Jumatatu, Agosti 31
Yakusanye machozi yangu katika kiriba chako cha ngozi.—Zab. 56:8.
Katika maisha yake, Daudi alikabili hali ngumu kadhaa zilizomfanya atokwe na machozi. Alichukiwa na watu wengine na hata kusalitiwa na wale ambao aliwatumaini. (1 Sam. 19:10, 11; 2 Sam. 15:10-14, 30) Pindi moja aliandika hivi: “Nimechoka kwa sababu ya kulia kwa uchungu; usiku kucha ninakilowesha kitanda changu kwa machozi; kochi langu nalifanya lifurike kwa machozi.” (Zab. 6:6) Licha ya hali ngumu ambazo Daudi alikabili, alikuwa na uhakika kwamba Yehova alimpenda. Aliandika hivi: “Yehova atasikia sauti ya kilio changu.” (Zab. 6:8) Maneno ya andiko letu yanaonyesha jinsi Yehova anavyotujali kwa wororo. Daudi alihisi kana kwamba Yehova alikuwa akikusanya machozi yake kwenye kiriba au kuyaandika kwenye kitabu. Daudi alikuwa na uhakika kwamba Yehova aliona na kukumbuka maumivu yake. Daudi alikuwa na uhakika kwamba Baba yake wa mbinguni mwenye upendo alijua mambo ambayo alikuwa amepitia na pia jinsi yalivyomwathiri. w24.12 51:11-12
Jumanne, Septemba 1
Endeleeni kujijaribu kama mko katika imani.—2 Kor. 13:5.
Ni lazima tujitahidi sana ili kufikia ukomavu wa kiroho na pia kuudumisha. Ili tufanikiwe tunahitaji kuepuka kujiamini kupita kiasi. (1 Kor. 10:12) Tunapaswa ‘kuendelea kujijaribu’ ili kuhakikisha kwamba tunaendelea kufanya maendeleo. Katika barua yake kwa Wakolosai, mtume Paulo anaonyesha tena kwamba tunahitaji kuendelea kuwa wakomavu. Ingawa Wakristo hao walikuwa wakomavu, Paulo aliwaonya wawe makini ili wasinaswe na njia ya kufikiri ya ulimwengu. (Kol. 2:6-10) Na Epafra, ambaye inawezekana aliwajua vizuri ndugu na dada kutanikoni, alisali bila kuacha kwamba ‘mwishowe wasimame wakiwa kamili,’ au wakomavu. (Kol. 4:12) Tunaweza kujifunza somo gani? Paulo na Epafra walijua kwamba ili tuendelee kuwa wakomavu tunahitaji kufanya jitihada nyingi na kupata msaada wa Mungu. Walitaka Wakristo Wakolosai waendelee kuwa wakomavu licha ya changamoto walizokuwa wakikabili. w24.04 14:16-17
Jumatano, Septemba 2
Yehova yuko pamoja nasi. Msiwaogope.—Hes. 14:9.
Tunapomwogopa Yehova kwa njia inayofaa, tutampenda sana hivi kwamba hatutafanya jambo lolote ambalo litamkasirisha. Tunajitahidi sana kujifunza tofauti kati ya mambo yaliyo sawa na yasiyo sawa, kati ya ukweli na uwongo, ili tupate kibali cha Yehova. (Met. 2:3-6; Ebr. 5:14) Ikiwa tunawaogopa wanadamu kuliko tunavyomwogopa Mungu, tunaweza kupeperushwa mbali kutoka katika kweli. Fikiria mfano wa wakuu 12 ambao walitumwa kupeleleza nchi ambayo Yehova alikuwa ameahidi kuwapa Waisraeli. Kwa wale wapelelezi kumi, hisia za kuwaogopa Wakanaani zilikuwa na nguvu kuliko upendo wao kwa Yehova. Waliwaambia hivi Waisraeli wenzao: “Hatuwezi kwenda kupigana na watu hao, kwa sababu wana nguvu kuliko sisi.” (Hes. 13:27-31) Kwa maoni ya wanadamu, Wakanaani walikuwa na nguvu. Hilo lilikuwa kweli. Lakini kusema kwamba Waisraeli hangeweza kuwashinda maadui wao kunaonyesha kwamba hawakumfikiria Yehova. w24.07 28:5-6