Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • cf sura 3 kur. 28-39
  • “Mimi Ni . . . Mnyenyekevu Moyoni”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Mimi Ni . . . Mnyenyekevu Moyoni”
  • ‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Sikuzote Yesu Amekuwa Mnyenyekevu
  • Unyenyekevu wa Yesu Akiwa Mwanadamu
  • Kuwafundisha Wafuasi Wake Kuwa Wanyenyekevu
  • Je, Utafuata Mfano wa Yesu?
  • Yesu Aliweka Kielelezo Cha Unyenyekevu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • Sitawisha Unyenyekevu wa Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Kwa Nini Kujivika Unyenyekevu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Unyenyekevu
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
Pata Habari Zaidi
‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
cf sura 3 kur. 28-39

SURA YA TATU

“Mimi Ni . . . Mnyenyekevu Moyoni”

Yesu akiwa amepanda punda huku watu walio kando ya barabara wakishangilia na kupunga kwa kutumia matawi ya miti. Wengine wameyatandaza mavazi yao ya nje na matawi hayo barabarani.

“Tazama! Mfalme wako anakuja kwako”

1-3. Yesu anaingia Yerusalemu jinsi gani, na kwa nini watu fulani wanashangaa?

WATU huko Yerusalemu wana shangwe nyingi. Mtu mkuu anakuja! Nje ya jiji, watu wamekusanyika kando ya barabara. Wana hamu kubwa ya kumpokea mtu huyo kwa sababu watu fulani kati yao wanasema kwamba ni mrithi wa Mfalme Daudi na ana haki ya kuwa Mtawala wa Israeli. Wengi wao wana matawi ya mitende ya kumpungia; na wengine wanatandaza mavazi yao na matawi ya miti barabarani ili kuonyesha kwamba wanamheshimu. (Mathayo 21:7, 8; Yohana 12:12, 13) Inaonekana wengi wao wanataka kuona jinsi atakavyoingia jijini.

2 Huenda wengine wanatazamia aingie kwa fahari nyingi. Bila shaka, wanawajua watu fulani mashuhuri waliokuwa na misafara ya kifahari. Kwa mfano, Absalomu mwana wa Daudi alipojitangaza kuwa mfalme, alituma wanaume 50 wakimbie mbele ya gari lake. (2 Samweli 15:1, 10) Mtawala Mroma, Kaisari Yulio alidai mengi hata zaidi; pindi moja aliongoza msafara wa ushindi hadi kwenye bunge la Roma, akiwa amezingirwa na tembo 40 waliokuwa wamebeba taa! Hata hivyo, sasa watu wa Yerusalemu wanamngojea mtu mkuu hata zaidi. Iwe umati huo unajua au haujui, huyo ndiye Masihi, mwanadamu mkuu zaidi aliyewahi kuishi. Lakini, Mfalme huyo wa wakati ujao anapoingia jijini, wengine wanashangaa.

3 Hawaoni magari, wakimbiaji, farasi, wala tembo. Yesu amepanda punda, mnyama ambaye watu humtumia kubeba mizigo.a Yesu pamoja na punda huyo hawakuwa na mapambo yoyote. Badala ya matandiko ya gharama kubwa, wafuasi wa karibu wa Yesu wametandika mavazi mgongoni mwa punda huyo. Kwa nini Yesu alichagua kuingia Yerusalemu kwa njia ya unyenyekevu, licha ya kwamba watu wengine ambao hawakuwa muhimu kama yeye walisisitiza kuingia kwa fahari kubwa?

4. Biblia ilitabiri nini kuhusu jinsi ambavyo Mfalme wa Kimasihi angeingia Yerusalemu?

4 Yesu anatimiza unabii huu: “Shangilia sana . . . Paza sauti kwa ushindi, Ee binti ya Yerusalemu. Tazama! mfalme wako anakuja kwako. Yeye ni mwadilifu, analeta wokovu, ni mnyenyekevu, na amepanda punda.” (Zekaria 9:9) Unabii huo ulionyesha kwamba siku moja Mtiwa Mafuta wa Mungu, Masihi, angeenda Yerusalemu na kuwaonyesha watu kwamba yeye ndiye Mfalme aliyewekwa rasmi na Mungu. Pia, kuingia jijini kwa kutumia punda kungefunua sifa yake yenye kupendeza ya unyenyekevu.

5. Kwa nini unyenyekevu wa Yesu unatuchochea sana tunapoutafakari, na kwa nini ni muhimu kwetu kujifunza kuiga unyenyekevu huo?

5 Unyenyekevu wa Yesu ni mojawapo ya sifa zake zenye kuvutia zaidi na inayogusa mioyo yetu tunapoitafakari. Kama tulivyozungumzia katika sura iliyotangulia, Yesu peke yake ndiye “njia na kweli na uzima.” (Yohana 14:6) Ni wazi kwamba kati ya mabilioni ya watu walioishi duniani hakuna mwanadamu aliye muhimu kama Mwana wa Mungu. Lakini, tofauti na wanadamu wengi wasio wakamilifu, Yesu hakuwa na kiburi hata kidogo, hakujivuna, wala hakujiona kuwa yeye ni muhimu. Ili tuwe wafuasi wa Kristo, tunapaswa kupambana ili kushinda mwelekeo wa kuwa na kiburi. (Yakobo 4:6) Kumbuka kwamba Yehova anachukia majivuno. Hivyo basi, ni muhimu kwetu kujifunza na kuiga unyenyekevu wa Yesu.

Sikuzote Yesu Amekuwa Mnyenyekevu

6. Unyenyekevu ni nini, na Yehova alijuaje kwamba Masihi angekuwa mnyenyekevu?

6 Unyenyekevu ni upole wa akili, kutokuwa na majivuno au kiburi. Ni sifa inayotoka moyoni, nayo huonekana katika mazungumzo, mwenendo, na jinsi mtu anavyoshughulika na wengine. Yehova alijuaje kwamba Masihi angekuwa mnyenyekevu? Alijua kwamba Mwana wake aliiga kikamili sifa yake mwenyewe ya unyenyekevu. (Yohana 10:15) Pia, alikuwa ameuona unyenyekevu wa Mwana wake. Jinsi gani?

7-9. (a) Mikaeli alionyeshaje unyenyekevu alipokuwa akibishana na Shetani? (b) Wakristo wanawezaje kumwiga Mikaeli katika kuonyesha unyenyekevu?

7 Kitabu cha Yuda kinafunua jambo lenye kupendeza: “Mikaeli, yule malaika mkuu alipopingana na Ibilisi na kubishana naye kuhusu mwili wa Musa, hakuthubutu kumhukumu kwa kumtukana, bali alimwambia: ‘Yehova na akukemee.’” (Yuda 9) Mikaeli ni jina linalotumiwa kumrejelea Yesu—kabla na baada ya kuishi hapa duniani—akiwa malaika mkuu, au mkuu wa jeshi la kimbingu la malaika wa Yehova.b (1 Wathesalonike 4:16) Hata hivyo, ona jinsi Mikaeli alivyoshughulikia bishano hilo kati yake na Shetani.

8 Masimulizi ya Yuda hayatuelezi Shetani alitaka kuufanyia nini mwili wa Musa, hata hivyo tuna uhakika kwamba Ibilisi alikuwa na nia mbaya. Huenda alitaka mwili wa mwanamume huyo aliyekuwa mwaminifu utumiwe vibaya katika ibada ya uwongo. Mikaeli alipopinga hila mbovu ya Shetani, alionyesha sifa ya kujizuia pia. Bila shaka, Shetani alistahili kukemewa, lakini Mikaeli, ambaye hakuwa amepewa “kazi yote ya kuhukumu” alipokuwa akibishana na Shetani, aliona kwamba Yehova Mungu tu ndiye anayepaswa kutoa hukumu hiyo. (Yohana 5:22) Akiwa malaika mkuu, Mikaeli alikuwa na mamlaka kubwa. Hata hivyo, alijinyenyekeza na kumwachia Yehova daraka hilo badala ya kujaribu kunyakua mamlaka zaidi. Licha ya kuonyesha unyenyekevu, alikuwa mwenye kiasi pia, yaani, alitambua mipaka yake.

9 Yuda aliongozwa na roho kuandika kuhusu tukio hilo kwa sababu fulani. Inasikitisha kwamba baadhi ya Wakristo katika siku za Yuda hawakuwa wanyenyekevu. Kwa majivuno, walikuwa ‘wanayatukana mambo yote ambayo kwa kweli hawakuyafahamu.’ (Yuda 10) Ni rahisi sana kwetu sisi wanadamu wasio wakamilifu kushindwa na kiburi! Tunaposhindwa kuelewa jambo fulani linalofanywa katika kutaniko la Kikristo, kama vile uamuzi fulani unaofanywa na baraza la wazee, tunatendaje? Ikiwa tungeanza kuchambua na kusema isivyofaa, ingawa hatuwezi kujua mambo yote yanayohusika katika uamuzi huo, je, huko si kukosa unyenyekevu? Badala ya kufanya hivyo, acheni tumwige Mikaeli, au Yesu, kwa kutoingilia mambo ambayo Mungu hajatupatia mamlaka ya kuyashughulikia.

10, 11. (a) Kwa nini utayari wa Yesu wa kukubali kuja duniani unaonyesha kwamba yeye ni mnyenyekevu? (b) Tunawezaje kuiga unyenyekevu wa Yesu?

10 Pia, Mwana wa Mungu alionyesha unyenyekevu kwa kukubali mgawo wa kuja hapa duniani. Fikiria mambo aliyolazimika kuacha. Alikuwa malaika mkuu. Pia, alikuwa “Neno,” Msemaji wa Yehova mwenyewe. (Yohana 1:1-3) Aliishi mbinguni, “makao [ya Yehova] yaliyoinuliwa ya utakatifu na utukufu.” (Isaya 63:15) Hata hivyo, Mwana huyo “alijiondolea hali yake na kuchukua umbo la mtumwa na kuwa mwanadamu.” (Wafilipi 2:7) Fikiria kuhusu yale ambayo angekabili katika mgawo wake hapa duniani! Uhai wake ulihamishwa na kuingizwa katika tumbo la uzazi la bikira Myahudi, ili ukue humo kwa miezi tisa, kisha azaliwe akiwa mtoto wa kibinadamu. Alizaliwa akiwa mtoto katika nyumba ya seremala maskini. Baada ya muda, akaanza kutambaa, akawa mvulana, na mwishowe akawa kijana. Ingawa alikuwa mkamilifu katika maisha yake yote ya ujana, aliendelea kuwatii wazazi wake wasio wakamilifu. (Luka 2:40, 51, 52) Huo ulikuwa unyenyekevu wa hali ya juu, sivyo!

11 Je, tunaweza kuiga unyenyekevu wa Yesu kwa kukubali kwa hiari migawo ya utumishi ambayo nyakati nyingine inaonekana kuwa ya hali ya chini? Kwa mfano, mgawo wetu wa kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu unaweza kuonekana kuwa kazi ya hali ya chini watu wasipopendezwa, wanapotudhihaki, au kututendea kikatili. (Mathayo 28:19, 20) Hata hivyo, tukiendelea kufanya kazi hiyo, tunaweza kusaidia kuokoa uhai wa watu. Pia, tutajifunza mengi kuhusu unyenyekevu, nasi tutafuata hatua za Bwana wetu, Yesu Kristo.

Unyenyekevu wa Yesu Akiwa Mwanadamu

12-14. (a) Yesu alionyesha unyenyekevu jinsi gani watu walipokuwa wakimsifu? (b) Yesu alionyesha unyenyekevu jinsi gani alipokuwa akishughulika na wengine? (c) Ni nini kinachoonyesha kwamba unyenyekevu wa Yesu haukuwa wa kidesturi tu?

12 Tangu mwanzo mpaka mwisho, Yesu alionyesha unyenyekevu katika huduma yake hapa duniani. Alionyesha sifa hiyo kwa jinsi alivyoelekeza sifa na utukufu wote kwa Baba yake. Nyakati nyingine watu walimsifu Yesu kwa maneno yake yenye hekima, miujiza yake yenye nguvu, na utu wake mwema. Tena na tena, badala ya kuukubali utukufu huo, Yesu aliuelekeza kwa Yehova.​—Marko 10:17, 18; Yohana 7:15, 16.

13 Yesu alionyesha unyenyekevu kwa jinsi alivyowatendea watu. Hata alisema waziwazi kwamba alikuja duniani kuwatumikia wengine bali si kutumikiwa. (Mathayo 20:28) Alionyesha unyenyekevu kwa kushughulika na watu kwa upole na usawaziko. Wafuasi wake walipotenda kinyume na alivyotarajia, hakuwagombeza, bali aliendelea kujitahidi kufikia mioyo yao. (Mathayo 26:39-41) Umati wa watu ulipokuja wakati alipokuwa akitafuta mahali patulivu pa kupumzika, na pasipo na watu, hakuwafukuza, bali alijitoa mwenyewe na kuwafundisha “mambo mengi.” (Marko 6:30-34) Mwanamke asiye Mwisraeli alipozidi kumsihi amponye binti yake, mwanzoni alionyesha kwamba hakuwa na nia ya kufanya hivyo. Hata hivyo, Yesu hakukataa kwa hasira; badala yake alibadili nia yake kwa sababu mwanamke huyo alikuwa na imani ya pekee, kama tutakavyoona katika Sura ya 14.​—Mathayo 15:22-28.

14 Kwa njia nyingi sana, Yesu aliishi kulingana na maneno yake mwenyewe: “Mimi ni mpole na mnyenyekevu moyoni.” (Mathayo 11:29) Unyenyekevu wake haukuwa wa kijuujuu, au wa kidesturi tu. Ulitoka ndani kabisa ya moyo wake. Basi, haishangazi kwamba Yesu aliona umuhimu wa kuwafundisha wafuasi wake kuwa wanyenyekevu!

Kuwafundisha Wafuasi Wake Kuwa Wanyenyekevu

15, 16. Yesu alitaja tofauti gani kati ya maoni ya watawala wa ulimwengu na mtazamo ambao wafuasi wake walipaswa kusitawisha?

15 Haikuwa rahisi kwa mitume wa Yesu kusitawisha unyenyekevu. Yesu alijitahidi kuwafundisha sifa hiyo tena na tena. Kwa mfano, pindi moja Yakobo na Yohana walimtumia mama yao kumwomba Yesu awaahidi vyeo vya juu katika Ufalme wa Mungu. Kwa unyenyekevu, Yesu alijibu hivi: “Kuketi upande wangu wa kuume na upande wangu wa kushoto si haki yangu kutoa, bali wataketi wale ambao Baba yangu amewatayarishia.” Wale mitume wengine kumi “wakawakasirikia” Yakobo na Yohana. (Mathayo 20:20-24) Yesu alishughulikia tatizo hilo jinsi gani?

16 Aliwashauri wote kwa fadhili, akisema: “Mnajua kwamba watawala wa mataifa hupiga ubwana juu yao na wakuu hutumia mamlaka juu yao. Haipaswi kuwa hivyo kati yenu; bali yeyote anayetaka kuwa mkubwa kati yenu lazima awe mhudumu wenu, na yeyote anayetaka kuwa wa kwanza kati yenu lazima awe mtumwa wenu.” (Mathayo 20:25-27) Inaonekana mitume walikuwa wamejionea jinsi “watawala wa mataifa” walivyokuwa na kiburi, wenye kujitakia makuu, na wenye ubinafsi. Yesu alionyesha kwamba wafuasi wake wanapaswa kuwa tofauti na watawala hao wa kimabavu. Walihitaji kuwa wanyenyekevu. Je, mitume walielewa?

17-19. (a) Usiku uliotangulia kifo chake, Yesu aliwafundisha mitume wake somo kuhusu unyenyekevu kwa njia gani isiyosahaulika? (b) Akiwa mwanadamu, Yesu alifundisha somo gani lenye kuchochea zaidi kuhusu unyenyekevu?

17 Haikuwa rahisi kwao. Hiyo haikuwa mara ya kwanza wala ya mwisho kwa Yesu kufundisha somo hilo. Mapema, walipokuwa wakibishana kuhusu ni nani kati yao aliye mkuu zaidi, alimweka mtoto mdogo katikati yao na kuwaambia wawe kama watoto, ambao kwa kawaida hawana kiburi, hawajitakii makuu, wala kuhangaikia vyeo kama watu wazima. (Mathayo 18:1-4) Lakini, usiku uliotangulia kifo chake, aliona kwamba ingawa mitume wake walikuwa wakifanya yote wawezayo kuondolea mbali kiburi, bado walikuwa na udhaifu huo. Kisha, akawafundisha somo ambalo hawangesahau. Alijifunga kitambaa kiunoni na kufanya kazi ya hali ya chini zaidi, ambayo watumishi wa siku hizo walikuwa wakiwafanyia wageni. Yesu aliosha miguu ya mitume wake wote, kutia ndani Yuda, ambaye angemsaliti muda mfupi baadaye!—Yohana 13:1-11.

18 Yesu alikazia jambo kuu aliposema: “Nimewawekea kielelezo.” (Yohana 13:15) Je, somo ambalo Yesu alikuwa akiwafundisha lilifikia mioyo yao wakati huo? Hapana! Kwa sababu baadaye usiku huo walianza kubishana tena kuhusu yule aliye mkuu zaidi kati yao! (Luka 22:24-27) Hata hivyo, bado Yesu aliendelea kuwaonyesha subira na kuwafundisha kwa unyenyekevu. Kisha, akawafundisha somo lenye kuchochea zaidi kuhusu unyenyekevu: “Alijinyenyekeza na kuwa mtiifu mpaka kifo, ndiyo, kifo juu ya mti wa mateso.” (Wafilipi 2:8) Yesu alikubali kufa kifo cha aibu, akiwa ameshtakiwa kwa uwongo kuwa mvunja sheria na mkufuru. Hivyo, Mwana wa Mungu alikuwa wa pekee, kwa kuwa kati ya viumbe wote wa Yehova, alionyesha unyenyekevu kikamili.

19 Huenda somo hilo la mwisho kuhusu unyenyekevu ambalo Yesu alifundisha akiwa mwanadamu ndilo lililokazia kabisa sifa hiyo katika mioyo ya mitume wake waaminifu. Biblia inatuambia kwamba mitume hao waliendelea kutumikia kwa unyenyekevu kwa miaka mingi, ndiyo, makumi ya miaka baadaye. Namna gani sisi?

Je, Utafuata Mfano wa Yesu?

20. Tunawezaje kujua ikiwa sisi ni wanyenyekevu moyoni?

20 Paulo anatuhimiza hivi: “Iweni na mtazamo huu wa akili ambao pia Kristo Yesu alikuwa nao.” (Wafilipi 2:5) Kama Yesu tunapaswa kuwa wanyenyekevu moyoni. Tunawezaje kujua ikiwa sisi ni wanyenyekevu moyoni? Paulo anatukumbusha kwamba hatupaswi ‘kufanya jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu tuwaone wengine kuwa bora kuliko sisi.’ (Wafilipi 2:3) Hivyo basi, tunaweza kujua ikiwa sisi ni wanyenyekevu moyoni kwa kuchunguza jinsi tunavyowaona wengine. Tunapaswa kuwaona kuwa bora na wa muhimu zaidi kuliko sisi. Je, utatii shauri hilo?

21, 22. (a) Kwa nini waangalizi Wakristo wanapaswa kuwa wanyenyekevu? (b) Tunawezaje kuonyesha kwamba tumejivika unyenyekevu?

21 Miaka mingi baada ya Yesu kufa, bado mtume Petro alikuwa akifikiria kuhusu faida ya unyenyekevu. Petro aliwafundisha waangalizi Wakristo watimize majukumu yao kwa unyenyekevu, na kutopiga ubwana juu ya kondoo wa Yehova. (1 Petro 5:2, 3) Kuwa na mapendeleo si kisingizio cha kuwa na kiburi. Badala yake, mtu anapokuwa na mapendeleo anapaswa kuonyesha unyenyekevu wa kweli hata zaidi. (Luka 12:48) Bila shaka, hiyo ni sifa muhimu kwa kila Mkristo, na si kwa waangalizi tu.

22 Kwa kweli, Petro hakuusahau usiku ambao Yesu aliiosha miguu yake, ingawa Petro hakutaka kuoshwa! (Yohana 13:6-10) Petro aliwaandikia hivi Wakristo: “Ninyi nyote mtendeane kwa [mjifunge] unyenyekevu.” (1 Petro 5:5) Neno “mjifunge” linadokeza wazo la mtumishi anayejifunga kitambaa kiunoni ili kufanya kazi ya hali ya chini. Neno hilo linaweza kutukumbusha wakati ambapo Yesu alijifunga kitambaa kiunoni kabla ya kupiga magoti ili kuosha miguu ya mitume wake. Ikiwa sisi ni wanyenyekevu kama Yesu, kamwe hatutahisi kwamba sisi ni muhimu sana hivi kwamba tushindwe kutimiza mgawo ambao Yehova anatuomba tufanye. Kama tu ambavyo ni rahisi kwa watu kuona mavazi tuliyovaa, wengine wanapaswa kuona kwamba sisi ni wanyenyekevu.

23, 24. (a) Kwa nini tunapaswa kupinga mwelekeo wowote wa kuwa na majivuno? (b) Sura inayofuata itasahihisha maoni gani yasiyofaa kuhusu unyenyekevu?

23 Majivuno ni kama sumu na matokeo yake yanaweza kuwa mabaya sana. Majivuno yanaweza kumfanya mtu mwenye vipawa vingi awe asiyefaa hata kidogo machoni pa Mungu. Kwa upande mwingine, unyenyekevu unaweza kumfanya hata mtu wa hali ya chini zaidi awe na thamani sana machoni pa Yehova. Tukisitawisha sifa hiyo yenye thamani kila siku kwa kufanya kila tuwezalo kutembea kwa unyenyekevu huku tukifuata hatua za Kristo, tutathawabishwa. Petro aliandika: “Kwa hiyo, jinyenyekezeni chini ya mkono wenye nguvu wa Mungu, ili awainue kwa wakati unaofaa.” (1 Petro 5:6) Bila shaka, Yehova alimwinua Yesu kwa kuwa alijinyenyekeza kabisa. Mungu wetu atafurahia kukuthawabisha wewe pia kwa sababu ya unyenyekevu wako.

24 Inasikitisha kwamba watu fulani wanaona unyenyekevu kuwa udhaifu. Mfano wa Yesu unatusaidia kuona kwamba hilo si kweli, kwa kuwa mwanadamu aliyekuwa mnyenyekevu zaidi ndiye pia aliyekuwa jasiri zaidi. Hilo ndilo litakalozungumziwa katika sura inayofuata.

a Kitabu kimoja kinapozungumzia tukio hilo, kinasema kwamba wanyama hao “ni viumbe wa hali ya chini.” Kwa kuongezea kinasema: “Wanajikokota-kokota, ni wakaidi, wanatumiwa na maskini kufanya kazi, na sura yao haivutii.”

b Ili kupata uthibitisho zaidi kwamba Mikaeli ni Yesu, tafuta sehemu ya “Majibu ya Maswali ya Biblia” katika makala yenye kichwa “Yule Malaika Mkuu Mikaeli Ni Nani?” kwenye tovuti rasmi ya Mashahidi wa Yehova ya jw.org.

Unawezaje Kumfuata Yesu?

  • Unaposhawishika kujisifu kuhusu mambo uliyotimiza maishani, mfano wa Yesu unawezaje kukusaidia?​—Mathayo 12:15-19; Marko 7:35-37.

  • Unawezaje kufuata mfano wa Yesu kwa kufanya kazi za hali ya chini ili kuwahudumia ndugu na dada zako wa kiroho?​—Yohana 21:1-13.

  • Mfano wa Yesu unaweza kukunufaishaje unaposhawishiwa kujitafutia makuu na mafanikio katika mfumo huu wa mambo?​—Yohana 6:14, 15.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki