SURA YA 3
“Mtakatifu, Mtakatifu, Mtakatifu Ni Yehova”
1, 2. Isaya alipokea maono gani, na maono hayo yanatufundisha nini kumhusu Yehova?
ISAYA alipoona maono kutoka kwa Mungu alishangaa sana. Ni kana kwamba aliona jambo halisi! Baadaye Isaya aliandika kwamba ‘alimwona Yehova’ akiwa ameketi kwenye kiti Chake cha Ufalme kilicho juu. Na pindo za kanzu yake zilijaa kwenye hekalu kubwa la Yerusalemu.—Isaya 6:1, 2.
2 Isaya alishangazwa na sauti aliyosikia, yaani, uimbaji wenye nguvu sana hivi kwamba ulitikisa hekalu na misingi yake. Wimbo huo uliimbwa na maserafi, viumbe wa roho wenye cheo cha juu. Waliimba wimbo rahisi lakini wenye ujumbe mzito: “Mtakatifu, mtakatifu, mtakatifu ni Yehova wa majeshi. Dunia yote imejaa utukufu wake.” (Isaya 6:3, 4) Kuimba neno “mtakatifu” mara tatu kulikazia neno hilo kwa njia ya pekee sana. Jambo hilo linafaa kwa sababu utakatifu wa Yehova ni wa hali ya juu sana. (Ufunuo 4:8) Utakatifu wa Yehova unakaziwa katika Biblia nzima. Kuna mistari mingi ya Biblia inayotaja jina lake pamoja na maneno “takatifu” na “utakatifu.”
3. Kwa nini mtazamo usiofaa kuhusu utakatifu wa Yehova umewafanya watu wengi wakatae kumkaribia Mungu?
3 Jambo moja muhimu ambalo Yehova anataka tujue kumhusu ni kwamba yeye ni mtakatifu. Lakini watu wengi leo wana mtazamo usiofaa kuhusu utakatifu. Wengine hata hufikiri kimakosa kwamba kuwa mtakatifu kunamaanisha kujiona mwadilifu au kujifanya kwamba unamtumikia Mungu. Watu wanaojiona kuwa hawafai huenda wakaogopa badala ya kuvutiwa na wazo la kuwa Mungu ni mtakatifu. Huenda wakahofu kwamba hawawezi kamwe kustahili kumkaribia Mungu huyo mtakatifu. Kwa hiyo, watu wengi hawataki kumkaribia Mungu kwa sababu ya utakatifu wake. Jambo hilo linasikitisha kwa sababu utakatifu wa Mungu unapaswa kutuchochea kumkaribia. Kwa nini? Kabla ya kujibu swali hilo, tuzungumzie maana halisi ya utakatifu.
Utakatifu Ni Nini?
4, 5. (a) Neno “utakatifu” linamaanisha nini, na halimaanishi nini? (b) Yehova ‘hujitenga’ katika njia zipi mbili muhimu?
4 Ingawa Mungu ni mtakatifu haimaanishi kwamba ana majivuno, kiburi, au anawadharau wengine. Badala yake, anachukia sifa hizo. (Methali 16:5; Yakobo 4:6) Basi neno “takatifu” linamaanisha nini hasa? Katika Biblia neno la Kiebrania lililotafsiriwa “takatifu” linatokana na neno linalomaanisha “kutenga.” Katika ibada, kitu “kitakatifu” ni kile kilichowekwa kando kwa ajili ya matumizi maalumu. Utakatifu pia hutoa wazo la usafi na utakaso. Neno hilo hutumiwaje kuhusiana na Yehova? Je, inamaanisha kwamba yeye ‘hujitenga’ na wanadamu wasio wakamilifu?
5 Hapana. Akiwa “Mtakatifu wa Israeli,” Yehova aliwahakikishia watu wake kwamba alikaa katikati yao licha ya kwamba walikuwa wenye dhambi. (Isaya 12:6; Hosea 11:9) Hivyo, ingawa yeye ni mtakatifu, hajitengi na watu wanaomwabudu. Yeye “hujitenga” kwa njia gani? Kupitia njia mbili muhimu. Kwanza, yeye amejitenga na viumbe wote katika maana ya kwamba yeye peke yake ndiye Aliye Juu Zaidi. Yeye ni msafi katika kila kitu na usafi wake ni wa hali ya juu. (Zaburi 40:5; 83:18) Pili, Yehova amejitenga kabisa na dhambi, na hilo linatufariji. Kwa nini?
6. Kwa nini inafariji kujua kwamba Yehova hawezi kufanya jambo lolote baya?
6 Tunaishi katika ulimwengu ambao utakatifu wa kweli ni haba. Kila jambo linalofanywa na wanadamu wasiomjua Mungu limepotoka kwa njia fulani, limechafuliwa na dhambi na kutokamilika. Sote tunapambana na dhambi iliyo mwilini mwetu. Sote tunakabili hatari ya kushindwa na dhambi tusipojihadhari. (Waroma 7:15-25; 1 Wakorintho 10:12) Yehova hakabili hatari hiyo. Yeye hana dhambi hata kidogo, hatachafuliwa kamwe na dhambi yoyote. Hilo linatuhakikishia kwamba Yehova ni Baba bora, kwa sababu anategemeka kabisa. Tofauti na akina baba wengi wenye dhambi, Yehova hawezi kupotoka, kuwa na maadili mabaya, au kutumia vibaya mamlaka yake. Hawezi kamwe kutenda mambo hayo kwa sababu yeye ni mtakatifu. Kwa kuwa utakatifu wa Yehova ni sababu kuu ya kumwamini, pindi fulani Yehova ametumia utakatifu huo kama msingi wa kutoa ahadi nzito. (Amosi 4:2) Je, hilo halitutii moyo?
7. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Yehova ni mtakatifu kabisa?
7 Yehova ni mtakatifu kabisa. Hilo linamaanisha nini? Kwa mfano: Fikiria maneno “mwanadamu” na “kutokamilika.” Huwezi kuelezea hali ya wanadamu bila kufikiria hali ya kutokamilika. Hali ya kutokamilika inaathiri kila jambo tunalofanya. Sasa fikiria maneno mawili tofauti kabisa—“Yehova” na “utakatifu.” Haiwezekani kumfikiria Yehova bila kufikiria utakatifu wake. Kila jambo linalomhusu ni safi, limetakata, na la uadilifu. Hatuwezi kumjua Yehova kikweli bila kufikiria kwa uzito na kufahamu neno hili muhimu—“utakatifu.”
“Utakatifu Ni wa Yehova”
8, 9. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova huwasaidia wanadamu wasio wakamilifu kuwa watakatifu kwa kadiri fulani?
8 Kwa kuwa Yehova ni mtakatifu kabisa, tunaweza kusema kwa uhakika yeye ndiye chanzo cha utakatifu. Yeye si mbinafsi na huwapatia wengine kwa ukarimu sifa hiyo yenye thamani. Mungu alipozungumza na Musa kupitia malaika kwenye kichaka kilichokuwa kikiwaka moto, ardhi yote iliyokuwa karibu na kichaka hicho ilikuwa takatifu kwa sababu Yehova alitumia sehemu hiyo!—Kutoka 3:5.
9 Je, wanadamu wasio wakamilifu wanaweza kuwa watakatifu kwa msaada wa Yehova? Ndiyo, kwa kadiri fulani. Mungu aliwaambia Waisraeli wangeweza kuwa “taifa takatifu.” (Kutoka 19:6) Alibariki taifa hilo kwa kuliandalia ibada iliyokuwa takatifu na safi. Ndiyo sababu Sheria ya Musa inakazia utakatifu mara nyingi. Kwa kweli, kuhani mkuu alivaa bamba la dhahabu upande wa mbele wa kilemba chake, na watu wote waliweza kuliona liking’aa kwenye mwangaza. Maneno haya yalichongwa kwenye bamba hilo: “Utakatifu ni wa Yehova.” (Kutoka 28:36) Kwa hiyo, Yehova alitaka ibada na hata njia yao ya maisha iwe safi kabisa. Yehova aliwaambia hivi: “Mnapaswa kuwa watakatifu, kwa sababu mimi, Yehova Mungu wenu, ni mtakatifu.” (Mambo ya Walawi 19:2) Kadiri Waisraeli walivyojitahidi kuishi kulingana na viwango vya Mungu, ndivyo alivyowaona kuwa watakatifu licha ya kutokuwa wakamilifu.
10. Ibada na njia ya maisha ya Waisraeli ilitofautianaje na mataifa yaliyowazunguka?
10 Umuhimu wa kuendelea kuwa watakatifu ulikaziwa sana katika taifa la Israeli ukilinganisha na ibada za mataifa yaliyolizunguka. Mataifa hayo ya kipagani yaliabudu miungu ya uwongo ambayo haikuwa na uhai na ilisifiwa kuwa yenye jeuri, pupa, na maadili mapotovu. Haikuwa mitakatifu kwa njia yoyote. Watu walioabudu miungu hiyo hawakuwa watakatifu. Hivyo, Yehova aliwaonya watumishi wake wajitenge na waabudu hao wapagani na kuepuka mazoea machafu ya dini hizo.—Mambo ya Walawi 18:24-28; 1 Wafalme 11:1, 2.
11. Utakatifu wa sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Yehova unaonyeshwaje kupitia (a) malaika? (b) maserafi? (c) Yesu?
11 Hata Waisraeli walipojitahidi kuwa watakatifu, hawakuweza kamwe kufikia utakatifu wa wale walio katika sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Mungu. Mamilioni ya malaika wanaomtumikia Mungu kwa uaminifu wanaitwa “makumi ya maelfu ya watakatifu.” (Kumbukumbu la Torati 33:2; Yuda 14) Wanaiga kikamili uzuri wa utakatifu wa Mungu. Kumbuka maserafi ambao Isaya aliona katika maono. Maneno ya wimbo wao yanadokeza kwamba viumbe hao wa roho wenye nguvu wanatimiza fungu muhimu sana katika kutangaza utakatifu wa Yehova ulimwenguni pote. Hata hivyo, kuna kiumbe mmoja wa roho aliye juu zaidi ya wote—Mwana mzaliwa pekee wa Mungu. Yesu anaonyesha utakatifu wa Yehova kwa kiwango cha juu zaidi. Kwa kufaa anaitwa, “Mtakatifu wa Mungu.”—Yohana 6:68, 69.
Jina Takatifu, Roho Takatifu
12, 13. (a) Kwa nini inafaa kusema kwamba jina la Mungu ni takatifu? (b) Kwa nini ni lazima jina la Mungu liondolewe shutuma?
12 Namna gani kuhusu jina la Mungu? Kama tulivyoona kwenye Sura ya Kwanza, hilo si jina la cheo au utambulisho tu. Linamwakilisha Yehova Mungu na sifa zake zote. Ndiyo sababu Biblia inatuambia kwamba “jina lake ni takatifu.” (Isaya 57:15) Kulingana na Sheria ya Musa, mtu yeyote aliyetukana jina la Mungu aliuawa. (Mambo ya Walawi 24:16) Ona jambo ambalo Yesu alitaja kwanza katika sala: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.” (Mathayo 6:9) Kutakasa kitu kunamaanisha kukiheshimu na kukiona kuwa kitakatifu. Hata hivyo, ikiwa jina la Mungu ni takatifu, kwa nini linahitaji kutakaswa?
13 Jina takatifu la Mungu limechafuliwa kwa uwongo na uchongezi na maadui wa Mungu. Katika Edeni, Shetani alisema uwongo kumhusu Yehova na akadai kwamba Yeye ni Mtawala asiye na haki. (Mwanzo 3:1-5) Tangu wakati huo, Shetani—mtawala wa ulimwengu huu usio mtakatifu—amehakikisha kwamba uwongo kumhusu Mungu umeenea kila mahali. (Yohana 8:44; 12:31; Ufunuo 12:9) Dini zimefundisha kwamba Mungu hatendi haki, hatujali, au ni mkatili. Wamedai kwamba Mungu anaunga mkono vita vyao vya kikatili. Mara nyingi, wamesema kwamba uumbaji wa Mungu wa kustaajabisha ulijitokeza wenyewe, au viumbe vilitokana na mageuzi. Naam, jina la Mungu limechafuliwa sana. Ni lazima litakaswe; na kurudishiwa tena utukufu wake unaostahili. Tunatazamia kwa hamu siku ambayo Yehova ataliondolea shutuma jina lake milele. Atafanya hivyo kupitia Ufalme utakaotawaliwa na Mwana wake. Tunafurahia kushiriki katika utimizo wa kusudi hilo.
14. Kwa nini roho ya Mungu inaitwa takatifu, na kwa nini kukufuru roho takatifu ni dhambi nzito?
14 Kuna kitu kingine ambacho sikuzote ni kitakatifu na kinatoka kwa Yehova. Kitu hicho kinaitwa roho takatifu, yaani, nguvu ya utendaji ya Mungu. (Mwanzo 1:2) Yehova hutumia roho takatifu kutimiza kusudi lake. Matendo yote ya Mungu ni matakatifu na safi, kwa hiyo nguvu yake ya utendaji kwa kufaa inaitwa roho takatifu, au roho ya utakatifu. (Luka 11:13; Waroma 1:4) Kukufuru roho takatifu, yaani, kupinga kusudi la Yehova kwa kukusudia, ni dhambi isiyoweza kusamehewa.—Marko 3:29.
Kwa Nini Utakatifu wa Yehova Unatuchochea Tumkaribie?
15. Kwa nini inafaa kumwogopa Yehova kwa sababu ya utakatifu wake, na hilo linahusisha nini?
15 Tunaweza kuelewa kwa nini Biblia inasema kwamba tunapaswa kumwogopa Mungu kwa kuwa ni mtakatifu. Kwa mfano, Zaburi 99:3 inasema hivi: “Na walisifu jina lako kuu, kwa maana linaogopesha, nalo ni takatifu.” Hilo linamaanisha kwamba tunapaswa kumheshimu sana na kuliheshimu jina lake. Inafaa kuhisi hivyo, kwa sababu hatuwezi kamwe kufikia utakatifu wa Mungu kwa kuwa umeng’aa sana na ni wenye utukufu. Hata hivyo, hilo halipaswi kutuzuia kumkaribia. Tukiwa na maoni yanayofaa kuhusu utakatifu wa Mungu tutaweza kumkaribia zaidi. Kwa nini?
16. (a) Utakatifu unahusianaje na uzuri? Toa mfano. (b) Biblia inafafanuaje uzuri wa Mungu wetu mtakatifu?
16 Kwanza, Biblia huhusianisha utakatifu na uzuri. Kwenye Isaya 63:15, mbingu inasemwa kuwa “makao . . . yaliyoinuliwa ya utakatifu na utukufu [au “uzuri,” maelezo ya chini].” Utukufu na uzuri hutuvutia. Kwa mfano, tazama picha iliyo kwenye ukurasa wa 33. Je, mazingira hayo hayakuvutii? Kwa nini yanavutia? Ona jinsi maji yalivyo safi. Bila shaka, hewa pia ni safi, kwa kuwa anga lina rangi ya bluu na nuru inang’aa. Ikiwa mazingira hayo yangebadilishwa—mto ujazwe takataka, miti na mawe yachafuliwe kwa maandishi, hewa ijae moshi—hayangetuvutia tena; yangetuchukiza. Kwa kawaida, kitu kinaonekana kizuri ikiwa ni safi, kimetakata, na kinang’aa. Maneno hayo yanaweza pia kutumiwa kufafanua utakatifu wa Yehova. Ndiyo sababu maono kumhusu Yehova yanatuvutia sana! Uzuri au utukufu wa Mungu wetu mtakatifu ni kama nuru, mawe yanayong’aa, moto unaowaka au madini safi yenye thamani yanayong’aa sana.—Ezekieli 1:25-28; Ufunuo 4:2, 3.
Utakatifu unapaswa kutuvutia kama uzuri unavyotuvutia
17, 18. (a) Mwanzoni Isaya alihisije alipopewa maono? (b) Yehova alimtumiaje mmoja wa maserafi ili kumfariji Isaya, na jambo alilofanya serafi huyo lilikuwa na maana gani?
17 Je, tunapaswa kuhisi kuwa sisi ni duni kwa sababu ya utakatifu wa Mungu? Bila shaka, jibu ni ndiyo. Ukweli ni kwamba sisi ni duni tunapolinganishwa na Yehova. Je, tunapaswa kujitenga naye kwa sababu sisi ni duni? Fikiria jambo alilotenda Isaya aliposikia maserafi wakitangaza utakatifu wa Yehova. “Kisha nikasema: ’Ole wangu! Kwa maana ni kama nimekufa, kwa maana mimi ni mtu asiye na midomo safi, nami ninaishi kati ya watu wasio na midomo safi; kwa maana macho yangu yamemwona Mfalme, Yehova wa majeshi mwenyewe!’” (Isaya 6:5) Isaya alipoona jinsi Yehova alivyo mtakatifu, alikumbuka kwamba yeye ni mwanadamu mwenye dhambi na asiye mkamilifu. Mwanzoni, mwanamume huyo mwaminifu alihuzunika sana. Lakini Yehova hakutaka mwanamume huyo mwaminifu ahisi hivyo.
18 Yehova alimtuma mmoja wa maserafi ili kumfariji Isaya. Jinsi gani? Kiumbe huyo wa roho mwenye nguvu alipaa kwenye madhabahu, akachukua kaa la moto, akagusa kinywa cha Isaya kwa kaa hilo. Huenda hilo likaonekana kuwa jambo lenye kuumiza sana badala ya kufariji. Hata hivyo, kumbuka kwamba hayo yalikuwa maono yenye maana nyingi. Isaya, Myahudi mwaminifu, alijua kwamba dhabihu zilitolewa kila siku kwenye madhabahu ya hekalu ili kulipia dhambi. Na kwa upendo, serafi huyo alimkumbusha nabii huyo kwamba ingawa alikuwa “mtu asiye na midomo safi,” ambaye si mkamilifu, bado angeweza kuwa mwadilifu machoni pa Mungu.a Yehova alikuwa tayari kumwona mwanadamu asiye mkamilifu, na mwenye dhambi kuwa mtakatifu kwa kadiri fulani.—Isaya 6:6, 7.
19. Kwa nini Yehova anaweza kutuona kuwa watakatifu ingawa sisi si wakamilifu?
19 Ndivyo ilivyo leo. Dhabihu zote zilizotolewa kwenye madhabahu huko Yerusalemu zilikuwa kivuli tu cha jambo kubwa zaidi—dhabihu pekee kamilifu, iliyotolewa na Yesu Kristo mwaka wa 33.W.K. (Waebrania 9:11-14) Tukitubu dhambi zetu kikweli, kurekebisha mwenendo wetu mbaya, na kudhihirisha imani katika dhabihu hiyo, tunapata msamaha. (1 Yohana 2:2) Sisi pia tunaweza kuwa safi machoni pa Mungu. Kwa hiyo, mtume Petro anatukumbusha hivi: “Imeandikwa: ‘Lazima muwe watakatifu, kwa sababu mimi ni mtakatifu.’” (1 Petro 1:16) Ona Yehova hakusema kwamba lazima tuwe watakatifu kama yeye. Yeye hatarajii kamwe tutimize mambo tusiyoweza. (Zaburi 103:13, 14) Badala yake, Yehova anatuambia tuwe watakatifu kwa sababu yeye ni mtakatifu. “Kama watoto wapendwa,” tunajitahidi kumwiga kadiri tuwezavyo tukiwa wanadamu wasio wakamilifu. (Waefeso 5:1) Kwa hiyo, kuwa watakatifu ni jitihada inayoendelea. Kadiri tunavyokua kiroho, tunajitahidi ‘kuukamilisha utakatifu’ siku baada ya siku.—2 Wakorintho 7:1.
20. (a) Kwa nini ni muhimu kutambua kwamba tunaweza kuwa safi machoni pa Mungu wetu mtakatifu? (b) Isaya alihisije alipotambua kwamba dhambi zake zimefunikwa?
20 Yehova anapenda uadilifu na usafi. Anachukia dhambi. (Habakuki 1:13) Lakini yeye hatuchukii. Yehova atatusamehe dhambi zetu tukichukia maovu na kupenda yaliyo mema na kufuata hatua kamilifu za Kristo Yesu. (Amosi 5:15; 1 Petro 2:21) Tunapoelewa kwamba tunaweza kuwa safi machoni pa Mungu wetu mtakatifu, matokeo yanaweza kuwa mazuri sana. Kumbuka, utakatifu wa Yehova ulimkumbusha Isaya kwamba hakuwa safi. Alisema hivi kwa sauti kubwa: “Ole wangu!” Lakini mara tu alipotambua kwamba dhambi zake zimefunikwa, mtazamo wake ulibadilika. Yehova alipotafuta mtu atakayejitolea kutimiza mgawo fulani, Isaya alikubali bila kukawia ingawa hakujua mgawo huo ulihusu nini. Alisema hivi kwa shauku: “Mimi hapa! Nitume mimi!”—Isaya 6:5-8.
21. Tuna uhakika gani kwamba tunaweza kuwa watakatifu?
21 Tumeumbwa kwa mfano wa Mungu wetu mtakatifu, hivyo tunaweza kuiga sifa zake na kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye. (Mwanzo 1:26) Sote tunaweza kuwa watakatifu. Yehova anafurahi kutusaidia tunapoendelea kusitawisha utakatifu. Tunapofanya hivyo, tutamkaribia zaidi Mungu wetu mtakatifu. Isitoshe, tutakapozungumzia sifa za Yehova katika sura zinazofuata, tutaona kwamba kuna sababu nyingi nzuri za kumkaribia!
a Maneno “asiye na midomo safi,” yanafaa, kwa kuwa midomo mara nyingi hutumiwa katika Biblia kwa njia ya mfano kumaanisha usemi au lugha. Sehemu kubwa ya dhambi za wanadamu wote wasio wakamilifu zinatokana na jinsi tunavyotumia uwezo wetu wa kusema.—Methali 10:19; Yakobo 3:2, 6.