Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • cf sura 10 kur. 114-125
  • “Imeandikwa”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Imeandikwa”
  • ‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Alinukuu Neno la Mungu
  • Kulitetea Neno la Mungu
  • Kufafanua Neno la Mungu
  • “Niliweka Kiolezo kwa Ajili Yenu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Je! Wewe ni Mwenye Matokeo Katika Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Ushike Sana Uzima Ulio Kweli Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
  • Yesu Kristo Ni Nani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
Pata Habari Zaidi
‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
cf sura 10 kur. 114-125

SURA YA KUMI

“Imeandikwa”

Yesu akisoma kitabu cha kukunjwa katika sinagogi.

“Leo andiko hili . . . limetimia”

1-3. Yesu anataka watu wa Nazareti watambue jambo gani muhimu, naye anatoa uthibitisho gani?

NI MWANZONI mwa huduma ya Yesu. Amerudi Nazareti, mji wa nyumbani. Lengo lake ni kuwasaidia watu watambue jambo hili: Yeye ndiye Masihi aliyeahidiwa tangu zamani za kale! Anatoa uthibitisho gani?

2 Huenda wengi wangetazamia afanye muujiza. Wamesikia kuhusu miujiza ambayo Yesu amefanya. Hata hivyo, pindi hii hafanyi muujiza wowote. Badala yake, anaingia katika sinagogi kama ilivyo desturi yake. Anasimama ili asome, naye anapewa kitabu cha kukunjwa cha Isaya. Ni kitabu kirefu ambacho inaelekea kimekunjwa katika vijiti viwili, naye Yesu anakikunjua kwa makini kutoka upande mmoja hadi mwingine mpaka anapopata fungu la maneno anayotafuta. Kisha, anasoma kwa sauti maneno ambayo sasa yanapatikana katika Isaya 61:1-3.​—Luka 4:16-19.

3 Bila shaka, wasikilizaji hao wanayajua maneno hayo. Ni unabii kumhusu Masihi. Kila mtu katika sinagogi anamtazama Yesu. Kila mtu amenyamaza na hakuna anayesema chochote. Kisha, Yesu anaanza kufafanua waziwazi: “Leo andiko hili ambalo mmetoka kusikia limetimia.” Wasikilizaji wanastaajabishwa na maneno yake yenye kuvutia sana, lakini inaonekana kwamba wengi bado wanataka kuona ishara fulani ya pekee. Badala ya kutoa ishara, kwa ujasiri Yesu anatumia mfano wa Kimaandiko kufunua ukosefu wao wa imani. Muda mfupi baadaye, watu wa Nazareti wanajaribu kumuua!—Luka 4:20-30.

4. Yesu alituwekea mfano gani katika huduma yake, na tutachunguza nini katika sura hii?

4 Katika kisa hicho, Yesu alifanya jambo ambalo aliendelea kufanya katika huduma yake yote. Alitegemea sana Neno la Mungu lililoongozwa na roho. Ni kweli kwamba miujiza yake ilisaidia sana kuthibitisha kuwa roho ya Mungu ilikuwa pamoja naye. Hata hivyo, hakuna chochote machoni pa Yesu kilichokuwa muhimu zaidi kuliko Maandiko Matakatifu. Acheni tuchunguze mfano aliotuwekea kuhusu jambo hilo. Tutaona jinsi Bwana wetu alivyonukuu, alivyolitetea, na kulifafanua Neno la Mungu.

Alinukuu Neno la Mungu

5. Yesu aliazimia kuwajulisha wasikilizaji wake nini, na alithibitishaje ukweli wa maneno yake?

5 Yesu alitaka watu wajue chanzo cha ujumbe wake. Alisema: “Mambo ninayofundisha si yangu, bali ni ya yule aliyenituma.” (Yohana 7:16) Pindi nyingine, alisema: “Sifanyi jambo lolote kwa uamuzi wangu mwenyewe; bali mambo ambayo Baba amenifundisha, ndiyo ninayosema.” (Yohana 8:28) Pia, alisema: “Mambo ninayowaambia sisemi kwa kujitungia, bali Baba ambaye hukaa katika muungano pamoja nami anafanya kazi zake.” (Yohana 14:10) Njia moja ambayo Yesu alithibitisha ukweli wa maneno hayo ni kwa kunukuu tena na tena Neno la Mungu lililoandikwa.

6, 7. (a) Yesu alinukuu Maandiko ya Kiebrania kadiri gani, na kwa nini hilo ni jambo linalopendeza? (b) Njia ya Yesu ya kufundisha ilitofautianaje na ile ya waandishi?

6 Kuchunguza kwa makini maneno ya Yesu yaliyoandikwa kunafunua kwamba alinukuu moja kwa moja au kwa njia isiyo ya moja kwa moja zaidi ya nusu ya vitabu vya Maandiko ya Kiebrania. Huenda hilo lisionekane kuwa jambo lenye kupendeza. Labda unaweza kujiuliza, katika kazi ya kufundisha na kuhubiri hadharani aliyofanya kwa miaka mitatu na nusu, kwa nini hakunukuu vitabu vyote vilivyoongozwa na roho vilivyokuwepo wakati huo? Kwa kweli, huenda alifanya hivyo. Kumbuka kwamba ni sehemu ndogo tu ya maneno na matendo ya Yesu yaliyoandikwa. (Yohana 21:25) Kwa kweli, unaweza kutumia muda mfupi tu kusoma kwa sauti maneno yote ya Yesu yaliyoandikwa. Sasa wazia kwamba unazungumza kumhusu Mungu na Ufalme wake kwa saa chache na kwa kipindi hicho kifupi unukuu zaidi ya nusu ya vitabu vya Maandiko ya Kiebrania! Huenda isiwe rahisi kufanya hivyo. Isitoshe, mara nyingi Yesu hakuwa na vitabu vya kukunjwa. Wakati wa Mahubiri yake ya Mlimani yanayojulikana sana, alinukuu moja kwa moja au kwa njia isiyo ya moja kwa moja Maandiko mengi ya Kiebrania kutoka katika kumbukumbu yake!

7 Nukuu za Yesu zinaonyesha kwamba aliheshimu sana Neno la Mungu. Wasikilizaji wake ‘walishangazwa na njia yake ya kufundisha, kwa maana alikuwa akiwafundisha kama mtu mwenye mamlaka, si kama waandishi.’ (Marko 1:22) Waandishi walipofundisha, walipenda kutaja sheria ya mdomo, wakiwanukuu marabi wenye elimu wa nyakati zilizopita. Kamwe Yesu hakunukuu sheria ya mdomo wala kuwanukuu marabi fulani. Badala yake, aliliona Neno la Mungu kuwa lenye mamlaka kuu. Alipokuwa akiwafundisha wafuasi wake na kusahihisha maoni yao yasiyofaa, Yesu alisema hivi tena na tena: “Imeandikwa.”

8, 9. (a) Yesu alitetea jinsi gani mamlaka ya Neno la Mungu aliposafisha hekalu? (b) Ni katika njia gani viongozi wa dini walilivunjia heshima Neno la Mungu hekaluni?

8 Yesu aliposafisha hekalu huko Yerusalemu, alisema: “Imeandikwa, ‘Nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala,’ lakini ninyi mnaifanya kuwa pango la wanyang’anyi.” (Mathayo 21:12, 13; Isaya 56:7; Yeremia 7:11) Siku moja kabla, alikuwa amefanya miujiza mingi yenye kustaajabisha akiwa huko. Wavulana wadogo waliovutiwa sana, walianza kumsifu. Hata hivyo, viongozi wa dini walimuuliza Yesu kwa ghadhabu ikiwa alisikia mambo ambayo watoto hao walisema. Alijibu: “Ndiyo. Je, hamkusoma jambo hili, ‘Kutoka katika vinywa vya watoto wadogo na wanaonyonya, umetoa sifa’?” (Mathayo 21:16; Zaburi 8:2) Yesu alitaka watu hao wajue kwamba jambo lililokuwa likitendeka linapatana na Neno la Mungu.

9 Baadaye viongozi hao wa dini walikutana, kisha wakamfuata Yesu na kumuuliza: “Unafanya mambo haya kwa mamlaka gani?” (Mathayo 21:23) Yesu alikuwa ametaja wazi kabisa Chanzo cha mamlaka yake. Hakuwa amejitungia wala kubuni mafundisho mapya. Alitumia tu mambo ambayo Neno la Baba yake lililoongozwa na roho linasema. Hivyo basi, makuhani na waandishi hao walikuwa wakimvunjia heshima Yehova na Neno lake. Walistahili kabisa kushutumiwa, na Yesu alifanya hivyo alipofunua nia zao mbaya.​—Mathayo 21:23-46.

10. Tunawezaje kuiga jinsi Yesu alivyotumia Neno la Mungu, na tuna vifaa gani ambavyo Yesu hakuwa navyo?

10 Kama Yesu, Wakristo wa kweli leo wanalitegemea Neno la Mungu katika huduma. Mashahidi wa Yehova wanajulikana ulimwenguni pote kwa bidii yao ya kuwahubiria wengine ujumbe kutoka katika Biblia. Machapisho yetu hunukuu na kurejelea Biblia. Pia, tunafanya hivyo katika huduma yetu kwa kuhakikisha kwamba tunayatumia Maandiko kila wakati tunapozungumza na watu. (2 Timotheo 3:16) Tunafurahi sana mtu anapoturuhusu tuisome Biblia na kuzungumzia faida na maana ya Neno la Mungu! Ingawa hatuwezi kukumbuka mambo kikamili kama Yesu alivyofanya, tuna vifaa vingi ambavyo Yesu hakuwa navyo. Zaidi tu ya kuwa na Biblia nzima inayoendelea kuchapishwa katika lugha nyingi, tuna vifaa vingi vinavyotegemea Biblia vinavyotusaidia kupata mstari wowote ambao huenda tukatafuta. Na tuazimie kuendelea kuinukuu Biblia na kuwaelekeza watu katika Biblia nyakati zote!

Kulitetea Neno la Mungu

11. Kwa nini Yesu alihitaji kulitetea Neno la Mungu mara nyingi?

11 Yesu aliona kwamba Neno la Mungu lilitumiwa vibaya mara nyingi, lakini hilo halikumshangaza. Alipokuwa akisali, Yesu alimwambia hivi Baba yake: “Neno lako ni kweli.” (Yohana 17:17) Yesu alijua vizuri kwamba Shetani, “mtawala wa ulimwengu,” ni “mwongo na ndiye baba ya uwongo.” (Yohana 8:44; 14:30) Alipopinga majaribu ya Shetani, Yesu aliyanukuu Maandiko mara tatu. Shetani alinukuu mstari mmoja kutoka katika kitabu cha Zaburi, akiutumia vibaya kimakusudi, naye Yesu akamjibu kwa kulitetea Neno la Mungu lisitumiwe vibaya.​—Mathayo 4:6, 7.

12-14. (a) Viongozi wa dini walionyeshaje kwamba hawaiheshimu Sheria ya Musa? (b) Yesu alilitetea Neno la Mungu jinsi gani?

12 Mara nyingi, Yesu alitetea Maandiko Matakatifu ili yasitumiwe vibaya au kupotoshwa. Walimu wa dini wa siku zake walilipotosha Neno la Mungu. Walikazia sana kufuata mambo madogo-madogo zaidi ya Sheria ya Musa lakini hawakutumia kanuni zilizotegemeza sheria hizo. Kwa kufanya hivyo, hawakuwasaidia watu kumwabudu Mungu katika njia inayofaa badala yake, waliwatia moyo watu wahangaikie zaidi jinsi wanavyoonekana mbele za wengine badala ya kuhangaikia mambo mazito zaidi, kama vile haki, rehema, na uaminifu. (Mathayo 23:23) Yesu aliitetea Sheria ya Mungu jinsi gani?

13 Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alitumia tena na tena maneno “mlisikia kwamba ilisemwa” kabla ya kutaja amri iliyo katika Sheria ya Musa. Kisha, angesema “lakini ninawaambia” halafu angeeleza kanuni iliyokazia mambo mazito zaidi kuliko tu kushika Sheria kijuujuu. Je, alikuwa akiipinga Sheria? Hapana, alikuwa akiitetea. Kwa mfano, watu waliijua vizuri amri iliyosema “Usiue.” Lakini Yesu aliwaambia kwamba kumchukia mtu ni kuvunja kanuni ya sheria hiyo. Vivyo hivyo, kusitawisha tamaa kuelekea mtu ambaye si mwenzi wako ni kuvunja kanuni inayotegemeza sheria ya Mungu inayokataza uzinzi.​—Mathayo 5:17, 18, 21, 22, 27-39.

14 Mwishowe, Yesu alisema: “Mlisikia kwamba ilisemwa: ‘Lazima umpende jirani yako na kumchukia adui yako.’ Hata hivyo, ninawaambia: Endeleeni kuwapenda adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi.” (Mathayo 5:43, 44) Je, amri inayosema ‘mchukie adui yako’ ilikuwa katika Neno la Mungu? Hapana, hilo lilikuwa fundisho ambalo viongozi wa dini walitunga. Walitumia mawazo ya wanadamu kudhoofisha Sheria kamilifu ya Mungu. Kwa ujasiri, Yesu alitetea Neno la Mungu lisiathiriwe na mapokeo ya wanadamu.​—Marko 7:9-13.

15. Yesu aliiteteaje Sheria ya Mungu ilipofanywa ionekane kuwa yenye kudai mambo mengi au yenye masharti magumu?

15 Pia, viongozi wa dini waliitumia vibaya Sheria ya Mungu kwa kuifanya ionekane kuwa inadai mambo mengi, au ina masharti magumu. Wanafunzi wa Yesu walipokata masuke ya nafaka walipokuwa wakipita katikati ya shamba, Mafarisayo fulani walidai kwamba wanafunzi hao wanaivunja sheria ya Sabato. Yesu alitumia mfano wa Kimaandiko kutetea Neno la Mungu dhidi ya maoni hayo yasiyofaa. Alirejelea Andiko moja tu linalozungumzia jinsi mikate ya wonyesho ya hekalu ilivyotumiwa nje ya patakatifu Daudi na wanaume wake wenye njaa walipokula. Yesu aliwaonyesha Mafarisayo hao kwamba hawakuelewa jinsi Yehova alivyo mwenye rehema na huruma.​—Marko 2:23-27.

16. Viongozi wa dini waliibadili amri ya Musa kuhusu talaka jinsi gani, na Yesu alisema nini kuhusu jambo hilo?

16 Pia, viongozi wa dini walibuni njia za kuepuka kutii Sheria ya Mungu. Kwa mfano, Sheria ilimruhusu mtu kumtaliki mke wake ikiwa angeona “jambo fulani lisilofaa” kwake, huenda ni tatizo zito lililoiletea aibu nyumba yake. (Kumbukumbu la Torati 24:1) Hata hivyo, kufikia siku za Yesu, viongozi wa dini walitumia sheria hiyo kuwa kisingizio cha kumruhusu mwanamume kumtaliki mke wake kwa sababu yoyote, kama vile kuunguza chakula!a Yesu alionyesha kwamba walikuwa wamepotosha sana maneno ya Musa yaliyoongozwa na roho. Kisha, akaonyesha wazi mpango wa awali wa Yehova kuhusu ndoa, yaani, kuwa na mke mmoja, na kuonyesha kwamba uzinzi ndio msingi pekee wa talaka.​—Mathayo 19:3-12.

17. Wakristo wanawezaje kumwiga Yesu wanapolitetea Neno la Mungu leo?

17 Vivyo hivyo, wafuasi wa Kristo leo wanachochewa kutetea Maandiko Matakatifu dhidi ya uwongo. Viongozi wa dini wanaposema kwamba viwango vya maadili vya Neno la Mungu vimepitwa na wakati, ni kana kwamba wanasema Biblia ni kitabu cha zamani ambacho hakiwezi kutusaidia maishani. Pia, Biblia inatumiwa vibaya dini inapofundisha mafundisho ya uwongo na kuyafanya yaonekane kuwa yametoka katika Biblia. Tunaliona kuwa pendeleo kutetea Neno la Mungu la kweli lililo safi, kama vile tunapothibitisha kwamba Mungu si Utatu. (Kumbukumbu la Torati 4:39) Wakati huohuo, tunalitetea kwa busara, upole na heshima kubwa.​—1 Petro 3:15.

Kufafanua Neno la Mungu

18, 19. Ni mifano gani inayoonyesha kwamba Yesu alikuwa na uwezo wa pekee wa kufafanua Neno la Mungu?

18 Yesu alikuwa mbinguni Maandiko ya Kiebrania yalipoandikwa. Bila shaka, alifurahi sana kupata pendeleo la kuja duniani ili kuwafundisha watu Neno la Mungu! Kwa mfano, fikiria siku aliyokutana na wanafunzi wake wawili kwenye barabara ya kwenda Emau baada ya ufufuo wake. Kabla ya kumtambua, walimwambia jinsi walivyohuzunika na kuchanganyikiwa kwa sababu ya kifo cha Bwana wao mpendwa. Alifanya nini? Aliwafafanulia “kuanzia Musa na Manabii wote, mambo yote ambayo Maandiko yalisema kumhusu.” Waliitikiaje? Baadaye waliambiana: “Je, mioyo yetu haikuwa ikiwaka alipokuwa akizungumza nasi barabarani, na alipokuwa akitufungulia Maandiko waziwazi?”​—Luka 24:15-32.

19 Baadaye siku hiyo, Yesu alikutana na mitume wake na wengine. Ona kile alichowafanyia: “Akafungua akili zao ili waelewe kabisa maana ya Maandiko.” (Luka 24:45) Bila shaka, tukio hilo lenye kufurahisha liliwakumbusha zile pindi nyingi sana ambazo Yesu aliwafanyia jambo kama hilo, wao na wengine ambao walimsikiliza. Mara nyingi, alinukuu maandiko yaliyojulikana sana na kuyaeleza kwa njia ambayo ilichochea sana akili za wasikilizaji wake, hivi kwamba walipata uelewaji mpya na wenye kina wa Neno la Mungu.

20, 21. Yesu alifafanua kwa njia gani maneno ambayo Yehova alimwambia Musa kwenye kichaka kilichokuwa kikiwaka moto?

20 Pindi moja kama hiyo, Yesu alikuwa akizungumza na kikundi cha Masadukayo. Walikuwa kikundi cha makuhani Wayahudi ambao walijitenga na dini ya Kiyahudi, nao hawakuamini ufufuo. Yesu aliwaambia: “Kuhusu ufufuo wa wafu, je, hamkusoma mliloambiwa na Mungu, aliposema: ‘Mimi ni Mungu wa Abrahamu na Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo’? Yeye si Mungu wa wafu, bali wa walio hai.” (Mathayo 22:31, 32) Hilo ni andiko walilolielewa vizuri sana, ambalo liliandikwa na Musa, mtu ambaye Masadukayo walimheshimu sana. Hata hivyo, je, unaona jinsi maneno ya Yesu yalivyokuwa na matokeo?

21 Musa alizungumza na Yehova mwaka wa 1514 hivi K.W.K., kwenye kichaka kilichokuwa kikiwaka moto. (Kutoka 3:2, 6) Kufikia wakati huo, miaka 329 ilikuwa imepita tangu Abrahamu afe, miaka 224 tangu Isaka afe, na miaka 197 tangu Yakobo afe. Hata hivyo, Yehova alisema: “Mimi ni” Mungu wao. Masadukayo hao walijua kwamba Yehova si kama mungu wa kipagani wa wafu anayetawala ulimwengu wa wafu. Yeye ni Mungu wa “walio hai,” kama Yesu alivyosema. Hilo linamaanisha nini? Yesu alimalizia kwa kusema hivi kwa usadikisho: “Kwake, wote wako hai.” (Luka 20:38) Watumishi wapendwa wa Yehova ambao wamekufa wako salama katika kumbukumbu yake isiyo na mipaka na isiyoweza kufutika. Hivyo, kusudi la Yehova la kuwafufua watu hao ni hakika sana hivi kwamba inaweza kusemwa wako hai. (Waroma 4:16, 17) Je, huo si ufafanuzi wenye kupendeza wa Neno la Mungu? Basi, haishangazi kwamba ‘umati ulishangaa’!—Mathayo 22:33.

22, 23. (a) Tunawezaje kumwiga Yesu tunapofafanua Neno la Mungu? (b) Tutachunguza nini katika sura inayofuata?

22 Leo, Wakristo wana pendeleo la kuiga jinsi Yesu alivyofafanua Neno la Mungu. Ingawa hatuna akili kamilifu, mara nyingi tunapata nafasi ya kuwaonyesha wengine andiko ambalo tayari wanalijua na kuwaeleza mambo fulani kulihusu ambayo huenda hawakuwa wameyafikiria. Kwa mfano, huenda wamekuwa wakirudia-rudia maneno “Jina lako litukuzwe” na “Ufalme wako uje” maisha yao yote, nao hawajui jina la Mungu au Ufalme wake ni nini. (Mathayo 6:9, 10, Union Version) Tunapata pendeleo kubwa sana mtu anapoturuhusu kufafanua kweli hizo za Biblia kwa njia rahisi na iliyo wazi!

23 Kunukuu Neno la Mungu, kulitetea, na kulifafanua ni kati ya njia kuu za kuiga ustadi wa Yesu wa kuwafundisha wengine kweli. Tutachunguza njia fulani zenye matokeo ambazo Yesu alitumia kufikia mioyo ya wasikilizaji wake alipowafundisha kweli za Biblia.

a Mwanahistoria wa karne ya kwanza Yosefo, Farisayo aliyemtaliki mke wake, alisema kwamba talaka iliruhusiwa “kwa sababu yoyote ile (na wanaume wanadai kwamba kuna sababu nyingi).”

Unawezaje Kumfuata Yesu?

  • Kwa nini tunapaswa kuwa waangalifu tusitangulize maoni au mapokeo ya wanadamu badala ya Neno la Mungu?​—Mathayo 15:2-11.

  • Kwa nini ni jambo la hekima kutumia Biblia tunapojibu maswali?​—Luka 10:25-28.

  • Tunawezaje kuiga utayari wa Yesu wa kuruhusu Neno la Mungu la kinabii liongoze maisha yake na maamuzi yake?​—Luka 18:31-34; 22:37.

  • Imani yetu inaposhambuliwa, kwa nini tunapaswa kuitetea kwa kutumia Neno la Mungu?​—Yohana 10:31-39.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki