Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • cl sura 10 kur. 116-127
  • “Iweni Waigaji wa Mungu” Mnapotumia Mamlaka

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Iweni Waigaji wa Mungu” Mnapotumia Mamlaka
  • Mkaribie Yehova
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Upendo Ni Muhimu
  • Katika Familia
  • Katika Kutaniko
  • “Nguvu za Ulimi”
  • Kumtumikia Yehova kwa ‘Nguvu Zetu Zote’
  • “Tafuteni Bwana na Nguvu Yake”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Wenye Furaha ni Wale Wanaotumia Uwezo kwa Njia Inayofaa!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • “Yehova . . . Ana Nguvu Nyingi”
    Mkaribie Yehova
  • Jilinde Usitumie Vibaya Uwezo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
Pata Habari Zaidi
Mkaribie Yehova
cl sura 10 kur. 116-127
Mashahidi wawili wa Yehova wakimhubiria mwanamke nyumbani kwake.

SURA YA 10

“Iweni Waigaji wa Mungu” Mnapotumia Mamlaka

1. Wanadamu wasio wakamilifu hutumbukia kwa urahisi katika mtego gani?

MSHAIRI mmoja alisema hivi: “Mtu anapokuwa na mamlaka sikuzote kunakuwa na hatari.” Ni hatari gani? Ni rahisi sana kutumia mamlaka vibaya. Inasikitisha kwamba wanadamu wasio wakamilifu hunaswa kwa urahisi katika mtego huo. Kwa kweli, katika historia ya wanadamu, “mwanadamu amemtawala mwanadamu mwenzake kwa kumuumiza.” (Mhubiri 8:9) Wanadamu wameteseka sana kwa sababu ya kutawaliwa na watawala wasio na upendo.

2, 3. (a) Ni nini kinachostaajabisha kuhusu jinsi Yehova anavyotumia nguvu zake? (b) Huenda tukawa na uwezo gani, na tunapaswa kutumia jinsi gani uwezo huo?

2 Hata hivyo, je, haistaajabishi kwamba Yehova Mungu hatumii vibaya kamwe nguvu zake zisizo na mipaka? Kama tulivyoona kwenye sura zilizotangulia, sikuzote yeye hutumia nguvu zake, yaani, katika kuumba, kuharibu, kulinda, au kurudisha hali nzuri—kulingana na kusudi lake lenye upendo. Tunapotafakari jinsi anavyotumia nguvu zake, tunachochewa kumkaribia. Na hilo linatuchochea ‘tuwe waigaji wa Mungu’ tunapotumia mamlaka tuliyo nayo. (Waefeso 5:1) Lakini sisi wanadamu duni tuna uwezo gani?

3 Kumbuka kwamba mwanadamu aliumbwa kwa sura na “mfano wa Mungu.” (Mwanzo 1:26, 27) Hivyo, sisi pia tuna uwezo kwa kadiri fulani. Uwezo wetu unaweza kutia ndani nguvu za kutimiza mambo kwa kufanya kazi; kuwa na mamlaka juu ya wengine; kuwachochea wengine, hasa wale wanaotupenda; tunaweza kuwa na nguvu ya kimwili; au uwezo wa kifedha. Mtunga-zaburi alisema hivi kumhusu Yehova: “Wewe ndiye chanzo cha uhai.” (Zaburi 36:9) Kwa hiyo, nguvu tulizo nazo ni kwa sababu Yehova ametupatia nguvu hizo au ameturuhusu kuwa na nguvu hizo. Kwa hiyo, tungependa kutumia uwezo wetu katika njia zinazompendeza. Tunawezaje kufanya hivyo?

Upendo Ni Muhimu

4, 5. (a) Tunahitaji sifa gani muhimu ili kutumia uwezo kwa njia inayofaa, na kielelezo cha Mungu kinaonyeshaje hivyo? (b) Upendo utatusaidiaje kutumia uwezo wetu kwa njia inayofaa?

4 Upendo ni muhimu ili kutumia uwezo kwa njia inayofaa. Yehova anatuwekea kielelezo kizuri kuhusiana na hilo. Kumbuka Sura ya 1 iliyozungumzia sifa nne kuu za Mungu, yaani, nguvu, haki, hekima na upendo. Kati ya sifa hizo nne ni ipi iliyo kuu zaidi? Ni upendo. 1 Yohana 4:8 inasema kwamba “Mungu ni upendo.” Ndiyo, Yehova ni upendo na sifa hiyo inamwongoza katika kila jambo analotenda. Kwa hiyo, kila jambo analotenda kwa nguvu zake, linachochewa na upendo na huwanufaisha wanaompenda.

5 Upendo utatusaidia pia kutumia uwezo wetu kwa njia inayofaa. Kwa kweli, Biblia inatuambia kwamba upendo ni wenye “fadhili” na “hautafuti faida zake wenyewe.” (1 Wakorintho 13:4, 5) Hivyo, tukiwa na upendo hatutakuwa wakali au wakatili kwa wale walio chini ya mamlaka yetu. Badala yake, tutawatendea wengine kwa heshima na kutanguliza mahitaji na hisia zao.​—Wafilipi 2:3, 4.

6, 7. (a) Kumwogopa Mungu kunamaanisha nini, na sifa hiyo itatusaidiaje kuepuka kutumia uwezo wetu vibaya? (b) Toa mfano unaoonyesha uhusiano uliopo kati ya kumpenda Mungu na kuogopa kumkosea.

6 Upendo unahusiana na sifa nyingine ambayo inaweza kutusaidia kuepuka kutumia uwezo wetu vibaya: kumwogopa Mungu. Kwa nini sifa hii ni muhimu? Methali 16:6 inasema hivi: “Kwa kumwogopa Yehova mtu hujiepusha na uovu.” Kutumia vibaya uwezo wetu ni kati ya mambo maovu tunayopaswa kuepuka. Kumwogopa Mungu kutatuzuia kuwakandamiza wale walio chini ya mamlaka yetu. Kwa nini? Kwa sababu tunajua kwamba tunawajibika kwa Mungu kwa jinsi tunavyowatendea wengine. (Nehemia 5:1-7, 15) Lakini kumwogopa Mungu kunahusisha mengi zaidi ya hilo. Maneno ya lugha ya awali yaliyotafsiriwa “kumwogopa” mara nyingi humaanisha kumheshimu sana Mungu. Biblia inaonyesha kwamba kuna uhusiano kati ya kumpenda Mungu na kumwogopa. (Kumbukumbu la Torati 10:12, 13) Heshima hiyo inatia ndani kuogopa kumkosea Mungu si kwa sababu tunaogopa kuadhibiwa, bali kwa sababu tunampenda kikweli.

7 Kwa mfano: Fikiria uhusiano mzuri uliopo kati ya mvulana mdogo na baba yake. Mvulana huyo anajua kwamba baba yake anampenda sana na anamjali. Lakini pia anajua mambo ambayo baba yake anatarajia afanye, na kwamba atatiwa nidhamu akikosa adabu. Mvulana huyo hamwogopi isivyofaa baba yake. Badala yake, anampenda sana baba yake. Anapenda kufanya mambo ambayo yatamfurahisha baba yake. Ndivyo ilivyo pia na kumwogopa Mungu. Kwa sababu tunampenda Yehova, Baba yetu wa mbinguni, tunaogopa kutenda jambo lolote litakalofanya moyo wake uhuzunike. (Mwanzo 6:6) Badala yake, tunatamani sana kuufanya moyo wake ushangilie. (Methali 27:11) Ndiyo sababu tunataka kutumia uwezo wetu kwa njia inayofaa. Tuchunguze jinsi tunavyoweza kufanya hivyo.

Katika Familia

8. (a) Waume wana mamlaka gani katika familia, na wanapaswa kuitumiaje? (b) Mume anawezaje kuonyesha kwamba anamheshimu mke wake?

8 Kwanza, tufikirie kuhusu familia. Waefeso 5:23 inasema kwamba “mume ni kichwa cha mke wake.” Mume anapaswa kutumiaje mamlaka aliyopewa na Mungu? Biblia inawaambia waume wakae na wake zao “kulingana na ujuzi” na ‘kuwapa heshima kama chombo dhaifu zaidi.’ (1 Petro 3:7) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “heshima” linamaanisha “thamani.” Neno hilo hutafsiriwa pia kuwa “zawadi” na “thamani.” (Matendo 28:10; 1 Petro 2:7) Mume anayemheshimu mke wake hawezi kamwe kumpiga; wala hawezi kumwaibisha au kumtukana, na kumfanya ajihisi hafai. Badala yake, anatambua kwamba mke wake ni mwenye thamani na anamtendea kwa heshima. Anaonyesha kwa maneno na matendo kwamba anamthamini sana mke wake iwe faraghani au mbele ya watu. (Methali 31:28) Mume huyo hupendwa na kuheshimiwa na mke wake, na jambo muhimu zaidi ni kwamba anapata kibali cha Mungu.

Wenzi wa ndoa wakitembea pamoja.

Waume na wake wanatumia uwezo wao kwa njia inayofaa kwa kuonyeshana upendo na heshima

9. (a) Wake wana mamlaka gani katika familia? (b) Ni nini kinachoweza kumsaidia mke atumie vipawa vyake kumuunga mkono mume wake, na matokeo yatakuwa nini?

9 Wake pia wana mamlaka fulani ya kadiri katika familia. Biblia hutaja wanawake fulani waliomwogopa Mungu ambao walichukua hatua ya kuwasaidia waume zao kufanya maamuzi yanayofaa, au kuwasaidia kuepuka kufanya maamuzi yasiyofaa bila kudharau ukichwa wao. (Mwanzo 21:9-12; 27:46–28:2) Mke anaweza kuwa na uwezo wa kuelewa mambo haraka kuliko mume wake, au anaweza kuwa na vipawa vingine ambavyo mume wake hana. Hata hivyo, anahitaji “kumheshimu sana” mume wake na ‘kujitiisha’ kwake “kama kwa Bwana.” (Waefeso 5:22, 33) Mke ambaye lengo lake ni kumpendeza Mungu atatumia vipawa vyake kumuunga mkono mume wake, badala ya kumdharau au kujaribu kumtawala. “Mwanamke ambaye kwa kweli ana hekima” hushirikiana kabisa na mume wake kuijenga familia. Kwa kufanya hivyo anakuwa na amani pamoja na Mungu.​—Methali 14:1.

10. (a) Mungu amewapatia wazazi mamlaka gani? (b) Neno “nidhamu” linamaanisha nini, na inapaswa kutolewaje? (Ona pia maelezo ya chini.)

10 Wazazi pia wamepewa mamlaka na Mungu. Biblia inasema hivi: “Akina baba, msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na maagizo ya Yehova.” (Waefeso 6:4) Katika Biblia, neno “nidhamu” linaweza kumaanisha “malezi, mazoezi, maagizo.” Watoto wanahitaji nidhamu; wanafurahi na kufanikiwa wanapopewa maagizo yaliyo wazi, na wanapowekewa mipaka na vizuizi. Biblia inasema kwamba nidhamu, au mafundisho hayo yanapaswa kutolewa kwa upendo. (Methali 13:24) Kwa hiyo, “fimbo ya nidhamu” haipaswi kamwe kuwaumiza watoto kihisia au kimwili.a (Methali 22:15; 29:15) Mzazi anayetoa nidhamu kwa ukali bila upendo anatumia vibaya mamlaka yake. Kufanya hivyo kunaweza kumvunja moyo mtoto. (Wakolosai 3:21) Kwa upande mwingine, kutoa nidhamu kwa usawaziko na kwa njia inayofaa kunawathibitishia watoto kwamba wazazi wanawapenda na wanataka wawe watu wazuri.

11. Watoto wanawezaje kutumia nguvu zao kwa njia inayofaa?

11 Vipi kuhusu watoto? Wanawezaje kutumia nguvu zao kwa njia inayofaa? Methali 20:29 inasema kwamba “utukufu wa vijana ni nguvu zao.” Njia bora zaidi ya vijana kutumia nguvu zao ni kwa kumtumikia ‘Muumba wetu Mkuu.’ (Mhubiri 12:1) Vijana wanapaswa kukumbuka kwamba matendo yao yanaweza kuathiri hisia za wazazi wao. (Methali 23:24, 25) Watoto wanapotii na kufuata mwenendo unaofaa, wanafurahisha mioyo ya wazazi wao wanaomwogopa Mungu. (Waefeso 6:1) Mwenendo huo “humpendeza Bwana.”​—Wakolosai 3:20.

Katika Kutaniko

12, 13. (a) Wazee wanapaswa kuwa na mtazamo gani kuhusu mamlaka yao kutanikoni? (b) Toa mfano unaoonyesha kwa nini wazee wanapaswa kuwatendea kondoo kwa wororo.

12 Yehova amewaweka waangalizi waongoze kutaniko la Kikristo. (Waebrania 13:17) Wanaume hao wenye sifa za kustahili wanapaswa kutumia mamlaka waliyopewa na Mungu kutoa msaada unaohitajika na kuchangia ukuzi wa kiroho wa kutaniko. Je, wazee wana mamlaka ya kupiga ubwana juu ya waamini wenzao? Hapana! Wazee wanahitaji kuwa wanyenyekevu na wenye usawaziko wanapotimiza daraka lao kutanikoni. (1 Petro 5:2, 3) Biblia inawaambia hivi waangalizi: ‘Lichungeni kutaniko la Mungu, ambalo alilinunua kwa damu ya Mwana wake mwenyewe.’ (Matendo 20:28) Hivyo, wazee wanapaswa kumtendea kila mshiriki wa kutaniko kwa wororo.

13 Mfano ufuatao unaonyesha jambo hilo: Rafiki yako mpendwa anakuomba umtunzie kitu fulani chenye thamani kubwa. Unajua kwamba kitu hicho kilimgharimu pesa nyingi sana. Bila shaka utakitunza sana ili kisiharibike. Vivyo hivyo, Mungu amewakabidhi wazee wajibu wa kutunza mali yenye thamani kubwa sana, yaani, kutaniko, ambalo washiriki wake wanalinganishwa na kondoo. (Yohana 21:16, 17) Yehova anawapenda sana kondoo wake hivi kwamba aliwanunua kwa damu yenye thamani ya Mwana wake mzaliwa pekee, Yesu Kristo. Yehova aliwanunua kondoo wake kwa bei ya juu sana. Wazee wanyenyekevu hukumbuka jambo hilo na huwatendea kondoo wa Yehova kwa njia inayofaa.

“Nguvu za Ulimi”

14. Ulimi una nguvu gani?

14 Biblia inasema kwamba “kifo na uhai viko katika nguvu za ulimi.” (Methali 18:21) Kwa kweli, ulimi unaweza kusababisha madhara makubwa. Sote huhisi vibaya mtu anaposema jambo linalotuumiza. Lakini maneno yetu yanaweza pia kujenga. Methali 12:18 inasema kwamba “ulimi wa mwenye hekima huponya.” Ndiyo, maneno yenye kutia moyo na yenye kujenga yanaweza kufariji na kutuliza moyo kama dawa. Fikiria mifano kadhaa.

15, 16. Tunawezaje kutumia ulimi wetu kuwatia moyo wengine?

15 Andiko la 1 Wathesalonike 5:14 linasema hivi: “Wafarijini wale walioshuka moyo.” Nyakati nyingine, hata watumishi waaminifu wa Yehova wanaweza kushuka moyo. Tunawezaje kuwasaidia watu hao? Toa pongezi hususa na ya kutoka moyoni ili watambue kwamba wanathaminiwa sana na Yehova. Tumia maandiko ya Biblia yatakayowaimarisha na kuwaonyesha kwamba Yehova anawapenda na anawajali kikweli wale “waliovunjika moyo” na “waliopondeka roho.” (Zaburi 34:18) Tunapotumia uwezo wa ulimi kuwafariji wengine, tunaonyesha kwamba tunamwiga Mungu wetu mwenye rehema, “ambaye huwafariji wale waliovunjika moyo.”​—2 Wakorintho 7:6

16 Tunaweza pia kutumia maneno yetu kuwatia moyo wengine. Je, mwamini mwenzetu amefiwa na mpendwa wake? Tunaweza kumfariji aliyefiwa kwa kuzungumza naye kwa huruma na kumwonyesha kwamba tunamjali na tunamhangaikia. Je, kuna ndugu au dada mwenye umri mkubwa ambaye anahisi kwamba hafai? Tunaweza kuwahakikishia wale wenye umri mkubwa kwamba wanathaminiwa sana kwa kuwaambia maneno yenye kujenga. Je, kuna mtu anayepambana na ugonjwa wa kudumu? Tunaweza kumtia moyo kwa kuzungumza naye kwa fadhili kupitia simu, barua, au kwa kumtembelea. Muumba wetu hufurahi sana anapoona tukitumia ulimi wetu kusema mambo ‘mema kwa ajili ya kujenga’!—Waefeso 4:29.

17. Tunaweza kutumia ulimi wetu kuwanufaisha wengine kwa njia gani bora zaidi, na kwa nini tufanye hivyo?

17 Njia bora zaidi ya kutumia uwezo wa ulimi ni kwa kuwahubiria wengine habari njema za Ufalme wa Mungu. Methali 3:27 inasema hivi: “Usiwanyime mema wale unaopaswa kuwatendea mema ikiwa una uwezo wa kuwasaidia.” Tuna wajibu wa kuwaeleza wengine habari njema zinazookoa uhai. Hatupaswi kuwanyima wengine ujumbe huo muhimu sana ambao Yehova ametupatia kwa ukarimu. (1 Wakorintho 9:16, 22) Hata hivyo, Yehova anataka tushiriki kwa kadiri gani katika kazi hiyo?

Kuhubiri habari njema ni njia bora ya kutumia uwezo wetu

Kumtumikia Yehova kwa ‘Nguvu Zetu Zote’

18. Yehova anatarajia nini kutoka kwetu?

18 Upendo wetu kwa Yehova hutuchochea kushiriki kikamili katika huduma ya Kikristo. Yehova anatarajia nini kutoka kwetu inapohusu huduma? Anataka tufanye yote tunayoweza licha ya hali zetu maishani: “Lolote mnalofanya, lifanyeni kwa nafsi yote kama kwa Yehova, na si kwa wanadamu.” (Wakolosai 3:23) Yesu alisema kwamba amri kuu kupita zote ni hii: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Marko 12:30) Ndiyo, Yehova anatarajia kwamba kila mmoja wetu ampende na kumtumikia kwa nafsi yote.

19, 20. (a) Kwa kuwa nafsi inatia ndani moyo, akili, na nguvu, kwa nini sehemu hizo zinatajwa kwenye Marko 12:30? (b) Inamaanisha nini kumtumikia Yehova kwa nafsi yote?

19 Inamaanisha nini kumtumikia Mungu kwa nafsi yote? Nafsi ni mtu mwenyewe, kutia ndani uwezo wake wote wa kimwili na kiakili. Kwa kuwa nafsi inatia ndani moyo, akili, na nguvu, kwa nini sehemu hizo zinatajwa kwenye Marko 12:30? Fikiria mfano mmoja. Katika nyakati za Biblia, mtu angeweza kujiuza (nafsi yake) na kuwa mtumwa. Lakini, huenda mtumwa asimtumikie bwana wake kwa moyo wake wote, kwa akili yake yote, na kwa nguvu yake yote. (Wakolosai 3:22) Kwa hiyo, ni wazi kwamba Yesu alitaja moyo, akili, na nguvu ili kukazia kwamba tunapaswa kumtumikia Mungu kwa uwezo wetu wote. Kumtumikia Mungu kwa nafsi yote kunamaanisha kujitoa wenyewe kikamili kwa kutumia nguvu zetu zote katika utumishi wetu.

20 Je, kutumikia kwa nafsi yote kunamaanisha kwamba ni lazima sote tutumie kiasi kilekile cha wakati na nguvu katika huduma? Hilo haliwezekani kwa kuwa hali na uwezo wetu hutofautiana. Kwa mfano, kijana mwenye nguvu na afya nzuri anaweza kuhubiri kwa saa nyingi zaidi kuliko mzee aliye dhaifu. Mseja asiye na wajibu wa familia anaweza kutimiza mengi zaidi kuliko mtu mwenye familia. Tunapaswa kushukuru sana ikiwa hali na nguvu zetu zinaturuhusu kufanya mengi katika huduma. Bila shaka, hatutaki kamwe kuwachambua wengine, wala kulinganisha utumishi wetu na wao. (Waroma 14:10-12) Badala yake, tunataka kutumia uwezo wetu kuwatia moyo wengine.

21. Ni njia gani bora kabisa na muhimu zaidi ya kutumia uwezo wetu?

21 Yehova ametuwekea kielelezo bora kabisa kwa kutumia uwezo wake kwa njia inayofaa. Tunapaswa kumwiga kadiri tuwezavyo tukiwa wanadamu wasio wakamilifu. Tunaweza kutumia uwezo wetu kwa njia inayofaa kwa kuwatendea kwa heshima wale walio chini ya mamlaka yetu. Kwa kuongezea, tunahitaji kutimiza kwa nafsi yote kazi ya kuhubiri inayookoa uhai, ambayo Yehova ametukabidhi. (Waroma 10:13, 14) Kumbuka kwamba Yehova anafurahi unapomtolea kilicho bora kabisa kulingana na uwezo wako. Bila shaka, ungependa kufanya yote uwezayo kumtumikia Mungu wetu mwenye fadhili na upendo. Hiyo ndiyo njia bora au muhimu zaidi ya kutumia uwezo wetu.

a Katika nyakati za Biblia, neno la Kiebrania linalotafsiriwa “fimbo” lilimaanisha kijiti au gongo kama lile lililotumiwa na mchungaji kuwaongoza kondoo. (Zaburi 23:4) Vivyo hivyo, “fimbo” ya mamlaka ya wazazi inamaanisha mwongozo wa upendo, wala si adhabu kali au ya kikatili.

Maswali ya Kutafakari

  • Methali 3:9, 10 Tuna ‘vitu gani vyenye thamani’ na tunawezaje kuvitumia kumheshimu Yehova?

  • Mhubiri 9:5-10 Kwa nini unapaswa kutumia nguvu zako sasa kwa njia itakayompendeza Mungu?

  • Matendo 8:9-24 Katika simulizi hilo mamlaka ilitumiwaje vibaya, na tunawezaje kuepuka kufanya kosa kama hilo?

  • Matendo 20:29-38 Wale walio na mapendeleo kutanikoni wanajifunza nini kutokana na kielelezo cha Paulo?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki