Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • cl sura 1 kur. 7-17
  • “Tazama! Huyu Ndiye Mungu Wetu!”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Tazama! Huyu Ndiye Mungu Wetu!”
  • Mkaribie Yehova
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Maana ya Jina la Mungu
  • Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova
  • Mungu Mwenye Utu
  • “Tazama! Huyu Ndiye Mungu Wetu!”
  • Mungu Ana Jina
    Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu
  • Mungu Ana Jina
    Kumsikiliza Mwalimu Mkuu
  • Kuzijua Njia za Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Liheshimu Jina Kuu La Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
Pata Habari Zaidi
Mkaribie Yehova
cl sura 1 kur. 7-17
Musa akificha uso wake karibu na kichaka kinachowaka moto.

SURA YA 1

“Tazama! Huyu Ndiye Mungu Wetu!”

1, 2. (a) Ungependa kumuuliza Mungu maswali gani? (b) Musa alimuuliza Mungu swali gani?

JE, UNAWEZA kuwazia ukizungumza na Mungu? Hilo ni wazo lenye kusisimua sana—kuzungumza na Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu! Mwanzoni unasitasita, hatimaye unafanikiwa kumjibu. Anakusikiliza, anaitikia, na hata anakuruhusu kuuliza swali lolote ulilo nalo. Sasa, utamwuliza nini?

2 Zamani, mwanamume mmoja alikuwa katika hali kama hiyo. Jina lake ni Musa. Huenda ukashangazwa na swali aliloamua kumuuliza Mungu. Hakuuliza kuhusu hali yake, wakati wake ujao, au matatizo wanayokabili wanadamu. Badala yake, aliuliza kuhusu jina la Mungu. Huenda hilo likakushangaza, kwa kuwa tayari Musa alijua jina la Mungu. Basi, lazima swali lake lilikuwa na maana kubwa zaidi. Kwa kweli, Musa aliuliza swali muhimu zaidi ya yote. Jibu la swali hilo linatuhusu sote. Linaweza kukusaidia kuchukua hatua muhimu sana ya kumkaribia Mungu. Jinsi gani? Hebu tuchunguze mazungumzo hayo ya pekee.

3, 4. Ni matukio gani yaliyotangulia mazungumzo ya Musa na Mungu, na jambo kuu la mazungumzo hayo lilikuwa nini?

3 Musa alikuwa na umri wa miaka 80. Kwa miaka 40 alikuwa uhamishoni mbali na watu wake Waisraeli, waliokuwa watumwa nchini Misri. Siku moja, alipokuwa akichunga mifugo ya baba-mkwe wake, aliona jambo la ajabu. Kichaka cha miiba kilikuwa kikiwaka moto, lakini hakikuteketea. Kiliendelea kuwaka moto, na kung’aa kama ishara mlimani. Musa alikaribia ili achunguze. Lazima iwe alishtuka sana aliposikia sauti ikizungumza naye kutoka katikati ya moto huo! Mungu alizungumza na Musa kwa muda mrefu kupitia malaika. Na huenda unajua kwamba Mungu alimwagiza Musa aliyesita, aache maisha yake matulivu na kurudi Misri ili kuwakomboa Waisraeli kutoka utumwani.​—Kutoka 3:1-12.

4 Musa angeweza kumuuliza Mungu swali lolote. Hata hivyo, ona swali aliloamua kumuuliza: “Tuseme niende kwa Waisraeli na kuwaambia, ‘Mungu wa mababu zenu amenituma kwenu,’ nao waniulize, ‘Jina lake ni nani?’ Niwaambie nini?”​—Kutoka 3:13.

5, 6. (a) Ni ukweli gani muhimu tunaojifunza kutokana na swali la Musa? (b) Watu wamelifanyia nini jina la Mungu, na kwa nini hilo ni jambo baya sana? (c) Mungu ametuonyesha nini kwa kutufunulia jina lake?

5 Kwanza kabisa, swali hilo linatufundisha kwamba Mungu ana jina. Hatupaswi kamwe kupuuza ukweli huo. Lakini watu wengi hupuuza jambo hilo. Jina la Mungu limeondolewa kwenye tafsiri nyingi sana za Biblia na kubadilishwa na majina ya cheo, kama vile “Bwana” na “Mungu.” Hilo ni mojawapo ya mambo yenye kusikitisha sana na yenye kuchukiza ambayo yamefanywa kwa sababu za kidini. Wewe hufanya nini unapokutana na mtu kwa mara ya kwanza? Bila shaka, unamuuliza jina lake. Ndivyo ilivyo na kumjua Mungu. Yeye si Mungu tu asiye na jina, asiye na hisia, asiyeweza kujulikana wala kufahamika. Ingawa haonekani, yeye ni halisi, na jina lake ni Yehova.

6 Isitoshe, Mungu anapofunua jina lake, yeye hutusaidia kutambua jambo la pekee na lenye kusisimua sana. Anatukaribisha tumjue. Anataka tufanye uamuzi bora zaidi maishani, yaani, kumkaribia yeye. Lakini Yehova amefanya mengi zaidi tu ya kutuambia jina lake. Ametufundisha pia maana ya jina hilo.

Maana ya Jina la Mungu

7. (a) Jina la Mungu linamaanisha nini? (b) Musa alitaka kujua nini alipomuuliza Mungu jina Lake?

7 Yehova alijichagulia jina lenye maana sana. Maana ya jina “Yehova” ni “Yeye Husababisha Kuwa.” Ni wa pekee sana kwa sababu aliumba kila kitu. Pia, yeye husababisha mapenzi yake yote yatimizwe, na hata anawawezesha watumishi wake wasio wakamilifu watimize chochote anachotaka. Hilo ni wazo lenye kupendeza sana. Lakini je, jina lake linamtambulisha tu kuwa Muumba? Ni wazi kwamba Musa alitaka kujifunza mengi zaidi. Ukweli ni kwamba jina hilo la Mungu halikuwa geni. Watu walikuwa wamelitumia kwa karne nyingi. Hapana shaka kwamba Musa alipouliza kuhusu jina la Mungu, alitaka kumjua Mungu anayewakilishwa na jina hilo. Ni kana kwamba alikuwa akisema: ‘Niwaambie nini watu wako Waisraeli kukuhusu ili waweze kukuamini na kusadiki kwamba kwa kweli utawakomboa?’

8, 9. (a) Yehova alijibuje swali la Musa, na kwa nini tafsiri nyingi zimekosea katika kutafsiri jibu Lake? (b) Usemi “Nitakuwa Kile Ninachochagua Kuwa” unamaanisha nini?

8 Yehova alimjibu kwa kueleza maana ya jina lake. Alimwambia Musa hivi: “Nitakuwa Kile Ninachochagua Kuwa.” (Kutoka 3:14) Tafsiri nyingi za Biblia husema hivi: “Mimi Niko Ambaye Niko.” Lakini tafsiri sahihi zaidi ya maneno hayo inaonyesha kwamba Mungu hakuwa tu akithibitisha kwamba yeye yupo. Badala yake, Yehova alikuwa akimfundisha Musa—na sisi sote—kwamba ‘angechagua kuwa,’ chochote alichohitaji ili kutimiza ahadi Zake. Tafsiri ya J. B. Rotherham inatafsiri mstari huo hivi: “Nitakuwa chochote nipendacho.” Mtaalamu mmoja wa lugha ya Kiebrania kilichotumika katika Biblia anasema hivi kuhusu maneno hayo: “Haidhuru ni hali au uhitaji gani uliopo . . . , Mungu ‘atakuwa’ suluhisho la uhitaji huo.”

9 Hilo lilimaanisha nini kwa Waisraeli? Licha ya kizuizi kilichowakabili au magumu ambayo wangepata, Yehova angekuwa chochote anachochagua kuwa ili kuwakomboa kutoka utumwani na kuwapeleka katika Nchi Iliyoahidiwa. Bila shaka, jina hilo liliwatia moyo wamtumaini Mungu. Linaweza kuwa na matokeo kama hayo kwetu. (Zaburi 9:10) Kwa nini?

10, 11. Jina la Yehova linatusaidiaje kuwa na uhakika kwamba yeye ni Baba bora anayeweza kutimiza majukumu yake yote? Toa mfano.

10 Kwa mfano: Wazazi wanajua jinsi ya kutimiza majukumu mbalimbali wanapowalea watoto wao. Kwa siku moja tu, mzazi anaweza kutenda kama muuguzi, mpishi, mwalimu, mtoa-nidhamu, hakimu, na kadhalika. Wengi hulemewa na majukumu mbalimbali wanayopaswa kutimiza. Wazazi wengi wanajua kwamba watoto wao huwategemea kabisa, hawana shaka kwamba Baba au Mama anaweza kupunguza maumivu ya jeraha, kusuluhisha mabishano, kurekebisha kitu chochote cha kuchezea kilichoharibika, na kujibu maswali yoyote wanayouliza kwa sababu ya udadisi. Baadhi ya wazazi huhisi kwamba hawastahili kutegemewa na watoto wao, na mara kwa mara wanavunjika moyo kwa sababu wanashindwa kutimiza kikamili majukumu yao.

11 Yehova pia ni Baba mwenye upendo. Yeye huwa chochote anachotaka ili kuwatunza watoto wake walio duniani kwa njia nzuri zaidi, bila kukiuka sheria zake kamilifu. Kwa hiyo, maana ya jina lake, Yehova, inatuhakikishia kwamba yeye ni Baba bora kabisa. (Yakobo 1:17) Baada ya muda, Musa na Waisraeli wengine waaminifu waliona kwamba Yehova hutenda kupatana na maana ya jina lake. Walishangaa sana jinsi Yehova alivyoamua kuwa chochote walichohitaji. Aliwashinda maadui wao wote, aligawanya Bahari Nyekundu, aliwapa sheria kamilifu, alikuwa hakimu mwenye haki, aliwapa chakula na maji walipokuwa jangwani, alihakikisha kwamba viatu na nguo zao hazichakai na mambo mengine mengi.

12. Mtazamo wa Farao kumwelekea Yehova ulitofautianaje na wa Musa?

12 Hivyo, Mungu amejulisha jina lake, ameeleza maana yake, na hata ametenda kupatana na maana ya jina lake. Ni wazi kwamba Mungu anataka tumjue. Tunaitikiaje? Musa alitaka kumjua Mungu. Tamaa hiyo ilimwongoza maishani mwake na ikamsaidia kumkaribia sana Baba yake wa mbinguni. (Hesabu 12:6-8; Waebrania 11:27) Inasikitisha kwamba watu wengi walioishi wakati huo hawakuwa na tamaa ya kumjua Mungu kama Musa. Musa alipomweleza Farao jina la Yehova, mfalme huyo wa Misri mwenye kiburi aliuliza hivi kwa ukali: “Yehova ni nani?” (Kutoka 5:2) Farao hakutaka kujifunza mengi kumhusu Yehova. Badala yake, alimpuuza Mungu wa Israeli na kumwona kuwa asiyefaa na duni. Watu wengi leo wana maoni kama hayo ambayo huwafanya wakose kutambua mojawapo ya kweli muhimu zaidi—Yehova ni Bwana Mwenye Enzi Kuu.

Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova

13, 14. (a) Kwa nini Yehova amepewa majina mengi ya cheo kwenye Biblia? Taja baadhi yake. (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 16.) (b) Kwa nini Yehova peke yake ndiye anayestahili kuitwa “Bwana Mwenye Enzi Kuu”?

13 Yehova anaweza kutimiza mambo mbalimbali ndio sababu Maandiko yanamtaja kwa majina mengi ya cheo. Majina hayo hayachukui mahali pa jina lake; badala yake, yanatufundisha mengi kuhusu maana ya jina lake. Kwa mfano, anaitwa “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.” (2 Samweli 7:22) Cheo hicho cha juu kinachotajwa mara nyingi katika Biblia kinatusaidia kutambua ukuu wa Yehova. Yeye pekee ndiye aliye na haki ya kuwa Mtawala wa ulimwengu mzima. Tuchunguze sababu.

14 Yehova ni wa pekee kwa sababu ni Muumba. Ufunuo 4:11 inasema hivi: “Unastahili, Ee Yehova Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilitokea navyo vikaumbwa.” Maneno hayo ya heshima yanamhusu Yehova peke yake. Kila kitu ulimwenguni kiliumbwa na Yehova! Ni wazi kwamba Yehova anastahili heshima, na nguvu, na utukufu kwa sababu yeye ni Bwana Mwenye Enzi Kuu na Muumba wa vitu vyote.

15. Kwa nini Yehova anaitwa “Mfalme wa umilele”?

15 Jina lingine la cheo linalotumiwa kumhusu Yehova peke yake ni “Mfalme wa umilele.” (1 Timotheo 1:17; Ufunuo 15:3) Hilo linamaanisha nini? Si rahisi kwetu kuelewa wazo hilo, lakini Yehova ni Mungu wa umilele kwa sababu hana mwanzo wala mwisho. Zaburi 90:2 inasema: “Tangu milele hadi milele, wewe ni Mungu.” Hivyo, Yehova hana mwanzo; yeye ni wa umilele. Kwa kufaa anaitwa “Mzee wa Siku,” kwa sababu amekuwepo sikuzote kabla ya mtu yeyote au kitu chochote kuumbwa! (Danieli 7:9, 13, 22) Ni nani anayeweza kupinga haki yake ya kuwa Bwana Mwenye Enzi Kuu?

16, 17. (a) Kwa nini hatuwezi kumwona Yehova, na kwa nini hilo halipaswi kutushangaza? (b) Kwa nini Yehova ni mkuu kuliko kitu chochote tunachoweza kugusa au kuona?

16 Lakini watu fulani hupinga haki yake kama alivyofanya Farao. Sababu moja ni kwamba wanadamu wasio wakamilifu huamini hasa vitu wanavyoweza kuona. Hatuwezi kumwona Bwana Mwenye Enzi Kuu. Yeye ni roho, na wanadamu hawawezi kumwona. (Yohana 4:24) Isitoshe, mwanadamu hawezi kumwona Yehova Mungu uso kwa uso na aendelee kuishi. Yehova mwenyewe alimwambia Musa hivi: “Huwezi kuuona uso wangu, kwa sababu hakuna mwanadamu anayeweza kuniona na aendelee kuishi.”​—Kutoka 33:20; Yohana 1:18.

17 Hatupaswi kushangazwa na jambo hilo. Ni wazi kwamba Musa aliona kwa kiasi kidogo utukufu wa Yehova kupitia malaika aliyemwakilisha. Matokeo yalikuwa nini? Uso wa Musa ulikuwa ‘ukitoa miale’ kwa muda fulani, na hata Waisraeli waliogopa kumtazama usoni. (Kutoka 33:21-23; 34:5-7, 29, 30) Hivyo, ni wazi kwamba hakuna mwanadamu yeyote anayeweza kumtazama Bwana Mwenye Enzi Kuu katika utukufu wake wote! Je, hilo linamaanisha kwamba yeye si halisi kama vitu tunavyoweza kuona na kugusa? Hapana, kuna vitu vingi tunavyoamini kuwa ni halisi ingawa hatuwezi kuviona—kwa mfano, upepo, mawimbi ya redio, na mawazo. Isitoshe, Yehova ni wa umilele, haathiriwi na kupita kwa wakati, hata kwa mabilioni ya miaka! Pia, vitu tunavyoweza kugusa au kuona huzeeka na kuharibika, lakini Yehova habadiliki hata muda mrefu upite. Hivyo, yeye ni mkuu kuliko kitu chochote tunachoweza kugusa au kuona. (Mathayo 6:19) Je, tumwone tu kuwa nguvu fulani isiyoonekana na isiyo na utu, au kwamba hatujali? Hebu tuone.

Mungu Mwenye Utu

18. Yehova alimwonyesha nini Ezekieli, na zile nyuso nne za “viumbe hai” walio karibu na Yehova zinawakilisha nini?

18 Ingawa hatuwezi kumwona Mungu, kuna maandiko ya Biblia yenye kusisimua yanayotusaidia kuelewa hali ya mbinguni. Mojawapo ni sura ya kwanza ya kitabu cha Ezekieli. Yehova alimwonyesha Ezekieli sehemu ya kimbingu ya tengenezo lake, lililofananishwa na gari kubwa la kimbingu. Jambo linalovutia zaidi ni maelezo kuhusu viumbe wa roho wenye nguvu wanaomzunguka Yehova. (Ezekieli 1:4-10) Hao “viumbe hai” wanashirikiana kwa ukaribu na Yehova, na umbo lao linatusaidia kuelewa jambo muhimu sana kuhusu Mungu wanayemtumikia. Kila kiumbe ana nyuso nne—uso wa ng’ombe dume, simba, tai, na mwanadamu. Ni wazi kwamba sifa hizo nne zinafanyiza msingi wa utu wa Yehova wenye kuvutia.​—Ufunuo 4:6-8, 10.

19. Ni sifa ipi inayowakilishwa na (a) uso wa ng’ombe dume? (b) uso wa simba? (c) uso wa tai? (d) uso wa mwanadamu?

19 Katika Biblia, ng’ombe dume hutumiwa kuwakilisha nguvu, na hilo linafaa kwa sababu ni mnyama mwenye nguvu sana. Pia, simba huwakilisha haki, kwa sababu haki ya kweli inahitaji ujasiri, sifa kuu ya simba. Tai ni maarufu kwa sababu ya uwezo wake mkubwa wa kuona, anaweza kuona hata vitu vidogo sana vilivyo mbali. Hivyo, kwa kufaa uso wa tai unawakilisha hekima ya Mungu ya kutambua mambo kabla hayajatokea. Vipi uso wa mwanadamu? Kwa kweli, mwanadamu, aliyeumbwa kwa mfano wa Mungu, ana uwezo mkubwa wa kuonyesha sifa ya upendo ambayo ndiyo sifa kuu zaidi ya Mungu. (Mwanzo 1:26) Sifa hizo mbalimbali za utu wa Yehova—nguvu, haki, hekima, na upendo—hutajwa mara nyingi katika Maandiko hivi kwamba zinaweza kuitwa sifa kuu za Mungu.

20. Je, tuwe na wasiwasi kwamba huenda utu wa Yehova umebadilika, na kwa nini unajibu hivyo?

20 Je, tuwe na wasiwasi kwamba huenda Mungu amebadilika tangu Biblia ilipotaja sifa zake maelfu ya miaka iliyopita? La, utu wa Mungu haubadiliki. Anatuambia hivi: “Mimi ni Yehova; sibadiliki.” (Malaki 3:6) Yehova habadili maoni yake bila sababu, badala yake yeye hujithibitisha kuwa Baba anayefaa kabisa kwa kukabiliana na kila hali inayotokea. Yeye huonyesha sifa muhimu za utu wake kwa wakati unaofaa. Kati ya sifa zote za Mungu, sifa kuu zaidi ni upendo. Upendo huonekana katika kila jambo ambalo Mungu anafanya. Yeye hutumia nguvu, haki, na hekima yake kwa njia ya upendo. Kwa kweli, Biblia husema jambo fulani la pekee kumhusu Mungu na sifa hii. Inasema: “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Ona kwamba haisemi Mungu ana upendo wala haisemi Mungu hupenda. Badala yake, inasema kwamba Mungu ni upendo. Upendo, ambao ni utu wake wa asili, huongoza matendo yake yote.

“Tazama! Huyu Ndiye Mungu Wetu!”

21. Tunahisije tunapoendelea kujua sifa za Yehova vizuri zaidi?

21 Je, umewahi kumwona mtoto mdogo akijivunia kumtambulisha kwa shangwe baba yake kwa rafiki zake akisema hivi, “Huyu ni baba yangu”? Waabudu wa Mungu wana sababu nzuri sana za kuhisi hivyo kumhusu Yehova. Biblia inatabiri kuhusu wakati ambapo watu waaminifu watasema hivi kwa shangwe: “Tazama! Huyu ndiye Mungu wetu!” (Isaya 25:8, 9) Kadiri unavyojua sifa za Yehova vizuri zaidi, ndivyo utakavyohisi kwamba una Baba bora zaidi.

22, 23. Biblia inasema nini kumhusu Baba yetu wa mbinguni, na tunajuaje kwamba anataka tumkaribie?

22 Yehova si Baba asiye na hisia au asiyejali kama vile wasomi wa mambo ya dini na wanafalsafa fulani washupavu wanavyofundisha. Hatuwezi kumkaribia Mungu asiye na hisia, wala Biblia haisemi kwamba Baba yetu wa mbinguni yuko hivyo. Badala yake, inamwita “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11) Ana hisia changamfu na zenye upendo. Biblia inasema kwamba ‘moyo wake ulihuzunika’ viumbe wake wenye akili walipokosa kutii maagizo aliyowapa ili kuwalinda. (Mwanzo 6:6; Zaburi 78:41) Lakini tunapotenda kwa hekima kulingana na Neno lake, tunafanya ‘moyo wake ushangilie.’​—Methali 27:11.

23 Baba yetu anataka tumkaribie. Neno lake hutuhimiza ‘tupapase-papase tukimtafuta na kwa kweli tumpate, ingawa, kwa hakika, hayuko mbali na kila mmoja wetu.’ (Matendo 17:27) Lakini, wanadamu wanawezaje kumkaribia Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu?

Baadhi ya Majina ya Yehova ya Cheo

  • Mweza-Yote. Nguvu zake hazina mipaka, haziwezi kushindwa.​—Ufunuo 15:3.

  • Baba. Ndiye Chanzo cha uhai wote, hata uhai wa milele, huwaonyesha watumishi wake upendo wa baba.​—Methali 27:11; Yohana 5:21.

  • Mfundishaji Mkuu. Yeye ni Mwalimu mwenye hekima isiyo na kifani. Tunapaswa kufuata maagizo na mwongozo wake.​—Isaya 30:20; 48:17.

  • Mwamba. Habadiliki, yeye ni kimbilio salama.​—Kumbukumbu la Torati 32:4.

  • Mchungaji. Huwaongoza na kuwalinda watumishi wake walio kama kondoo na kuwapatia mahitaji yao ya kiroho.​—Zaburi 23:1.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki