-
Fanya Maendeleo Yako Yawe WaziMnara wa Mlinzi—2009 | Desemba 15
-
-
6 Paulo alimwandikia Timotheo hivi: “Uwe kielelezo kwa waaminifu katika kusema, katika mwenendo, katika upendo, katika imani, katika usafi wa kiadili.”
-
-
Fanya Maendeleo Yako Yawe WaziMnara wa Mlinzi—2009 | Desemba 15
-
-
Uwe Kielelezo Katika Kusema
8. Usemi wetu una matokeo gani kwa ibada yetu?
8 Timotheo alipaswa pia kuwa kielelezo katika kusema. Tunaweza kufanya maendeleo yetu yawe wazi namna gani katika jambo hilo? Usemi wetu unafunua mambo mengi kutuhusu. Yesu alisema wazi hivi: “Kinywa kinasema kutokana na mambo yaliyojaa katika moyo.” (Mt. 12:34) Yakobo, ndugu wa kambo wa Yesu, alitambua pia kwamba usemi wetu unaweza kuwa na matokeo mabaya kwa ibada yetu. Aliandika hivi: “Ikiwa mtu yeyote anajiona kuwa mwabudu anayeshikilia vizuri namna ya ibada na bado hauongozi ulimi wake, bali anaendelea kuudanganya moyo wake mwenyewe, namna ya ibada ya mtu huyo ni ya ubatili.”—Yak. 1:26.
9. Tunapaswa kuwa kielelezo katika usemi kwa njia gani?
9 Usemi wetu unaweza kuwafunulia wengine kutanikoni kadiri ambavyo tumefanya maendeleo ya kiroho. Kwa hiyo, badala ya kusema mambo yasiyo ya heshima, yenye kubomoa, ya kuchambua, au yenye kuumiza, Wakristo wakomavu wanajitahidi kuwajenga, kuwafariji, kuwatuliza, na kuwatia moyo wengine. (Met. 12:18; Efe. 4:29; 1 Tim. 6:3-5, 20) Kuwa tayari kuzungumza na wengine kuhusu mambo ya kimaadili ambayo tunaamini na kutetea waziwazi viwango vya juu vya Mungu kunaweza kuonyesha kwamba tumejitoa kwa Mungu. (Rom. 1:15, 16) Bila shaka, watu wenye mioyo minyoofu wataona jinsi tunavyotumia zawadi ya usemi na huenda wakafuata kielelezo chetu.—Flp. 4:8 9.
Tuwe Kielelezo Katika Mwenendo Wetu na Usafi wa Kiadili
10. Kwa nini imani isiyo na unafiki inaweza kutusaidia sana kufanya maendeleo ya kiroho?
10 Zaidi ya kuwa kielelezo kizuri katika usemi wenye kujenga, kuna mambo mengine ambayo Mkristo anahitaji kufanya. Mtu anayesema mambo yanayofaa lakini hafanyi mambo yanayofaa ni mnafiki. Paulo alijua vizuri sana unafiki wa Mafarisayo na madhara ya mwenendo wao. Alimwonya Timotheo tena na tena ajiepushe na unafiki na ukosefu huo wa unyoofu. (1 Tim. 1:5; 4:1, 2) Lakini Timotheo hakuwa mnafiki. Katika barua yake ya pili kwa Timotheo, Paulo aliandika hivi: “Naikumbuka imani iliyo ndani yako isiyo na unafiki wowote.” (2 Tim. 1:5) Hata hivyo, Timotheo alihitaji kuonyesha wazi mbele ya wengine unyoofu wake akiwa Mkristo. Alipaswa kuwa kielelezo katika mwenendo.
11. Paulo alimwandikia Timotheo nini kuhusu utajiri?
11 Katika barua zake mbili kwa Timotheo, Paulo alitoa himizo juu ya mambo mbalimbali yanayohusu mwenendo. Kwa mfano, alimhimiza Timotheo aepuke kufuatia utajiri. Paulo aliandika hivi: “Kupenda pesa ni chanzo cha mambo mabaya ya namna zote, na kwa kujitahidi kufikia upendo huo wengine wamepotoshwa kutoka kwenye imani nao wamejichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi.” (1 Tim. 6:10) Kupenda utajiri kunaonyesha kwamba mtu ana udhaifu wa kiroho. Kwa upande mwingine, Wakristo wanaotosheka kuishi maisha rahisi, ‘wakiwa na chakula na kitu cha kujifunika,’ wanaonyesha kwamba wamefanya maendeleo ya kiroho.—1 Tim. 6:6-8; Flp. 4:11-13.
12. Tunaweza kufanya nini ili maendeleo yetu yawe wazi katika maisha yetu binafsi?
12 Paulo alimweleza Timotheo jinsi ambavyo ni jambo la maana sana kwa wanawake Wakristo ‘kujipamba kwa mavazi yenye mpangilio mzuri, pamoja na kiasi na utimamu wa akili.’ (1 Tim. 2:9) Wanawake wenye kiasi na utimamu wa akili katika mavazi na kujipamba, na pia katika mambo mengine ya kibinafsi, wanaweka kielelezo bora. (1 Tim. 3:11) Kanuni hiyo inawahusu pia wanaume Wakristo. Paulo aliwashauri waangalizi wawe ‘wenye kiasi katika mazoea, wenye utimamu wa akili, wenye utaratibu.’ (1 Tim. 3:2) Tunapoonyesha sifa hizo katika shughuli zetu za kila siku, maendeleo yetu yatakuwa wazi kwa watu wote.
13. Tunaweza jinsi gani kuwa vielelezo katika usafi wa kiadili kama Timotheo alivyokuwa?
13 Timotheo alipaswa pia kuwa kielelezo katika usafi wa kiadili. Paulo alipotumia maneno hayo, alikuwa akizungumza kuhusu jambo fulani hususa la mwenendo, yaani, maadili katika ngono. Timotheo alipaswa kuwa na mwenendo usiolaumika aliposhughulika hasa na wanawake. Alipaswa kuwatendea “wanawake wazee kama mama, wanawake vijana kama dada kwa usafi wote wa kiadili.” (1 Tim. 4:12; 5:2) Mungu anajua hata matendo mapotovu kiadili ambayo huenda yamefichwa kama siri na bila shaka wanadamu wenzetu watayajua mwishowe. Lakini ni kweli pia kwamba matendo mazuri ya Mkristo hayawezi kufichwa. (1 Tim. 5:24, 25) Kila mtu katika kutaniko ana nafasi ya kufanya maendeleo yake yawe wazi katika mwenendo na usafi wa kiadili.
Upendo na Imani Ni Sifa za Maana Sana
14. Maandiko yanakazia jinsi gani uhitaji wa kuwa na upendo kati yetu wenyewe?
14 Upendo ni sifa ya maana sana katika Ukristo wa kweli. Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yoh. 13:35) Tunaonyesha upendo huo namna gani? Neno la Mungu linatusihi ‘tuvumiliane katika upendo,’ na kuwa ‘wenye fadhili sisi kwa sisi, wenye huruma nyororo, tukisameheana kwa hiari,’ na kuwa wakaribishaji-wageni. (Efe. 4:2, 32; Ebr. 13:1, 2) Mtume Paulo aliandika hivi: “Katika upendo wa kindugu iweni na upendo mwororo kwa mtu na mwenzake.”—Rom. 12:10.
15. Kwa nini sifa ya upendo ni ya maana sana kwa wote, hasa waangalizi Wakristo?
15 Ikiwa Timotheo angeshughulika na Wakristo wenzake kwa ukali au bila fadhili, angeharibu kazi nzuri aliyotimiza akiwa mwalimu na mwangalizi. (Soma 1 Wakorintho 13:1-3.) Kwa upande mwingine, maneno ya Timotheo ambayo yalionyesha jinsi alivyowapenda kikweli ndugu zake, pamoja na matendo ya ukarimu na mambo mazuri aliyowatendea, bila shaka yalionyesha wazi maendeleo yake ya kiroho. Basi, ni vizuri kwamba katika barua yake kwa Timotheo, mtume Paulo alitaja hasa upendo ukiwa moja ya sifa ambazo Timotheo alipaswa kuweka kielelezo.
16. Kwa nini Timotheo alihitaji kuwa na imani yenye nguvu?
16 Imani ya Timotheo ilijaribiwa alipokuwa akiishi huko Efeso. Wakristo fulani walikuwa wakieneza mafundisho ambayo hayakupatana na kweli ya Kikristo. Wengine walikuwa wakieneza “hadithi za uwongo” au kufanya utafiti kuhusu mawazo ambayo hayakujenga kamwe hali ya kiroho ya kutaniko. (Soma 1 Timotheo 1:3, 4.) Paulo alieleza kwamba watu kama hao ‘walijivuna kwa kiburi, hawakuelewa jambo lolote, bali walikuwa wagonjwa kiakili juu ya maswali na mabishano juu ya maneno.’ (1 Tim. 6:3, 4) Je, Timotheo angejihatarisha kwa kuchunguza-chunguza mawazo hayo yenye kudhuru ambayo yalikuwa yakiingia ndani ya kutaniko? Hangefanya hivyo, kwa kuwa Paulo alimhimiza Timotheo ‘apigane pigano zuri la imani’ na kugeuka mbali “kutoka kwenye maneno matupu ambayo huchafua mambo matakatifu na kutoka kwenye maneno yanayopingana ya ule unaoitwa kwa uwongo ‘ujuzi.’” (1 Tim. 6:12, 20, 21) Bila shaka Timotheo alifuata mashauri hayo ya Paulo yenye hekima.—1 Kor. 10:12.
17. Imani yetu inaweza kujaribiwa jinsi gani leo?
17 Ona kwamba Timotheo aliambiwa kuwa katika “vipindi vya nyakati za mwisho wengine [wangeanguka] kutoka kwenye imani, wakisikiliza maneno yaliyoongozwa kwa roho yenye kupotosha na mafundisho ya roho waovu.” (1 Tim. 4:1) Watu wote katika kutaniko, kutia ndani wale walio na madaraka fulani, wanahitaji kuwa kama Timotheo katika kuonyesha imani yenye nguvu isiyoyumba-yumba. Kwa kuchukua msimamo imara na kupinga kabisa uasi-imani, tunaweza kufanya maendeleo yetu yawe wazi na kuwa kielelezo katika imani.
-