Mwanzo
42 Mwishowe Yakobo akaona kwamba kuna nafaka Misri.+ Kisha akawauliza wanawe: “Kwa nini mnaendelea kutazamana?” 2 Tena akawaambia: “Tazama nimesikia kwamba kuna nafaka Misri.+ Shukeni huko mkatununulie nafaka, tupate kuendelea kuishi ili tusife.” 3 Basi ndugu+ kumi za Yosefu wakashuka waende kununua nafaka Misri. 4 Lakini Yakobo hakumruhusu Benyamini,+ ndugu ya Yosefu, aende pamoja na wale ndugu zake wengine, kwa sababu alisema: “Ili tukio lenye kufisha lisimpate.”+
5 Kwa hiyo wana wa Israeli wakafuatana na wengine waliokuwa wakienda kununua, kwa sababu kulikuwa na njaa katika nchi ya Kanaani.+ 6 Na Yosefu ndiye aliyekuwa mwenye mamlaka juu ya nchi hiyo.+ Ndiye aliyewauzia watu wote wa dunia.+ Basi ndugu za Yosefu wakaja na kumwinamia kifudifudi.+ 7 Yosefu alipowaona ndugu zake, akawatambua mara moja, lakini akajifanya asitambulike kwao.+ Basi, akaongea nao kwa ukali na kusema: “Mmetoka wapi?” nao wakajibu: “Tumetoka nchi ya Kanaani ili kununua vyakula.”+
8 Hivyo Yosefu akawatambua ndugu zake, lakini wao hawakumtambua. 9 Papo hapo Yosefu akakumbuka ndoto alizokuwa ameota juu yao,+ naye akaendelea kuwaambia: “Ninyi ni wapelelezi! Mmekuja kuona hali ya ukosefu wa ulinzi wa nchi hii!”+ 10 Kisha wakamwambia: “Sivyo, bwana wangu,+ bali watumishi wako+ wamekuja kununua vyakula. 11 Sisi sote ni wana wa mtu mmoja tu. Sisi ni watu wanyoofu. Watumishi wako si wapelelezi.”+ 12 Lakini akawaambia: “Sivyo! Kwa sababu ninyi mmekuja kuona hali ya ukosefu wa ulinzi wa hii nchi!”+ 13 Ndipo wakamwambia: “Watumishi wako ni ndugu kumi na wawili.+ Sisi ni wana wa mtu mmoja+ tu katika nchi ya Kanaani; na tazama, yule mdogo zaidi yuko na baba yetu leo,+ naye yule mwingine hayuko.”+
14 Hata hivyo, Yosefu akawaambia: “Ni kama nilivyowaambia, nikisema: ‘Ninyi ni wapelelezi!’ 15 Hivyo ndivyo mtakavyojaribiwa. Kama Farao anavyoishi, hamtatoka hapa mpaka ndugu yenu mdogo atakapokuja hapa.+ 16 Mtumeni mmoja wenu akamlete ndugu yenu, huku ninyi mkiwa mmefungwa, ili maneno yenu yajaribiwe kama ni ya kweli.+ Ikiwa sivyo, basi, kama Farao anavyoishi, ninyi ni wapelelezi.” 17 Kisha akawatia pamoja kifungoni kwa siku tatu.
18 Baada ya hayo Yosefu akawaambia siku ya tatu. “Fanyeni hili ili mwendelee kuishi. Mimi ninamwogopa+ Mungu wa kweli. 19 Ikiwa ninyi ni wanyoofu, acheni mmoja wa ndugu zenu afungwe katika nyumba yenu ya kifungo,+ lakini ninyi wengine mwende, chukueni nafaka kwa sababu ya njaa iliyo katika nyumba zenu.+ 20 Kisha mtaniletea ndugu yenu mdogo, ili maneno yenu yaonekane kuwa yenye kutegemeka; nanyi hamtakufa.”+ Basi wakafanya hivyo.
21 Nao wakaanza kusemezana: “Bila shaka tuna hatia kuhusiana na ndugu yetu,+ kwa sababu tuliona nafsi yake ikitaabika alipotuomba kwa bidii tumwonee huruma, lakini sisi hatukusikiliza. Ndiyo sababu taabu hii imetupata.”+ 22 Kisha Rubeni akawajibu, akawaambia: “Je, sikuwaambia, ‘Msimtendee mtoto huyo dhambi,’ lakini hamkusikia?+ Na sasa damu yake inadaiwa tena.”+ 23 Lakini wao hawakujua kwamba Yosefu alikuwa akisikiliza, kwa sababu kulikuwako mtafsiri kati yao. 24 Basi akajitenga nao, akaanza kulia.+ Kisha akarudi kwao, akaongea nao, akamchukua Simeoni+ kati yao na kumfunga mbele ya macho yao.+ 25 Baada ya hayo Yosefu akatoa amri, nao wakavijaza kabisa vyombo vyao nafaka. Pia, walipaswa kurudisha pesa za watu hao kwenye gunia la kila mmoja wao+ na kuwapa vyakula kwa ajili ya safari.+ Ndivyo walivyofanyiwa.
26 Basi wakapakia nafaka yao juu ya punda zao na kuondoka huko. 27 Mmoja wao alipofungua gunia lake ili ampe punda wake chakula wakiwa mahali pa kukaa usiku,+ akaona pesa zake, na tazama, zilikuwa katika kinywa cha mfuko wake.+ 28 Basi akawaambia ndugu zake: “Pesa zangu zimerudishwa na tazama, ziko hapa mfukoni mwangu!” Ndipo mioyo yao ikazimia, hivi kwamba wakageukiana wakitetemeka,+ wakisema: “Ni nini hili Mungu ametutendea?”+
29 Mwishowe wakafika kwa Yakobo baba yao katika nchi ya Kanaani, wakamwambia mambo yote yaliyokuwa yamewapata, wakisema: 30 “Bwana wa nchi hiyo alisema nasi kwa ukali,+ kwa kuwa alituwazia kuwa sisi ni watu wanaoipeleleza nchi.+ 31 Lakini tukamwambia, ‘Sisi ni watu wanyoofu.+ Sisi si wapelelezi. 32 Sisi ni ndugu kumi na wawili,+ wana wa baba yetu.+ Mmoja hayuko,+ na yule mdogo leo yuko na baba yetu katika nchi ya Kanaani.’+ 33 Lakini huyo mtu aliye bwana wa nchi hiyo akatuambia,+ ‘Kwa njia hii nitajua kama ninyi ni wanyoofu:+ Mmoja wa ndugu zenu akae nami.+ Kisha chukueni vitu fulani kwa sababu ya njaa iliyo katika nyumba zenu, mwende.+ 34 Nanyi mkamlete ndugu yenu mdogo, ili nijue kwamba ninyi si wapelelezi bali ni watu wanyoofu. Nitawarudishia ndugu yenu, nanyi mnaweza kufanya biashara yenu nchini.’”+
35 Ikawa kwamba walipokuwa wakitoa vilivyokuwa ndani ya magunia yao tazama, kifurushi cha pesa cha kila mmoja wao kilikuwa katika gunia lake. Na wao na baba yao pia wakapata kuona vifurushi vyao vya pesa, nao wakaogopa. 36 Kisha Yakobo baba yao akawaambia: “Mmefanya mimi nifiwe!+ Yosefu hayuko naye Simeoni hayuko,+ na Benyamini mtamchukua! Mambo yote hayo yamenijia mimi!” 37 Lakini Rubeni akamwambia baba yake: “Nisipomrudisha kwako uwaue wanangu wawili.+ Nipe yeye, nami ndimi nitakayemrudisha kwako.”+ 38 Lakini, akasema: “Mwanangu hatashuka kwenda nanyi, kwa sababu ndugu yake amekufa naye amebaki peke yake.+ Tukio lenye kufisha likimpata katika njia mtakayoiendea, basi bila shaka mtazishusha mvi zangu kwa huzuni mpaka katika Kaburi.”*+