mwenye hofu hakukamilishwa katika pendo.” Kwa kutazama mara ya kwanza wengine wameazimia kwamba hawawezi kabisa kuwa wakamilifu katika upendo, kwa maana woga unawafanya wazunguke au kukimbia hatari wakati wo wote inapowezekana. Lakini je! hiyo ndiyo namna ya woga ambayo mtume anazungumza juu yake hapa?

11 Kusoma habari inayozunguka ya 1 Yohana 4:18 (NW) kutatusaidia kuona maana ya pekee ya mstari huu wa Andiko. Mstari uliotangulia unaonyesha kwamba mazungumzo ya Yohana ni mazungumzo yanayoendelea juu ya kuwa na “uhuru wa kusema.” Hapa hazungumzi juu ya uhuru wa kusema katika kuzihubiri habari njema za Ufalme. Bali, anazungumza juu ya uhuru wa kusema kwa habari ya usemi wa mtu kwa Mungu. Hii inaonyeshwa katika sura ya tatu ya Yohana wa Kwanza mistari ya 19-21. Kwa hiyo mtu aliye na upendo mwingi wa Mungu ndani yake anajiona yu huru kumjia Baba yake wa kimbinguni kwa matumaini yote. Hali yake ya kutokamilika na yenye dhambi haimzuii asimjie Yehova kuomba msaada katika kuyafanya mapenzi ya Yehova. Kama vile mtoto awezavyo kumjia baba mwenye upendo kwa matumaini yote kwamba baba yake atamwelewa na kumsaidia, hata anapokuwa amefanya kosa, ndivyo impasavyo mtu ajione kwa Baba yake wa kimbinguni, Yehova. Imempasa mtu awe huru kumkaribia na ugumu wo wote anaoweza kuwa nao, kuomba msaada wa kuyafanya mapenzi ya Baba yake. Haimpasi mtu awe na woga mbaya kwa Baba wa kimbinguni, kwamba Yehova atalipiza hukumu kabisa kwa kiumbe kisicho kikamilifu chenye dhambi, kwamba atamlaani mtu kabisa kwa sababu ya hali yake ya akili na moyo yenye dhambi. Hii si kusema kwamba imempasa mtu ajifurahishie kutenda mabaya kisha amwendee Baba wa kimbinguni kuomba msamaha, kwa njia hiyo akitumia rehema ya Yehova kwa njia mbaya. Lakini inamaanisha kwamba haimpasi mtu aogope kumwendea Baba yake wa kimbinguni kujaribu kunyosha kilichopotoka, kuyaondoa mawazo yake au matendo yasiyokamilika, akijua kwamba Yehova anayajua yote yampasayo kujua juu ya mtu.​—Zab. 139:1-3, 15-18, 23, 24.

12. Ufahamu unaofaa wa 1 Yohana 4:18 unatufaidije sisi kama mtu mmoja mmoja?

12 Akiwa na ufahamu huu mzuri wa 1 Yohana 4:18, mtu anakuja kuujua ubora mwingi wa ujamaa wa kiroho wa mtu na Yehova Muumba wake. Mtu anazungumza kutoka moyoni mwake na Yehova na anaomba uongozi juu ya maisha yake, kusudi kwamba yawe ya kumpendeza Yehova. Kwa hiyo ‘kukamilishwa kwetu katika upendo’ maana yake ni kwamba upendo wa Mungu ndani yetu si usiositawishwa hata kidogo, bali, kwa sababu ya upendo huu mkamilifu tunasukumwa wakati wote kufanya mapenzi yake kwa moyo wote tukiwa na matumaini yote katika Muumba wetu na Baba wa kimbinguni. Hii, nayo, inatupa uhuru katika kumkaribia kwetu Mungu kwa sala.​—Efe. 3:12; Ebr. 4:16; 1 Yohana 5:14.

KUTUMIA ANDIKO LA UNABII KWA HALALI

13. (a) Nini kilicho cha muhimu kukumbuka juu ya unabii mbalimbali wa Maandiko ya Kiebrania, na hii inaonyeshwaje kwa habari ya unabii katika Isaya 35:1, 7? (b) Utimizo wa unabii juu ya watu wa Yehova wa nyakati za kale ni uhakika kabisa wa nini?

13 Tunapojifunza Neno la Mungu na kuwa wenye kuuzoea ujumbe wake mzuri na maana yake zaidi na zaidi katika maisha zetu, tunakubali kwamba kulifahamu katika njia ambayo Yehova amekusudia kunatajirisha na kuthawabisha. Ni mara nyingi kama nini tulipotaja katika unabii mbalimbali wa Maandiko ya Kiebrania juu ya baraka zinazowangoja wanadamu katika taratibu mpya yenye haki ya Mungu, na kwa haki hivyo! Lakini huenda tukawa tumeshindwa mara nyingi kuona kwamba mwingi wa unabii mbalimbali tayari umetimizwa kwa kadiri ndogo kwa Israeli wa kale. Chukua, kwa mfano, maneno ya Isaya 35:1, 7, ambapo twasoma: “Nyika na mahali palipo ukiwa patafurahi; jangwa litashangilia na kuchanua maua kama waridi. Na mchanga ung’aao mfano wa maji utakuwa ziwa la maji, na nchi yenye kiu itakuwa chemchemi za maji; katika makao ya mbweha, walipokuwa wamelala, patakuwa na majani, pamoja na mianzi na manyasi.” Habari inayozunguka ya andiko hili inaonyesha waziwazi kwamba lilitumika kwa wahamishwa wa Kiyahudi waliokuwa wanarudi katika siku za Gavana Zerubabeli. Mstari wa 10 unasema kwamba “hao waliokombolewa na [Yehova] watarudi, watafika Sayuni.” Lilikuwa kusudi lake kuifanya nchi hiyo paradiso ndogo kwa ajili yao, na hii ilihitaji kwamba yeye aifanye nyika na mahali pasipo na maji, na vile vile jangwa, kuwa viziwa vyenye manyasi na chemchemi za maji. Kwa matumizi yanayofaa ya misemo ya Mungu, tutakubali kwamba kufanya kwake miujiza kwa ajili ya watu wake aliowachagua wa wakati wa kale ni uhakika kabisa wa utimizo mkubwa zaidi wa ahadi kama hizo chini ya utawala wa Mwanawe, Bwana Yesu Kristo. Ni wazi sana kwamba Yehova atamimina baraka juu ya dunia hii kweli kweli chini ya utawala wa Ufalme wa Kristo Yesu, kwa kulifanya si jangwa peke yake ‘lishangilie na kuchanua maua kama waridi,’ lakini vile vile kufumbua macho yasiyoona na masikio yaliyozibika na kuwarudishia vilema afya, kama vile unabii huu unavyosema.​—Isa. 35:5, 6.

14. Kwa sababu gani imewapasa Wakristo wote wa kweli watake kulitumia Neno la Mungu la kweli kwa halali?

14 Bila shaka twaweza kusema kwamba “Neno la Mungu li hai, tena lina nguvu.” (Ebr. 4:12) Mungu yu hai. Yeye anasema na wanadamu kupitia kwa kurasa za Biblia yake iliyo hai, kwa njia hiyo akiwapa watumishi wake uwezo na ufahamu wa kweli nzito juu yake mwenyewe na kusudi lake kwa wanadamu. Kila shahidi wa Kikristo wa Yehova Mungu amepaswa atake kulitumia neno hilo kwa halali, kusudi aweze kulitumia kwa matokeo katika kuwafundisha wengine na katika kuyaondoa mafundisho ya kidini ya uongo yaliyozipofusha akili na mioyo ya mamilioni mengi waliotekwa nyara katika Babeli Mkuu, milki ya ulimwengu ya dini ya uongo. Anasema Paulo kwa Timotheo: “Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe kamili, amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema.”​—2 Tim. 3:16, 17.

15. Ili tulifahamu na kushukuru kwa Neno la Mungu, imetupasa tufanye jitihada gani?

15 Ili kulitumia Neno la Mungu kwa halali ni lazima mtu alisome na kujifunza, akizitafuta hazina zilizofichwa humo. Ufahamu huo haujileti wenyewe, bali unahitaji kazi ngumu na kutafuta kwa bidii. Inasema Mithali: “Mwanangu, kama ukiyakubali maneno yangu, na kuyaweka akiba maagizo yangu; hata ukatega sikio lako kusikia hekima, ukauelekeza moyo wako upate kufahamu; naam, ukiita busara, na kupaza sauti yako upate ufahamu; ukiutafuta kama fedha, na kuutafutia kama hazina iliyositirika; ndipo utakapofahamu kumcha [Yehova], na kupata kumjua Mungu.” (Mit. 2:1-5) Kutokana na yale tuliyoyaangalia katika mafungu haya, ni wazi kwamba imetupasa tutake kujua sababu gani mambo yalisemwa kama yalivyosemwa katika Neno la Mungu na ni matumizi gani yanayoweza kufanywa juu ya maneno hayo. Imetupasa sikuzote tutafute sababu za maelezo kutolewa namna hiyo na kutafuta kulitumia Neno la Mungu kwa halali.

16. Ni habari gani zaidi itakayotusaidia kulitumia Neno la Mungu kwa halali?

16 Makala inayofuata itaonyesha kwamba kuna vitabu vizima vya Biblia walivyoandikiwa watu fulani na vikiwa na ujumbe fulani wa kujulisha. Katika kulitumia neno hili la Mungu lililo bora katika njia inayofaa, tutafaidika kwa kutafuta habari juu ya jambo hili, kuujua msingi, kusudi na ubora wa maneno yaliyoongozwa na roho ya Mungu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki