Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Uwe Mfuasi Wangu”—Yesu alimaanisha nini?
    ‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
    • SURA YA KWANZA

      Yesu Alimaanisha Nini Aliposema—“Uwe Mfuasi Wangu”?

      Mtawala kijana tajiri akiwa amepiga magoti huku akimuuliza Yesu maswali.

      “Ninapaswa kufanya nini ili niurithi uzima wa milele?”

      1, 2. Ni mwaliko gani bora zaidi ambao mwanadamu anaweza kupata, na tunaweza kujiuliza swali gani?

      NI MWALIKO gani bora zaidi uliowahi kupata? Huenda ni wakati ulipoalikwa kuhudhuria tukio la pekee, kama vile harusi ya watu unaowapenda sana. Au huenda ni siku uliyokaribishwa kufanya kazi muhimu. Ikiwa umewahi kupata mialiko kama hiyo, bila shaka ulifurahi na uliliona kuwa pendeleo kubwa sana. Hata hivyo, ukweli ni kwamba umepata mwaliko bora hata zaidi. Kila mmoja wetu amepata mwaliko huo. Na maisha yetu hutegemea sana ikiwa tunaukubali au kuukataa. Huo ndio uamuzi muhimu zaidi tutakaofanya maishani.

      2 Ni mwaliko gani huo? Ni mwaliko kutoka kwa Yesu Kristo, Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu Mweza Yote, Yehova, nao unapatikana katika Biblia. Yesu alisema hivi katika Marko 10:21: ‘Njoo uwe mfuasi wangu.’ Huo ni mwaliko wa Yesu kwa kila mmoja wetu. Tunapaswa kujiuliza, ‘Nitaitikiaje mwaliko huo?’ Huenda jibu likaonekana kuwa wazi. Ni nani anayeweza kukataa mwaliko mzuri kama huo? Jambo la kushangaza ni kwamba watu wengi huukataa. Kwa nini?

      3, 4. (a) Mtu aliyemwendea Yesu kuuliza kuhusu uzima wa milele alikuwa na mambo gani ambayo watu wangeweza kuyaonea wivu? (b) Huenda Yesu aliona sifa gani nzuri za kijana huyo tajiri mwenye mamlaka?

      3 Kwa mfano, mfikirie mwanamume mmoja aliyepata mwaliko huo moja kwa moja miaka 2,000 hivi iliyopita. Aliheshimiwa sana. Alikuwa na angalau mambo matatu ambayo wanadamu huyatamani, au hata kuyaonea wivu—ujana, mali, na mamlaka. Biblia inamtaja kuwa “mwanamume kijana,” aliyekuwa “tajiri sana,” na “mtawala.” (Mathayo 19:20; Luka 18:18, 23) Hata hivyo, kijana huyo alikuwa na sifa nyingine muhimu zaidi. Alikuwa amesikia kumhusu Mwalimu Mkuu, Yesu, naye alipenda mambo aliyosikia.

      4 Watawala wengi wa siku hizo hawakumpa Yesu heshima aliyostahili. (Yohana 7:48; 12:42) Lakini mtawala huyo alitenda kwa njia tofauti. Biblia inatuambia hivi: “[Yesu] alipokuwa akiondoka, mwanamume fulani akamkimbilia, akapiga magoti mbele yake na kumuuliza: ‘Mwalimu Mwema, ninapaswa kufanya nini ili niurithi uzima wa milele?’” (Marko 10:17) Ona jinsi ambavyo kijana huyo alivyotamani sana kuzungumza na Yesu, hata alimkimbilia Yesu hadharani, kama tu jinsi ambavyo maskini na watu wa hali ya chini wangefanya. Isitoshe, alipiga magoti kwa heshima mbele ya Kristo. Hivyo, kwa kadiri fulani alikuwa mnyenyekevu na alitambua uhitaji wake wa kiroho. Yesu alithamini sifa hizo nzuri. (Mathayo 5:3; 18:4) Basi, haishangazi kwamba ‘Yesu alimtazama na kumpenda.’ (Marko 10:21) Yesu alimjibu kijana huyo jinsi gani?

      Mwaliko wa Pekee

      5. Yesu alimjibu kijana huyo tajiri jinsi gani, na kwa nini “jambo moja” alilokosa si umaskini? (Ona pia maelezo ya chini.)

      5 Yesu alionyesha kwamba tayari Baba yake alikuwa amejibu swali hilo muhimu kuhusu kupata uzima wa milele. Alirejelea Maandiko, naye kijana huyo akasisitiza kwamba alikuwa akitii Sheria ya Musa kwa uaminifu. Hata hivyo, kwa kuwa alikuwa na utambuzi wa pekee, Yesu angeweza kuona mambo yaliyokuwa moyoni mwa kijana huyo. (Yohana 2:25) Alitambua kwamba mtawala huyo ana tatizo kubwa la kiroho. Hivyo, Yesu akamwambia: “Bado unahitaji kufanya jambo moja.” Ni “jambo” gani hilo? Yesu alimwambia: “Nenda ukauze vitu ulivyo navyo, uwape maskini.” (Marko 10:21) Je, Yesu alimaanisha kwamba ni lazima mtu awe maskini ili amtumikie Mungu? Hapana.a Kristo alikuwa akifunua jambo fulani muhimu.

      6. Yesu alitoa mwaliko gani, na jibu la kijana huyo tajiri lilifunua jambo gani lililokuwa katika moyo wake?

      6 Ili kuonyesha waziwazi jambo ambalo kijana huyo alikosa, Yesu alimpa mwaliko huu wa pekee: ‘Njoo uwe mfuasi wangu.’ Hebu wazia—Mwana wa Mungu Aliye Juu Zaidi alimwalika mwanamume huyo uso kwa uso, ili amfuate! Pia, Yesu aliahidi kumthawabisha kwa njia kubwa sana. Alimwambia: “Utakuwa na hazina mbinguni.” Je, kijana huyo tajiri alikubali mwaliko huo wa pekee? Masimulizi hayo yanasema: “Akasikitishwa na jibu hilo, akaenda zake akiwa na huzuni, kwa maana alikuwa na mali nyingi.” (Marko 10:21, 22) Hivyo, maneno hayo ya Yesu yasiyotazamiwa yalifunua tatizo lililokuwa katika moyo wa mwanamume huyo. Alipenda sana mali zake, na bila shaka alipenda pia umaarufu na mamlaka aliyopata kwa sababu ya mali hizo. Inasikitisha kwamba alipenda sana vitu hivyo kuliko alivyompenda Kristo. Basi, “jambo moja” ambalo kijana huyo alikosa ni kumpenda Yehova na Yesu kwa moyo wake wote. Kwa kuwa mwanamume huyo kijana hakuwa na upendo huo, alikataa mwaliko huo wa pekee! Hata hivyo, mwaliko huo unakuhusu wewe jinsi gani?

      7. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba mwaliko wa Yesu unatuhusu sisi pia leo?

      7 Mwaliko wa Yesu haukuwa kwa ajili ya mwanamume huyo tu wala watu wachache. Yesu alisema: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, . . . na aendelee kunifuata.” (Luka 9:23) Ona kwamba “mtu yeyote” anaweza kuwa mfuasi wa Kristo ikiwa kwa kweli ‘anataka.’ Mungu anawavuta watu wenye mioyo minyoofu kwa Mwana wake. (Yohana 6:44) Si matajiri, maskini, watu wa jamii au taifa fulani, au wale walioishi katika kipindi chake cha wakati, bali watu wote wanapewa nafasi ya kukubali mwaliko wa Yesu. Hivyo, maneno ya Yesu ‘Njoo uwe mfuasi wangu,’ yanakuhusu wewe pia. Hata hivyo, kwa nini utake kumfuata Kristo? Na kumfuata kunahusisha nini?

  • “Uwe Mfuasi Wangu”—Yesu alimaanisha nini?
    ‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
    • a Yesu hakumwambia kila mtu aliyemfuata aache mali zake zote. Na ingawa alisema ingekuwa vigumu sana kwa tajiri kuingia katika Ufalme wa Mungu, aliongeza hivi: “Mambo yote yanawezekana kwa Mungu.” (Marko 10:23, 27) Kwa kweli, baadhi ya watu matajiri walikuja kuwa wafuasi wa Kristo. Walipata shauri hususa katika kutaniko la Kikristo, lakini hawakuagizwa wawape maskini mali zao zote.​—1 Timotheo 6:17.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki