Jumapili, Aprili 12
Ninakusifu, Ee Yehova Mungu wangu, kwa moyo wangu wote, nami nitalitukuza jina lako milele.—Zab. 86:12.
Yehova ni mwenye rehema na huruma. (Zab. 103:13; Isa. 49:15) Ni mwenye hisia mwenzi; tunapoumia, yeye pia anaumia. (Zek. 2:8) Anafanya iwe rahisi kwetu kumkaribia akiwa Rafiki yetu. (Zab. 25:14; Mdo. 17:27) Na ni mnyenyekevu; yeye “huinama chini ili atazame mbingu na dunia, akimwinua mtu wa hali ya chini kutoka mavumbini.” (Zab. 113:6, 7) Hivyo basi, mtu anawezaje kukataa kumpa utukufu Mungu wetu mkuu? Tunampa Yehova utukufu kwa sababu tunataka wengine wamjue. Watu wengi hawajui ukweli kumhusu Yehova. Kwa nini? Kwa sababu Shetani amepofusha akili zao kwa kueneza uwongo mbaya kumhusu. (2 Kor. 4:4) Shetani amefanya watu waamini kwamba Yehova ni mwenye kulipiza kisasi, hajali, na anasababisha matatizo mengi yanayofanya watu wateseke. Lakini tunajua ukweli kumhusu Mungu wetu! Tuna fursa ya kuwasaidia watu wasahihishe maoni yao yasiyo ya kweli na hivyo kumpa Yehova utukufu.—Isa. 43:10. w25.01 3 ¶6-7
Jumatatu, Aprili 13
Shetani [anaipotosha] dunia nzima inayokaliwa.—Ufu. 12:9.
Ingawa Yesu, Mwana wa Mungu, alikuwa mkamilifu na alifanya miujiza mingi mikubwa, Shetani aliwatumia baadhi ya watu kueneza uwongo mwingi kumhusu. Kwa mfano, viongozi wa dini waliwaambia watu kwamba nguvu za kuwaondoa roho waovu ambazo Yesu alikuwa nazo, zilitoka kwa “mtawala wa roho waovu.” (Marko 3:22) Yesu alipokuwa akihukumiwa, viongozi wa dini walimshtaki kuwa mkufuru na wakaushawishi umati wa watu uombe Yesu auawe. (Mt. 27:20) Baadaye, wafuasi wa Kristo walipokuwa wakihubiri habari njema, wale waliowapinga ‘wakawachochea watu na kuwafanya wawachukie’ Wakristo na kuwatesa. (Mdo. 14:2, 19) Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Desemba 1, 1998 linasema hivi kuhusu Matendo 14:2: “Kwa kutoridhika na kukataa kwao wenyewe ujumbe huo, Wayahudi wapinzani walianza kampeni ya mashtaka yasiyoweza kuthibitishwa, wakijaribu kuwafanya wasio Wayahudi wawabague Wakristo.” Leo, Shetani bado anaendelea ‘kuipotosha dunia nzima inayokaliwa. w24.04 11 ¶15-16
Jumanne, Aprili 14
Je, Mwamuzi wa dunia yote hatatenda jambo la haki?—Mwa. 18:25.
Wakati ujao wa milele wa mtu hautegemei anakufa wakati gani. Yehova ni Mwamuzi mkamilifu—anafanya maamuzi kwa uadilifu na haki. (Zab. 33:4, 5) Tunaweza kuwa na uhakika kwamba “Mwamuzi wa dunia yote” atatenda jambo la haki. Pia, inafaa kufikia mkataa kwamba wakati ujao wa milele wa mtu hautegemei mahali anapoishi. Yehova hawezi kamwe kuwahukumu mamilioni ya watu kuwa “mbuzi” kwa sababu tu wanaishi katika nchi ambazo hawakuwa na fursa ya kusikia ujumbe wa Ufalme. (Mt. 25:46) Mwamuzi wa dunia yote ambaye ni mwadilifu anawajali watu hao kuliko hata sisi tunavyowajali. Hatujui jinsi Yehova atakavyoongoza mambo wakati wa dhiki kuu. Huenda baadhi ya watu hao watapata nafasi ya kujifunza kumhusu Yehova, kuonyesha imani kwake, na kuchukua msimamo upande wa Yehova atakapojitakasa mwenyewe mbele ya mataifa yote.—Eze. 38:16. w24.05 12 ¶14-15