SURA YA 30
Endeleeni “Kutembea Katika Upendo”
1-3. Tunapata manufaa gani tunapomwiga Yehova katika kuonyesha upendo?
“KUNA furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Maneno hayo ya Yesu yanakazia ukweli huu muhimu sana: Upendo usio na ubinafsi unathawabisha. Tunafurahi sana wengine wanapotuonyesha upendo, lakini tunapata furaha hata zaidi tunapowaonyesha wengine upendo.
2 Hakuna anayeelewa jambo hilo vizuri kama Baba yetu wa mbinguni. Kama tulivyoona katika sura zilizotangulia za sehemu hii, Yehova ndiye mfano bora zaidi wa upendo. Yehova ameonyesha upendo kwa njia za pekee sana na kwa muda mrefu kuliko mtu yeyote. Ndiyo sababu Yehova anaitwa “Mungu mwenye furaha.”—1 Timotheo 1:11.
3 Mungu wetu mwenye upendo anataka tujitahidi kumwiga, hasa katika kuonyesha upendo. Andiko la Waefeso 5:1, 2 linasema hivi: “Iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa, na mwendelee kutembea katika upendo.” Tunapomwiga Yehova katika kuonyesha upendo, tunapata furaha zaidi inayotokana na kutoa. Tunaridhika pia kujua kwamba tunampendeza Yehova, kwa sababu Neno lake linatuhimiza ‘tupendane.’ (Waroma 13:8) Lakini kuna sababu nyingine zinazotufanya tuendelee “kutembea katika njia ya upendo.”
Kwa Nini Upendo Ni Muhimu?
Upendo hutuchochea tuwaamini ndugu zetu
4, 5. Kwa nini ni muhimu tuwaonyeshe waamini wenzetu upendo wa kujidhabihu?
4 Kwa nini ni muhimu tuwapende waamini wenzetu? Kwa ufupi, upendo ndio msingi wa Ukristo wa kweli. Hatuwezi kuwa na uhusiano mzuri na Wakristo wenzetu ikiwa hatuwapendi, na jambo baya hata zaidi ni kwamba bila upendo tunakuwa bure machoni pa Yehova. Fikiria jinsi ambavyo Neno la Mungu linakazia ukweli huo.
5 Yesu aliwaambia hivi wafuasi wake usiku wa mwisho wa maisha yake duniani: “Ninawapa ninyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda, nanyi mpendane vivyo hivyo. Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu—mkiwa na upendo miongoni mwenu.” (Yohana 13:34, 35) Yesu aliposema “kama vile ambavyo nimewapenda” alikuwa akituamuru tuwe na upendo kama ule aliotuonyesha. Katika Sura ya 29, tuliona kwamba Yesu alikuwa mfano bora katika kuonyesha upendo wa kujidhabihu, akitanguliza masilahi ya wengine. Sisi pia, tunapaswa kupendana bila ubinafsi. Na upendo wetu unapaswa kuonekana wazi kabisa hata kwa watu ambao wako nje ya kutaniko la Kikristo. Kwa kweli, upendo wa kindugu wa kujidhabihu unatutambulisha kuwa Wakristo wa kweli.
6, 7. (a) Tunajuaje kwamba Neno la Yehova linakazia sana umuhimu wa kuonyesha upendo? (b) Maneno ya Paulo kwenye 1 Wakorintho 13:4-8 yanakazia nini kuhusu upendo?
6 Vipi ikiwa hatuna upendo? Mtume Paulo alisema kwamba ikiwa “sina upendo, nimekuwa chuma kinachovuma au toazi linalolia.” (1 Wakorintho 13:1) Toazi na chuma kinacholia hutokeza sauti kali zisizopendeza. Mifano hiyo inafaa sana! Mtu asiye na upendo ni kama ala ya muziki inayolia kwa sauti kubwa yenye kuchukiza watu badala ya kuwavutia. Je, kweli mtu kama huyo anaweza kufurahia uhusiano mzuri na wengine? Paulo alisema hivi pia: “Ikiwa nina imani yenye nguvu hata niweze kuhamisha milima, lakini sina upendo, mimi si kitu.” (1 Wakorintho 13:2) Hebu wazia, mtu asiye na upendo “si kitu,” licha ya mambo anayofanya! Je, hilo halionyeshi kwamba Neno la Yehova linakazia sana umuhimu wa kuonyesha upendo?
7 Lakini tutaonyeshaje sifa hiyo tunaposhughulika na wengine? Tujibu swali hilo kwa kuchunguza maneno ya Paulo kwenye 1 Wakorintho 13:4-8. Mistari hii haikazii jinsi Mungu anavyotupenda au jinsi tunavyompenda Mungu. Badala yake, Paulo alikazia jinsi sisi tunavyoweza kupendana. Alieleza mambo fulani kuhusu jinsi upendo ulivyo na jinsi usivyo.
Jinsi Upendo Ulivyo
8. Subira inawezaje kutusaidia tunaposhughulika na wengine?
8 “Upendo ni wenye subira.” Hivyo, upendo unamaanisha kuwavumilia wengine kwa subira. (Wakolosai 3:13) Tunahitaji kuwa na subira, sivyo? Kwa sababu ya kufanya kazi bega kwa bega katika hali yetu ya kutokamilika, ni kawaida kwamba mara kwa mara huenda tukakosewa au tukawakosea ndugu zetu Wakristo. Lakini sifa ya subira na ustahimilivu zinaweza kutusaidia kuvumiliana na kutovuruga amani ya kutaniko tunapokosana na kutoelewana na wengine kwa sababu ya mambo madogo-madogo.
9. Tunaweza kuwaonyesha wengine fadhili katika njia zipi?
9 “Upendo ni wenye . . . fadhili.” Fadhili huonyeshwa kwa kuwasaidia wengine na kuzungumza nao kwa njia inayoonyesha kwamba tunawajali. Upendo hutuchochea kutafuta fursa za kuwaonyesha wengine fadhili, hasa wale wanaohitaji sana msaada. Kwa mfano, huenda mwamini mwenzetu mwenye umri mkubwa ni mpweke na anahitaji kutembelewa na kutiwa moyo. Huenda mama asiye na mume au dada anayeishi katika familia ambayo imegawanyika kidini anahitaji msaada fulani. Mtu aliye mgonjwa au aliyepata msiba huenda akahitaji kutiwa moyo kwa fadhili na rafiki mshikamanifu. (Methali 12:25; 17:17) Tunapochukua hatua ya kuonyesha fadhili kwa njia kama hizo, tunathibitisha kwamba upendo wetu ni halisi.—2 Wakorintho 8:8.
10. Upendo unatusaidiaje kutetea na kusema kweli, hata wakati ambapo si rahisi kwetu kufanya hivyo?
10 “Upendo . . . hushangilia pamoja na kweli.” Tafsiri nyingine inasema: “Upendo . . . huunga mkono ukweli kwa shangwe.” Upendo unatuchochea kutetea kweli na ‘kuwaambia wenzetu ukweli.’ (Zekaria 8:16) Kwa mfano, ikiwa mtu tunayempenda amefanya dhambi nzito, upendo kwa Yehova na kwa yule aliyefanya dhambi, utatusaidia tushikamane na kanuni za Mungu badala ya kujaribu kuficha, kutoa visingizio, au hata kusema uwongo kuhusu dhambi yake. Ni kweli kwamba huenda isiwe rahisi kwetu kukubali kuwa amefanya dhambi. Lakini ikiwa tunamjali kikweli mpendwa wetu, tungetaka akubali na kunufaika na nidhamu ya upendo kutoka kwa Mungu. (Methali 3:11, 12) Tukiwa Wakristo wenye upendo, tunataka pia “kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.”—Waebrania 13:18.
11. Kwa kuwa upendo “huhimili mambo yote,” tunapaswa kujitahidi kufanya nini kuhusu kasoro za waamini wenzetu?
11 “Upendo . . . huhimili mambo yote.” Usemi huo unamaanisha kwamba upendo “unafunika mambo yote.” (Kingdom Interlinear) Andiko la 1 Petro 4:8 linasema: “Upendo hufunika dhambi nyingi.” Naam, Mkristo ambaye anaongozwa na upendo hatafunua kasoro na mapungufu ya ndugu zake Wakristo. Mara nyingi, makosa na kasoro za waamini wenzetu ni ndogo sana na zinaweza kufunikwa na upendo.—Methali 10:12; 17:9.
12. Mtume Paulo alionyeshaje kwamba aliamini Filemoni angetenda kwa njia inayofaa, na tunajifunza nini kutokana na mfano wa Paulo?
12 “Upendo . . . huamini mambo yote.” Tafsiri ya Moffat inasema kwamba ‘sikuzote upendo hujitahidi kuamini mambo mazuri.’ Hatutaki kutilia shaka mambo ambayo waamini wenzetu wanafanya, au kutilia shaka nia yao ya kufanya mambo hayo. Upendo unatusaidia “kuamini mambo mazuri” kuwahusu ndugu zetu na kuwatumaini.a Fikiria mfano unaotajwa katika barua ya Paulo kwa Filemoni. Paulo alimwandikia Filemoni ili kumtia moyo amkaribishe kwa fadhili Onesimo yule mtumwa aliyetoroka, ambaye sasa alikuwa Mkristo. Badala ya kujaribu kumlazimisha Filemoni, Paulo alijitahidi kumsihi kwa upendo. Alionyesha kwamba aliamini Filemoni angetenda kwa njia inayofaa, kwa kusema: “Ninakuandikia nikiwa na uhakika kwamba utakubali, nikijua utafanya hata zaidi ya jambo ninalokuomba.” (Mstari wa 21) Upendo unapotuchochea kuwaamini ndugu zetu, wanachochewa kuonyesha sifa zao nzuri.
13. Tunawezaje kuonyesha kwamba tunawatakia mema ndugu zetu?
13 “Upendo . . . hutumaini mambo yote.” Kama tu upendo unavyotuchochea kuwaamini ndugu zetu, pia upendo huo unatuchochea kuwatakia mema. Kwa mfano, ndugu “akichukua hatua isiyofaa kabla hajajua,” tunatumaini kwamba atakubali jitihada za wale wanaojitahidi kumsaidia kwa upendo. (Wagalatia 6:1) Tunatumaini pia kwamba wale walio dhaifu katika imani watapata nguvu tena. Tunashughulika nao kwa subira, kwa kufanya yote tunayoweza ili kuwasaidia wawe na imani yenye nguvu. (Waroma 15:1; 1 Wathesalonike 5:14) Hata ikiwa mpendwa wetu ataacha kumtumikia Yehova, bado tunatumaini kwamba siku moja atarudiwa na fahamu na kumrudia Yehova, kama yule mwana mpotevu katika mfano wa Yesu.—Luka 15:17, 18.
14. Uvumilivu wetu unaweza kujaribiwa jinsi gani kutanikoni, na upendo utatusaidia tutende jinsi gani?
14 “Upendo. . . huvumilia mambo yote.” Uvumilivu hutuwezesha kubaki imara tunapokabili magumu au mambo yanayovunja moyo. Mara nyingi, majaribu tunayokabili hutoka kwa watu ambao hawamjui Yehova. Lakini nyakati nyingine, majaribu tunayokabili hutoka kwa ndugu na dada zetu. Kwa sababu ya hali ya kutokamilika, huenda nyakati nyingine ndugu zetu wakatuvunja moyo. Maneno yanayosemwa bila kufikiri yanaweza kuumiza hisia zetu. (Methali 12:18) Labda jambo fulani kutanikoni limeshughulikiwa kwa njia ambayo hatukutarajia au ndugu fulani anayeheshimiwa kutanikoni ametenda kwa njia inayotuumiza, na hivyo kufanya tujiulize: ‘Mkristo anawezaje kufanya hivyo?’ Tunapokabili hali kama hizo, je, tutaacha kushirikiana na kutaniko na kuacha kumtumikia Yehova? Hatuwezi kufanya hivyo ikiwa tuna upendo! Hatutakazia tu kasoro za ndugu yetu hivi kwamba tukose kuona sifa yoyote nzuri aliyo nayo au kukosa kuona uzuri wowote wa kutaniko. Upendo unatusaidia kuendelea kuwa waaminifu kwa Mungu na kuunga mkono kutaniko licha ya kile ambacho mwanadamu mwingine asiye mkamilifu atasema au kutenda.—Zaburi 119:165.
Jinsi Upendo Usivyo
15. Kwa nini hatupaswi kuwaonea wengine wivu, na upendo unatusaidiaje kuepuka hisia hiyo hatari?
15 “Upendo hauna wivu.” Hatupaswi kuwaonea wengine wivu kwa sababu ya vitu walivyo navyo—mali zao, mapendeleo yao, au uwezo wao. Wivu ni hisia hatari sana ya ubinafsi ambayo isipodhibitiwa inaweza kuvuruga amani ya kutaniko. Ni nini kitakachotusaidia kupinga mwelekeo wa wivu? (Yakobo 4:5) Ni upendo. Sifa hiyo muhimu sana inaweza kutufanya tushangilie pamoja na wale ambao wana mapendeleo fulani ambayo hatuna. (Waroma 12:15) Upendo hutuzuia kukasirika mtu fulani anapopongezwa kwa sababu ya kuwa na uwezo fulani wa pekee au kwa kutimiza jambo fulani kubwa.
16. Ikiwa tunawapenda ndugu zetu kikweli, kwa nini tunapaswa kuepuka kujigamba kwa sababu ya mapendeleo yetu katika utumishi wa Yehova?
16 “Upendo . . . haujigambi, haujivuni.” Upendo hutuzuia kujigamba kwa sababu ya uwezo wetu au mafanikio yetu. Ikiwa tunawapenda ndugu zetu kikweli, je, tutajigamba kwa sababu ya mafanikio yetu katika huduma au kwa sababu ya mapendeleo yetu kutanikoni? Kujigamba kwa njia hiyo kunaweza kuwavunja wengine moyo, na kuwafanya wajione hawafai. Upendo hutuzuia kujigamba kwa sababu ya mapendeleo ya utumishi ambayo Mungu ametupatia. (1 Wakorintho 3:5-9) Zaidi ya hayo, upendo “haujivuni,” au kama tafsiri moja inavyosema ‘haujioni kuwa bora.’ Upendo hutuzuia kujiona kuwa bora kuliko wengine.—Waroma 12:3.
17. Upendo hutuchochea kuwajali wengine kwa njia gani, na kufanya hivyo kutatusaidia kuepuka mwenendo wa aina gani?
17 “Upendo . . . haujiendeshi bila adabu.” Mtu asiye na adabu anatenda kwa njia mbaya sana au yenye kuudhi. Mtu anayejiendesha kwa njia hiyo hana upendo kwa sababu hajali hisia na hali njema ya wengine. Kinyume chake, upendo ni wenye fadhili na unatuchochea kuwajali wengine. Tukiwa na upendo tutakuwa na adabu, tutajiendesha kwa njia inayompendeza Mungu, na tutawaheshimu waamini wenzetu. Kwa hiyo, tukiwa na upendo tutaepuka “mwenendo wa aibu,” au tabia yoyote ile ambayo itawashtua au kuwaudhi ndugu zetu Wakristo.—Waefeso 5:3, 4.
18. Kwa nini mtu mwenye upendo halazimishi kila jambo lifanywe kwa njia anayopenda?
18 “Upendo . . . hautafuti faida zake wenyewe.” Tafsiri nyingine inasema hivi: “Upendo hausisitizi kufuata njia yake.” Mtu mwenye upendo hasisitizi kila jambo lifanywe kwa njia anayopenda, kana kwamba maoni yake ni sawa sikuzote. Hawashawishi wengine ili kuwalazimisha wafuate maoni yake. Ukaidi wa aina hiyo unaonyesha kwamba ana kiasi fulani cha kiburi, na Biblia inasema: “Kiburi hutangulia kuanguka kwa kishindo.” (Methali 16:18) Ikiwa tunawapenda kikweli ndugu zetu, tutaheshimu maoni yao, na inapowezekana tutakuwa tayari kuyakubali. Maneno haya ya Paulo yanatutia moyo kuwa na roho hiyo: “Kila mmoja na aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali faida ya yule mtu mwingine.”—1 Wakorintho 10:24.
19. Upendo unatusaidia tutende jinsi gani tunapokosewa na wengine?
19 ‘Upendo . . . hauchokozeki . . . , hauweki hesabu ya ubaya.’ Upendo hauchokozeki kwa urahisi na mambo ambayo wengine wanasema au kufanya. Ni jambo la kawaida kukasirika tunapokosewa. Lakini hata tukiwa na sababu nzuri ya kukasirika, hatutaendelea kuchokozeka ikiwa tuna upendo. (Waefeso 4:26, 27) Hatutaweka hesabu ya maneno au matendo yenye kuumiza kana kwamba tunayaandika katika kitabu ili tusiyasahau. Badala yake, upendo unatuchochea kumwiga Mungu wetu mwenye upendo. Kama tulivyoona katika Sura ya 26, Yehova husamehe kunapokuwa na sababu nzuri ya kufanya hivyo. Yeye husamehe na kusahau, yaani, hatatuadhibu baadaye kwa sababu ya dhambi hizo. Je, hatushukuru kwamba Yehova haweki hesabu ya ubaya?
20. Tunapaswa kutenda jinsi gani mwamini mwenzetu anapofanya dhambi na kupata madhara?
20 “Upendo . . . haushangilii ukosefu wa uadilifu.” Tafsiri nyingine inasema: “Upendo . . . haushangilii dhambi za wengine.” Tafsiri ya Moffat inasema: “Upendo haufurahii kamwe wengine wanapokosea.” Upendo haufurahii uovu, kwa hiyo tunakataa kabisa ukosefu wowote wa uadilifu. Tutatendaje mwamini mwenzetu anapofanya dhambi na kupata madhara? Tukiwa na upendo hatutashangilia kana kwamba tunasema, ‘Safi sana! Amepata anachostahili!’ (Methali 17:5) Hata hivyo, tunashangilia ndugu aliyetenda dhambi anapochukua hatua zinazofaa ili ajirekebishe na kufanya maendeleo ya kiroho.
“Njia Iliyo Bora Zaidi”
21-23. (a) Paulo alimaanisha nini aliposema kwamba “upendo haushindwi kamwe”? (b) Tutazungumzia nini katika sura ya mwisho?
21 “Upendo haushindwi kamwe.” Paulo alimaanisha nini aliposema hivyo? Muktadha unaonyesha kwamba alikuwa anazungumzia zawadi za roho za Wakristo wa mapema. Zawadi hizo zilithibitisha kwamba Mungu aliunga mkono kutaniko hilo jipya. Lakini si Wakristo wote wangeweza kuponya, kutoa unabii, au kuzungumza kwa lugha mbalimbali. Hata hivyo, hilo halikuwa muhimu kwa sababu mwishowe zawadi hizo zote zingekoma. Lakini sifa fulani haingekoma, sifa ambayo kila Mkristo angeweza kusitawisha. Sifa hiyo ilikuwa muhimu zaidi, na ya kudumu kuliko zawadi yoyote ya kimuujiza. Paulo aliiita sifa hiyo “njia iliyo bora zaidi.” (1 Wakorintho 12:31) Ni “njia [gani] iliyo bora zaidi”? Ilikuwa njia ya upendo.
22 Upendo wa Kikristo ambao Paulo alizungumzia “haushindwi kamwe,” yaani, hautafikia kikomo. Leo pia, upendo wa kindugu wa kujidhabihu unawatambulisha wafuasi wa kweli wa Kristo. Je, hatuoni upendo huo katika makutaniko ya waabudu wa Yehova duniani kote? Upendo huo utadumu milele, kwa sababu Yehova anawaahidi watumishi wake waaminifu uzima wa milele. (Zaburi 37:9-11, 29) Na tujitahidi kufanya yote tunayoweza ili ‘tuendelee kutembea katika upendo.’ Tukifanya hivyo, tunaweza kupata furaha nyingi sana inayotokana na kutoa. Isitoshe, tunaweza kuendelea kuishi na kuendelea kupenda—milele na milele kama Mungu wetu mwenye upendo, Yehova.
Watu wa Yehova wanatambuliwa kupita upendo ulio miongoni mwao
23 Katika sura hii inayomalizia sehemu ya upendo, tumezungumzia jinsi tunavyoweza kupendana. Kwa kuwa tunafaidika katika njia nyingi kutokana na upendo wa Yehova—na vilevile kutokana na nguvu, haki, na hekima yake—tunapaswa kujiuliza hivi, ‘Nitamthibitishiaje Yehova kwamba kwa kweli ninampenda?’ Swali hilo litazungumziwa katika sura ya mwisho.
a Bila shaka, upendo wa Kikristo haupumbaziki. Biblia inatuhimiza hivi: “Waangalieni wale wanaosababisha migawanyiko na kuweka vikwazo . . . , nanyi mjiepushe nao.”—Waroma 16:17.