SURA YA 28
“Wewe Peke Yako Ni Mshikamanifu”
1, 2. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Mfalme Daudi alijua matokeo mabaya ya kukosa ushikamanifu?
MFALME DAUDI alijua matokeo mabaya ya kukosa ushikamanifu. Pindi moja, utawala wake wenye misukosuko ulikabili matatizo wakati watu wa taifa lake walipopanga njama ya kunyakua ufalme kutoka kwake. Isitoshe, Daudi alisalitiwa na baadhi ya watu ambao tungetarajia wawe rafiki zake wa karibu. Mfikirie Mikali, mke wa kwanza wa Daudi. Mwanzoni, “alimpenda Daudi” na bila shaka, alimuunga mkono katika majukumu yake ya kifalme. Hata hivyo, baadaye ‘alimdharau moyoni mwake,’ hata akamwona Daudi kama ‘mtu asiye na akili.’—1 Samweli 18:20; 2 Samweli 6:16, 20.
2 Pia, kulikuwa na Ahithofeli aliyekuwa mshauri wa Daudi. Ushauri wake ulithaminiwa sana kana kwamba ulitoka moja kwa moja kwa Yehova. (2 Samweli 16:23) Lakini mwishowe, mshauri huyo aliyetumainiwa alimsaliti Daudi na kujiunga na waasi. Ni nani aliyepanga njama hiyo? Absalomu, mwana wa Daudi! Mhaini huyo mwenye kujitafutia makuu aliendelea “kuiba mioyo ya Waisraeli,” na akajitawaza mwenyewe kuwa mfalme mpinzani. Uasi wa Absalomu uliongezeka sana hivi kwamba Mfalme Daudi alilazimika kukimbia ili kujiokoa.—2 Samweli 15:1-6, 12-17.
3. Daudi alikuwa na uhakika gani?
3 Je, hakukuwa na mtu yeyote aliyebaki akiwa mshikamanifu kwa Daudi? Katika shida zake zote, Daudi alikuwa na uhakika kwamba kulikuwa na mmoja aliyekuwa mshikamanifu kwake. Nani? Yehova Mungu mwenyewe. Daudi alisema hivi kumhusu Yehova: “Kwa mtu mshikamanifu unatenda kwa ushikamanifu.” (2 Samweli 22:26) Ushikamanifu ni nini, na Yehova anaonyeshaje sifa hii kwa njia bora zaidi?
Ushikamanifu Ni Nini?
4, 5. (a) “Ushikamanifu” ni nini? (b) Ushikamanifu unatofautianaje na uaminifu?
4 “Kulingana na Maandiko ya Kiebrania, “ushikamanifu” ni fadhili ambayo inashikamana kabisa kwa upendo na kitu fulani hadi kusudi lake kuhusiana na kitu hicho linapotimia. Ushikamanifu unahusisha mambo mengi zaidi tu ya uaminifu. Mtu anaweza kuwa mwaminifu kwa sababu tu ya wajibu. Kinyume chake, ushikamanifu unategemea upendo.a Isitoshe, neno “aminifu” linaweza kutumiwa kurejelea vitu visivyo hai. Kwa mfano, mtunga-zaburi alisema kwamba mwezi ni “shahidi mwaminifu angani” kwa sababu unaangaza kwa ukawaida wakati wa usiku. (Zaburi 89:37) Lakini hatuwezi kusema kwamba mwezi ni mshikamanifu. Kwa nini? Kwa sababu ushikamanifu unategemea upendo. Na vitu visivyo hai haviwezi kuonyesha sifa hiyo.
Mwezi unaitwa shahidi mwaminifu, lakini ni viumbe wenye akili tu wanaoweza kuiga ushikamanifu wa Yehova
5 Maandiko yanaonyesha kwamba ushikamanifu hudhihirisha upendo. Ni wazi kwamba kuna uhusiano fulani uliopo kati ya mtu anayeonyeshwa sifa hiyo na yule anayeionyesha. Ushikamanifu huo haubadiliki. Si kama mawimbi ya bahari yanayopeperushwa huku na huku kwa sababu ya kubadilika kwa mwelekeo wa upepo. Kinyume chake, sifa ya ushikamanifu au upendo mshikamanifu, ni imara sana hivi kwamba inaweza kumsaidia mtu kushinda matatizo makubwa sana anayokabili.
6. (a) Ushikamanifu umepungua kwa kadiri gani miongoni mwa wanadamu, na Biblia inathibitishaje jambo hilo? (b) Ni njia gani bora ya kujifunza kuhusu ushikamanifu, na kwa nini?
6 Ni kweli kwamba ushikamanifu huo umepungua sana leo. Mara nyingi, marafiki wa karibu huwa “tayari kuangamizana.” Tunasikia visa vingi vya watu wanaowaacha wenzi wao wa ndoa. (Methali 18:24; Malaki 2:14-16) Matendo ya hila ni mengi sana hivi kwamba tunaweza kurudia maneno ya nabii Mika: “Mtu mshikamanifu ameangamia duniani.” (Mika 7:2) Ingawa mara nyingi wanadamu hushindwa kuonyesha ushikamanifu, Yehova huonyesha sifa hiyo kwa njia ya pekee sana. Njia bora ya kujifunza kuhusu ushikamanifu ni kwa kuchunguza jinsi Yehova anavyoonyesha sifa hii kuu ya upendo wake.
Ushikamanifu wa Yehova Usio na Kifani
7, 8. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba ni Yehova peke yake aliye mshikamanifu?
7 Biblia inasema hivi kumhusu Yehova: “Wewe peke yako ni mshikamanifu.” (Ufunuo 15:4) Kwa nini Biblia inasema hivyo, hata ingawa nyakati fulani wanadamu na malaika wameonyesha ushikamanifu wa pekee? (Ayubu 1:1; Ufunuo 4:8) Na vipi kumhusu Yesu Kristo? Yeye ndiye mtu “mshikamanifu” zaidi mbele za Mungu. (Zaburi 16:10) Basi, kwa nini inaweza kusemwa kwamba ni Yehova peke yake aliye mshikamanifu?
8 Kwanza, kumbuka kwamba ushikamanifu ni sifa ya upendo. Kwa kuwa “Mungu ni upendo,” yaani, yeye ndiye wonyesho halisi wa upendo, hakuna anayeweza kuwa mshikamanifu kikamili zaidi kuliko Yehova. (1 Yohana 4:8) Ingawa malaika na wanadamu wanaweza kuiga sifa za Mungu, hawawezi kuwa washikamanifu kwa kiwango cha juu kama yeye. Amekuwa akionyesha ushikamanifu kwa muda mrefu kuliko kiumbe yeyote duniani au mbinguni, kwa sababu yeye ni “Mzee wa Siku.” (Danieli 7:9) Kwa hiyo, Yehova ndiye mfano bora wa ushikamanifu. Yehova anaonyesha sifa hiyo kwa njia isiyo na kifani. Fikiria mifano kadhaa.
9. Yehova ni “mshikamanifu katika kila jambo analotenda” jinsi gani?
9 Yehova ni “mshikamanifu katika kila jambo analotenda.” (Zaburi 145:17) Katika njia gani? Zaburi 136 inajibu swali hilo. Andiko hilo linataja matendo kadhaa ya Yehova ya kuokoa, kutia ndani alipowaokoa Waisraeli kwa njia yenye kustaajabisha katika Bahari Nyekundu. Ona kwamba kila mstari wa zaburi hiyo unakaziwa na usemi: “Kwa maana upendo wako mshikamanifu unadumu milele.” Zaburi hiyo imetajwa katika “Maswali ya Kutafakari” kwenye ukurasa wa 347. Unaposoma mistari hiyo, utavutiwa sana kuona jinsi Yehova alivyoonyesha ushikamanifu kwa watu wake katika njia mbalimbali. Naam, Yehova huwaonyesha upendo mshikamanifu watumishi wake waaminifu kwa kusikia vilio vyao vya kuomba msaada na kwa kuchukua hatua kwa wakati unaofaa. (Zaburi 34:6) Yehova huendelea kuwaonyesha watumishi wake upendo mshikamanifu ikiwa tu wanaendelea kuwa waaminifu kwake.
10. Yehova anaonyesha ushikamanifu kuhusiana na viwango vyake jinsi gani?
10 Zaidi ya hayo, Yehova huwaonyesha watumishi wake ushikamanifu kwa kushikamana kabisa na viwango vyake. Wanadamu wasiotegemeka au wasio na msimamo wanafuata tu hisia zao, lakini maoni ya Yehova kuhusu mema na mabaya hayabadiliki. Kwa mfano, hajabadili maoni yake kuhusu kuwasiliana na roho, ibada ya sanamu, na kuua. Alisema hivi kupitia nabii wake Isaya, “hata utakapozeeka nitakuwa yuleyule.” (Isaya 46:4) Kwa hiyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba tutafaidika tukifuata mwongozo kuhusu maadili unaoelezwa waziwazi katika Neno la Mungu.—Isaya 48:17-19.
11. Toa mifano inayoonyesha kwamba Yehova hutimiza ahadi zake kwa ushikamanifu.
11 Yehova huonyesha pia ushikamanifu kwa kutimiza ahadi zake. Kila jambo analotabiri linatimia. Yehova alisema hivi: “Neno langu, linalotoka katika kinywa changu . . . halitarudi kwangu bila matokeo, bali hakika litatimiza jambo lolote linalonipendeza, na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.” (Isaya 55:11) Yehova anaonyesha ushikamanifu kwa watu wake kwa kutimiza ahadi zake. Yeye hawaahidi mambo ambayo hatatimiza. Yehova amethibitisha kabisa kwamba anatimiza ahadi zake hivi kwamba mtumishi wake Yoshua aliweza kusema: “Hakuna ahadi hata moja iliyokosa kutimia kati ya ahadi zote nzuri ambazo Yehova aliwaahidi Waisraeli; zote zilitimia.” (Yoshua 21:45) Hivyo basi, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova hatatukatisha tamaa kwa kukosa kutimiza ahadi zake.—Isaya 49:23; Waroma 5:5.
12, 13. Ni katika njia zipi ushikamanifu wa Yehova unadumu milele?
12 Kama tulivyoona hapo awali, Biblia inatuambia kwamba upendo mshikamanifu wa Yehova “unadumu milele.” (Zaburi 136:1) Jinsi gani? Njia moja ni jinsi Yehova anavyotenda anaposamehe dhambi. Kama Sura ya 26 ilivyoonyesha, Yehova hakumbuki au kumhukumu mtu kwa sababu ya dhambi ambazo tayari amesamehewa. Kila mmoja wetu anapaswa kushukuru kwamba upendo mshikamanifu wa Yehova ni wa milele kwa sababu ‘wote tumefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.’—Waroma 3:23.
13 Lakini upendo mshikamanifu wa Yehova ni wa milele katika njia nyingine. Neno lake linasema kwamba mtu mwadilifu “atakuwa kama mti uliopandwa kando ya vijito vya maji, mti unaozaa matunda yake katika majira yake, na majani yake hayanyauki. Na kila jambo analofanya litafanikiwa.” (Zaburi 1:3) Wazia mti mkubwa sana ambao majani yake hayanyauki! Vivyo hivyo, ikiwa tutapenda kusoma Neno la Mungu na kujifunza, tutaishi muda mrefu, tutakuwa na amani, na kufanikiwa. Yehova anawaahidi watumishi wake waaminifu baraka za milele. Kwa kweli, katika ulimwengu mpya wenye uadilifu ambao Yehova ataleta, wanadamu watiifu watafurahia upendo wake mshikamanifu milele.—Ufunuo 21:3, 4.
Yehova “Hatawaacha Washikamanifu Wake”
14. Yehova anaonyeshaje kwamba anathamini ushikamanifu wa watumishi wake?
14 Yehova ameonyesha ushikamanifu wake tena na tena. Kwa kuwa Yehova habadiliki kamwe, yeye huwaonyesha watumishi wake ushikamanifu wa kudumu. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Nilikuwa kijana lakini sasa nimezeeka; lakini sijamwona mtu yeyote mwadilifu akiwa ameachwa, wala watoto wake wakitafuta mkate. Kwa maana Yehova anapenda haki, naye hatawaacha washikamanifu wake.” (Zaburi 37:25, 28) Ni kweli kwamba Yehova anastahili ibada yetu, kwa kuwa yeye ni Muumba. (Ufunuo 4:11) Hata hivyo, Yehova anathamini sana uaminifu wetu kwa sababu yeye ni mshikamanifu.—Malaki 3:16, 17.
15. Eleza jinsi Yehova alivyoonyesha ushikamanifu wake aliposhughulika na Waisraeli.
15 Kwa sababu ya upendo wake ushikamanifu, sikuzote Yehova huwasaidia watu wake wanapopatwa na matatizo. Mtunga zaburi anatuambia hivi: “Anaulinda uhai wa washikamanifu wake, huwaokoa kutoka katika mkono wa mwovu.” (Zaburi 97:10) Fikiria jinsi alivyoshughulika na taifa la Israeli. Baada ya kuokolewa kimuujiza katika Bahari Nyekundu, Waisraeli walitangaza hivi katika wimbo waliomwimbia Yehova: “Kwa upendo wako mshikamanifu umewaongoza watu uliowakomboa.” (Kutoka 15:13) Bila shaka, Yehova alionyesha upendo mshikamanifu alipowaokoa katika Bahari Nyekundu. Musa aliwaambia Waisraeli hivi: “Yehova hakuwapenda na kuwachagua ninyi eti kwa sababu mlikuwa wengi kuliko mataifa yote, kwa maana mlikuwa taifa dogo zaidi kati ya mataifa yote. Badala yake, ni kwa sababu Yehova anawapenda na alitimiza kiapo alichowaapia mababu zenu, ndiyo maana Yehova aliwatoa Misri kwa mkono wake wenye nguvu na kuwakomboa kutoka katika nyumba ya utumwa, kutoka katika nguvu za Farao mfalme wa Misri.”—Kumbukumbu la Torati 7:7, 8.
16, 17. (a) Waisraeli walionyeshaje kwamba hawakuwa na shukrani kabisa kuelekea upendo mshikamanifu wa Yehova, lakini Yehova aliwaonyeshaje rehema? (b) Waisraeli wengi walionyeshaje kwamba ‘hawangeweza kuponywa,’ na hilo linatupatia onyo gani?
16 Bila shaka, taifa la Israeli halikuthamini ushikamanifu wa Yehova. Baada ya kukombolewa, ‘waliendelea kumtendea dhambi Yehova kwa kumwasi yule Aliye Juu Zaidi.’ (Zaburi 78:17) Kadiri miaka ilivyopita, waliasi tena na tena. Walimwacha Yehova na kuabudu miungu ya uwongo, na hilo likawafanya waharibu uhusiano wao na Yehova. Hata hivyo, Yehova hakuvunja agano lake. Badala yake, Yehova aliwasihi hivi watu wake kupitia nabii Yeremia: “Rudi, Ee Israeli mwasi . . . Sitakutazama kwa hasira, kwa maana mimi ni mshikamanifu.” (Yeremia 3:12) Lakini kama Sura ya 25 ilivyoonyesha, Waisraeli wengi walikataa kubadilika. Hata, “waliendelea kuwadhihaki wajumbe wa Mungu wa kweli, wakadharau maneno yake na kuwakejeli manabii wake.” Matokeo yalikuwa nini? Mwishowe, ‘ghadhabu ya Yehova ikaja juu ya watu wake, hivi kwamba hawangeweza kuponywa.’—2 Mambo ya Nyakati 36:15, 16.
17 Tunajifunza nini kutokana na mambo hayo? Tunajifunza kwamba ushikamanifu wa Yehova si wa kipumbavu au kwamba anapuuza mambo mabaya ambayo watu wanafanya. Ni kweli kwamba Yehova ana “upendo mwingi mshikamanifu” naye hupenda kuonyesha rehema kunapokuwa na msingi wa kufanya hivyo. Lakini Yehova huchukua hatua gani mtu mwovu anapokataa kubadilika? Inapokuwa hivyo, Yehova hushikamana na kanuni zake za uadilifu naye humhukumu mtu mwovu. Yehova alimwambia Musa: “Sikosi kamwe kuwaadhibu wenye hatia.”—Kutoka 34:6, 7.
18, 19. (a) Yehova anaonyeshaje ushikamanifu kwa kuwaadhibu waovu? (b) Yehova ataonyeshaje ushikamanifu kwa watumishi wake ambao wameteswa na kuuawa?
18 Mungu huonyesha pia ushikamanifu kwa kuwaadhibu waovu. Jinsi gani? Amri ambazo Yehova anawapa wale malaika saba katika kitabu cha Ufunuo zinaonyesha jambo hilo: “Nendeni mkamwage yale mabakuli saba ya hasira ya Mungu juu ya dunia.” Malaika wa tatu anapomwaga bakuli lake “ndani ya mito na chemchemi za maji,” yanakuwa damu. Kisha malaika huyo anamwambia Yehova hivi: “Wewe, Ambaye uko na uliyekuwako, Mshikamanifu, wewe ni mwadilifu, kwa kuwa umetoa hukumu hizi, kwa sababu waliimwaga damu ya watakatifu na ya manabii, nawe umewapa damu wanywe; wanastahili hivyo.”—Ufunuo 16:1-6.
19 Ona kwamba malaika huyo anapotangaza ujumbe huo wa hukumu anasema Yehova ni “Mshikamanifu.” Kwa nini? Kwa sababu anapowaangamiza waovu, Yehova anaonyesha ushikamanifu kwa watumishi wake ambao wameteswa na kuuawa. Kwa ushikamanifu, Yehova anawakumbuka vizuri watumishi hao. Anatamani kuwaona tena waaminifu hao waliokufa, na Biblia inaonyesha waziwazi kwamba anakusudia kuwathawabisha kwa kuwafufua. (Ayubu 14:14, 15) Yehova hawasahau watumishi wake washikamanifu kwa sababu tu wamekufa. Badala yake, “kwake, wote wako hai.” (Luka 20:37, 38) Kusudi la Yehova la kuwafufua wale walio katika kumbukumbu lake linathibitisha kabisa kwamba yeye ni mshikamanifu.
Kwa ushikamanifu Yehova atawakumbuka na kuwafufua wale ambao wamedumu wakiwa washikamanifu hadi kifo
Wanazi waliwaua Bernard Luimes (juu) na Wolfgang Kusserow (katikati)
Kikundi cha kisiasa kilimuua Moses Nyamussua kwa kumchoma mkuki
Upendo Mshikamanifu wa Yehova Huandaa Njia ya Wokovu
20. “Vyombo vya rehema” ni nani, na Yehova anawaonyeshaje ushikamanifu?
20 Katika historia yote, Yehova ameonyesha ushikamanifu wa pekee kwa wanadamu waaminifu. Kwa maelfu ya miaka, Yehova ‘amevumilia kwa subira nyingi vyombo vya ghadhabu vilivyo tayari kwa ajili ya uharibifu.’ Kwa nini? “Ili ajulishe utajiri wa utukufu wake kwa vyombo vya rehema, alivyotayarisha awali kwa ajili ya utukufu.” (Waroma 9:22, 23) “Vyombo vya rehema” ni wale walio na mtazamo unaofaa ambao wametiwa mafuta kwa roho takatifu ili wawe warithi pamoja na Kristo katika Ufalme wake. (Mathayo 19:28) Kwa kuandaa njia ya wokovu kwa ajili ya vyombo hivyo vya rehema, Yehova alionyesha ushikamanifu kwa Abrahamu, kwa sababu alikuwa amemwahidi hivi alipofanya agano naye: “Kupitia uzao wako mataifa yote ya dunia yatajipatia baraka kwa sababu umeisikiliza sauti yangu.”—Mwanzo 22:18.
Watumishi wote waaminifu wa Yehova wana tumaini hakika la wakati ujao kwa sababu yeye ni mshikamanifu
21. (a) Yehova anaonyeshaje ushikamanifu kwa “umati mkubwa” ambao unatumaini kuokoka “dhiki kuu”? (b) Ushikamanifu wa Yehova unakuchochea kufanya nini?
21 Yehova anaonyesha ushikamanifu pia kwa “umati mkubwa” ambao unatumaini kuokoka “dhiki kuu” na kuishi milele katika paradiso duniani. (Ufunuo 7:9, 10, 14) Kwa ushikamanifu, Yehova anawapa watumishi wake fursa ya kuishi milele katika dunia paradiso ingawa wao si wakamilifu. Jinsi gani? Anawapa fursa hiyo kupitia fidia—wonyesho mkubwa zaidi wa ushikamanifu wa Yehova. (Yohana 3:16; Waroma 5:8) Ushikamanifu wa Yehova unawavuta wale ambao wana njaa ya uadilifu mioyoni mwao. (Yeremia 31:3) Je, huhisi ukiwa karibu zaidi na Yehova kwa sababu ya ushikamanifu wa dhati ambao amekuonyesha na atakaokuonyesha? Kwa sababu tunatamani kumkaribia Mungu, na acheni tuthamini upendo wake kwa kuimarisha azimio letu la kumtumikia kwa ushikamanifu.
a Inapendeza kwamba neno linalotafsiriwa “ushikamanifu” kwenye 2 Samweli 22:26 linatafsiriwa “upendo mshikamanifu” kwenye mistari mingine.