Jumamosi, Agosti 29
Mhakikishe mambo muhimu zaidi.—Flp. 1:10.
Fikiria mfano huu. Unatafuta kazi itakayokusaidia kuitegemeza familia yako. Kuna kazi mbili ambazo zimepatikana. Umetafuta habari kamili kuhusu kazi hizo, kama vile, ni kazi za aina gani, zina ratiba gani, utatumia muda gani kufika kazini, na kadhalika. Kazi zote mbili hazivunji kanuni za Kimaandiko. Huenda unapendelea chaguo mojawapo kwa sababu ya aina ya kazi utakayofanya au kwa sababu mshahara ni mkubwa zaidi. Hata hivyo, kuna mambo mengine ya kufikiria kabla ya kufanya uamuzi. Kwa mfano, je, kazi hizo zinaingiliana na ratiba yenu ya mkutano wa kutaniko? Je, kazi hizo zitachukua muda ambao unahitaji kutumia ili kushughulikia mahitaji ya kihisia na ya kiroho ya familia yako? Kujiuliza maswali kama hayo kutakusaidia kutanguliza maishani “mambo muhimu zaidi,” yaani, ibada yako na mahitaji ya familia yako, badala ya manufaa ya kimwili. Kisha, utaweza kufanya uamuzi ambao Yehova ataubariki. w25.01 3:11-13
Jumapili, Agosti 30
Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo.—Zab. 34:18.
Hata ikiwa wengine wamekutendea kwa njia isiyofaa, unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anakupenda na anakuthamini. Ikiwa unahisi ‘umepondeka roho,’ kumbuka kwamba Yehova aliona mambo mazuri moyoni mwako na alikuvuta kibinafsi kwake. (Yoh. 6:44) Sikuzote yuko tayari kukusaidia kwa sababu wewe ni mwenye thamani kwake. Tunaweza kujifunza kuhusu hisia za Yehova kwa kuchunguza mfano wa Yesu. Wakati wa huduma yake duniani, Yesu aliwaonyesha fadhili wale ambao walidharauliwa na wengine, naye aliwatendea kwa huruma. (Mt. 9:9-12) Wakati mwanamke aliyetamani kuponywa ugonjwa wake mbaya alipogusa vazi lake, Yesu alimfariji na kumpongeza kwa sababu ya imani yake. (Marko 5:25-34) Yesu anaiga kikamilifu utu wa Baba yake. (Yoh. 14:9) Hivyo, unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anakuthamini na anaona sifa zako nzuri, kutia ndani imani yako na upendo wako kwake. w24.10 40:4-5
Jumatatu, Agosti 31
Yakusanye machozi yangu katika kiriba chako cha ngozi.—Zab. 56:8.
Katika maisha yake, Daudi alikabili hali ngumu kadhaa zilizomfanya atokwe na machozi. Alichukiwa na watu wengine na hata kusalitiwa na wale ambao aliwatumaini. (1 Sam. 19:10, 11; 2 Sam. 15:10-14, 30) Pindi moja aliandika hivi: “Nimechoka kwa sababu ya kulia kwa uchungu; usiku kucha ninakilowesha kitanda changu kwa machozi; kochi langu nalifanya lifurike kwa machozi.” (Zab. 6:6) Licha ya hali ngumu ambazo Daudi alikabili, alikuwa na uhakika kwamba Yehova alimpenda. Aliandika hivi: “Yehova atasikia sauti ya kilio changu.” (Zab. 6:8) Maneno ya andiko letu yanaonyesha jinsi Yehova anavyotujali kwa wororo. Daudi alihisi kana kwamba Yehova alikuwa akikusanya machozi yake kwenye kiriba au kuyaandika kwenye kitabu. Daudi alikuwa na uhakika kwamba Yehova aliona na kukumbuka maumivu yake. Daudi alikuwa na uhakika kwamba Baba yake wa mbinguni mwenye upendo alijua mambo ambayo alikuwa amepitia na pia jinsi yalivyomwathiri. w24.12 51:11-12