Jumanne, Septemba 30
Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili, bali pamoja na majaribu hayo ataifanya pia njia ya kutokea ili mweze kuyavumilia.—1 Kor. 10:13.
Ukitafakari sala uliyotoa ulipojiweka wakfu kwa Yehova, utapata nguvu za kushinda kishawishi chochote. Kwa mfano, je, utamchezea kimapenzi mwenzi wa ndoa wa mtu mwingine? Bila shaka hapana! Tayari ulishamwahidi Yehova kwamba hutafanya jambo kama hilo. Ikiwa hutaruhusu tamaa mbaya zisitawi, hutahitaji kupambana baadaye ili kuzing’oa. ‘Utajiepusha’ na “kijia cha waovu.” (Met. 4:14, 15) Ukikumbuka azimio la Yesu la kumpendeza Baba yake, utakataa haraka na kwa uthabiti jambo lolote ambalo unajua halitampendeza Mungu ambaye umejiweka wakfu kwake. (Mt. 4:10; Yoh. 8:29). Ukweli ni kwamba majaribu na vishawishi vinakupa nafasi ya kuonyesha kwamba umeazimia ‘kuendelea kumfuata’ Yesu. Unapofanya hivyo, unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atakusaidia. w24.03 10:8-10
Jumatano, Oktoba 1
Hekima inayotoka juu . . . [iko] tayari kutii.—Yak. 3:17.
Je, wakati mwingine ni vigumu kwako kutii? Mfalme Daudi alikabili changamoto hiyo naye alisali hivi kwa Mungu: “Chochea ndani yangu utayari wa kukutii.” (Zab. 51:12) Daudi alimpenda Yehova. Hata hivyo, wakati mwingine ilikuwa vigumu kwake kutii, na inakuwa hivyo pia kwetu. Kwa nini? Kwanza, tumerithi mwelekeo wa kutotii. Pili, sikuzote Shetani anajaribu kutuchochea tuasi, kama yeye alivyofanya. (2 Kor. 11:3) Tatu, tumezungukwa na ulimwengu huu wenye roho ya uasi, “roho ambayo sasa inafanya kazi katika wana wa kutotii.” (Efe. 2:2) Tunapaswa kujitahidi kushinda mwelekeo wetu wa kutenda dhambi na pia kupinga mkazo wa kutotii unaotoka kwa Ibilisi na ulimwengu huu. Tunapaswa kujitahidi kumtii Yehova na wale ambao amewapatia mamlaka. w23.10 42:1
Alhamisi, Oktoba 2
Lakini wewe umehifadhi divai nzuri mpaka sasa.—Yoh. 2:10.
Tunaweza kujifunza nini kutokana na muujiza wa Yesu wa kugeuza maji kuwa divai? Tunajifunza somo kuhusu unyenyekevu. Yesu hakujigamba kuhusu muujiza huo; kwa kweli, hakujigamba kamwe kuhusu mambo aliyotimiza. Kinyume chake, kwa unyenyekevu, tena na tena alimpa sifa na utukufu Baba yake. (Yoh. 5:19, 30; 8:28) Ikiwa tutamwiga Yesu kwa kuwa wanyenyekevu, hatutajigamba kuhusu mambo tunayotimiza. Acheni tujigambe si kujihusu sisi wenyewe, bali kumhusu Mungu mwenye kustaajabisha ambaye tuna pendeleo la kumtumikia. (Yer. 9:23, 24) Acheni tumpe sifa anazostahili. Isitoshe, hatuwezi kamwe kutimiza jambo lolote zuri bila msaada wa Yehova? (1 Kor. 1:26-31) Tunapokuwa wanyenyekevu, hatujitafutii sifa kwa mambo mazuri tunayowafanyia wengine. Tunaridhika kujua kwamba Yehova anaona na kuthamini mambo tunayofanya. (Linganisha Mathayo 6:2-4; Ebr. 13:16) Kwa kweli, tunamfurahisha Yehova tunapomwiga Yesu kwa kuonyesha unyenyekevu.—1 Pet. 5:6. w23.04 15:9, 11-12