Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • cl sura 9 kur. 104-115
  • “Kristo Ni Nguvu za Mungu”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Kristo Ni Nguvu za Mungu”
  • Mkaribie Yehova
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Nguvu za Mwana Mzaliwa Pekee wa Mungu
  • Alisema “Maneno Yenye Nguvu”
  • Alifanya ‘Miujiza Yenye Nguvu’
  • Alitumia Nguvu Bila Ubinafsi, kwa Njia Inayofaa, na Huruma
  • Miujiza Ilionyesha Baraka Zitakazokuja
  • Kristo—Nguvu za Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
  • Miujiza ya Yesu Unaweza Kujifunza Nini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Aliwapenda Watu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
  • Yesu Kristo Ni Nani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
Pata Habari Zaidi
Mkaribie Yehova
cl sura 9 kur. 104-115
Yesu akitembea juu ya Bahari ya Galilaya wakati wa usiku wenye dhoruba.

SURA YA 9

“Kristo Ni Nguvu za Mungu”

1-3. (a) Wanafunzi walipatwa na tukio gani lenye kuogopesha katika Bahari ya Galilaya, na Yesu alifanya nini? (b) Kwa nini ilifaa kwa mtume Paulo kusema kwamba “Kristo ni nguvu za Mungu”?

WANAFUNZI waliogopa sana. Dhoruba ilitokea ghafla walipokuwa wakivuka Bahari ya Galilaya kwa mashua. Bila shaka walikuwa wamezoea kuona dhoruba katika bahari hiyo, kwa sababu baadhi yao walikuwa wavuvi hodari sana.a (Mathayo 4:18, 19) Lakini hiyo ilikuwa “dhoruba kali ya upepo.” Bahari ilichafuka kwa sababu ya dhoruba hiyo. Wanaume hao walijitahidi sana kuongoza mashua, lakini dhoruba ilikuwa kali sana. Mawimbi makubwa “yakaipiga mashua,” na ikaanza kujaa maji. Licha ya vurugu hiyo, Yesu alikuwa amelala usingizi katika tezi, akiwa amechoka baada ya kuwafundisha watu siku nzima. Wanafunzi waliogopa kwamba watakufa hivyo walimwamsha na kumsihi hivi: “Bwana, tuokoe, tuko karibu kuangamia!”​—Marko 4:35-38; Mathayo 8:23-25.

2 Yesu hakuogopa. Kwa ujasiri, aliukemea upepo na bahari: “Nyamaza! Tulia!” Mara moja, upepo na bahari vikatii—dhoruba ikakoma, mawimbi yakatulia tuli, “kukawa shwari kabisa.” Wanafunzi wakashangaa na wakasema: “Huyu ni mtu wa aina gani?” Kwa kweli, ni mwanadamu gani angeweza kuukemea upepo na bahari kana kwamba anamkemea mtoto mtukutu?​—Marko 4:39-41; Mathayo 8:26, 27.

3 Lakini Yesu hakuwa mwanadamu wa kawaida. Yehova alidhihirisha nguvu zake kupitia Yesu, na Yesu alizitumia kwa njia za pekee sana. Mtume Paulo aliongozwa na roho takatifu kusema hivi: “Kristo ni nguvu za Mungu.” (1 Wakorintho 1:24) Mungu anaonyeshaje nguvu zake kupitia Yesu? Na jinsi Yesu anavyotumia nguvu hizo kunaweza kuwa na matokeo gani maishani mwetu?

Nguvu za Mwana Mzaliwa Pekee wa Mungu

4, 5. (a) Yehova alimpa Mwana wake mzaliwa pekee nguvu na mamlaka ya kufanya nini? (b) Mwana huyo angetumia nini kutimiza kusudi la uumbaji la Baba yake?

4 Fikiria nguvu alizokuwa nazo Yesu kabla ya kuja duniani. Yehova alitumia “nguvu zake za milele” alipomuumba Mwana wake mzaliwa pekee, ambaye jina lake ni Yesu Kristo. (Waroma 1:20; Wakolosai 1:15) Baadaye, Yehova alimpa Mwana huyo mamlaka na nguvu nyingi sana. Alimpa kazi ya kutimiza kusudi Lake la kuumba. Biblia inasema hivi kumhusu Mwana huyo: “Vitu vyote vilikuja kuwako kupitia kwake, na bila yeye hakuna hata kitu kimoja kilichokuja kuwako.”​—Yohana 1:3.

5 Hatuwezi kufahamu kikamili ukubwa wa mgawo huo. Hebu wazia nguvu zinazohitajiwa kuumba mamilioni ya malaika wenye uwezo, mabilioni ya makundi ya nyota, dunia, na viumbe wote waliomo. Ili kutimiza kazi hiyo, Yehova alimpatia Mwana wake nguvu isiyo na kifani, yaani, roho takatifu. Mwana huyo alifurahia kuwa Mfanyakazi Stadi, na alitumiwa na Yehova kuumba vitu vingine vyote.​—Methali 8:22-31.

6. Baada ya kufa na kufufuliwa, Yesu alipewa nguvu na mamlaka gani?

6 Je, Mwana huyo mzaliwa pekee angeweza kupewa nguvu na mamlaka zaidi? Yesu alisema hivi baada ya kufa na kufufuliwa: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.” (Mathayo 28:18) Ndiyo, Yesu amepewa uwezo na haki ya kutawala viumbe vyote. Akiwa “Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana,” amepewa mamlaka ya ‘kuangamiza serikali yote na mamlaka yote na nguvu zote’​—zinazoonekana na zile zisizoonekana—ambazo zinampinga Baba yake. (Ufunuo 19:16; 1 Wakorintho 15:24-26) ‘Vitu vyote vilitiishwa chini ya’ Yesu, isipokuwa Yehova Mungu mwenyewe.​—Waebrania 2:8; 1 Wakorintho 15:27.

7. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba kamwe Yesu hatatumia vibaya nguvu alizopewa na Yehova?

7 Je, tuna wasiwasi kwamba huenda Yesu akatumia nguvu zake vibaya? Hapana! Yesu anampenda sana Baba yake na hawezi kamwe kutenda jambo lolote lisilompendeza. (Yohana 8:29; 14:31) Yesu anajua vizuri kwamba Yehova hawezi kamwe kutumia nguvu zake vibaya. Yesu ameona kwamba Yehova hutafuta fursa “ili adhihirishe nguvu zake kwa niaba ya wale ambao moyo wao ni kamili kumwelekea yeye.” (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Bila shaka, Yesu anawapenda wanadamu kama Baba yake anavyowapenda, kwa hiyo tunaweza kuwa na uhakika kwamba sikuzote Yesu atatumia nguvu zake kwa manufaa yetu. (Yohana 13:1) Yesu hajawahi kamwe kutumia nguvu zake vibaya. Sasa, tuchunguze nguvu alizokuwa nazo alipokuwa duniani na jinsi alivyozitumia.

Alisema “Maneno Yenye Nguvu”

8. Baada ya kutiwa mafuta, Yesu alipewa nguvu za kufanya nini, naye alitumiaje nguvu zake?

8 Yesu alipokuwa mvulana huko Nazareti, hakufanya miujiza. Lakini hilo lilibadilika alipobatizwa mwaka wa 29 W.K., akiwa na miaka 30 hivi. (Luka 3:21-23) Biblia inatuambia hivi: ‘Mungu alimtia mafuta kwa roho takatifu na nguvu, naye akapita katika nchi akitenda mema na kuwaponya wote waliokandamizwa na Ibilisi.’ (Matendo 10:38) Bila shaka, maneno “akitenda mema” yanaonyesha kwamba alitumia nguvu zake ifaavyo. Baada ya kutiwa mafuta, akawa “nabii aliyefanya miujiza na kusema maneno yenye nguvu.”​—Luka 24:19.

9-11. (a) Mara nyingi Yesu alifundisha wapi, na alikabili changamoto gani? (b) Kwa nini umati ulishangazwa na njia ya Yesu ya kufundisha?

9 Yesu alikuwa mwenye nguvu katika neno jinsi gani? Mara nyingi alifundisha nje—kando ya ziwa, milimani, barabarani na kwenye masoko. (Marko 6:53-56; Luka 5:1-3; 13:26) Wale waliomsikiliza walikuwa huru kuondoka ikiwa maneno yake hayakuwapendeza. Wasikilizaji waliothamini mafundisho ya Yesu walihifadhi mafundisho hayo katika akili na mioyo yao kwa sababu hawakuwa na vitabu wakati huo. Hivyo, Yesu alihitaji kufundisha kwa njia yenye kugusa moyo sana, iliyo wazi, na yenye kueleweka kwa urahisi. Hilo halikuwa tatizo kwa Yesu. Hebu fikiria Mahubiri yake ya Mlimani.

10 Asubuhi moja mapema mwaka wa 31 W.K., umati ulikusanyika mlimani karibu na Bahari ya Galilaya. Baadhi yao walikuwa wametoka Yudea na Yerusalemu, umbali wa kilomita 100 hadi 110 hivi. Wengine walikuwa wametoka upande wa kaskazini katika eneo la pwani la Tiro na Sidoni. Wagonjwa wengi walimkaribia Yesu na kumgusa, naye aliwaponya wote. Baada ya kuwaponya wagonjwa wote, alianza kufundisha. (Luka 6:17-19) Alipomaliza kuwafundisha, walishangazwa na mambo waliyosikia. Kwa nini?

11 Miaka mingi baadaye, mmoja wa waliosikia mahubiri hayo aliandika hivi: “Umati ukashangazwa na njia yake ya kufundisha, kwa maana alikuwa akiwafundisha kama mtu mwenye mamlaka.” (Mathayo 7:28, 29) Walihisi kwamba Yesu alizungumza kwa mamlaka. Alimwakilisha Mungu na mafundisho yake yalitegemea Neno la Mungu. (Yohana 7:16) Yesu aliwafundisha kwa maneno yaliyoeleweka, aliwasadikisha, na kutoa sababu zisizoweza kupingwa. Alikazia mambo muhimu na kugusa mioyo ya wasikilizaji wake. Aliwafundisha jinsi ya kupata furaha, kusali, kutafuta Ufalme wa Mungu, na kuwa na wakati ujao salama. (Mathayo 5:3–7:27) Maneno yake yalichochea mioyo ya wale waliokuwa na njaa ya uadilifu na kweli. Watu hao walikuwa tayari ‘kujikana’ wenyewe na kuacha kila kitu ili wamfuate. (Mathayo 16:24; Luka 5:10, 11) Hilo lilithibitisha kwamba maneno ya Yesu yalikuwa yenye nguvu!

Alifanya ‘Miujiza Yenye Nguvu’

12, 13. Yesu alifanya ‘miujiza yenye nguvu’ jinsi gani, naye alifanya miujiza gani mbalimbali?

12 Yesu alifanya ‘miujiza yenye nguvu.’ (Luka 24:19) Vitabu vya Injili vinataja miujiza hususa zaidi ya 30 ambayo Yesu alifanya—kwa maana ‘Yehova alikuwa amempa nguvu.’b (Luka 5:17) Maelfu ya watu walinufaika na miujiza ya Yesu. Fikiria miujiza hii miwili—alipolisha wanaume 5,000 na baadaye wanaume 4,000. Ukitia ndani wanawake na watoto, huenda umati huo ulikuwa na maelfu ya watu zaidi!—Mathayo 14:13-21; 15:32-38.

13 Yesu alifanya miujiza mbalimbali. Alikuwa na mamlaka ya kudhibiti roho waovu naye aliwafukuza kwa urahisi sana kutoka kwa watu. (Luka 9:37-43) Alikuwa na mamlaka juu ya vitu vya asili—aligeuza maji yakawa divai. (Yohana 2:1-11) Wanafunzi wake walishangaa ‘walipomwona Yesu akitembea juu ya bahari.’ (Yohana 6:18, 19) Alikuwa na uwezo wa kuponya ulemavu, magonjwa sugu, na magonjwa hatari. (Marko 3:1-5; Yohana 4:46-54) Aliponya kwa njia mbalimbali. Baadhi ya watu aliowaponya walikuwa mbali, na wengine aliwaponya kwa kuwagusa. (Mathayo 8:2, 3, 5-13) Baadhi ya watu aliwaponya mara moja na wengine aliwaponya hatua kwa hatua.​—Marko 8:22-25; Luka 8:43, 44.

“Wakamwona Yesu akitembea juu ya bahari”

14. Yesu alionyesha kwamba alikuwa na nguvu za kufufua katika hali gani mbalimbali?

14 Jambo la kupendeza hata zaidi, Yesu alikuwa na nguvu za kuwafufua wafu. Biblia inasema kwamba aliwafufua watu watatu. Alimfufua binti mwenye umri wa miaka 12 na kumrudisha kwa wazazi wake, alimfufua mwana wa pekee wa mjane, na akamfufua ndugu mpendwa wa dada fulani. (Luka 7:11-15; 8:49-56; Yohana 11:38-44) Yesu aliweza kumfufua mtu katika hali zozote. Alimfufua yule msichana mwenye umri wa miaka 12 muda mfupi baada ya kufa. Alimfufua mwana wa mjane kutoka kwenye jeneza siku ileile aliyokufa. Naye Lazaro alifufuliwa na Yesu baada ya kukaa siku nne kaburini.

Alitumia Nguvu Bila Ubinafsi, kwa Njia Inayofaa, na Huruma

15, 16. Kuna uthibitisho gani kwamba Yesu hakutumia nguvu zake kwa ubinafsi?

15 Hebu wazia jinsi ambavyo mtawala asiye mkamilifu angeweza kuwakandamiza watu ikiwa angepewa nguvu za Yesu. Lakini Yesu hakuwa na dhambi. (1 Petro 2:22) Hakujiruhusu kuathiriwa na ubinafsi, tamaa ya kutaka makuu, na pupa ambayo huwafanya wanadamu wasio wakamilifu watumie mamlaka yao kuwakandamiza wengine.

16 Yesu hakutumia nguvu zake kwa ubinafsi ili kujinufaisha. Alipohisi njaa, alikataa kugeuza mawe yawe mkate. (Mathayo 4:1-4) Yesu hakuwa na mali nyingi. Hilo linaonyesha kwamba hakutumia nguvu zake kujitajirisha. (Mathayo 8:20) Kuna mambo mengine yanayothibitisha kwamba hakufanya miujiza kwa sababu ya ubinafsi. Alipofanya miujiza, alijidhabihu kwa kadiri fulani. Nguvu zilimtoka alipowaponya wagonjwa. Alihisi nguvu zikimtoka hata alipomponya mtu mmoja tu. (Marko 5:25-34) Na bado aliruhusu umati umguse, naye akawaponya. (Luka 6:19) Kwa kweli, Yesu hakuwa na ubinafsi.

17. Yesu alitumiaje nguvu zake kwa njia inayofaa?

17 Yesu alitumia nguvu zake kwa njia inayofaa. Hakufanya miujiza ili kujionyesha au kuwastaajabisha watu. (Mathayo 4:5-7) Alikataa kufanya miujiza ili kumfurahisha tu Herode. (Luka 23:8, 9) Badala ya kutangaza nguvu zake, mara nyingi Yesu aliwaagiza wale aliowaponya wasimwambie mtu yeyote. (Marko 5:43; 7:36) Hakutaka watu waamini kwamba alikuwa Masihi kwa sababu tu walisikia habari zenye kusisimua kuhusu miujiza aliyofanya.​—Mathayo 12:15-19.

18-20. (a) Yesu alionyesha sifa zipi alipotumia nguvu zake? (b) Unahisije kuhusu jinsi ambavyo Yesu alimponya mwanamume mmoja aliyekuwa kiziwi?

18 Ingawa Yesu alikuwa na nguvu nyingi, alikuwa tofauti kabisa na watawala ambao wamekuwa wakitumia nguvu zao bila kujali mahitaji na kuteseka kwa wengine. Yesu aliwajali watu. Alisikitika sana alipowaona watu wakiteseka hivi kwamba alichochewa kukomesha mateso yao. (Mathayo 14:14) Alijali hisia na mahitaji yao, hivyo alitumia nguvu zake kwa upendo. Kisa kimoja kinachogusa moyo kinapatikana kwenye Marko 7:31-37.

19 Pindi hiyo, umati mkubwa ulimfikia Yesu na kumletea wagonjwa wengi, naye akawaponya wote. (Mathayo 15:29, 30) Hata hivyo, Yesu alitambua kwamba mwanamume mmoja alihitaji msaada wa pekee. Mtu huyo alikuwa kiziwi na mwenye tatizo la kuzungumza. Inaelekea Yesu alitambua wasiwasi au aibu ya mtu huyo. Yesu alionyesha kwamba anamjali kwa kumpeleka faraghani, mbali na umati. Kisha Yesu akamwonyesha ishara fulani ili kumjulisha jambo ambalo alitaka kufanya. Akaweka ‘vidole masikioni mwa mtu huyo, baada ya kutema mate, akamgusa ulimi.’c (Marko 7:33) Kisha, Yesu akatazama juu mbinguni na kuvuta pumzi kwa nguvu huku akisali. Ni kana kwamba alikuwa akimwambia mtu huyo, ‘Muujiza ninaotaka kukufanyia unategemea nguvu za Mungu.’ Hatimaye, Yesu akasema: “Funguka.” (Marko 7:34) Basi, masikio yake yakafunguliwa, kisha mtu huyo akaanza kuzungumza vizuri.

20 Inatia moyo sana kujua kwamba Yesu alijali hisia za wagonjwa aliowaponya kwa nguvu za Mungu! Je, haifariji kujua kwamba Yehova amemchagua Mtawala anayejali na mwenye huruma ili awe Mtawala wa Ufalme wake wa Kimasihi?

Miujiza Ilionyesha Baraka Zitakazokuja

21, 22. (a) Miujiza ya Yesu ilionyesha nini? (b) Kwa kuwa Yesu anaweza kudhibiti nguvu za asili, tunaweza kutarajia nini chini ya Ufalme wake?

21 Miujiza ambayo Yesu alifanya duniani ilionyesha kwamba baraka nyingi sana zitaletwa na Ufalme wake. Katika ulimwengu mpya wa Mungu, Yesu atafanya tena miujiza—lakini katika pindi hii atafanya hivyo ulimwenguni pote! Ni mambo gani yenye kusisimua tunayotarajia wakati ujao?

22 Yesu atarekebisha uharibifu wote wa mazingira. Kumbuka kwamba alionyesha uwezo wake wa kudhibiti nguvu za asili kwa kutuliza dhoruba kali. Hivyo, wakati wa utawala wa Ufalme wa Kristo, wanadamu hawatahitaji kuogopa vimbunga, matetemeko ya ardhi, milipuko ya volkano, au misiba mingine ya asili. Kwa kuwa Yesu ni Mfanyakazi Stadi aliyetumiwa na Yehova kuumba dunia na viumbe wote, anajua kila kitu kuhusu dunia. Anajua jinsi ya kutumia ifaavyo rasilimali za dunia. Wakati wa utawala wake, dunia nzima itakuwa Paradiso.​—Luka 23:43.

23. Akiwa Mfalme, Yesu atatoshelezaje mahitaji ya wanadamu?

23 Vipi kuhusu mahitaji ya wanadamu? Uwezo wa Yesu wa kulisha maelfu ya watu kwa vyakula vichache tu unatuhakikishia kwamba utawala wake utakomesha kabisa njaa. Kwa kweli, njaa itakoma milele kwa sababu kila mtu atakuwa na chakula cha kutosha. (Zaburi 72:16) Uwezo wa Yesu wa kuponya unatuhakikishia kwamba wagonjwa, vipofu, viziwi, na vilema wataponywa—kabisa. (Isaya 33:24; 35:5, 6) Uwezo wake wa kufufua wafu unatuhakikishia kwamba akiwa Mfalme wa mbinguni, ana nguvu za kufufua mamilioni ya watu ambao Baba yake anawakumbuka.​—Yohana 5:28, 29.

24. Tunapotafakari kuhusu nguvu za Yesu, tunapaswa kukumbuka nini, na kwa nini?

24 Tunapotafakari kuhusu nguvu za Yesu, tukumbuke kwamba Mwana huyo humwiga kikamili Baba yake. (Yohana 14:9) Jinsi Yesu anavyotumia nguvu zake kunatuonyesha waziwazi namna Yehova anavyotumia nguvu zake. Kwa mfano, fikiria jinsi ambavyo Yesu alimponya kwa fadhili mtu fulani mwenye ukoma. Yesu alimsikitikia mtu huyo, akamgusa na kumwambia: “Ninataka.” (Marko 1:40-42) Kupitia masimulizi kama hayo, ni kana kwamba Yehova anasema, ‘Hivyo ndivyo ninavyotumia nguvu zangu!’ Je, wewe huchochewi kumsifu Mungu wetu mweza yote na kumshukuru kwa sababu anatumia nguvu zake kwa upendo?

a Bahari ya Galilaya hupata dhoruba za ghafla mara nyingi. Kwa sababu bahari hiyo iko chini sana (mita 200 chini ya usawa wa bahari), eneo hilo lina joto kuliko maeneo ya karibu, kwa hiyo, hali ya hewa hubadilika ghafla. Upepo mkali huvuma kwenye Bonde la Yordani kutoka kwenye Mlima Hermoni ulio kaskazini. Dhoruba kali inaweza kutokea ghafla na kuvuruga bahari.

b Kwa kuongezea, nyakati nyingine Vitabu vya Injili hutaja miujiza mingi kwa ujumla. Kwa mfano, pindi moja “jiji lote” lilikuja kumwona, naye akawaponya wagonjwa “wengi.”​—Marko 1:32-34.

c Kutema mate kulikuwa njia au ishara ya kuponya iliyokubaliwa na Wayahudi na Watu wa Mataifa. Na maandishi ya marabi yanataja tiba ya kutumia mate. Huenda Yesu alitema mate ili kumjulisha mtu huyo kwamba alitaka kumponya. Vyovyote vile, Yesu hakuwa akitumia mate yake kama dawa ya asili.

Maswali ya Kutafakari

  • Isaya 11:1-5 Yesu anatumiaje “roho ya . . . nguvu,” na tunaweza kuwa na uhakika gani kuhusu utawala wake?

  • Marko 2:1-12 Uponyaji wa Yesu wa kimuujiza unaonyesha amepewa mamlaka gani?

  • Yohana 6:25-27 Ingawa Yesu alitosheleza kimuujiza mahitaji ya kimwili ya watu, lengo kuu la huduma yake lilikuwa nini?

  • Yohana 12:37-43 Kwa nini baadhi ya watu ambao waliiona miujiza ya Yesu hawakumwamini, na hilo linatufundisha nini?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki