Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • cf sura 14 kur. 163-175
  • “Umati Mkubwa Ukamjia”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Umati Mkubwa Ukamjia”
  • ‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Watu Wengi Walifurahia Kuwa Pamoja na Yesu
  • Kwa Nini Watu Walijihisi Huru Kumkaribia Yesu?
  • Je, Watu Wanajihisi Huru Kukukaribia?
  • Je! Wewe Unaambilika Kweli?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Thamini Kikamili Sifa za Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Iga Unyenyekevu wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Je, Una “Akili ya Kristo”?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
Pata Habari Zaidi
‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
cf sura 14 kur. 163-175

SURA YA KUMI NA NNE

“Umati Mkubwa Ukamjia”

Kwa upendo, Yesu anawakumbatia watoto wadogo wenye umri tofauti-tofauti huku wazazi wao wakiwatazama.

“Waacheni watoto wadogo waje kwangu”

1-3. Ni nini kinachotokea wazazi wanapowaleta watoto wao kwa Yesu, na kisa hicho kinaonyesha nini kumhusu Yesu?

YESU alijua kwamba anakaribia sana mwisho wa maisha yake duniani. Ni majuma machache tu yalikuwa yamebaki, na bado alikuwa na kazi nyingi sana ya kufanya! Anahubiri pamoja na mitume wake huko Perea, eneo lililo upande wa mashariki wa Mto Yordani. Wanahubiri wakielekea Yerusalemu, ambako Yesu atahudhuria kwa mara ya mwisho Pasaka itakayomalizika kwa tukio la pekee sana.

2 Baada ya Yesu kuwa na mazungumzo muhimu pamoja na viongozi fulani wa dini, kunakuwa na vurugu kidogo. Watu wanawaleta watoto wao wamwone. Inaonekana watoto hao wana umri mbalimbali, kwa kuwa Marko anawataja kwa kutumia neno lilelile alilotumia alipokuwa akizungumzia mtoto wa miaka 12, na Luka anatumia neno linaloweza kutafsiriwa ‘watoto wadogo.’ (Luka 18:15; Marko 5:41, 42; 10:13) Bila shaka, kwa kawaida mahali popote penye watoto huwa na kelele na vurugu. Wanafunzi wa Yesu wanawakemea wazazi, labda wakifikiri kwamba Bwana ana shughuli nyingi sana hivi kwamba hawezi kuwa pamoja na watoto. Yesu anafanya nini?

3 Yesu anapoona kinachoendelea, anakasirika. Ni nani wanaomkasirisha? Je, ni watoto au wazazi? Hapana, Badala yake ni wanafunzi wake! Anasema: “Waacheni watoto wadogo waje kwangu; msijaribu kuwazuia, kwa maana Ufalme wa Mungu ni wa wale walio kama hao. Kwa kweli ninawaambia, yeyote asiyeupokea Ufalme wa Mungu kama mtoto mdogo hataingia kamwe ndani yake.” Kisha, Yesu “akawakumbatia” watoto hao na kuwabariki. (Marko 10:13-16) Maneno ambayo Marko anatumia hapa yanadokeza kwamba Yesu anawakumbatia kwa shauku, labda hata akiwabeba watoto fulani wadogo. Ni wazi kwamba Yesu anawapenda watoto. Hata hivyo, kisa hicho kinatufundisha jambo lingine kumhusu, kwamba watu walikuwa huru kumkaribia.

4, 5. (a) Ni nini kinachotuonyesha kwamba ilikuwa rahisi kumkaribia Yesu? (b) Tutachunguza maswali gani katika sura hii?

4 Ikiwa Yesu angekuwa mtu mkali, asiye na urafiki, au mwenye kiburi, huenda watoto hao hawangevutiwa naye wala wazazi wao hawangekuwa huru kumkaribia. Hebu wazia jinsi wazazi wa watoto hao wanavyohisi mtu huyo mwenye fadhili anapowaonyesha upendo watoto wao, anapowabariki na kusema kwamba watoto hao ni wenye thamani machoni pa Mungu! Kwa kweli, ingawa Yesu alikuwa na majukumu mazito sana, watu walipenda kumkaribia zaidi kuliko mwanadamu mwingine yeyote.

5 Ni nani wengine waliokuwa huru kumkaribia Yesu? Kwa nini ilikuwa rahisi kuzungumza na Yesu? Nasi tunawezaje kumwiga Yesu katika jambo hilo? Acheni tuone.

Watu Wengi Walifurahia Kuwa Pamoja na Yesu

6-8. Mara nyingi Yesu alishirikiana na nani, na mtazamo wake kuwaelekea watu hao ulitofautiana jinsi gani na ule wa viongozi wa kidini?

6 Unaposoma masimulizi ya Injili, huenda ukashangazwa kuona jinsi watu wengi walivyokuwa huru kumkaribia Yesu. Kwa mfano, anapozungumziwa, mara nyingi tunasoma kuhusu “umati mkubwa.” “Umati mkubwa ukamfuata kutoka Galilaya.” “Umati mkubwa sana ukakusanyika karibu naye.” “Umati mkubwa ukamjia.” “Alikuwa akisafiri pamoja na umati mkubwa.” (Mathayo 4:25; 13:2; 15:30; Luka 14:25) Ndiyo, mara nyingi, Yesu alizungukwa na umati wa watu.

7 Kwa ujumla, hao walikuwa watu wa kawaida ambao viongozi wa kidini waliwaita kwa dharau “watu wa nchi.” Mafarisayo na makuhani walisema hivi waziwazi: “Umati huu usiojua Sheria ni watu waliolaaniwa.” (Yohana 7:49) Baadaye, maandishi ya marabi yalithibitisha maoni hayo. Viongozi wengi wa kidini waliwaona watu hao kuwa watu wa kudharaulika, wakakataa kula nao, kununua kutoka kwao, au kushirikiana nao. Hata baadhi yao walisisitiza kwamba watu hao wasiojua sheria ya mdomo hawana tumaini la ufufuo! Hiyo ndiyo sababu watu wengi wa hali ya chini waliwaepuka viongozi hao badala ya kuwaomba msaada au mwongozo. Lakini Yesu alikuwa tofauti.

8 Yesu alishirikiana kwa uhuru na watu wa kawaida. Alikula pamoja nao, aliwaponya, aliwafundisha, na kuwapa tumaini. Bila shaka, Yesu aliona mambo kihalisi, akitambua kwamba wengi wangekataa kumtumikia Yehova. (Mathayo 7:13, 14) Hata hivyo, alikuwa na maoni yanayofaa kuhusu kila mtu, naye alijua kwamba wengi wanaweza kutenda mema. Alikuwa tofauti kabisa na makuhani na Mafarisayo wenye mioyo migumu! Hata hivyo, inashangaza kwamba hata makuhani na Mafarisayo walimkaribia Yesu, na baadhi yao walibadili njia zao na kumfuata. (Matendo 6:7; 15:5) Pia, baadhi ya watu waliokuwa matajiri na wenye mamlaka walikuwa huru kumkaribia Yesu.​—Marko 10:17, 22.

9. Kwa nini wanawake walikuwa huru kumkaribia Yesu?

9 Wanawake walijihisi huru kumkaribia Yesu. Mara nyingi, walidharauliwa sana na viongozi wa kidini. Kwa kawaida marabi walidharau wazo la kuwafundisha wanawake. Wanawake hata hawakuruhusiwa kutoa ushahidi katika kesi za kisheria; walionwa kuwa mashahidi wasiotegemeka. Marabi hata walitoa sala ya kumshukuru Mungu kwamba wao si wanawake! Lakini Yesu hakuwadharau wanawake. Wengi wao walimkaribia wakitaka kujifunza. Kwa mfano, Maria, dada ya Lazaro, aliketi miguuni pa Bwana, akisikiliza kwa makini maneno ya Yesu huku dada yake, Martha, akijishughulisha na kuhangaikia sana kutayarisha chakula. Yesu alimpongeza Maria kwa kutanguliza mambo muhimu.​—Luka 10:39-42.

10. Tofauti na viongozi wa kidini, Yesu aliwatendeaje wagonjwa?

10 Pia, wagonjwa wengi walimwendea Yesu ingawa mara nyingi viongozi wa kidini waliwaona kuwa watu wasiopaswa kuwa katika jamii. Sheria ya Musa ilisema kwamba watu wenye ukoma wanapaswa kutengwa kwa sababu za kiafya, lakini haikuruhusu watendewe kwa ukatili. (Mambo ya Walawi, sura ya 13) Hata hivyo, baadaye sheria za marabi zilisema kwamba watu wenye ukoma walikuwa wenye kuchukiza kama kinyesi. Baadhi ya viongozi wa kidini hata waliwarushia mawe watu wenye ukoma ili wasiwakaribie! Ni vigumu kuwazia watu waliotendewa hivyo wakiwa na ujasiri wa kumkaribia mwalimu yeyote, hata hivyo, watu wenye ukoma walimkaribia Yesu. Mmoja wao alisema maneno haya yanayojulikana sana ambayo yanaonyesha imani: “Bwana, ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa.” (Luka 5:12) Katika sura inayofuata, tutazungumzia jibu la Yesu. Kwa sasa, inatosha kusema kwamba huo ndio uthibitisho ulio wazi zaidi unaoonyesha kuwa watu walijihisi huru kumkaribia Yesu.

11. Ni mfano gani unaoonyesha kwamba wale waliolemewa na hatia walijihisi huru kumkaribia Yesu, na kwa nini hilo ni muhimu?

11 Wale waliolemewa na hatia walijihisi huru kumkaribia Yesu. Kwa mfano, fikiria wakati ambapo Yesu alikuwa akila nyumbani kwa Farisayo fulani. Mwanamke aliyejulikana kuwa mtenda dhambi aliingia na kupiga magoti miguuni pa Yesu, akilia kwa sababu ya hatia yake. Aliilowesha miguu ya Yesu kwa machozi na kutumia nywele zake kuikausha. Ingawa mwenye nyumba alichukizwa na jambo hilo na kumchambua Yesu vikali kwa kumruhusu mwanamke huyo amkaribie, kwa fadhili Yesu alimpongeza mwanamke huyo kwa kutubu kikweli naye akamhakikishia kwamba Yehova amemsamehe. (Luka 7:36-50) Kuliko wakati mwingine wowote, leo watu wanaolemewa na hatia wanahitaji kujihisi huru kuwakaribia wale wanaoweza kuwasaidia kurekebisha uhusiano wao pamoja na Mungu! Kwa nini watu walijihisi huru kumkaribia Yesu?

Kwa Nini Watu Walijihisi Huru Kumkaribia Yesu?

12. Kwa nini haishangazi kwamba watu walijihisi huru kumkaribia Yesu?

12 Kumbuka kwamba Yesu alimwiga kikamili Baba yake mpendwa wa mbinguni. (Yohana 14:9) Biblia inatukumbusha kwamba Yehova “hayuko mbali na kila mmoja wetu.” (Matendo 17:27) Akiwa “Msikiaji wa sala,” sikuzote watumishi waaminifu wa Yehova na watu wengine wowote ambao kwa unyoofu wanataka kumpata na kumtumikia wanaweza kumkaribia. (Zaburi 65:2) Hebu wazia, tunaweza kumkaribia kwa urahisi na kuzungumza na mtu muhimu na mwenye nguvu zaidi katika ulimwengu! Kama Baba yake, Yesu anawapenda watu. Katika sura zinazofuata, tutazungumzia jinsi Yesu alivyowapenda watu kutoka moyoni. Hata hivyo, watu walijihisi huru kumkaribia Yesu hasa kwa sababu upendo wake kwao ulionekana kwa urahisi. Acheni tuchunguze baadhi ya mambo ambayo Yesu alifanya ili kuonyesha upendo huo.

13. Wazazi wanawezaje kumwiga Yesu?

13 Haikuwa vigumu kwa watu kutambua kwamba Yesu alipendezwa nao kibinafsi. Hata alipokuwa chini ya hali ngumu hakuacha kupendezwa na watu. Kama tulivyoona, wazazi walipomletea watoto wao, Yesu alikubali wamkaribie hata alipokuwa na shughuli nyingi na majukumu mazito. Aliwawekea wazazi mfano mzuri sana! Si rahisi kulea watoto katika ulimwengu wa leo. Hata hivyo, ni muhimu watoto wajihisi huru wanapokuwa na wazazi wao. Ikiwa wewe ni mzazi, unajua kwamba kuna nyakati ambazo unaweza kuwa na shughuli nyingi hivi kwamba unashindwa kumpa mtoto wako uangalifu anaohitaji. Je, unaweza kumhakikishia kwamba utatenga wakati wa kuwa pamoja naye haraka iwezekanavyo? Ukitimiza ahadi yako, mtoto wako atajifunza faida ya kuwa na subira. Pia, atajua kwamba anaweza kukueleza jambo lolote linalomhangaisha wakati wowote.

14-16. (a) Ni hali gani zilizomchochea Yesu afanye muujiza wake wa kwanza, na kwa nini ulikuwa muujiza wenye kustaajabisha? (b) Muujiza ambao Yesu alifanya huko Kana unafunua nini kumhusu, na wazazi wanaweza kujifunza nini?

14 Yesu alihakikisha watu walijua kwamba alijali hisia zao. Kwa mfano, fikiria muujiza wa kwanza ambao Yesu alifanya. Alikuwa amehudhuria karamu ya ndoa huko Kana, mji wa Galilaya. Tatizo fulani lilitokea—divai iliisha! Maria, mama ya Yesu, alimwambia mwana wake kilichokuwa kimetokea. Yesu alifanya nini? Aliwaagiza wahudumu wajaze maji katika mitungi sita mikubwa ya mawe. Msimamizi wa karamu alipopelekewa kiasi fulani aonje, ilikuwa divai nzuri sana! Je, hayo yalikuwa mazingaombwe? Hapana, maji halisi ‘yaligeuzwa kuwa divai.’ (Yohana 2:1-11) Kwa muda mrefu, wanadamu wametamani sana kugeuza kitu kimoja kiwe kingine. Kwa karne nyingi, wataalamu fulani walijaribu kugeuza madini ya risasi yawe dhahabu. Hawakufanikiwa hata ingawa risasi na dhahabu ni madini yanayofanana sana.a Vipi kuhusu maji na divai? Maji ni mchanganyiko wa aina mbili za madini ya msingi. Nayo divai imefanyizwa kwa visehemu elfu moja hivi, vingi kati ya visehemu hivyo vikiwa na miundo tata! Kwa nini Yesu alifanya muujiza huo wenye kustaajabisha ili kutatua tatizo dogo la upungufu wa divai kwenye karamu ya ndoa?

15 Hilo halikuwa tatizo dogo kwa bwana na bibi-arusi. Zamani, katika Mashariki ya Kati, kuwaonyesha wageni ukarimu lilikuwa jambo muhimu. Ingekuwa aibu kubwa kwa wanaofanya karamu ya ndoa kuishiwa na divai katika karamu yao ya ndoa, kungeitia doa siku yao ya ndoa, na jambo hilo lingekumbukwa kwa miaka mingi. Jambo hilo lilikuwa muhimu kwa wenzi hao wa ndoa na kwa Yesu pia. Kwa hiyo, alichukua hatua. Je, unaona ni kwa nini watu walimwendea walipokuwa na shida?

Mama akimbembeleza binti yake ambaye amekasirika kwa sababu mkono wa mdoli wake umevunjika.

Mwonyeshe mtoto wako kwamba anaweza kukukaribia na kwamba unamjali kikweli

16 Wazazi pia wanaweza kujifunza somo muhimu katika kisa hicho. Wazia kwamba mtoto wako anakuja kwako akiwa amelemewa na tatizo fulani. Huenda ukaliona tatizo lake kuwa dogo. Labda hata unaweza kuliona kuwa jambo la kuchekesha. Unapolinganisha na matatizo yako, huenda kwa kweli tatizo la mtoto wako likaonekana kuwa dogo. Hata hivyo, kumbuka kwamba kwa mtoto wako si tatizo dogo! Ikiwa linamhangaisha mtu unayempenda sana, je, halipaswi kukuhangaisha pia? Kumwambia mtoto wako kwamba unajali mahangaiko yake kutamfanya ajihisi huru kukukaribia.

17. Yesu alituwekea mfano gani wa upole, na kwa nini kuwa na sifa hiyo kunaonyesha kwamba mtu ana nguvu?

17 Kama tulivyojifunza katika Sura ya 3, Yesu alikuwa mpole na mnyenyekevu. (Mathayo 11:29) Upole ni sifa yenye kuvutia, nayo inaonyesha kwamba mtu ni mnyenyekevu moyoni. Ni sehemu ya tunda la roho takatifu ya Mungu na inahusianishwa na hekima inayotoka kwa Mungu. (Wagalatia 5:22, 23; Yakobo 3:13) Hata alipokasirishwa sana, Yesu alijizuia. Upole wake haukuwa udhaifu hata kidogo. Mtaalamu mmoja alisema hivi kuhusu upole: “Upole ni sifa yenye nguvu sana.” Kwa kweli, mara nyingi tunahitaji nguvu ili kuzuia hasira yetu na kuwatendea wengine kwa upole. Lakini Yehova anapoona jitihada zetu, anaweza kutupatia nguvu ili tuwe wapole na wenye fadhili kama Yesu, na hivyo watu watajihisi huru kutukaribia.

18. Ni mfano gani unaoonyesha kwamba Yesu alikuwa mwenye usawaziko, na kwa nini unafikiri sifa hiyo inaweza kuwafanya watu wajihisi huru kumkaribia mtu?

18 Yesu alikuwa mwenye usawaziko. Yesu alipokuwa Tiro, mwanamke fulani alikuja kwake kwa sababu binti yake alikuwa “anasumbuliwa kikatili na roho mwovu.” Kwa njia tatu tofauti, Yesu alionyesha kwamba hakutaka kufanya kile ambacho mwanamke huyo alitaka. Kwanza, alinyamaza; pili, alimpa sababu iliyoonyesha kwa nini hakupaswa kufanya kile ambacho mwanamke huyo aliomba; tatu, alitoa mfano ili kuonyesha wazi kwa nini hangefanya jambo hilo. Hata hivyo, je, Yesu alizungumza kwa ukali na mwanamke huyo na kukataa kubadili uamuzi wake? Je, Yesu alimfanya mwanamke huyo ahisi kwamba hakuwa na heshima kwa kuwa yeye alikuwa mwalimu mkuu? Hapana, mwanamke huyo alijihisi akiwa salama. Hakuomba tu msaada, bali aliendelea kusisitiza hata ingawa Yesu alionyesha kwamba hakutaka kumsaidia. Yesu aliona imani yake ya pekee iliyomchochea kusisitiza, naye akamponya binti yake. (Mathayo 15:22-28) Bila shaka, watu walijihisi huru kumkaribia Yesu kwa sababu alikuwa mwenye usawaziko, alikuwa tayari kusikiliza, na kubadilikana kulingana na hali!

Je, Watu Wanajihisi Huru Kukukaribia?

19. Tunawezaje kujua ikiwa kwa kweli wengine wanajihisi huru kutukaribia?

19 Kwa kawaida, watu hufikiri kwamba wengine wanajihisi huru kuwakaribia. Kwa mfano, watu fulani wenye mamlaka wanapenda kusema kwamba wanaweza kufikiwa kwa urahisi, na kwamba watu walio chini yao wako huru kuwafikia wakati wowote. Hata hivyo, Biblia inatoa onyo hili kali: “Watu wengi hutangaza upendo wao mshikamanifu, lakini ni nani anayeweza kumpata mtu mwaminifu?” (Methali 20:6) Ni rahisi kusema kwamba watu wanajihisi huru kutukaribia, lakini, je, tunaiga upendo wa Yesu kwa kuwatendea kama tu ambavyo Yesu aliwatendea? Jibu la swali hilo linategemea maoni ya wengine kutuhusu, na si maoni yetu. Paulo alisema: “Usawaziko wenu na ujulikane kwa watu wote.” (Wafilipi 4:5) Kila mmoja wetu anahitaji kujiuliza hivi: ‘Wengine wana maoni gani kunihusu? Ninajulikana kuwa mtu wa aina gani?’

Mzee wa kutaniko anamkaribisha kwa uchangamfu ndugu ambaye amemkaribia.

Wazee hujitahidi kuwa wenye kufikika

20. (a) Kwa nini ni muhimu kwa wazee wa kutaniko kuwa wenye kufikika? (b) Kwa nini tunapaswa kuwa wenye usawaziko kuhusiana na yale tunayotarajia kutoka kwa wazee kutanikoni?

20 Wazee wa kutaniko hasa hujitahidi kuwafanya wengine wajihisi huru kuwakaribia. Wanatamani sana kutimiza yale yanayosemwa kwenye Isaya 32:1, 2: “Kila mmoja atakuwa kama mahali pa kujificha kutokana na upepo, na mahali pa kujisitiri kutokana na dhoruba ya mvua, kama vijito vya maji katika nchi isiyo na maji, kama kivuli cha jabali kubwa katika nchi iliyokauka.” Mzee anaweza kutoa ulinzi kama huo, burudisho, na kitulizo ikiwa tu ataendelea kuwafanya wengine wajihisi huru kumkaribia. Ni kweli kwamba kufanya hivyo si rahisi sikuzote kwa kuwa wazee wana majukumu mazito katika nyakati hizi ngumu. Lakini, wazee hujitahidi wasionekane kuwa wenye shughuli nyingi sana hivi kwamba washindwe kushughulikia mahitaji ya kondoo wa Yehova. (1 Petro 5:2) Washiriki wengine wa kutaniko wanajitahidi kuwa wenye usawaziko kuhusiana na yale wanayotarajia kutoka kwa wanaume hao waaminifu kwa kuonyesha roho ya unyenyekevu na ya ushirikiano.​—Waebrania 13:17.

21. Wazazi wanaweza kufanya nini ili watoto wao wajihisi huru kuwakaribia, na tutazungumzia nini katika sura inayofuata?

21 Nyakati zote wazazi hujitahidi kushughulikia mahitaji ya watoto wao. Hilo ni jambo zito! Wanataka watoto wao wajue kwamba wanapaswa kujihisi huru kumweleza baba au mama mahangaiko yao. Hivyo, wazazi Wakristo wanajitahidi kuwa wapole na wenye usawaziko badala ya kukasirika mtoto anapomweleza mzazi wake kwamba amefanya kosa au anapokuwa na maoni yasiyofaa. Wazazi wanapoendelea kuwazoeza watoto wao kwa subira, wao hujitahidi kuwa na mawasiliano mazuri. Kwa kweli, sote tunataka kuendelea kuwafanya wengine wajihisi huru kutukaribia, kama Yesu alivyofanya. Katika sura inayofuata, tutazungumzia jinsi Yesu alivyoonyesha huruma kutoka moyoni, mojawapo ya sifa kuu zilizofanya wengine wajihisi huru kumkaribia.

a Wanafunzi wa kemia wanajua kwamba madini ya risasi na dhahabu yanakaribiana sana katika jedwali la elementi. Kiini cha atomu ya risasi kina protoni tatu zaidi kuliko zile za dhahabu. Wanafizikia wa siku hizi hata wamefaulu kugeuza kiasi kidogo cha madini ya risasi kuwa dhahabu, lakini inagharimu sana kufanya hivyo, kwa kuwa nishati nyingi sana inahitajika.

Unawezaje Kumfuata Yesu?

  • Kwa nini kuuliza maswali na kusikiliza kwa makini majibu kutawafanya wengine wajihisi huru kutukaribia?​—Mathayo 16:13-17.

  • Yesu alionyeshaje kwamba watu wangeweza kuzungumza naye hata alipohitaji kuwa peke yake, na tunawezaje kufuata mfano wake?​—Marko 6:31-34.

  • Yesu alikuwa na maoni gani kuhusu watu ambao hawakumwamini, na kuiga maoni yake yenye usawaziko kutatusaidiaje kuwa wenye kufikika?​—Luka 5:29-32.

  • Ni kwa njia gani kuiga maoni ya Yesu yanayofaa kuwahusu watu kutafanya wengine wajihisi huru zaidi kutukaribia?​—Yohana 1:47.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki