SURA YA 18
Hekima ya “Neno la Mungu”
1, 2. Yehova ametuandikia “barua” gani, na kwa nini?
JE, UNAKUMBUKA mara ya mwisho ulipopokea barua kutoka kwa mpendwa wako anayeishi mbali sana? Kupokea barua yenye kugusa moyo kutoka kwa mtu tunayempenda ni mojawapo ya mambo yanayotufurahisha sana. Tunafurahi sana anapotujulisha hali yake, maisha yake, na mipango yake. Tunakuwa na uhusiano wa karibu na wapendwa wetu tunapowasiliana nao, hata ikiwa wanaishi mbali.
2 Basi, hakuna jambo lingine lolote linaloweza kutufurahisha sana kama kupokea ujumbe ulioandikwa na Mungu tunayempenda. Tunaweza kusema kwamba Yehova ametuandikia “barua,” yaani, Neno lake Biblia. Katika Biblia, anatueleza yeye ni nani, amefanya nini, anakusudia kufanya nini, na mambo mengine mengi. Yehova ametupatia Neno lake kwa sababu anataka tumkaribie. Mungu wetu mwenye hekima kamili alichagua njia bora ya kuwasiliana nasi. Biblia imeandikwa kwa njia inayoonyesha hekima ya hali ya juu sana, na ujumbe wake unaonyesha hekima hiyo pia.
Kwa Nini Yehova Alitupatia Neno Lake?
3. Yehova alimpa Musa Sheria kwa njia gani?
3 Huenda watu fulani wakauliza, ‘Kwa nini Yehova hakutumia njia nyingine kuwasiliana na wanadamu kama vile kuzungumza nao moja kwa moja kutoka mbinguni?’ Nyakati nyingine, Yehova aliongea kutoka mbinguni kupitia malaika. Kwa mfano, alifanya hivyo alipowapa Waisraeli Sheria. (Wagalatia 3:19) Sauti iliyotoka mbinguni ilikuwa yenye kuogopesha sana hivi kwamba Waisraeli walioogopa, walimwomba Yehova asiwasiliane nao kwa njia hiyo bali awasiliane nao kupitia Musa. (Kutoka 20:18-20) Kwa hiyo, Musa alipewa Sheria yenye amri 600 hivi, kwa njia ya mdomo, yaani, neno kwa neno.
4. Eleza kwa nini kupitisha sheria za Mungu kwa njia ya mdomo hakungetegemeka.
4 Ni nini kingetokea ikiwa Sheria hiyo isingeandikwa? Je, Musa angeweza kukumbuka vizuri kila neno la Sheria hiyo yenye mambo mengi, kisha aiwasilishe kwa taifa hilo bila kukosea? Namna gani kuhusu vizazi vijavyo? Je, wangehitaji kutegemea tu yale waliyoambiwa? Hiyo isingekuwa njia nzuri ya kuhakikisha kwamba kila mtu anajua Sheria ya Mungu kwa usahihi. Wazia jambo ambalo linaweza kutokea ikiwa utamwambia mtu mmoja hadithi fulani kisha ipitishwe kutoka kwa mtu mmoja hadi mwingine kwenye kikundi cha watu wengi. Inaelekea kwamba hadithi ambayo itamfikia mtu wa mwisho katika kikundi hicho, itakuwa imebadilika kabisa. Sheria ya Mungu haikukabili hatari hiyo.
5, 6. Yehova alimwagiza Musa afanye nini kuhusiana na maneno Yake, na kwa nini Biblia ni zawadi yenye thamani kutoka kwa Yehova?
5 Kwa hekima Yehova aliamua maneno yake yaandikwe. Alimwagiza Musa hivi: “Unapaswa kuandika maneno haya, kwa sababu kulingana na maneno haya, ninafanya agano pamoja nawe na pamoja na Israeli.” (Kutoka 34:27) Hivyo, Biblia ikaanza kuandikwa mwaka wa 1513 K.W.K. Kwa miaka 1,610 iliyofuata, Yehova ‘alizungumza . . . katika pindi nyingi na kwa njia nyingi’ na wanadamu 40 hivi walioandika Biblia. (Waebrania 1:1) Ili kuhifadhi Maandiko hayo, wanakili wenye bidii waliyanakili kwa usahihi na kwa uangalifu.—Ezra 7:6; Zaburi 45:1.
6 Kwa kweli, Biblia ni zawadi yenye thamani kutoka kwa Yehova. Je, umewahi kupokea barua uliyoithamini sana—labda kwa sababu ilikupa faraja uliyohitaji—hivi kwamba uliitunza na kuisoma tena na tena? Biblia ni kama “barua” hiyo kutoka kwa Yehova. Kwa kuwa Yehova aliongoza maneno yake yaandikwe, tunaweza kuyasoma kwa ukawaida na kuyatafakari. (Zaburi 1:2) Tunaweza kupata “faraja kutoka kwa Maandiko” wakati wowote tunapoihitaji.—Waroma 15:4.
Kwa Nini Yehova Alitumia Wanadamu Kuandika Biblia?
7. Yehova alionyeshaje hekima kwa kuwatumia wanadamu kuandika Neno lake?
7 Yehova alionyesha hekima kwa kuwatumia wanadamu kuandika Neno lake. Hebu wazia: Kama Yehova angetumia malaika kuandika Biblia, je, ingevutia kwa njia ileile? Kwa kweli, malaika wangeeleza jinsi Yehova alivyo kulingana na maoni yao ya hali ya juu, wangeeleza jinsi wanavyojitoa kwake, na kuandika kuhusu wanadamu waliomtumikia Mungu kwa uaminifu. Lakini je, kweli tungeweza kuelewa maoni ya viumbe hao wakamilifu wa roho, ambao wana ujuzi, ufahamu, na uwezo wa hali ya juu kuliko sisi?—Waebrania 2:6, 7.
8. Yehova aliwaruhusu waandikaji wa Biblia kufanya nini? (Ona pia maelezo ya chini.)
8 Kwa kuwatumia wanadamu kuandika Neno lake, Yehova alitupatia kile tunachohitaji—kitabu ambacho ‘kimeongozwa na roho ya Mungu’ na kinachogusa pia hisia zetu tukiwa wanadamu. (2 Timotheo 3:16) Alifanyaje hivyo? Mara nyingi, inaonekana kwamba aliwaruhusu waandishi watumie akili zao katika kuchagua “maneno yanayopendeza, na kuandika maneno sahihi ya kweli.” (Mhubiri 12:10, 11) Hiyo ndiyo sababu Biblia imeandikwa kwa njia mbalimbali; njia hizo hutegemea malezi na utu wa kila mwandishi.a Hata hivyo, wanadamu hao “walisema yaliyotoka kwa Mungu kama walivyoongozwa na roho takatifu.” (2 Petro 1:21) Kwa hiyo, Biblia ni “neno la Mungu.”—1 Wathesalonike 2:13.
“Kila Andiko limeongozwa na roho ya Mungu”
9, 10. Kwa nini kutumia wanadamu kuandika Biblia kunagusa hisia zetu?
9 Kwa kuwa Yehova alitumia wanadamu kuandika Biblia, kitabu hicho kinagusa hisia zetu. Waandishi wa Biblia walikuwa wanadamu wenye hisia kama zetu. Wakiwa wanadamu wasio wakamilifu, walikabili majaribu na changamoto kama zetu. Nyakati nyingine, roho ya Yehova iliwaongoza kuandika kuhusu hisia zao na matatizo waliyokabili. (2 Wakorintho 12:7-10) Kwa hiyo, waliandika kwa maneno yao wenyewe kuhusu mambo waliyopitia, jambo ambalo hakuna malaika ambaye angeweza kufanya.
10 Kwa mfano, fikiria kumhusu Mfalme Daudi wa Israeli. Baada ya kufanya dhambi nzito sana, Daudi alitunga zaburi ambayo inaeleza mambo yaliyokuwa moyoni mwake, na jinsi alivyomwomba Mungu msamaha. Aliandika hivi: “Nioshe kabisa kutoka katika kosa langu, na unisafishe kutoka katika dhambi yangu. Kwa maana ninajua vizuri makosa yangu, na dhambi yangu iko mbele yangu daima. Tazama! Nilizaliwa nikiwa na hatia ya kosa, na mama yangu alinichukua mimba katika dhambi. Usinitupe kutoka mbele zako; wala usiniondolee roho yako takatifu. Dhabihu zinazompendeza Mungu ni roho iliyovunjika; moyo uliovunjika na kupondeka, Ee Mungu, hutaukataa.” (Zaburi 51:2, 3, 5, 11, 17) Je, huguswi moyo na hisia za huzuni za mwandishi huyo? Ni mwanadamu asiyekamilika tu ndiye angeweza kuandika maneno hayo yenye kugusa moyo.
Kwa Nini Biblia Inatuambia Mambo Mengi Kuhusu Watu?
11. Ni masimulizi gani halisi yaliyoandikwa katika Biblia ili “kutufundisha”?
11 Kuna jambo lingine linalofanya Biblia ivutie. Kwa kadiri kubwa, ni kitabu kinachohusu watu—watu halisi, wale wanaomtumikia Mungu na wale ambao hawamtumikii. Tunasoma kuhusu maisha, matatizo, na shangwe yao. Tunaona matokeo ya maamuzi waliyofanya maishani. Masimulizi hayo yaliandikwa ili “kutufundisha.” (Waroma 15:4) Kupitia masimulizi hayo halisi, Yehova anatufundisha kwa njia zinazogusa mioyo yetu. Fikiria mifano kadhaa.
12. Masimulizi ya Biblia kuhusu wanadamu wasio waaminifu yanatusaidiaje?
12 Biblia inatuambia kuhusu wanadamu wasio waaminifu, na hata waovu na mambo yaliyowapata. Masimulizi hayo yanaonyesha jinsi watu walivyoonyesha sifa zisizofaa, na hilo linatusaidia kuelewa sifa hizo. Kwa mfano, hakuna amri inayoweza kukazia kabisa matokeo mabaya ya kutokuwa mshikamanifu kuliko mfano wa Yuda aliyepanga njama ya kumsaliti Yesu. (Mathayo 26:14-16, 46-50; 27:3-10) Masimulizi kama hayo hugusa sana mioyo yetu, na kutusaidia kutambua sifa zinazochukiza na kujitahidi kuziepuka.
13. Biblia inatusaidiaje kuelewa na kusitawisha sifa zinazofaa?
13 Biblia inasimulia pia kuhusu watumishi wengi wa Mungu waliokuwa waaminifu. Tunasoma kuhusu ujitoaji na ushikamanifu wao. Pia, tunasoma kuhusu watu wenye sifa ambazo tunahitaji kusitawisha ili kumkaribia Mungu. Kwa mfano, fikiria kuhusu sifa ya imani. Biblia inafafanua maana ya imani na kwa nini tunahitaji kuwa nayo ili kumpendeza Mungu. (Waebrania 11:1, 6) Lakini Biblia inaeleza pia mifano halisi ya watu waliokuwa na imani. Fikiria imani ambayo Abrahamu alionyesha alipojaribu kumtoa Isaka kuwa dhabihu. (Mwanzo, sura ya 22; Waebrania 11:17-19) Masimulizi kama hayo yanatusaidia kuthamini na kuelewa vizuri zaidi maana ya neno “imani.” Kwa hekima Yehova, anatuhimiza tusitawishe sifa zinazofaa, na pia anatuonyesha mifano ya watu waliokuwa na sifa hizo!
14, 15. Biblia inatuambia nini kuhusu mwanamke fulani aliyekuja hekaluni, na simulizi hilo linatufundisha nini kumhusu Yehova?
14 Mara nyingi, masimulizi halisi yaliyo katika Biblia hutufundisha kuhusu utu wa Yehova. Fikiria simulizi la mwanamke fulani ambaye Yesu alimwona hekaluni. Alipokuwa ameketi karibu na masanduku ya hazina, Yesu aliangalia jinsi watu walivyokuwa wakitumbukiza michango yao humo. Matajiri wengi walikuja na kutumbukiza “kutokana na ziada yao.” Lakini Yesu alimtazama sana mjane mmoja maskini. Mjane huyo alitoa mchango wa “sarafu mbili ndogo zenye thamani ndogo sana.”b Alitoa fedha zote alizokuwa nazo. Yesu, ambaye alionyesha kikamili maoni ya Yehova, alisema hivi: “Mjane huyu maskini ametumbukiza zaidi ya wote waliotumbukiza pesa ndani ya masanduku ya hazina.” Kulingana na maneno hayo, machoni pa Yehova, mjane huyo alitumbukiza fedha nyingi kuliko fedha zote zilizotolewa na watu wengine.—Marko 12:41-44; Luka 21:1-4; Yohana 8:28.
15 Je, haishangazi kwamba kati ya watu wote waliokuja hekaluni siku hiyo, ni mjane huyo peke yake ndiye aliyetajwa katika Biblia? Kupitia mfano huo, Yehova anatufundisha kwamba yeye ni Mungu anayethamini mambo tunayofanya. Anapendezwa na michango tunayomtolea kwa nafsi yetu yote, na halinganishi michango yetu na ile ambayo watu wengine wanatoa. Bila shaka, Yehova ametumia njia bora sana kutufundisha ukweli huo wenye kutia moyo!
Mambo Ambayo Biblia Haitaji
16, 17. Yehova anaonyeshaje hekima yake kwa kutoandika mambo fulani katika Neno lake?
16 Unapomwandikia mpendwa wako barua, huwezi kuandika kila jambo. Kwa hiyo, unachagua kwa busara mambo ya kuandika. Vivyo hivyo, Yehova alichagua kuwataja watu na matukio fulani katika Neno lake. Lakini Biblia haielezi kila jambo kuhusiana na masimulizi hayo. (Yohana 21:25) Kwa mfano, Biblia inapozungumzia hukumu ya Mungu, haijibu kila swali tulilo nalo kuhusu hukumu hiyo. Yehova anaonyesha pia hekima yake kwa kutoandika mambo fulani katika Neno lake. Jinsi gani?
17 Biblia imeandikwa kwa njia inayokusudiwa kutusaidia kutambua mambo yaliyo moyoni mwetu. Andiko la Waebrania 4:12 linasema hivi: “Neno [au, ujumbe] la Mungu liko hai nalo ni lenye nguvu na lina makali kuliko upanga wowote wenye makali pande mbili . . . nalo linaweza kutambua fikira na makusudio ya moyo.” Ujumbe wa Biblia hupenya ndani kabisa, na kufunua mawazo na nia yetu halisi. Mara nyingi, wale wanaousoma wakiwa na nia ya kuuchambua wanakwazika wanapopata masimulizi ambayo hayana habari za kutosha kuwaridhisha. Watu wa aina hiyo huenda hata wakatilia shaka ikiwa Yehova ni mwenye upendo, hekima, na haki.
18, 19. (a) Kwa nini hatupaswi kushangaa wakati simulizi fulani la Biblia linapotokeza maswali ambayo hatuwezi kujibu mara moja? (b) Tunahitaji kufanya nini ili kuelewa vizuri Neno la Mungu, na jambo hilo linaonyeshaje hekima kuu ya Yehova?
18 Kwa upande mwingine, tunapojifunza Biblia kwa makini na kwa unyoofu, tunapata kumjua Yehova kama anavyofafanuliwa katika Biblia nzima. Kwa hiyo, hatushangai wakati simulizi fulani la Biblia linapotokeza maswali ambayo hatuwezi kupata majibu mara moja. Kwa mfano: Tunapounganisha vipande vya mchezo wa chemshabongo, huenda tusipate kipande fulani mwanzoni au tusielewe jinsi kipande fulani kinavyoungana na vingine. Lakini, labda tumeunganisha vipande vya kutosha kutusaidia kuelewa jinsi picha kamili itakavyokuwa. Vivyo hivyo, tunapojifunza Biblia hatua kwa hatua, tunajifunza jinsi Yehova Mungu alivyo, na hatimaye tunapata kumjua vizuri. Hata ikiwa mwanzoni hatuelewi simulizi fulani au hatuoni jinsi linavyopatana na utu wa Mungu, tayari tumejifunza kupitia funzo letu la Biblia mambo mengi sana ya kutusadikisha kwamba bila shaka Yehova ni Mungu mwenye upendo, asiyependelea, na mwenye haki.
19 Hivyo, tunaweza kulielewa vizuri Neno la Mungu, ikiwa tu tutasoma na kujifunza tukiwa na nia nzuri. Jambo hilo linaonyesha hekima kuu ya Yehova, sivyo? Wanadamu wenye akili nyingi wanaweza kuandika vitabu ambavyo ni watu “wenye hekima na wenye elimu” tu wanaoweza kuvielewa. Lakini ni Mungu mwenye hekima peke yake anayeweza kuandika kitabu ambacho watu wenye mwelekeo unaofaa tu ndio wanaoweza kukielewa!—Mathayo 11:25.
Kitabu Chenye “Hekima Inayotumika”
20. Kwa nini Yehova peke yake ndiye anayeweza kutuambia njia bora ambayo tunaweza kuifuata maishani, na Biblia inawezaje kutusaidia?
20 Katika Neno lake, Yehova hutuambia njia bora ambayo tunapaswa kuifuata maishani. Akiwa Muumba wetu, anajua vizuri zaidi mahitaji yetu kuliko sisi tunavyoyajua. Na sikuzote wanadamu wamekuwa na mahitaji—yaleyale ya msingi, kama vile—tamaa ya kupendwa, kuwa na furaha, na kuwa na mahusiano mazuri. Biblia ina “hekima inayotumika” ambayo inaweza kutusaidia kuwa na kusudi maishani. (Methali 2:7) Kila sehemu ya kitabu hiki ina sura ambayo inaonyesha jinsi tunavyoweza kutumia ushauri wenye hekima unaopatikana katika Biblia. Tuchunguze mfano mmoja.
21-23. Ni mashauri gani yenye hekima yanayoweza kutusaidia kuwasamehe wengine?
21 Je, umegundua kwamba watu ambao hawapendi kusamehe wengine mara nyingi hujiumiza wenyewe? Kinyongo humlemea sana mtu. Tunapobaki na kinyongo moyoni, tunakuwa na mkazo, na tunakosa amani na shangwe. Utafiti wa kisayansi unasema kwamba kuendelea kuwa na hasira moyoni kunaweza kuongeza uwezekano wa kupata ugonjwa wa moyo na magonjwa mengine mengi ya kudumu. Miaka mingi kabla ya uchunguzi huo wa kisayansi, Biblia ilisema hivi kwa hekima: “Acha hasira na uache ghadhabu.” (Zaburi 37:8) Tunawezaje kufanya hivyo?
22 Neno la Mungu linatoa ushauri huu wenye hekima: “Ufahamu wa mtu hakika hutuliza hasira yake, na ni fahari kwake kuachilia kosa.” (Methali 19:11) Ufahamu ni uwezo wa kuchanganua jambo kwa undani zaidi, kutambua sababu zisizoonekana wazi. Ufahamu hutokeza uelewaji, kwa kuwa unaweza kutusaidia kutambua sababu iliyomfanya mtu mwingine aseme au kutenda kwa njia fulani. Kujitahidi kuelewa nia, hisia, na hali zake kunaweza kutusaidia kuondoa mawazo au hisia zozote mbaya tulizo nazo kumwelekea.
23 Biblia inatupatia ushauri huu pia: “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari.” (Wakolosai 3:13) Maneno “endeleeni kuvumiliana” yanamaanisha hali ya kuwa na subira kuelekea wengine, kuvumilia sifa ambazo huenda zinatuudhi. Subira hiyo inaweza kutusaidia kuepuka kuweka kinyongo moyoni kwa sababu ya mambo madogo-madogo. Maneno “kusameheana” yanamaanisha kuondoa kabisa kinyongo. Mungu wetu mwenye hekima anajua kwamba tunahitaji kuwasamehe wengine kunapokuwa na sababu nzuri ya kufanya hivyo. Tunapowasamehe wengine, hatuwanufaishi tu wale waliotukosea bali pia sisi wenyewe tunakuwa na amani ya akilini na ya moyoni. (Luka 17:3, 4) Kwa kweli, Neno la Mungu lina hekima!
24. Tunapata matokeo gani tunapotumia hekima ya Mungu maishani?
24 Yehova alitaka kuwasiliana nasi kwa sababu anatupenda sana. Alichagua njia bora sana—“barua” iliyoandikwa na wanadamu walioongozwa na roho takatifu. Ndiyo sababu Biblia ina hekima ya Yehova mwenyewe. Hekima hiyo ‘inategemeka sana.’ (Zaburi 93:5) Kadiri tunavyotumia hekima hiyo maishani, na tunavyowafundisha wengine hekima hiyo, ndivyo tunavyozidi kumkaribia zaidi Mungu wetu mwenye hekima. Katika sura inayofuata, tutazungumzia mfano mwingine wenye kuvutia wa hekima ya Yehova ya kuona matukio ya wakati ujao: uwezo wake wa kutabiri matukio ya wakati ujao na kutimiza kusudi lake.
a Kwa mfano, Daudi, aliyekuwa mchungaji, anatumia mifano inayohusiana na ufugaji wa wanyama. (Zaburi 23) Mathayo, ambaye mwanzoni alikuwa mkusanya kodi, mara nyingi anataja tarakimu na thamani ya fedha. (Mathayo 17:27; 26:15; 27:3) Luka, ambaye alikuwa daktari, anatumia maneno yanayohusiana na kazi yake ya udaktari.—Luka 4:38; 14:2; 16:20.
b Kila moja ya sarafu hizo iliitwa leptoni. Hiyo ndiyo iliyokuwa sarafu ya Kiyahudi yenye thamani ndogo zaidi wakati huo. Lepta mbili zilikuwa sawa na thamani ya 1/64 ya mshahara wa siku moja. Sarafu hizo mbili hazikutosha hata kununua shore mmoja, ambaye alikuwa ndege mwenye gharama ya chini sana aliyeliwa na watu maskini.