Jumatano, Septemba 2
Yehova yuko pamoja nasi. Msiwaogope.—Hes. 14:9.
Tunapomwogopa Yehova kwa njia inayofaa, tutampenda sana hivi kwamba hatutafanya jambo lolote ambalo litamkasirisha. Tunajitahidi sana kujifunza tofauti kati ya mambo yaliyo sawa na yasiyo sawa, kati ya ukweli na uwongo, ili tupate kibali cha Yehova. (Met. 2:3-6; Ebr. 5:14) Ikiwa tunawaogopa wanadamu kuliko tunavyomwogopa Mungu, tunaweza kupeperushwa mbali kutoka katika kweli. Fikiria mfano wa wakuu 12 ambao walitumwa kupeleleza nchi ambayo Yehova alikuwa ameahidi kuwapa Waisraeli. Kwa wale wapelelezi kumi, hisia za kuwaogopa Wakanaani zilikuwa na nguvu kuliko upendo wao kwa Yehova. Waliwaambia hivi Waisraeli wenzao: “Hatuwezi kwenda kupigana na watu hao, kwa sababu wana nguvu kuliko sisi.” (Hes. 13:27-31) Kwa maoni ya wanadamu, Wakanaani walikuwa na nguvu. Hilo lilikuwa kweli. Lakini kusema kwamba Waisraeli hangeweza kuwashinda maadui wao kunaonyesha kwamba hawakumfikiria Yehova. w24.07 28:5-6
Alhamisi, Septemba 3
Je, Mwamuzi wa dunia yote hatatenda jambo la haki?—Mwa. 18:25.
Je, tuna sababu nzuri za kuwa na uhakika kwamba Yehova anapowahukumu watu, sikuzote hukumu zake zote ni za haki? Ndiyo! Abrahamu alielewa vizuri kwamba Yehova ni “Mwamuzi wa dunia yote” ambaye ni mkamilifu, mwenye hekima yote, na mwenye rehema. Amemzoeza Mwana wake na kumkabidhi kazi yote ya kuhukumu. (Yoh. 5:22) Yehova na Mwana wake wanaweza kusoma mambo yaliyo moyoni mwa kila mwanadamu. (Mt. 9:4) Katika kila kisa, watafanya “jambo la haki”! Acheni tuendelee kuazimia kumtumaini Yehova na maamuzi yake yote. Tunatambua kwamba sisi hatustahili kutoa hukumu—lakini yeye anastahili! (Isa. 55:8, 9) Kwa hiyo, tukiwa na uhakika, tunamwachia kazi yote ya kuhukumu yeye na Mwana wake, Mfalme ambaye anaiga kikamilifu haki na rehema ya Baba yake.—Isa. 11:3, 4. w24.05 18:18-19
Ijumaa, Septemba 4
Yehova humchukia mtu mwenye hila, lakini ana urafiki wa karibu na watu wanyoofu.—Met. 3:32.
Tunaweza kujifunza kuhusu umuhimu wa kuwa na moyo mnyoofu kwa kuchunguza pindi Yesu na Nathanaeli walipokutana kwa mara ya kwanza. Filipo alipomleta Nathanaeli, rafiki yake, akutane na Yesu, jambo la pekee lilitukia. Ingawa Yesu hakuwa amewahi kukutana na Nathanaeli, alisema hivi: “Ona, Mwisraeli kwa hakika ambaye hamna udanganyifu ndani yake.” (Yoh. 1:47) Yesu aliona unyoofu wa pekee wa Nathanaeli. Kama tu sisi, Nathanaeli alikuwa mtu ambaye si mkamilifu. Lakini hakuwa na unafiki wowote, badala yake alikuwa mnyoofu katika mambo yote. Yesu alivutiwa na jambo hilo na akampongeza Nathanaeli. Matakwa mengi ya kumpendeza Yehova yaliyoorodheshwa kwenye Zaburi ya 15 yanahusu jinsi tunavyowatendea wengine. Zaburi 15:3 inasema kwamba mgeni katika hema la Yehova “hachongei kwa ulimi wake, hamtendei jirani yake jambo lolote ovu, naye hawaharibii sifa rafiki zake.” Kutumia usemi wetu vibaya katika njia hizo kunaweza kuwadhuru sana wengine.—Yak. 1:26. w24.06 24:7, 9-10