Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • cf sura 9 kur. 101-113
  • “Nendeni Mkafanye Wanafunzi”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Nendeni Mkafanye Wanafunzi”
  • ‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kwa Nini Wafanyakazi Wengi Zaidi Walihitajika?
  • Walizoezwa Kutoa Ushahidi
  • Mgawo Unaotuhusu
  • “Nipo Pamoja Nanyi Sikuzote”
  • “Mkafanye Wanafunzi, Kuwabatiza”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
  • ‘Wafundisheni Kushika Mambo Yote Ambayo Nimewaamuru Ninyi’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • “Nifuateni, Nami Nitawafanya Kuwa Wavuvi Watu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Usichoke Kutenda Yaliyo Mema
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
Pata Habari Zaidi
‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
cf sura 9 kur. 101-113

SURA YA TISA

“Nendeni Mkafanye Wanafunzi”

Mazao yako tayari kwa ajili ya kuvunwa.

Mkulima anaweza kufanya nini ikiwa mazao ni mengi sana na hawezi kuyakusanya akiwa peke yake?

1-3. (a) Mkulima anafanya nini mazao yanapokuwa mengi sana hivi kwamba hawezi kuyavuna akiwa peke yake? (b) Yesu anakabili tatizo gani mwaka wa 33 W.K., naye analishughulikiaje?

MKULIMA anakabili tatizo kubwa. Miezi michache mapema alilima mashamba yake na kupanda mbegu. Alifurahia kuona mimea ya kwanza ikichipua, na akashangilia kuona ikikomaa. Sasa, kazi ngumu aliyofanya inazaa matunda kwa kuwa wakati wa mavuno umefika. Lakini ana tatizo hili: Mazao ni mengi sana hivi kwamba hawezi kuyavuna akiwa peke yake. Ili kutatua tatizo hilo, kwa hekima anaamua kuajiri wafanyakazi na kuwatuma katika mashamba yake. Ana muda mfupi tu wa kuvuna mazao yake yenye thamani.

2 Yesu anakabili tatizo kama hilo mwaka wa 33 W.K., baada ya kufufuliwa. Wakati wa huduma yake duniani, alipanda mbegu za ile kweli. Sasa, mavuno ni mengi na yanahitaji kukusanywa. Watu wengi wanaopendezwa wanahitaji kukusanywa ili wawe wanafunzi. (Yohana 4:35-38) Yesu anashughulikiaje tatizo hilo? Akiwa mlimani huko Galilaya, muda mfupi kabla ya kwenda mbinguni, Yesu anaamuru wanafunzi wake watafute wanafunzi zaidi anaposema: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza . . . , na kuwafundisha kushika mambo yote niliyowaamuru.”​—Mathayo 28:19, 20.

3 Kufanya tu kile ambacho Yesu aliamuru ndiko kunaweza kumfanya mtu awe mfuasi wa kweli wa Kristo. Hivyo basi, acheni tuchunguze maswali matatu. Kwa nini Yesu aliamuru wafanyakazi zaidi watafutwe? Aliwazoeza wanafunzi wake jinsi gani kuwatafuta? Ni kwa njia gani tunahusika katika kazi hiyo?

Kwa Nini Wafanyakazi Wengi Zaidi Walihitajika?

4, 5. Kwa nini Yesu hangeweza kumaliza kazi aliyokuwa ameanzisha, na ni nani ambao wangehitaji kuendeleza kazi hiyo baada ya yeye kurudi mbinguni?

4 Yesu alipoanza huduma yake mwaka wa 29 W.K., alijua kwamba anaanzisha kazi ambayo hangeweza kuimaliza akiwa peke yake. Kwa kuwa muda ambao angekaa duniani ulikuwa mfupi, hangeweza kuhubiri maeneo yote wala kumweleza kila mtu ujumbe wa Ufalme. Ni kweli kwamba aliwahubiria hasa Wayahudi na wageuzwa imani, “kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.” (Mathayo 15:24) Hata hivyo, ‘kondoo hao waliopotea’ walikuwa wametawanyika kotekote Israeli, nchi yenye ukubwa wa maelfu ya kilomita. Pia, watu wanaoishi katika sehemu zote za ulimwengu walipaswa kuhubiriwa habari njema.​—Mathayo 13:38; 24:14.

5 Yesu alitambua kwamba bado kazi kubwa ingehitaji kufanywa baada ya kifo chake. Aliwaambia hivi mitume wake 11 waaminifu: “Kwa kweli ninawaambia, yeyote anayeniamini atafanya pia kazi ambazo mimi hufanya; naye atafanya kazi kubwa kuliko hizi, kwa sababu ninaenda zangu kwa Baba.” (Yohana 14:12) Kwa kuwa Mwana angerudi mbinguni, wafuasi wake, yaani, mitume pamoja na wale ambao wangekuwa wanafunzi wake baadaye, walipaswa kuendeleza kazi ya kuhubiri na kufundisha. (Yohana 17:20) Kwa unyenyekevu, Yesu alikubali kwamba wangefanya kazi “kubwa kuliko” zake. Jinsi gani? Katika njia tatu.

6, 7. (a) Ni katika njia gani wafuasi wa Yesu wangefanya kazi kubwa kuliko zake? (b) Tunawezaje kuonyesha kwamba Yesu hakukosea kwa kuwatumaini wafuasi wake?

6 Kwanza, wafuasi wa Yesu wangehubiri katika maeneo mengi zaidi. Leo, kazi yao ya kutoa ushahidi imefika kwenye miisho ya dunia, mbali na mipaka ya nchi ambayo Yesu alihubiri. Pili, wangewahubiria watu wengi zaidi. Kikundi kidogo cha wanafunzi ambao Yesu aliwaacha duniani kiliongezeka haraka na kuwa maelfu ya watu. (Matendo 2:41; 4:4) Sasa, wamekuwa mamilioni, na mamia ya maelfu ya wapya wanabatizwa kila mwaka. Tatu, wangehubiri kwa muda mrefu zaidi. Yesu alihubiri kwa muda wa miaka mitatu na nusu, lakini wafuasi wake wanaendelea kuhubiri hadi leo, miaka 2000 hivi baadaye.

7 Yesu alionyesha kwamba anawatumaini wafuasi wake aliposema kwamba wangefanya “kazi kubwa kuliko hizi.” Aliwapa kazi iliyokuwa muhimu zaidi kwake, kazi ya kuhubiri na kufundisha “habari njema ya Ufalme wa Mungu.” (Luka 4:43) Aliamini kwamba watatimiza mgawo wao kwa uaminifu. Hilo linamaanisha nini kwetu leo? Tunaposhiriki katika huduma kwa bidii na kwa moyo wote, tunaonyesha kwamba Yesu hakukosea kuwatumaini wafuasi wake. Je, hilo si pendeleo la pekee?​—Luka 13:24.

Walizoezwa Kutoa Ushahidi

Dada akimhubiria msimamizi wa duka.

Upendo unatuchochea kuhubiri popote ambapo watu wanapatikana

8, 9. Yesu alituwekea mfano gani katika huduma, nasi tunawezaje kuufuata?

8 Yesu aliwapa wanafunzi wake mazoezi bora kwa ajili ya huduma. Isitoshe, aliwawekea mfano mzuri. (Luka 6:40) Katika sura iliyotangulia, tulizungumzia mtazamo wake kuhusu huduma. Kwa mfano, wafikirie wanafunzi waliokuwa wakitembea pamoja na Yesu katika safari zake za kuhubiri. Waliona kwamba alihubiri popote ambapo watu walipatikana—kando ya ziwa na kwenye milima, katika majiji na masoko, na katika nyumba za watu. (Mathayo 5:1, 2; Luka 5:1-3; 8:1; 19:5, 6) Waliona kwamba alikuwa mwenye bidii, aliamka mapema na kufanya kazi mpaka usiku. Hakushiriki katika huduma ili tu kupoteza wakati! (Luka 21:37, 38; Yohana 5:17) Bila shaka, wafuasi wake walitambua kwamba alifanya hivyo kwa sababu aliwapenda sana watu. Huenda walipoutazama uso wake waliona huruma aliyokuwa nayo moyoni. (Marko 6:34) Unafikiri mfano wa Yesu uliwasaidiaje wanafunzi wake? Mfano huo ungekunufaisha wewe jinsi gani?

9 Tukiwa wafuasi wa Kristo, tunafuata mfano wake katika huduma yetu. Hivyo, tunafanya yote tuwezayo ili kutoa “ushahidi kamili.” (Matendo 10:42) Kama alivyofanya Yesu, tunawatembelea watu nyumbani kwao. (Matendo 5:42) Tunabadili ratiba yetu, ikihitajika, ili tuwatembelee wakati wanapokuwa nyumbani. Pia, tunawatafuta na kuwahubiria watu kwa busara katika sehemu ambazo wanapatikana—barabarani, kwenye bustani, kwenye maduka, na kazini. Tunaendelea ‘kufanya kazi kwa bidii na kujitahidi’ katika huduma, kwa sababu tunachukua kwa uzito kazi hiyo. (1 Timotheo 4:10) Upendo wa kutoka moyoni kuwaelekea wengine unatuchochea kuendelea kutafuta nafasi za kuhubiri mahali popote na wakati wowote ambapo watu wanaweza kupatikana.​—1 Wathesalonike 2:8.

Kwa shangwe, wanafunzi wa Yesu wanamweleza kuhusu matokeo mazuri waliyopata katika mgawo wao wa kuhubiri.

“Wale 70 wakarudi wakiwa na shangwe”

10-12. Yesu aliwafundisha wanafunzi wake masomo gani muhimu kabla ya kuwatuma kwenda kuhubiri?

10 Pia, Yesu aliwazoeza wanafunzi wake kwa kuwapa maagizo kamili. Kabla ya kuwatuma wale mitume 12 na baadaye wale wanafunzi 70 kwenda kuhubiri, Yesu alitumia pindi mbalimbali kuwazoeza. (Mathayo 10:1-15; Luka 10:1-12) Mazoezi hayo yalikuwa na matokeo mazuri, kwa kuwa andiko la Luka 10:17 linasema: “Wale 70 wakarudi wakiwa na shangwe.” Ingawa hali katika nyakati za Biblia zilikuwa tofauti na zetu, bado tunaweza kujifunza masomo muhimu. Sasa tutazungumzia mambo mawili kati ya maagizo ambayo Yesu aliwapa.

11 Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kumtumaini Yehova. Aliwaambia: “Msichukue dhahabu, fedha, wala shaba kwenye mishipi yenu ya pesa, wala mfuko wa chakula kwa ajili ya safari, wala mavazi mawili, wala viatu, wala fimbo, kwa maana mfanyakazi anastahili chakula chake.” (Mathayo 10:9, 10) Ilikuwa kawaida kwa wasafiri kuchukua mshipi wa kubebea pesa, mfuko wa chakula, na viatu vya ziada.a Kwa kuwafundisha wanafunzi wake wasihangaikie mambo hayo, ni kana kwamba Yesu alikuwa akiwaambia: “Mtumaini Yehova kabisa, kwa maana atatosheleza mahitaji yenu.” Yehova angetosheleza mahitaji yao kwa kuwachochea wale ambao wangekubali habari njema waonyeshe ukarimu, kama ilivyokuwa desturi huko Israeli.​—Luka 22:35.

12 Pia, Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kuepuka mambo yasiyo ya lazima ambayo yangewakengeusha. Alisema hivi: “Msimsalimu mtu yeyote njiani.” (Luka 10:4) Je, Yesu aliwaambia wasiwe na urafiki na waepuke kuzungumza na wengine? Hapana! Katika nyakati za Biblia, mara nyingi salamu zilitia ndani mambo mengi. Kwa kawaida, salamu zilitia ndani desturi fulani pamoja na mazungumzo marefu. Msomi mmoja wa Biblia anasema: “Watu wa Mashariki hawakusalimiana kama tunavyofanya, yaani, kwa kuinama kidogo, au kwa kupeana mkono, bali walikumbatiana mara nyingi na kuinamisha kichwa na hata kusujudu. Yote hayo yalihitaji wakati mwingi.” Kwa kuwaambia wanafunzi wake wasisalimiane kulingana na desturi hizo, ni kana kwamba Yesu aliwaambia: “Mnapaswa kutumia wakati wenu vizuri kwa maana ujumbe mnaohubiri ni wa haraka.”b

13. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunatii maagizo ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake katika karne ya kwanza?

13 Tunatii maagizo ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake wa karne ya kwanza. Tunapotimiza huduma yetu, tunamtumaini Yehova kabisa. (Methali 3:5, 6) Tunajua kwamba hatutakosa mambo ya lazima maishani ‘tukiendelea kuutafuta kwanza ufalme.’ (Mathayo 6:33) Ulimwenguni pote, wahubiri wa Ufalme wa wakati wote wamejionea kwamba hata katika hali ngumu, mkono wa Yehova si mfupi. (Zaburi 37:25) Pia, tunatambua kwamba tunahitaji kuepuka mambo yanayoweza kutukengeusha. Tusipokuwa waangalifu, mfumo huu wa mambo unaweza kutukengeusha kwa urahisi. (Luka 21:34-36) Hata hivyo, huu si wakati wa kukengeushwa. Kwa kuwa maisha ya watu yako hatarini, ujumbe wetu ni wa haraka. (Waroma 10:13-15) Tukiendelea kutambua kwamba kazi yetu inahitaji kufanywa haraka, hatutaruhusu mambo ya ulimwengu huu yanayoweza kutukengeusha yachukue wakati na nguvu ambazo tungetumia katika huduma. Kumbuka kwamba wakati uliobaki ni mfupi na mavuno ni mengi.​—Mathayo 9:37, 38.

Mgawo Unaotuhusu

14. Ni nini kinachoonyesha kwamba mgawo ulio kwenye Mathayo 28:18-20 unawahusu wafuasi wote wa Kristo? (Ona pia maelezo ya chini.)

14 Baada ya kufufuliwa, Yesu aliwapa wafuasi wake mgawo mzito aliposema: “Nendeni mkafanye wanafunzi.” Maneno hayo hayakuwahusu tu wanafunzi waliokuwa mlimani huko Galilaya.c Kazi ambayo Yesu aliagiza ifanywe inatia ndani kuwafikia “watu wa mataifa yote,” nayo itaendelea “mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” Bila shaka, mgawo huo unawahusu wafuasi wote wa Kristo, kutia ndani sisi leo. Basi, acheni tuchunguze maneno ya Yesu kwenye Mathayo 28:18-20.

15. Kwa nini ni jambo la hekima kutii amri ya Yesu ya kufanya wanafunzi?

15 Kabla ya kuwapa mgawo huo, Yesu anasema: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.” (Mstari wa 18) Je, kweli Yesu ana mamlaka kubwa hivyo? Bila shaka! Yeye ndiye malaika mkuu, mwenye mamlaka juu ya makumi ya maelfu ya makumi ya maelfu ya malaika. (1 Wathesalonike 4:16; Ufunuo 12:7) Akiwa “kichwa cha kutaniko,” ana mamlaka juu ya wafuasi wake walio duniani. (Waefeso 5:23) Tangu mwaka wa 1914, amekuwa akitawala akiwa Mfalme wa Kimasihi mbinguni. (Ufunuo 11:15) Mamlaka yake inafika hata kaburini, kwa kuwa ana uwezo wa kuwafufua wafu. (Yohana 5:26-28) Kwa kutangaza kwanza mamlaka yake kubwa, Yesu anaonyesha kwamba maneno anayosema kwenye mistari inayofuata, ni amri na si pendekezo. Litakuwa jambo la hekima kumtii, kwa kuwa hakujichukulia mamlaka, bali alipewa na Mungu.​—1 Wakorintho 15:27.

16. Yesu anapotuambia “nendeni,” anatuamuru tufanye nini, nasi tunatimiza mgawo huo jinsi gani?

16 Sasa Yesu anataja mgawo wenyewe ambao unaanza kwa neno moja: “Nendeni.” (Mstari wa 19) Hivyo, anatuamuru tuchukue hatua ya kuwaeleza wengine ujumbe wa Ufalme. Ili kutimiza mgawo huo, tunaweza kutumia njia mbalimbali. Kuhubiri nyumba kwa nyumba ni njia nzuri zaidi ya kuzungumza na watu kibinafsi. (Matendo 20:20) Pia, tunatafuta nafasi za kufanya mahubiri yasiyo rasmi; tunapofanya shughuli zetu za kila siku tunajaribu kuanzisha mazungumzo kuhusu habari njema mahali popote inapowezekana. Huenda njia zetu za kuhubiri zikatofautiana, kwa kuwa tunazibadili kulingana na mahitaji na hali za watu wa eneo letu. Hata hivyo, kuna jambo moja lisilobadilika: ‘Tunaenda’ kuwatafuta wanaostahili.​—Mathayo 10:11.

17. Tunawezaje ‘kufanya wanafunzi’?

17 Kisha, Yesu anaeleza kusudi la mgawo huo, yaani, ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’ (Mstari wa 19) Tunaweza ‘kufanya wanafunzi’ jinsi gani? Kwa kawaida mwanafunzi ni mtu anayejifunza, au anayefundishwa. Hata hivyo, kufanya wanafunzi hakumaanishi tu kuwaelimisha watu. Tunapojifunza Biblia pamoja na watu wanaopendezwa, kusudi letu ni kuwasaidia wawe wafuasi wa Kristo. Wakati wowote inapowezekana, tunakazia mfano wa Yesu ili wanafunzi wetu wajifunze kumwona kuwa Mwalimu wao na Kielelezo chao, wakiishi kama alivyoishi na kufanya kazi aliyofanya.​—Yohana 13:15.

18. Kwa nini ubatizo ndio hatua muhimu zaidi katika maisha ya mwanafunzi?

18 Maneno yafuatayo yanaonyesha jambo muhimu katika mgawo huo: “Mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu.” (Mstari wa 19) Ubatizo ndio hatua muhimu zaidi katika maisha ya mwanafunzi, kwa kuwa inaonyesha kwamba amejiweka wakfu kwa Mungu kwa moyo wote. Hivyo basi, ubatizo ni hatua muhimu ili kupata wokovu. (1 Petro 3:21) Mwanafunzi aliyebatizwa akiendelea kufanya yote awezayo ili kumtumikia Yehova, anaweza kutazamia kupata baraka milele katika ulimwengu mpya unaokuja. Je, umemsaidia mtu fulani awe mwanafunzi aliyebatizwa wa Kristo? Hakuna jambo lingine katika huduma ya Kikristo linaloleta shangwe nyingi kama hilo.​—3 Yohana 4.

19. Ni mambo gani tunayowafundisha wanafunzi wapya, na kwa nini huenda tukahitaji kuendelea kuwafundisha baada ya ubatizo wao?

19 Yesu anaeleza sehemu inayofuata ya mgawo huo, anaposema: “Kuwafundisha kushika mambo yote niliyowaamuru.” (Mstari wa 20) Tunawafundisha wapya kutii amri za Yesu, kutia ndani amri ya kumpenda Mungu, kumpenda jirani, na kufanya wanafunzi. (Mathayo 22:37-39) Hatua kwa hatua, tunawafundisha kuwaeleza wengine kweli za Biblia na kutetea imani yao inayoongezeka. Wanapostahili kuhubiri pamoja na kutaniko, tunahubiri pamoja nao na kuwafundisha kwa maneno na mfano wetu jinsi wanavyoweza kupata matokeo katika kazi hiyo. Wanafunzi wapya wanaweza kuendelea kufundishwa hata baada ya kubatizwa. Huenda wale waliobatizwa hivi karibuni wakahitaji kufundishwa zaidi ili wakabiliane na hali ngumu zinazoweza kuwapata wanapomfuata Kristo.​—Luka 9:23, 24.

“Nipo Pamoja Nanyi Sikuzote”

20, 21. (a) Kwa nini hatupaswi kuogopa tunapotimiza mgawo tuliopewa na Yesu? (b) Kwa nini huu si wakati wa kupunguza bidii, na tunapaswa kuazimia kufanya nini?

20 Maneno haya ya mwisho katika mgawo ambao Yesu alitupatia yanatoa uhakikisho huu mkubwa: “Tazama! mimi nipo pamoja nanyi sikuzote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 28:20) Yesu anatambua kwamba mgawo huo ni muhimu sana. Pia, anajua kwamba nyakati nyingine kuutimiza kutafanya tuchukiwe na wanaotupinga. (Luka 21:12) Hata hivyo, hatupaswi kuogopa. Kiongozi wetu hatazamii tutimize mgawo huo bila msaada au tukiwa peke yetu. Je, haifariji kujua kwamba Yule aliye na “mamlaka yote mbinguni na duniani” yupo pamoja nasi ili kututegemeza tunapotimiza mgawo huo?

21 Yesu aliwahakikishia wanafunzi wake kwamba atakuwa pamoja nao katika huduma yao sikuzote “mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” Ni lazima tuendelee kutimiza mgawo tuliopewa na Yesu, hadi mwisho utakapokuja. Huu si wakati wa kupunguza bidii. Kazi kubwa ya mavuno ya kiroho inaendelea! Watu wanaopendezwa wanakusanywa kwa wingi. Tukiwa wafuasi wa Kristo, na tuazimie kutimiza mgawo muhimu ambao tumepewa. Na tuazimie kutumia wakati wetu, nguvu zetu, na mali zetu kutimiza amri hii ya Kristo: “Nendeni mkafanye wanafunzi.”

a Mshipi wa pesa ulikuwa aina ya mshipi uliokuwa na mfuko wa kubebea sarafu. Mfuko wa chakula ulikuwa mkubwa zaidi na kwa kawaida ulitengenezwa kwa ngozi, nao ulibebwa begani na ulitumiwa kubebea chakula au vitu vingine vya lazima.

b Pindi fulani, nabii Elisha alitoa maagizo kama hayo. Alipokuwa akimtuma mtumishi wake Gehazi kwenye nyumba ya mwanamke aliyefiwa na mwana wake, Elisha alisema: “Ukikutana na yeyote, usimsalimu.” (2 Wafalme 4:29) Mgawo huo ulihitaji kufanywa haraka, kwa hiyo hakupaswa kupoteza wakati.

c Kwa kuwa wengi kati ya wafuasi wake walikuwa Galilaya, huenda pindi inayotajwa katika Mathayo 28:16-20 ni ile ambayo Yesu aliwatokea “ndugu zaidi ya 500” baada ya kufufuliwa. (1 Wakorintho 15:6) Kwa hiyo, huenda mamia ya watu walikuwapo Yesu alipowapa wafuasi wake kazi ya kufanya wanafunzi.

Unawezaje Kumfuata Yesu?

  • Tunapaswa kuwahubiria watu habari njema ya Ufalme jinsi gani?​—Mathayo 10:11-13; Luka 10:5.

  • Kazi yetu ya kuhubiri inapopingwa, maneno ya Yesu yanaweza kutusaidia jinsi gani kuvumilia hali hiyo?​—Marko 13:9-13.

  • Tunapaswa kuwatendeaje wale wasiopendezwa na ujumbe wetu?​—Luka 10:10, 11.

  • Tunapotanguliza kazi ya kuhubiri, tunaweza kuwa na uhakika gani?​—Luka 12:22-31.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki