Alhamisi, Aprili 23
Kristo Yesu alikuja ulimwenguni ili kuwaokoa watenda dhambi.—1 Tim. 1:15.
Wazia kwamba umempatia mtu unayempenda zawadi ya pekee ambayo ni maridadi na yenye manufaa. Ungevunjika moyo sana ikiwa mtu huyo angeiweka tu kwenye sanduku na kutoifikiria tena! Kwa upande mwingine, bila shaka ungefurahi ikiwa mtu huyo angeitumia vizuri na kukushukuru kwa zawadi hiyo. Mfano huo unatufundisha nini? Yehova amemtoa Mwana wake kwa ajili yetu. Ni lazima Yehova anafurahi sana tunapoonyesha kwamba tunashukuru kwa zawadi hiyo yenye thamani na kwa upendo wake uliomchochea kuandaa fidia! (Yoh. 3:16; Rom. 5:7, 8.) Hata hivyo, kadiri muda unavyopita tunaweza kuanza kutoithamini zawadi ya fidia. Hilo linaweza kufananishwa na kuiweka kwenye sanduku zawadi ya Mungu. Tunafurahi kwamba tuna zawadi hiyo, lakini tumeiweka mahali ambapo hatuioni wala kuifikiria. Ili kuzuia jambo hilo, ni lazima tuyafikirie kwa ukawaida mambo yote ambayo Mungu na Kristo wametufanyia. w25.01 26 ¶1-2
Ijumaa, Aprili 24
Tafakari mambo haya; zama katika hayo, ili maendeleo yako yaonekane wazi kwa watu wote.—1 Tim. 4:15.
Ndugu anayestahili kuwa mzee si mtu aliyegeuka hivi karibuni. Ingawa huhitaji kuwa umebatizwa kwa miaka mingi, unahitaji muda ili kuwa Mkristo mkomavu. Kabla ya kuwekwa rasmi kuwa mzee, lazima uonyeshe kwamba kama Yesu, wewe ni mnyenyekevu na umeridhika kumngojea Yehova akupatie mgawo wowote. (Mt. 20:23; Flp. 2:5-8) Unaweza kuthibitisha kwamba wewe ni “mshikamanifu” kwa kushikamana na Yehova na viwango vyake vya uadilifu na kwa kufuata miongozo inayotolewa na tengenezo lake. Maandiko yanaonyesha wazi kwamba ni lazima mwangalizi awe mwenye uwezo wa kufundisha. Je, hilo linamaanisha kwamba ni lazima uwe msemaji mwenye uwezo wa pekee? Hapana. Ingawa wazee wengi wenye kustahili si wasemaji wenye uwezo wa pekee, wanafundisha kwa njia yenye matokeo katika huduma na kwenye ziara za uchungaji. w24.11 23-24 ¶14-15
Jumamosi, Aprili 25
Ninazipenda amri zako Kuliko dhahabu, hata dhahabu bora.—Zab. 119:127.
Unaposoma andiko ambalo hulielewi vizuri, fanya utafiti. Kisha, siku hiyo yote, tafakari kuhusu mambo mapya ambayo umejifunza na yale uliyojifunza kumhusu Yehova, Mwana wake, na upendo wao kukuelekea. (Zab. 119:97, maelezo ya chini) Usivunjike moyo ikiwa hutapata jambo jipya au lenye kusisimua kila mara unapojifunza au kufanya utafiti. Kwa njia ya mfano, wewe ni kama mtu anayetafuta dhahabu. Kwa subira, wale wanaotafuta dhahabu hutumia saa au siku nyingi kabla ya kupata hata kipande kidogo sana cha dhahabu. Hata hivyo, wanaendelea kutafuta kwa sababu kila kipande cha dhahabu ni chenye thamani kwao. Kwa kweli, kila hazina ya kweli ya Biblia ni yenye thamani kubwa hata zaidi! (Met. 8:10) Hivyo, uwe na subira na ushikamane na ratiba yako ya usomaji wa Biblia.—Zab. 1:2. w25.01 25 ¶14-15