-
“Hamwijui Ile Siku Wala Saa”Mnara wa Mlinzi—2012 | Septemba 15
-
-
“Hamwijui Ile Siku Wala Saa”
“Kwa hiyo, endeleeni kukesha kwa sababu hamwijui ile siku wala saa.”—MT. 25:13.
-
-
“Hamwijui Ile Siku Wala Saa”Mnara wa Mlinzi—2012 | Septemba 15
-
-
1-3. (a) Ni hali gani zinazoonyesha somo la mifano miwili ambayo Yesu alitoa? (b) Tunahitaji kujibu maswali gani?
WAZIA kwamba ofisa fulani mashuhuri anakuomba umpeleke kwa gari kwenye mkutano muhimu. Hata hivyo, dakika chache kabla ya kwenda kumchukua ili umpeleke kwenye mkutano huo, unagundua kwamba gari halina mafuta ya kutosha. Unahitaji kwenda haraka kuongeza mafuta. Unapoenda, ofisa huyo anawasili. Anakutafuta kila mahali lakini hakupati. Hawezi kungoja, kwa hiyo, anamwomba dereva mwingine ampeleke kwenye mkutano huo. Punde si punde, unafika na kugundua kwamba ofisa huyo alienda zake na kukuacha. Ungehisije?
2 Sasa wazia kwamba wewe ni ofisa huyo na umewachagua wanaume watatu wenye uwezo ili wafanye kazi fulani muhimu. Unawaeleza kuhusu mgawo huo, na wote watatu wanaukubali kwa utayari. Hata hivyo, unaporudi muda mfupi baadaye, unagundua kwamba ni wawili tu kati yao waliofanya kazi uliyowapa. Isitoshe, yule ambaye hakufanya kazi yake anatoa visingizio. Ukweli ni kwamba hata hakujaribu kuifanya. Ungehisije?
3 Katika mifano yake kuhusu mabikira na talanta, Yesu alitumia hali zinazofanana na hizo ili kuonyesha kwa nini katika nyakati za mwisho, baadhi ya Wakristo watiwa-mafuta wangethibitika kuwa waaminifu na wenye busara, lakini wengine hawangekuwa hivyo.a (Mt. 25:1-30) Alikazia somo la mifano hiyo kwa kusema hivi: “Kwa hiyo, endeleeni kukesha kwa sababu hamwijui ile siku wala saa,” yaani, wakati ambapo kwa kweli Yesu atakuja kutekeleza hukumu ya Mungu juu ya ulimwengu wa Shetani. (Mt. 25:13) Tunaweza kutumia shauri hilo leo. Tunaweza kufaidikaje kwa kuendelea kukesha kama Yesu alivyotutia moyo tufanye? Ni nani ambao wamethibitisha kwamba wako tayari kuokolewa? Na ni lazima tufanye nini sasa ili tuendelee kukesha?
-