SURA YA 25
“Huruma Nyororo za Mungu Wetu”
1, 2. (a) Kwa kawaida mama hutendaje mtoto wake mchanga anapolia? (b) Ni hisia gani iliyo na nguvu zaidi kuliko huruma ya mama?
MTOTO mchanga anaanza kulia usiku wa manane. Mama yake anaamka mara moja. Mama huyo halali kwa utulivu tangu alipojifungua mtoto. Amejua kutofautisha vilio mbalimbali vya mtoto wake. Hivyo, anaweza kujua ikiwa mtoto wake anahitaji kunyonya, kubebwa, au kushughulikiwa kwa njia nyingine. Mama humshughulikia mtoto wake hata iwe analia kwa sababu gani. Hawezi kupuuza mahitaji ya mtoto wake kwa sababu anampenda sana.
2 Huruma ya mama kumwelekea mtoto wake ni moja kati ya hisia zenye nguvu sana ambazo wanadamu huonyesha. Hata hivyo, kuna hisia ambayo ni yenye nguvu kupita hisia zote—huruma nyororo za Mungu wetu, Yehova. Kujifunza mengi kuhusu sifa hii yenye kuvutia kunaweza kutusaidia kumkaribia zaidi Yehova. Basi, tuzungumzie maana ya huruma na jinsi ambavyo Mungu wetu huonyesha sifa hiyo.
Huruma Ni Nini?
3. Kitenzi cha Kiebrania kinachotafsiriwa “onyesha rehema” au “kuwa na huruma” kinamaanisha nini?
3 Katika Biblia, kuna uhusiano mkubwa kati ya huruma na rehema. Maneno kadhaa ya Kiebrania na Kigiriki yanadokeza sifa ya huruma yenye upendo. Kwa mfano, fikiria kitenzi cha Kiebrania ra·chamʹ, ambacho mara nyingi hutafsiriwa “onyesha rehema” au “kuwa na huruma.” Kitabu kimoja cha marejeo kinaeleza kwamba kitenzi ra·chamʹ “kinaonyesha huruma nyingi na yenye upendo, kama ile tunayohisi tunapowaona wapendwa wetu au wale wanaohitaji msaada wetu wakiteseka au kuumia.” Neno hilo la Kiebrania, ambalo Yehova anatumia kueleza jinsi anavyohisi, linahusiana na neno linalomaanisha “tumbo la uzazi” nalo linaweza kutafsiriwa kuwa “huruma ya mama.”a—Kutoka 33:19; Yeremia 33:26.
“Je! mwanamke anaweza kumsahau . . . mwana wa tumbo lake?”
4, 5. Biblia inatumiaje hisia ambazo mama huwa nazo kumwelekea mtoto wake mchanga, kutufundisha kuhusu sifa ya Yehova ya huruma?
4 Biblia inatumia hisia ambazo mama huwa nazo kwa mtoto wake mchanga kutufundisha maana ya huruma za Yehova. Tunasoma hivi kwenye Isaya 49:15: “Je, mwanamke anaweza kumsahau mtoto wake anayenyonya au asimhurumie mwana wa tumbo lake? Hata wanawake hawa wakisahau, mimi siwezi kamwe kukusahau.” Maelezo hayo yenye kugusa moyo yanakazia jinsi Yehova alivyo na huruma nyingi kwa watu wake. Jinsi gani?
5 Ni vigumu kuwazia kwamba mama anaweza kusahau kumnyonyesha na kumtunza mtoto wake mchanga. Kwa kuwa mtoto mchanga hana uwezo wa kufanya jambo lolote; anahitaji kupendwa na kutunzwa na mama yake usiku na mchana. Hata hivyo, inasikitisha kupata habari kuhusu akina mama wanaowatupa watoto wao, hasa katika “nyakati [hizi] za hatari” kwa sababu watu hawana “upendo wa asili.” (2 Timotheo 3:1, 3) Hata hivyo, Yehova anasema: “Mimi siwezi kamwe kukusahau.” Yehova hakosi kamwe kuwaonyesha watumishi wake huruma nyororo. Huruma hiyo ni yenye nguvu zaidi ya hisia yenye nguvu tunayoweza kuwazia, yaani, huruma ambayo kwa kawaida mama humwonyesha mtoto wake mchanga. Haishangazi kwamba msomi mmoja wa Biblia alisema hivi kuhusu Isaya 49:15: “Hili ndilo neno linalofafanua upendo wa Mungu waziwazi zaidi katika Agano la Kale.”
6. Wanadamu wengi wasio wakamilifu wamekuwa na maoni gani kuhusu huruma nyororo, lakini Yehova anatuhakikishia nini?
6 Je, kuwa na huruma nyororo ni udhaifu? Wanadamu wengi wasio wakamilifu wamekuwa na maoni hayo. Kwa mfano, mwanafalsafa Mroma Seneca, msomi maarufu wa Roma ambaye aliishi wakati wa Yesu, alifundisha kwamba “huruma ni udhaifu wa akili.” Seneca aliunga mkono falsafa ya kwamba njia bora ya kuishi ni kuepuka kuwa na hisia kama maumivu, huzuni, au furaha. Seneca alisema kwamba mtu mwenye hekima anaweza kuwasaidia wale wanaotaabika, lakini hapaswi kuwahurumia kwa sababu atakosa utulivu akifanya hivyo. Maoni hayo ya ubinafsi kuhusu maisha yaliwazuia watu wasionyeshe huruma kutoka moyoni. Lakini Yehova hayuko hivyo! Yehova anatuhakikishia katika Neno lake kwamba yeye “ni mwenye huruma sana na mwenye rehema.” (Yakobo 5:11, maelezo ya chini) Kama tutakavyoona, kuonyesha huruma si udhaifu bali ni sifa muhimu sana yenye nguvu. Tuone jinsi Yehova anavyoonyesha sifa hiyo kama mzazi mwenye upendo.
Yehova Alipolihurumia Taifa la Israeli
7, 8. Waisraeli walikabili mateso gani katika Misri ya kale, na Yehova alichukua hatua gani kwa sababu ya mateso yao?
7 Huruma ya Yehova inaonekana wazi kutokana na jinsi alivyoshughulika na taifa la Israeli. Kufikia mwishoni mwa karne ya 16 K.W.K., mamilioni ya Waisraeli waliteswa sana walipokuwa watumwa katika Misri ya kale. Wamisri ‘walifanya maisha yao yawe machungu kwa kazi ngumu ya kutengeneza saruji ya udongo wa mfinyanzi na matofali na katika kila aina ya utumwa.’ (Kutoka 1:11, 14) Waisraeli walimlilia Yehova awasaidie walipokuwa wakiteseka. Mungu mwenye huruma nyororo alichukua hatua gani?
8 Yehova aliwahurumia sana. Alisema: “Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walio Misri, nami nimesikia kilio chao kwa sababu ya wale wanaowalazimisha kufanya kazi; ninajua vema maumivu yao.” (Kutoka 3:7) Yehova hakuweza kamwe kutazama watu wake wakiteseka au kusikia vilio vyao bila kuwahurumia. Kama tulivyoona katika Sura ya 24 ya kitabu hiki, Yehova ni Mungu anayehisi maumivu ya watumishi wake kana kwamba ni yake. Lakini Yehova hakuwahurumia tu watu wake; alichochewa kuwasaidia. Andiko la Isaya 63:9 linasema: “Kwa upendo na huruma yake aliwakomboa.” Yehova aliwaokoa Waisraeli kutoka Misri “kwa mkono wenye nguvu.” (Kumbukumbu la Torati 4:34) Baadaye, aliwalisha kimuujiza na kuwapa nchi yenye rutuba.
9, 10. (a) Kwa nini Yehova aliwakomboa Waisraeli tena na tena baada ya kuingia katika Nchi ya Ahadi? (b) Katika siku za Yeftha, Yehova aliwakomboa Waisraeli kutoka katika mateso gani, na ni nini kilichomchochea kufanya hivyo?
9 Huruma ya Yehova haikuishia hapo. Waisraeli walimwasi tena na tena baada ya kuingia katika Nchi ya Ahadi na hivyo wakateseka. Lakini walirudiwa na fahamu na kumlilia Yehova. Aliwakomboa tena na tena. Kwa nini? “Kwa sababu aliwahurumia watu wake.”—2 Mambo ya Nyakati 36:15; Waamuzi 2:11-16.
10 Fikiria mambo yaliyotukia katika siku za Yeftha. Kwa kuwa Waisraeli walianza kuitumikia miungu ya uwongo, Yehova aliwaacha wateswe na Waamoni kwa miaka 18. Mwishowe, Waisraeli walitubu. Biblia inatuambia hivi: “Wakaondoa miungu ya kigeni waliyokuwa nayo na kumtumikia Yehova, naye hakuweza tena kuvumilia kuwaona Waisraeli wakiteseka.”b (Waamuzi 10:6-16) Mara tu baada ya watu wake kutubu kikweli, Yehova hakuweza kuvumilia kuwaona wakiteseka. Kwa hiyo, Mungu mwenye huruma nyororo alimpa Yeftha nguvu ili awakomboe Waisraeli kutoka mikononi mwa adui zao.—Waamuzi 11:30-33.
11. Tunajifunza nini kuhusu huruma tunapofikiria jinsi Yehova alivyoshughulika na Waisraeli?
11 Tunajifunza nini kuhusu huruma nyororo ya Yehova tunapofikiria jinsi alivyoshughulika na taifa la Israeli? Jambo moja muhimu tunalojifunza ni kwamba kuonyesha huruma kunahusisha mengi zaidi ya kuwasikitikia tu wanaoteseka. Kumbuka mfano wa mama ambaye anachochewa na huruma kumsaidia mtoto wake mchanga anayelia. Vivyo hivyo, Yehova hapuuzi vilio vya watu wake. Huruma yake nyororo humchochea kukomesha mateso yao. Pia, tunajifunza kwamba huruma si udhaifu, kwa sababu sifa hii ya kutoka moyoni ilimchochea Yehova achukue hatua ya kuwatetea watu wake. Lakini je, Yehova anawahurumia watumishi wake wakiwa kikundi tu?
Huruma ya Yehova Kuelekea Mtu Mmoja-Mmoja
12. Sheria ilionyeshaje huruma ya Yehova kumwelekea mtu mmoja-mmoja?
12 Sheria ambayo Mungu alilipatia taifa la Israeli ilionyesha kwamba alimhurumia mtu mmoja-mmoja. Kwa mfano, fikiria jinsi alivyowajali maskini. Yehova alijua kwamba Mwisraeli angeweza kuwa maskini kwa sababu ya hali zisizotazamiwa. Maskini walipaswa kutendewaje? Yehova aliwapa Waisraeli amri hii: “Msiifanye mioyo yenu iwe migumu au kumfumbia mkono ndugu yenu maskini. Mnapaswa kumpa kwa ukarimu, nanyi hampaswi kumpa huku mkinung’unika, kwa sababu hiyo Yehova Mungu wenu atabariki kila kazi na kila jambo mnalofanya.” (Kumbukumbu la Torati 15:7, 10) Pia, Yehova aliwaagiza Waisraeli wasivune kabisa kwenye ukingo wa mashamba yao au kukusanya masalio. Masalio hayo yaliachwa kwa ajili ya maskini. (Mambo ya Walawi 23:22; Ruthu 2:2-7) Taifa la Israeli lilipotii sheria hiyo, Waisraeli maskini hawakuhitaji kuombaomba chakula. Bila shaka, hilo lilionyesha huruma nyororo ya Yehova.
13, 14. (a) Maneno ya Daudi yanatuhakikishiaje kwamba Yehova anamjali sana kila mmoja wetu? (b) Toa mfano unaoonyesha kwamba Yehova yuko karibu na wale “waliovunjika moyo” au “waliopondeka roho.”
13 Leo pia, Mungu wetu mwenye upendo anamjali sana kila mmoja wetu. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba anajua kabisa mateso yoyote ambayo huenda tunapitia. Mtunga-zaburi Daudi aliandika hivi: “Macho ya Yehova yanawatazama waadilifu, na masikio yake yanasikiliza kilio chao cha kuomba msaada. Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; huwaokoa waliopondeka roho.” (Zaburi 34:15, 18) Mwanamume mmoja anasema hivi kuhusu wale wanaotajwa na andiko hilo: “Ni watu waliovunjika moyo na wenye majuto, yaani, watu walionyenyekezwa na dhambi, wasiojiheshimu; wanaojiona kuwa duni, na wasiojiamini.” Huenda wakahisi kwamba Yehova yuko mbali nao, na kwamba wao ni duni hivi kwamba hawezi kuwajali. Lakini hilo si kweli. Maneno ya Daudi yanatuhakikishia kwamba Yehova hawaachi wale “wanaojiona kuwa duni.” Mungu wetu mwenye huruma anajua kwamba tunahitaji sana msaada wake tunapohisi hivyo, naye yuko tayari kutusaidia.
14 Fikiria kisa hiki. Mama mmoja nchini Marekani alimpeleka mwana wake mwenye umri wa miaka miwili hospitali kwa sababu alikuwa na ugonjwa mbaya wa kifaduro. Baada ya kumchunguza, madaktari walimwambia mama huyo kwamba mwana wake angelazwa hospitali usiku huo. Mama huyo alikesha wapi usiku huo? Alikesha kwenye kiti cha hospitali, karibu na kitanda cha mwana wake! Mwana wake alikuwa mgonjwa na mama yake alitaka sana kuwa karibu naye. Bila shaka, tunaweza kutarajia kwamba Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo atufanyie mengi zaidi, kwa kuwa tumeumbwa kwa mfano wake. (Mwanzo 1:26) Maneno yenye kugusa moyo ya Zaburi 34:18 yanatueleza kwamba ‘tunapovunjika moyo’ au ‘kupondeka roho,’ Yehova, kama baba mwenye upendo, sikuzote “yuko karibu”—akiwa mwenye huruma na tayari kutusaidia.
15. Yehova anamsaidiaje kila mmoja wetu?
15 Yehova anamsaidiaje kila mmoja wetu? Haondoi chanzo cha mateso yetu sikuzote. Lakini Yehova amewapa maandalizi mengi wale wanaomwomba msaada. Neno lake, Biblia, lina mashauri yanayofaa ambayo yanaweza kutusaidia kukabiliana na hali yoyote. Katika kutaniko, Yehova ameweka waangalizi wanaostahili kiroho, ambao wanajitahidi kuwa na huruma kama yeye wanapowasaidia waabudu wenzao. (Yakobo 5:14, 15) Akiwa “Msikiaji wa sala,” yeye huwapa “roho takatifu wale wanaomwomba.” (Zaburi 65:2; Luka 11:13) Roho hiyo inaweza kututia “nguvu zinazopita zile za kawaida” ili tuweze kuvumilia hadi Ufalme wa Mungu utakapokomesha matatizo yote yanayotuhangaisha. (2 Wakorintho 4:7) Tunashukuru sana kwa maandalizi yote ambayo Yehova anatupa! Tusisahau kwamba maandalizi hayo ni uthibitisho wa huruma nyororo ya Yehova.
16. Yehova alionyesha huruma yake kwa njia gani bora, na inamnufaishaje kila mmoja wetu?
16 Bila shaka, Yehova alionyesha huruma yake kwa njia bora zaidi alipomtoa Mwana wake mpendwa awe fidia kwa ajili yetu. Yehova alionyesha upendo kwa kutoa dhabihu hiyo ambayo ilitufungulia njia ya kupata wokovu. Kumbuka kwamba fidia hiyo inamnufaisha kila mmoja wetu. Hiyo ndiyo sababu Zekaria, baba ya Yohana Mbatizaji, alitabiri kwamba zawadi hiyo ilithibitisha “huruma nyororo za Mungu wetu.”—Luka 1:78.
Yehova Anapoacha Kuonyesha Huruma
17-19. (a) Biblia inaonyeshaje kwamba huruma ya Yehova ina mwisho? (b) Kwa nini Yehova aliacha kuwaonyesha watu wake huruma?
17 Je, tunapaswa kufikiri kwamba huruma nyororo ya Yehova haina mwisho? Hapana, Biblia inaonyesha waziwazi kwamba Yehova hawahurumii watu ambao wanakataa njia zake za uadilifu. (Waebrania 10:28) Ili kuelewa sababu inayomfanya atende hivyo, tuchunguze tena mfano wa taifa la Israeli.
18 Ingawa Yehova aliwakomboa tena na tena kutoka kwa maadui wao, huruma yake ilifika mwisho. Watu hao wakaidi waliabudu sanamu, hata walileta sanamu zao zenye kuchukiza ndani ya hekalu la Yehova! (Ezekieli 5:11; 8:17, 18) Zaidi ya hayo, Biblia inasema hivi: “Waliendelea kuwadhihaki wajumbe wa Mungu wa kweli, wakadharau maneno yake na kuwakejeli manabii wake, mpaka ghadhabu ya Yehova ilipokuja dhidi ya watu wake, hivi kwamba hawangeweza kuponywa.” (2 Mambo ya Nyakati 36:16) Waisraeli waliendelea kutenda mabaya hivi kwamba hakukuwa tena na msingi wowote wa kuwahurumia, nao walichochea hasira ya uadilifu ya Yehova. Matokeo yalikuwa nini?
19 Yehova hakuweza tena kuwahurumia watu wake. Alitangaza hivi: “Sitawahurumia wala kuwasikitikia kamwe wala kuwaonyesha rehema yoyote; hakuna kitakachonizuia nisiwaangamize.” (Yeremia 13:14) Basi, Yerusalemu na hekalu lake liliharibiwa, na Waisraeli wakachukuliwa mateka hadi Babiloni. Inahuzunisha sana wanadamu wanapokosa kumtii Yehova hivi kwamba huruma yake inafika mwisho!—Maombolezo 2:21.
20, 21. (a) Ni nini kitakachotukia huruma ya Mungu itakapofika mwisho katika siku zetu? (b) Tutazungumzia uandalizi gani wa huruma ya Yehova katika sura inayofuata?
20 Je, Yehova anahisi hivyo kuhusu watu wake leo? Yehova hajabadilika. Kwa sababu ya huruma yake, amewaamuru Mashahidi wake wahubiri “habari njema ya Ufalme” katika dunia yote inayokaliwa. (Mathayo 24:14) Watu wenye mioyo minyoofu wanapotaka kujifunza kumhusu, Yehova huwasaidia kuelewa ujumbe wa Ufalme. (Matendo 16:14) Lakini kazi hii haitaendelea milele. Bila shaka, Yehova hangekuwa akionyesha huruma ikiwa angeruhusu ulimwengu huu mwovu pamoja na mateso na taabu zake ziendelee milele. Yehova atahukumu mfumo huu wa mambo huruma yake itakapofika mwisho. Hata wakati huo, atakuwa akionyesha huruma—huruma kwa ajili ya ‘jina lake takatifu’ na kwa ajili ya watumishi wake waaminifu. (Ezekieli 36:20-23) Yehova ataondoa kabisa uovu na kuleta ulimwengu mpya wenye uadilifu. Yehova anatangaza hivi kuhusu waovu: “Jicho langu halitasikitika; wala sitawahurumia. Nitawaletea madhara ya njia yao juu ya kichwa chao wenyewe.”—Ezekieli 9:10.
21 Kabla ya wakati huo, Yehova anawahurumia watu, hata wale ambao wako katika hatari ya kuharibiwa pamoja na ulimwengu huu mwovu. Wanadamu wenye dhambi ambao wanatubu kikweli wanaweza kufaidika na mojawapo ya zawadi bora zaidi za huruma ya Yehova, yaani, msamaha. Katika sura inayofuata, tutazungumzia baadhi ya masimulizi ya Biblia yanayoonyesha jinsi Yehova anavyosamehe kabisa.
a Hata hivyo, kwenye Zaburi 103:13, kitenzi cha Kiebrania ra·chamʹ kinamaanisha rehema, au huruma, ambayo baba huwaonyesha watoto wake.
b Usemi unaotafsiriwa “hakuweza tena kuvumilia” unamaanisha ‘subira yake ilifika mwisho.’ Biblia Habari Njema inasema: “Hakuweza kuvumilia zaidi kuona taabu za Waisraeli.” Kitabu Tanakh—A New Translation of the Holy Scriptures kinasema hivi: “Hakuweza kustahimili kuona Israeli ikitaabika.”