SURA YA 20
“Yeye Ni Mwenye Hekima Moyoni”—Lakini Mnyenyekevu
1-3. Tunajuaje kwamba Yehova ni mnyenyekevu?
BABA anataka kumfundisha mtoto wake mdogo somo muhimu. Anatamani somo hilo liguse moyo wa mtoto wake. Atafanyaje hivyo? Je, atasimama, na kutazama chini na kumtisha mtoto huyo kwa maneno makali? Au atainama chini kufikia kimo cha mtoto huyo na kuzungumza naye kwa upole, na kwa urafiki? Ikiwa baba ni mnyenyekevu na mwenye hekima atamtendea mtoto wake kwa njia ya upole.
2 Yehova ni Baba wa aina gani—je, yeye ni mwenye kiburi au mnyenyekevu, mkali au mpole? Yehova anajua kila jambo, na ana hekima kamili. Huenda umejionea kwamba mara nyingi watu wenye ujuzi na akili si wanyenyekevu. Ni kama Biblia inavyosema, “ujuzi huleta majivuno.” (1 Wakorintho 3:19; 8:1) Lakini Yehova, ni “mwenye hekima moyoni,” na mnyenyekevu pia. (Ayubu 9:4) Yehova hana kiburi licha ya kwamba ana cheo cha juu na fahari. Kwa nini?
3 Yehova ni mtakatifu. Hivyo, hana sifa yoyote mbaya ambayo humchafua mtu kama vile kiburi. (Marko 7:20-22) Pia, ona maneno ambayo nabii Yeremia alimwambia Yehova: “Kwa hakika utakumbuka na kuinama juu yangu.”a (Maombolezo 3:20, NW) Hebu wazia! Yehova, Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu, alikuwa tayari “kuinama,” au kujinyenyekeza kufikia kimo cha Yeremia. Alifanya hivyo ili amtie moyo mwanadamu huyo asiye mkamilifu. (Zaburi 113:7) Naam, Yehova ni mnyenyekevu. Lakini Mungu anaonyeshaje unyenyekevu? Unyenyekevu unahusianaje na hekima? Na kwa nini unyenyekevu ni muhimu kwetu?
Jinsi Yehova Anavyoonyesha Unyenyekevu
4, 5. (a) Unyenyekevu ni nini, na unaonyeshwaje, na kwa nini unyenyekevu haupaswi kuonwa kuwa udhaifu au woga? (b) Yehova alionyeshaje unyenyekevu aliposhughulika na Daudi, na tunanufaikaje na unyenyekevu wa Yehova?
4 Unyenyekevu unamaanisha kutojifikiria kupita kiasi kutojivuna na kutokuwa na kiburi. Unyenyekevu ni sifa ya moyoni na huonyeshwa kupitia sifa kama vile upole, subira, na usawaziko. (Wagalatia 5:22, 23) Lakini sifa hizo za kimungu hazipaswi kamwe kuonwa kuwa udhaifu au woga. Sifa hizo hazipingani na hasira ya Yehova ya uadilifu au jinsi anavyotumia nguvu zake za kuangamiza. Badala yake, unyenyekevu na upole wa Yehova unaonyesha kwamba ana nguvu nyingi, yaani, uwezo wa kujidhibiti kikamili. (Isaya 42:14) Unyenyekevu unahusianaje na hekima? Kitabu kimoja cha marejeo kinachozungumzia Biblia kinasema hivi: “Unyenyekevu unafafanuliwa kuwa . . . hali ya kutokuwa na ubinafsi na ni chanzo muhimu cha hekima yote.” Hivyo basi, haiwezekani kuwa na hekima ya kweli bila unyenyekevu. Tunanufaikaje kutokana na unyenyekevu wa Yehova?
Baba mwenye hekima huwatendea watoto wake kwa upole na unyenyekevu
5 Mfalme Daudi alimwimbia Yehova hivi: “Wewe hunipa ngao yako ya wokovu, mkono wako wa kuume hunitegemeza, na unyenyekevu wako hunifanya niwe mkuu.” (Zaburi 18:35) Ni kana kwamba Yehova aliinama ili amsaidie mwanadamu huyo asiye mkamilifu, alimlinda na kumtunza siku baada ya siku. Daudi alijua kwamba angeweza kuokolewa kutoka kwa maadui wake na kuwa mfalme mkuu kwa sababu Yehova alijinyenyekeza na kumsaidia. Kwa kweli, ni nani kati yetu angeweza kuwa na tumaini lolote la kuokolewa ikiwa Yehova hangekuwa mnyenyekevu, na hangekuwa tayari kujishusha ili kushughulika nasi akiwa Baba mpole na mwenye upendo?
6, 7. (a) Kwa nini Biblia haisemi kamwe kwamba Yehova ni mwenye kiasi? (b) Kuna uhusiano gani kati ya upole na hekima, na ni nani aliye mfano bora kabisa wa sifa hizo?
6 Inafaa kukumbuka kwamba kuna tofauti kati ya unyenyekevu na kiasi. Kiasi ni sifa nzuri sana ambayo wanadamu waaminifu wanapaswa kusitawisha. Kama tu sifa ya unyenyekevu, sifa ya kiasi pia inahusiana na hekima. Kwa mfano, Methali 11:2, inasema: “Wenye kiasi wana hekima.” Hata hivyo, Biblia haisemi kamwe kwamba Yehova ni mwenye kiasi. Kwa nini? Kulingana na Maandiko, mtu mwenye kiasi ni yule anayetambua mipaka yake mwenyewe. Mungu Mweza-Yote hana mipaka yoyote isipokuwa mipaka anayojiwekea mwenyewe kwa sababu ya kanuni zake za uadilifu. (Marko 10:27; Tito 1:2) Isitoshe, hajitiishi kwa yeyote kwa sababu yeye ni Aliye Juu Zaidi. Kwa hiyo, sifa hiyo ya kiasi haimhusu Yehova.
7 Hata hivyo, Yehova ni mnyenyekevu na mpole. Yeye huwafundisha watumishi wake kwamba hawawezi kuwa na hekima ya kweli wasipokuwa wapole. Neno lake linazungumzia “upole unaotokana na hekima.”b (Yakobo 3:13) Fikiria jinsi Yehova anavyoonyesha sifa hizo.
Yehova Huwapa Wengine Majukumu Naye Huwasikiliza kwa Unyenyekevu
8-10. (a) Kwa nini inashangaza kwamba Yehova yuko tayari kuwapa wengine majukumu na kuwasikiliza? (b) Mweza-Yote ameonyeshaje unyenyekevu anaposhughulika na malaika wake?
8 Utayari wa Yehova wa kusikiliza na kuwapa wengine majukumu unaonyesha kwamba yeye ni mnyenyekevu. Inashangaza kwamba Yehova yuko tayari kufanya hivyo ingawa yeye hahitaji msaada wala ushauri. (Isaya 40:13, 14; Waroma 11:34, 35) Hata hivyo, Biblia inatuonyesha tena na tena kwamba Yehova hujinyenyekeza katika njia hizo.
9 Kwa mfano, fikiria kisa kimoja cha pekee kilichotukia katika maisha ya Abrahamu. Abrahamu alitembelewa na wageni watatu, alimwita mmoja wao “Yehova.” Wageni hao walikuwa malaika, lakini mmoja wao alikuja kwa jina la Yehova na alikuwa akitenda kwa jina la Yehova. Malaika huyo alipozungumza na kutenda, ni kana kwamba Yehova mwenyewe alikuwa akizungumza na kutenda. Kupitia malaika huyo, Yehova alimwambia Abrahamu kwamba alikuwa amesikia “kilio dhidi ya Sodoma na Gomora.” Yehova alisema hivi: “Nitashuka chini ili nione kama mambo wanayotenda yanalingana na kilio kilichonifikia. Na kama sivyo, nitajua.” (Mwanzo 18:3, 20, 21) Bila shaka, ujumbe huo wa Yehova haukumaanisha kwamba Mweza-Yote ‘angeshuka’ kihalisi. Badala yake, aliwatuma tena malaika ili wamwakilishe. (Mwanzo 19:1) Kwa nini? Je, Yehova ambaye ana uwezo wa kuona kila jambo hangeweza ‘kujua’ hali ya eneo hilo bila msaada? Bila shaka angeweza. Lakini badala yake, kwa unyenyekevu Yehova aliwapa malaika hao kazi ya kuchunguza jinsi hali ilivyo na kumtembelea Loti na familia yake iliyokuwa ikiishi Sodoma.
10 Isitoshe, Yehova husikiliza. Pindi moja, aliwaomba malaika wake watoe maoni kuhusu njia mbalimbali za kumwangamiza Mfalme Ahabu aliyekuwa mwovu. Yehova hakuhitaji msaada huo. Lakini, alikubali maoni ya malaika mmoja, naye akamtuma atekeleze jambo hilo. (1 Wafalme 22:19-22) Tukio hilo linaonyesha kwamba yeye ni mnyenyekevu, sivyo?
11, 12. Abrahamu alipataje kuelewa unyenyekevu wa Yehova?
11 Yehova yuko tayari pia kuwasikiliza wanadamu wasio wakamilifu ambao wanataka kumweleza mahangaiko yao. Kwa mfano, Yehova alipomwambia Abrahamu kwamba alikusudia kuharibu Sodoma na Gomora, mwanamume huyo mwaminifu alishtuka. Abrahamu akasema: “Ni jambo usiloweza kuwazia. Je, Mwamuzi wa dunia yote hatatenda jambo la haki?” Alimuuliza Yehova ikiwa kuna watu 50 waadilifu, je, hangelisamehe jiji hilo? Yehova alimjibu kwamba angelisamehe. Lakini Abrahamu akamuuliza swali hilo tena na tena, na kupunguza idadi hiyo hadi 45, kisha 40, na kuendelea. Abrahamu aliendelea kuuliza maswali hadi idadi hiyo ilipofikia kumi licha ya Yehova kumhakikishia kwamba hangeangamiza miji hiyo. Huenda Abrahamu hakufahamu vizuri rehema ya Yehova. Lakini kwa subira Yehova alimruhusu rafiki na mtumishi wake Abrahamu aeleze mahangaiko yake.—Mwanzo 18:23-33.
12 Ni wanadamu wangapi wenye akili, na wenye elimu ambao wangemsikiliza kwa subira mtu asiye na akili nyingi sana?c Lakini Mungu wetu alionyesha unyenyekevu mkubwa kwa kumsikiliza Abrahamu. Wakati wa mazungumzo hayo, Abrahamu alitambua pia kwamba Yehova “si mwepesi wa hasira.” (Kutoka 34:6) Huenda Abrahamu alijua kwamba hakuwa na haki ya kumwuliza Aliye Juu Zaidi mambo aliyokusudia kufanya, kwa hiyo alimsihi hivi mara mbili: “Tafadhali Yehova, usiwake hasira.” (Mwanzo 18:30, 32) Bila shaka, Yehova hakukasirika. Kwa kweli, Yehova ana “upole unaotokana na hekima.”
Yehova Ni Mwenye Usawaziko
13. Neno “usawaziko” hutumiwa katika Biblia kumaanisha nini, na kwa nini sifa hiyo inamfaa kabisa Yehova?
13 Tunaweza kuona unyenyekevu wa Yehova kupitia sifa nyingine yenye kupendeza—usawaziko. Inasikitisha kwamba wanadamu wengi wasio wakamilifu hawaonyeshi sifa hiyo. Yehova yuko tayari kuwasikiliza viumbe wake wenye akili, na yuko tayari pia kukubali maoni yao ikiwa tu hayapingani na kanuni zake za uadilifu. Neno “usawaziko” hutumiwa katika Biblia kumaanisha ‘kukubali maoni ya wengine.’ Usawaziko wa Yehova unaonyesha pia yeye ni mwenye hekima. Andiko la Yakobo 3:17 linasema hivi: ‘Hekima inayotoka juu ni yenye usawaziko.’ Ni katika njia gani Yehova Mungu wetu mwenye hekima ni mwenye usawaziko? Kwanza, yeye hubadilikana kulingana na hali. Kumbuka kwamba jina lake linatufundisha kwamba Yeye huwa chochote anachochagua kuwa ili kutimiza kusudi lake. (Kutoka 3:14) Je, hilo halionyeshi kwamba yeye hubadilikana kulingana na hali na ni mwenye usawaziko?
14, 15. Maono ya Ezekieli kuhusu gari la kimbingu la Yehova yanatufundisha nini kuhusu sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Yehova, na hilo linatofautianaje na mashirika ya wanadamu?
14 Kuna mistari fulani ya Biblia inayotusaidia kuelewa jinsi Yehova anavyobadilikana kulingana na hali. Nabii Ezekieli alipata maono ya sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Yehova linalofanyizwa na viumbe wa roho. Aliona “gari” kubwa sana na Yehova mwenyewe ndiye anayeliongoza gari hilo sikuzote. Lilisonga kwa njia yenye kustaajabisha sana. Magurudumu yake makubwa yenye pande nne, yalijaa macho hivi kwamba yaliweza kuona kila mahali na kusafiri kuelekea upande wowote ghafla bila kusimama wala kugeuka. Na gari hilo kubwa sana halikujikokota polepole kama gari lililotengenezwa na wanadamu. Lingeweza kwenda kwa mwendo kama wa radi na hata kugeuka ghafla! (Ezekieli 1:1, 14-28) Naam, tengenezo la Yehova linaweza kubadilikana kulingana na hali mbalimbali na kushughulikia mahitaji yanayotokea kama anavyofanya Mungu Mwenye Enzi Kuu na Mweza-Yote ambaye analiongoza.
15 Huenda wanadamu wakajitahidi kubadilikana kulingana na hali lakini mara nyingi, wanashindwa kukubaliana na mabadiliko hayo kwa uharaka. Kwa mfano: Meli ya mafuta au treni ya kubeba mizigo inaweza kuwa kubwa sana na yenye injini iliyo na nguvu. Lakini je, treni au meli inaweza kugeuka mara moja hali zikibadilika? Treni ya mizigo haiwezi kugeuka ikiwa kitu fulani kitaanguka kwenye reli mbele yake. Pia, haiwezi kusimama ghafla. Baada ya breki kufungwa, treni yenye mizigo mizito inaweza kuendelea kusonga kwa umbali wa kilomita mbili hivi kabla ya kusimama! Vivyo hivyo, huenda meli kubwa ya mafuta ikasafiri umbali wa kilomita nane baada ya injini kuzimwa. Hata injini zikiendeshwa kurudi nyuma bado meli hiyo inaweza kusonga mbele umbali wa kilomita tatu! Ndivyo ilivyo na mashirika ya wanadamu ambayo mara nyingi hushikilia sana sera zake na kukataa mawazo mapya. Mara nyingi, watu hukataa kubadilikana kulingana na mahitaji au hali kwa sababu ya kiburi. Mashirika mengi yamefilisika na hata serikali nyingi kupinduliwa kwa sababu ya kukataa kubadilikana kulingana na hali. (Methali 16:18) Tunafurahi sana kwamba Yehova na tengenezo lake ni tofauti sana na mashirika hayo ya wanadamu!
Jinsi Yehova Anavyoonyesha Usawaziko
16. Yehova alionyeshaje sifa ya usawaziko aliposhughulika na Loti kabla ya kuangamizwa kwa Sodoma na Gomora?
16 Fikiria tena kuhusu kuangamizwa kwa Sodoma na Gomora. Malaika wa Yehova alimpa Loti na familia yake maagizo yaliyo wazi kabisa: “Kimbilieni eneo lenye milima.” Lakini Loti hakutaka kwenda huko. Alimsihi Yehova hivi: “Tafadhali Yehova, acha nisiende huko!” Akiamini kwamba angekufa ikiwa angekimbilia milimani, Loti aliomba kwamba yeye na familia yake waruhusiwe kukimbilia mji wa karibu ulioitwa Soari. Kumbuka kwamba Yehova alikuwa amekusudia kuangamiza mji huo. Isitoshe, Loti hakuwa na sababu nzuri ya kuogopa. Bila shaka, Yehova angeweza kumlinda Loti huko milimani! Hata hivyo, Yehova alikubali ombi la Loti, kwa kumtuma malaika amwambie Loti hivi: “Sawasawa, nitakutendea pia kwa fadhili, sitauangamiza mji uliotaja.” (Mwanzo 19:17-22) Je, jambo hilo halionyeshi kwamba Yehova ni mwenye usawaziko?
17, 18. Yehova alionyeshaje sifa ya usawaziko aliposhughulika na Waninawi?
17 Yehova hukubali pia toba ya kutoka moyoni. Sikuzote yeye huonyesha rehema na kutenda yaliyo sawa. Fikiria jambo lililotukia nabii Yona alipotumwa kwenye jiji la Ninawi liliokuwa na uovu na jeuri. Yona alitangaza ujumbe ulio wazi kutoka kwa Mungu kotekote katika Ninawi: Jiji hilo mashuhuri lingeangamizwa baada ya siku 40. Lakini, mambo yalibadilika ghafla. Waninawi walitubu!—Yona, sura ya 3.
18 Tunajifunza jambo fulani tunapolinganisha jinsi Yehova alivyohisi hali ilipobadilika na pia jinsi Yona alivyohisi. Yehova alibadilikana kulingana na hali hiyo mara moja, akawa mwenye kusamehe dhambi badala ya kuwa “shujaa mwenye nguvu.”d (Kutoka 15:3) Lakini Yona hakuwa tayari kubadilika wala hakuonyesha rehema kama Yehova alivyofanya. Badala ya kuonyesha usawaziko kama Yehova, alikuwa kama treni ya mizigo au meli kubwa ya mafuta tuliyoitaja awali. Alitaka mji huo uangamizwe tu kama alivyokuwa ametangaza! Hata hivyo, kwa subira Yehova alimfundisha nabii wake asiye na subira somo lisilosahaulika kuhusu kuwa na usawaziko na kuonyesha rehema.—Yona, sura ya 4.
Yehova ni mwenye usawaziko na anajua udhaifu wetu
19. (a) Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova ni mwenye usawaziko kuhusiana na mambo anayotarajia tufanye? (b) Andiko la Methali 19:17 linaonyeshaje kwamba Yehova ni Bwana ‘mwema na mwenye usawaziko,’ na kwamba unyenyekevu wake hauna kifani?
19 Yehova ni mwenye usawaziko kuhusiana na mambo anayotarajia tufanye. Mfalme Daudi alisema: “Kwa maana anajua vema umbo letu akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.” (Zaburi 103:14) Yehova anajua udhaifu wetu na hali yetu ya kutokamilika kuliko tunavyojijua. Hatarajii kamwe tufanye mambo yanayozidi uwezo wetu. Biblia inasema kwamba kuna mabwana ‘wema na wenye usawaziko’ na wengine ni “wagumu kupendeza.” (1 Petro 2:18) Yehova ni Bwana wa aina gani? Methali 19:17 inasema: “Anayemwonyesha kibali mtu wa hali ya chini anamkopesha Yehova.” Ni wazi kwamba bwana aliye mwema na mwenye usawaziko ndiye tu anayeweza kuzingatia kila tendo la fadhili ambalo watu wa hali ya chini wanafanyiwa. Isitoshe, andiko hilo pia linadokeza kwamba Muumba wa ulimwengu anajiona kuwa na deni kwa wanadamu duni wanaofanya matendo hayo ya rehema! Huo ni unyenyekevu usio na kifani.
20. Tuna uhakika gani kwamba Yehova husikiliza na kujibu sala zetu?
20 Leo pia, Yehova hushughulika na watumishi wake kwa upole na usawaziko. Yeye husikiliza tunaposali kwa imani. Hatupaswi kufikiri kwamba hajibu sala zetu kwa sababu tu hawatumi malaika ili wazungumze nasi. Kumbuka kwamba mtume Paulo alipowaomba waamini wenzake ‘waendelee kusali’ ili aweze kuachiliwa kutoka gerezani, aliongeza hivi: “[Ili] nirudi kwenu haraka iwezekanavyo.” (Waebrania 13:18, 19) Kwa hiyo, sala zetu zinaweza kumchochea Yehova atende jambo ambalo huenda hangetenda!—Yakobo 5:16.
21. Hatupaswi kuwa na maoni gani kuhusu unyenyekevu wa Yehova? Wewe unahisije kuhusu unyenyekevu wa Yehova?
21 Bila shaka, sifa zinazoonyesha unyenyekevu wa Yehova, yaani, upole, utayari wa kutusikiliza, subira, na usawaziko—hazimaanishi kwamba Yehova hulegeza kanuni zake za uadilifu. Huenda makasisi wa Jumuiya ya Wakristo wakadhani kwamba wana usawaziko, wanapofurahisha masikio ya wafuasi wao kwa kulegeza kanuni za Yehova za maadili. (2 Timotheo 4:3) Wanadamu hukubaliana na mambo yasiyo sawa kwa sababu ni rahisi kufanya hivyo, nao husema kwamba kufanya hivyo ni kuonyesha kwamba wana usawaziko. Lakini hiyo si njia ya Yehova ya kuonyesha usawaziko. Yehova ni mtakatifu; hawezi kamwe kupotosha kanuni zake za uadilifu. (Mambo ya Walawi 11:44) Hivyo, tunahitaji kuelewa kwamba sababu kuu ya Yehova kuwa mwenye usawaziko ni unyenyekevu. Unahisije kujua kwamba ingawa Yehova Mungu ndiye mwenye hekima isiyo na kifani katika ulimwengu wote, Yeye ndiye mnyenyekevu zaidi? Inapendeza kama nini kumkaribia Mungu huyu mtukufu ambaye ni mpole, mwenye subira, na mwenye usawaziko!
a Waandishi wa kale, au Wasoferi, walibadili mstari huu na kusema kwamba ni Yeremia anayeinama wala si Yehova. Inaonekana kwamba walidhani haifai kusema kwamba Mungu “aliinama” ili kumsaidia mwanadamu. Ndiyo sababu tafsiri nyingi hazitoi maana ya mstari huu wenye kupendeza. Hata hivyo, The New English Bible inasema kwa usahihi kwamba Yeremia alimwambia Mungu hivi: “Kumbuka, Ee kumbuka, na uniinamie.”
b Tafsiri nyingine husema “unyenyekevu unaotokana na hekima” na “upole wa hekima.” UV
c Biblia inaonyesha kwamba subira ni kinyume cha kiburi. (Mhubiri 7:8) Subira ya Yehova inathibitisha hata zaidi kwamba yeye ni mnyenyekevu.—2 Petro 3:9.
d Zaburi 86:5 inasema kwamba Yehova ni ‘mwema na yuko tayari kusamehe.’ Zaburi hiyo ilipotafsiriwa katika Kigiriki, usemi “tayari kusamehe” ulitafsiriwa kuwa e·pi·ei·kesʹ, au “mwenye usawaziko.”