-
“Zawadi Zikiwa Wanadamu” Ili Kutunza Kondoo za YehovaMnara wa Mlinzi—1999 | Juni 1
-
-
Uhitaji wa ‘Kurekebisha Upya’ Unapozuka
8. Nyakati nyingine sisi sote huhitaji kurekebishwa upya katika njia zipi?
8 Kwanza, “zawadi zikiwa wanadamu” huandaliwa “kwa kusudi la kuwarekebisha upya watakatifu,” Paulo asema. (Waefeso 4:12) Nomino ya Kigiriki inayotafsiriwa ‘kurekebisha upya’ hurejezea “kunyosha” kitu. Tukiwa wanadamu wasiokamilika, sote tunahitaji kurekebishwa upya mara kwa mara—ili kufikiri kwetu, mitazamo yetu, au mwenendo wetu “zinyoshwe” kwa kupatana na kufikiri kwa Mungu na mapenzi yake. Yehova ametuandalia kwa upendo “zawadi zikiwa wanadamu” ili watusaidie kufanya marekebisho yanayohitajika. Wao hufanyaje hivyo?
9. Mzee anaweza kusaidiaje kumrekebisha upya kondoo aliyekosea?
9 Nyakati fulani, huenda mzee akahitaji kumsaidia kondoo aliyekosea, ambaye labda ‘amechukua hatua fulani isiyo ya kweli kabla ya kuijua.’ Mzee anaweza kusaidiaje? Andiko la Wagalatia 6:1 lasema kwamba “jaribuni kumrekebisha upya mtu wa namna hiyo katika roho ya upole.” Kwa hiyo mzee atoapo shauri, hamkemei mkosaji kwa maneno makali. Shauri lapasa kumtia moyo, wala si ‘kumwogofya,’ yule anayelipokea. (2 Wakorintho 10:9; linganisha Ayubu 33:7.) Huenda mtu huyo tayari ameaibika, kwa hiyo mchungaji mwenye upendo huepuka kuiponda roho yake. Wakati shauri, hata karipio zito, linapotolewa kwa upendo, yaelekea litanyosha kufikiri au mwenendo wa mkosaji, na kwa njia hiyo limrekebishe.—2 Timotheo 4:2.
10. Kuwarekebisha upya wengine kunatia ndani nini?
10 Yehova alipoandaa “zawadi zikiwa wanadamu” ili kuturekebisha upya, alitazamia wazee wawe wenye kuburudisha kiroho na wenye kustahili kuigwa na watu wake. (1 Wakorintho 16:17, 18; Wafilipi 3:17) Kurekebisha upya wengine kunatia ndani kuwasaidia waaminifu wadumu kufuata mwendo unaofaa, na kuwasahihisha wale wanaofuatilia mwendo wenye makosa.a Leo, kwa kuwa kuna matatizo mengi sana yanayoelekea kuvunja moyo, wengi wanahitaji kitia-moyo ili waendelee. Huenda wengine wakahitaji msaada unaotolewa kwa wororo ili kufikiri kwao kunyoshwe kupatana na kufikiri kwa Mungu. Kwa mfano, baadhi ya Wakristo waaminifu hupambana na hisia za ndani zinazowafanya wahisi kwamba hawastahili wala hawafai. “Nafsi zilizoshuka moyo” kama hao huenda wakaona kuwa Yehova hawezi kamwe kuwapenda na kwamba Mungu hawezi hata kuzikubali jitihada zao bora za kumtumikia. (1 Wathesalonike 5:14) Lakini kufikiri hivyo hakupatani na jinsi Mungu awaonavyo waabudu wake kikweli.
11. Wazee wanaweza kufanya nini ili kuwasaidia wale wanaopambana na hisia za kuona kuwa hawafai?
11 Enyi wazee, mnaweza kufanya nini ili kuwasaidia watu kama hao? Waonyesheni kwa fadhili uthibitisho wa Kimaandiko unaoonyesha kuwa Yehova humjali kila mmoja wa watumishi wake, nanyi wahakikishieni kuwa maandiko hayo ya Biblia huwahusu wao kibinafsi. (Luka 12:6, 7, 24) Wasaidieni waelewe kuwa Yehova ‘amewavuta’ ili wamtumikie, na basi ni lazima awe anawathamini. (Yohana 6:44) Wahakikishieni kuwa si wao pekee—watumishi wengi waaminifu wa Yehova wamekuwa na hisia kama hizo. Wakati mmoja nabii Eliya alishuka moyo sana hivi kwamba akatamani kufa. (1 Wafalme 19:1-4) Baadhi ya Wakristo watiwa-mafuta katika karne ya kwanza walihisi kuwa mioyo yao ‘inawalaumu.’ (1 Yohana 3:20) Tunafarijika kujua kwamba watu waaminifu katika nyakati za Biblia walikuwa na “hisia kama zetu.” (Yakobo 5:17) Mnaweza pia kupitia makala zenye kutia moyo zilizo katika Mnara wa Mlinzi na Amkeni! mkiwa pamoja na watu waliovunjika moyo. Mungu ambaye amewakabidhi nyinyi mkiwa “zawadi zikiwa wanadamu” hatakosa kuona jitihada zenu zenye upendo za kumfanya awe na matumaini tena.—Waebrania 6:10.
-
-
“Zawadi Zikiwa Wanadamu” Ili Kutunza Kondoo za YehovaMnara wa Mlinzi—1999 | Juni 1
-
-
‘Kulijenga’ Kundi
12. Ni nini kionyeshwacho na usemi “kuujenga mwili wa Kristo,” na ufunguo wa kulijenga kundi ni nini?
12 Pili, “zawadi zikiwa wanadamu” wamekabidhiwa kwa kusudi la “kuujenga mwili wa Kristo.” (Waefeso 4:12) Hapo Paulo anatumia usemi wa mfano. ‘Kujenga’ hutukumbusha ujenzi, na “mwili wa Kristo” hurejezea watu—washiriki wa kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta. (1 Wakorintho 12:27; Waefeso 5:23, 29, 30) Wazee wanahitaji kuwasaidia ndugu zao waimarike kiroho. Kusudi lao ni ‘kulijenga na si kulibomoa’ kundi. (2 Wakorintho 10:8) Ufunguo wa kulijenga kundi ni upendo, kwa sababu “upendo hujenga.”—1 Wakorintho 8:1.
13. Inamaanisha nini kuwa mwenye hisia-mwenzi, na kwa nini ni muhimu wazee waonyeshe hisia-mwenzi?
13 Sehemu moja ya upendo inayowasaidia wazee kulijenga kundi ni hisia-mwenzi. Kuwa na hisia-mwenzi kwamaanisha kuwahurumia wengine—kujiweka katika hali ya fikira zao na hisia zao, mkikumbuka mapungukio yao. (1 Petro 3:8) Kwa nini ni muhimu kwa wazee kuwa na hisia-mwenzi? Sababu muhimu zaidi ni kwamba Yehova—yeye ambaye huandaa “zawadi zikiwa wanadamu”—ni Mungu mwenye hisia-mwenzi. Watumishi wake wanapoteseka au wakiwa katika maumivu, yeye huwahurumia. (Kutoka 3:7; Isaya 63:9) Yeye hufikiria udhaifu wao. (Zaburi 103:14) Basi, wazee wanaweza kuonyeshaje hisia-mwenzi?
14. Wazee wanaweza kuwaonyesha wengine hisia-mwenzi kwa njia zipi?
14 Mtu ambaye amevunjika moyo anapowajia, wao husikiliza, wakitambua hisia zake. Wao hujaribu kuelewa malezi, utu, na hali mbalimbali za ndugu zao. Kisha wazee wanapotoa msaada wa Kimaandiko wenye kujenga, itakuwa rahisi kwa kondoo kuukubali kwa sababu unatoka kwa wachungaji wanaowaelewa na kuwajali kikweli. (Mithali 16:23) Hisia-mwenzi pia husababisha wazee kufikiria mapungukio ya wengine na hisia ambazo zinaweza kutokezwa na mapungukio hayo. Kwa mfano, huenda Wakristo fulani waaminifu wakahisi wana hatia kwa sababu hawawezi kufanya zaidi katika kumtumikia Mungu, labda kwa sababu ya uzee au ugonjwa. Kwa upande mwingine, huenda wengine wakahitaji kitia-moyo ili kuiboresha huduma yao. (Waebrania 5:12; 6:1) Hisia-mwenzi itawafanya wazee watafute “maneno yapendezayo” yanayowajenga wengine. (Mhubiri 12:10) Kondoo za Yehova wanapojengwa na kuchochewa, upendo wao kwa Mungu utawasukuma kufanya yote wawezayo katika kumtumikia!
-
-
“Zawadi Zikiwa Wanadamu” Ili Kutunza Kondoo za YehovaMnara wa Mlinzi—1999 | Juni 1
-
-
a Katika tafsiri ya Septuagint ya Kigiriki, kitenzi hikihiki kilichotafsiriwa “kurekebisha upya” kilitumiwa katika Zaburi 17:5, ambapo Daudi mwaminifu alisali kwamba hatua zake zishikamane kabisa na njia za Yehova.
-