SURA YA KUMI NA MOJA
“Hakuna Mtu Mwingine Yeyote Ambaye Amewahi Kuzungumza Hivyo”
1, 2. (a) Kwa nini maofisa waliotumwa kumkamata Yesu walirudi mikono mitupu? (b) Ni nini kilichomfanya Yesu awe mwalimu wa pekee?
MAFARISAYO wamewaka hasira. Yesu yuko hekaluni akifundisha kumhusu Baba yake. Wanaomsikiliza wamegawanyika; wengi wanamwamini Yesu, lakini wengine wanataka akamatwe. Wakiwa wameshindwa kuzuia hasira yao, viongozi wa dini wanawatuma maofisa wakamkamate Yesu. Hata hivyo, maofisa hao wanarudi mikono mitupu. Wakuu wa makuhani na Mafarisayo wanauliza hivi kwa hasira: “Kwa nini hamkumleta?” Maofisa wakajibu: “Hakuna mtu mwingine yeyote ambaye amewahi kuzungumza hivyo.” Walivutiwa sana na mafundisho ya Yesu hivi kwamba hawakupata sababu ya kumkamata.a—Yohana 7:45, 46.
2 Kuna wengine pia waliovutiwa na njia ya Yesu ya kufundisha. Watu wengi walikusanyika ili kumsikiliza Yesu akifundisha. (Marko 3:7, 9; 4:1; Luka 5:1-3) Ni nini kilichomfanya Yesu awe mwalimu wa pekee? Kama tulivyoona katika Sura ya 8, alipenda kweli alizofundisha na aliwapenda watu aliowafundisha. Pia, alikuwa stadi wa kutumia njia mbalimbali za kufundisha. Tuchunguze njia tatu zenye matokeo alizotumia na jinsi tunavyoweza kumwiga.
Alifundisha kwa Njia Rahisi
3, 4. (a) Kwa nini Yesu alitumia lugha ya kawaida alipofundisha? (b) Mahubiri ya Mlimani yanaonyeshaje jinsi Yesu alivyofundisha kwa njia rahisi?
3 Wazia maneno ambayo Yesu angeweza kutumia kwa sababu ya ujuzi mwingi aliokuwa nao. Hata hivyo, alipokuwa akifundisha, hakutumia maneno magumu ambayo wasikilizaji wake hawangeweza kuelewa. Wengi wao walikuwa “watu wasio na elimu na wa kawaida tu.” (Matendo 4:13) Kwa kuwa alijua uwezo wao ulikuwa na mipaka, hakuwalemea na habari nyingi sana. (Yohana 16:12) Maneno yake yalikuwa rahisi, lakini kweli alizofundisha zilikuwa muhimu sana.
4 Kwa mfano, fikiria yale Mahubiri ya Mlimani, yaliyo katika Mathayo 5:3–7:27. Mashauri ambayo Yesu anatoa katika mahubiri hayo si ya kijuujuu tu bali yaligusa mioyo yao. Hatumii hoja wala sentensi ngumu. Alitumia maneno rahisi ambayo hata mtoto mdogo angeweza kuyaelewa kwa urahisi! Basi, haishangazi kwamba Yesu alipomaliza, umati—ambao inaelekea ulitia ndani wakulima, wachungaji, na wavuvi—‘ulishangazwa na njia yake ya kufundisha.’—Mathayo 7:28.
5. Toa mifano ya maneno yaliyosemwa na Yesu ambayo yalikuwa rahisi lakini yaliyokuwa na maana.
5 Mara nyingi, Yesu alipofundisha alitumia sentensi fupi zilizoeleweka kwa urahisi na kutumia maneno yaliyokuwa na maana. Nyakati hizo hakukuwa na vitabu vilivyochapishwa. Hivyo, kwa kutumia lugha ya kawaida, Yesu alikazia ujumbe wake katika akili na mioyo ya wasikilizaji wake hivi kwamba hawangeweza kusahau. Fikiria mifano fulani: “Acheni kuhukumu ili msihukumiwe.” “Watu wenye afya hawahitaji daktari, lakini wagonjwa wanamhitaji.” “Roho inataka lakini mwili ni dhaifu.” “Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, na Mungu vitu vya Mungu.” “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”b (Mathayo 7:1; 9:12; 26:41; Marko 12:17; Matendo 20:35) Maneno hayo bado yanakumbukwa ingawa yalisemwa miaka 2,000 hivi iliyopita.
6, 7. (a) Kwa nini ni muhimu kutumia lugha ya kawaida ili tufundishe kwa njia rahisi? (b) Tunaweza kufanya nini ili tusimlemee mwanafunzi wa Biblia na habari nyingi?
6 Tunawezaje kufundisha kwa njia rahisi na inayoeleweka? Njia moja kuu ni kutumia lugha ya kawaida ambayo watu wengi wanaweza kuielewa kwa urahisi. Kweli za msingi za Neno la Mungu si ngumu. Yehova amewafunulia kusudi lake watu walio wanyoofu na wanyenyekevu moyoni. (1 Wakorintho 1:26-28) Maneno rahisi yaliyochaguliwa kwa uangalifu, yanaweza kuwa na matokeo yanapotumiwa kuwasaidia watu kuelewa kweli za Neno la Mungu.
Unapofundisha, tumia njia rahisi
7 Ili tufundishe kwa njia rahisi, tunapaswa kuwa waangalifu tusimlemee mwanafunzi wa Biblia na habari nyingi. Hivyo, tunapoongoza funzo la Biblia, si lazima tueleze kila jambo; na hatupaswi kuzungumzia habari haraka-haraka kana kwamba jambo kuu ni kumaliza idadi fulani ya kurasa. Badala yake, ni jambo la hekima kuongoza funzo kulingana na mahitaji na uwezo wa mwanafunzi. Lengo letu ni kumsaidia mwanafunzi awe mfuasi wa Kristo na mwabudu wa Yehova. Kwa hiyo, tunahitaji kutumia wakati unaohitajika ili mwanafunzi aelewe vizuri mambo anayojifunza. Tukifanya hivyo, kweli za Biblia zitaingia moyoni mwake na kumchochea atumie mambo ambayo amejifunza.—Waroma 12:2.
Kuuliza Maswali Yanayofaa
8, 9. (a) Kwa nini Yesu aliuliza maswali? (b) Yesu alitumia maswali jinsi gani kumsaidia Petro afikie mkataa sahihi kuhusu kulipa kodi ya hekalu?
8 Mara nyingi, Yesu alitumia maswali hata wakati ambapo angetumia muda mfupi zaidi kumweleza msikilizaji jambo fulani moja kwa moja. Kwa nini alitumia maswali? Nyakati nyingine, aliuliza maswali yaliyofunua nia mbaya za wale waliokuwa wakimpinga na kuwanyamazisha. (Mathayo 21:23-27; 22:41-46) Hata hivyo, mara nyingi alitumia maswali ili wanafunzi wake wafunue mambo yaliyokuwa akilini mwao na ili achochee fikira zao na kuwazoeza watumie uwezo wao wa kufikiri. Hivyo, aliuliza maswali kama vile, “Mnaonaje?” na “Je, unaamini hilo?” (Mathayo 18:12; Yohana 11:26) Maswali ya Yesu yalifikia na kugusa mioyo ya wanafunzi wake. Fikiria mfano huu.
9 Pindi moja, wakusanya kodi walimuuliza Petro ikiwa Yesu analipa kodi ya hekalu.c Mara moja, Petro alijibu: “Ndiyo.” Baadaye, Yesu alimuuliza: “Unaonaje Simoni? Wafalme wa dunia hupokea ushuru au kodi kutoka kwa nani? Kutoka kwa wana wao au kutoka kwa wageni?” Petro akajibu: “Kutoka kwa wageni.” Kisha Yesu akasema: “Basi, kwa kweli wana hawalipi kodi.” (Mathayo 17:24-27) Bila shaka, Petro alitambua kusudi la maswali hayo, kwa kuwa watu wa familia za wafalme hawakulipa kodi. Hivyo basi, kwa sababu Yesu ni Mwana mzaliwa pekee wa Mfalme wa mbinguni aliyekuwa akiabudiwa hekaluni, hakuhitaji kulipa kodi. Ona kwamba badala ya kumjibu Petro kwa njia ya moja kwa moja, kwa busara Yesu alitumia maswali ili kumsaidia Petro afikie mkataa sahihi, na kuona uhitaji wa kufikiri kwa uangalifu kabla ya kujibu ikiwa hali kama hiyo ingetokea tena.
Uliza maswali yanayopatana na hali za mwenye nyumba
10. Tunawezaje kutumia maswali kwa ustadi tunapohubiri nyumba kwa nyumba?
10 Tunawezaje kutumia maswali kwa ustadi katika huduma yetu? Tunapohubiri nyumba kwa nyumba, tunaweza kutumia maswali yanayochochea upendezi ambayo huenda yakatufungulia njia ya kuhubiri habari njema. Kwa mfano, tukimkuta mtu mwenye umri mkubwa tunapohubiri, tunaweza kumuuliza hivi kwa heshima, “Umeona mabadiliko gani ulimwenguni?” Baada ya kumruhusu ajibu, unaweza kumuuliza, “Unafikiri ni nini kinachoweza kufanya maisha yawe mazuri zaidi ulimwenguni?” (Mathayo 6:9, 10) Tukimkuta mama mwenye watoto wadogo, tunaweza kumuuliza, “Unafikiri ulimwengu huu utakuwaje watoto wako watakapokuwa watu wazima?” (Zaburi 37:10, 11) Kuwa na utambuzi tunapohubiri kutatuwezesha kuchagua swali linalopatana na hali za mwenye nyumba.
11. Tunawezaje kutumia maswali kwa ustadi tunapoongoza funzo la Biblia?
11 Tunawezaje kutumia maswali kwa ustadi tunapoongoza funzo la Biblia? Maswali yaliyochaguliwa vizuri yanaweza kutusaidia kutambua mambo yaliyo katika moyo wa mwanafunzi. (Methali 20:5) Kwa mfano, wazia tunajifunza somo la 43, lenye kichwa: “Wakristo Wanapaswa Kuwa na Maoni Gani Kuhusu Kileo?,” katika kitabu Furahia Maisha Milele!d Somo hilo linazungumzia maoni ya Mungu kuhusu kunywa pombe kupita kiasi na ulevi. Huenda majibu ya mwanafunzi yakaonyesha kwamba anaelewa mambo ambayo Biblia inafundisha, lakini je, anakubaliana nayo? Tunaweza kumuuliza, “Je, unafikiri maoni ya Mungu kuhusu mambo hayo yanafaa?” Pia, tunaweza kumuuliza, “Unawezaje kutumia habari hii maishani mwako?” Unapofanya hivyo, kumbuka kuwa mwenye busara na kumheshimu mwanafunzi. Hatungependa kuuliza maswali yanayoweza kumwaibisha.—Methali 12:18.
Kutoa Hoja Zenye Kusadikisha
12-14. (a) Ni katika njia gani Yesu alitumia uwezo wake kufikia mkataa unaofaa? (b) Yesu alitoa hoja gani yenye kusadikisha, Mafarisayo walipodai kwamba anatumia nguvu za Shetani?
12 Akiwa na akili kamilifu, Yesu alikuwa stadi wa kutoa hoja zenye kusadikisha. Nyakati nyingine, alitoa hoja zenye kusadikisha ili kukanusha mashtaka ya uwongo ya wale waliokuwa wakimpinga. Mara nyingi, alitumia hoja zenye kushawishi kuwafundisha wafuasi wake masomo muhimu. Acheni tuchunguze baadhi ya mifano.
13 Baada ya Yesu kumponya mtu mwenye roho mwovu aliyekuwa kipofu na asiyeweza kuzungumza, Mafarisayo walimshutumu hivi: “Mtu huyu anawafukuza roho waovu kwa nguvu za Beelzebuli [Shetani], mtawala wa roho waovu.” Maneno yao yalionyesha walitambua kwamba nguvu zisizo za kawaida zilihitajika ili kuwafukuza roho hao. Hata hivyo, walidai kwamba nguvu za Yesu zilitoka kwa Shetani. Shtaka hilo lilikuwa la uwongo na lisilopatana na akili. Akifunua maoni yao yenye kasoro, Yesu alijibu: “Kila ufalme uliogawanyika dhidi yake wenyewe utaangamia, na kila jiji au nyumba iliyogawanyika dhidi yake yenyewe haitasimama. Vivyo hivyo, ikiwa Shetani anamfukuza Shetani, amegawanyika dhidi yake mwenyewe; basi, ufalme wake utawezaje kusimama?” (Mathayo 12:22-26) Ni kana kwamba Yesu alikuwa akisema: “Ikiwa ninamwakilisha Shetani, na ninaharibu kazi zake, basi Shetani anajipinga mwenyewe na hivi karibuni atashindwa.” Wangewezaje kukanusha hoja yenye kusadikisha kama hiyo?
14 Lakini Yesu hakuwa amemaliza kuzungumza na watu hao. Akijua kwamba baadhi ya wanafunzi wa Mafarisayo hao walikuwa wamewafukuza roho waovu, aliuliza swali rahisi lakini lenye kuchochea fikira: “Ikiwa ninawafukuza roho waovu kupitia Beelzebuli, wana [au, wanafunzi] wenu wanawafukuza kupitia nani?” (Mathayo 12:27) Ni kana kwamba Yesu alikuwa akisema: “Ikiwa mimi ninawatoa roho waovu kwa nguvu za Shetani, basi wanafunzi wenu wanatumia nguvu hizohizo.” Mafarisayo hawakuwa na la kusema. Hawangeweza kukubali kwamba wanafunzi wao wanatumia nguvu za Shetani. Basi, Yesu alitumia mawazo yao yaliyopotoka ili wao wenyewe wakubali jambo ambalo hawakutaka. Je, haisisimui kusoma jinsi ambavyo Yesu alisababu nao? Basi wazia jinsi umati uliomsikiliza Yesu moja kwa moja ulivyohisi, kwa kuwa sauti yake na kuwapo kwake kuliongeza uzito wa maneno yake.
15-17. Toa mfano unaoonyesha jinsi Yesu alivyotumia maneno “hata zaidi,” alipofundisha kweli zenye kugusa moyo kumhusu Baba yake.
15 Pia, Yesu alitumia hoja zenye kusadikisha na zinazopatana na akili alipokuwa akifundisha kweli zenye kuchochea mioyo kumhusu Baba yake. Mara nyingi, alifanya hivyo kwa kutumia maneno “hata zaidi” kuwasaidia wasikilizaji wake wasadiki zaidi kweli wanayoifahamu. Njia hiyo ya kutoa hoja kwa kulinganisha mambo iligusa mioyo yao. Acheni tuchunguze mifano miwili.
16 Alipokuwa akijibu ombi la wanafunzi wake la kuwafundisha kusali, Yesu alieleza jinsi wazazi wa kibinadamu wasio wakamilifu wanavyowapa watoto wao “zawadi nzuri.” Kisha akasema: “Ingawa ninyi ni waovu, mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi nzuri, je, Baba aliye mbinguni hatawapa hata zaidi roho takatifu wale wanaomwomba!” (Luka 11:1-13) Yesu alitoa hoja yake kwa kulinganisha mambo. Ikiwa wazazi wenye dhambi wanawatimizia watoto wao mahitaji yao, Baba yetu wa mbinguni ambaye ni mkamilifu na mwadilifu katika mambo yote atawapa hata zaidi roho takatifu waabudu wake washikamanifu wanaomwomba kwa unyenyekevu!
17 Yesu alitumia njia kama hiyo alipotoa shauri lenye hekima kuhusu jinsi ya kushughulika na mahangaiko. Alisema: “Kunguru . . . hawapandi mbegu wala hawavuni, nao hawana bohari wala ghala; lakini Mungu huwalisha. Je, ninyi si wenye thamani kuliko ndege? Angalieni jinsi mayungiyungi yanavyokua: Hayafanyi kazi wala hayasokoti; . . . Basi, ikiwa Mungu huivika hivyo mimea ya shambani, ambayo ipo leo na kesho hutupwa ndani ya jiko, je, hatawavika vizuri zaidi ninyi wenye imani ndogo?” (Luka 12:24, 27, 28) Ikiwa Yehova anatunza ndege na maua, atawatunza hata zaidi wanadamu wanaompenda na kumwabudu! Bila shaka, kwa kutumia njia hiyo yenye kuchochea fikira, Yesu aligusa mioyo ya wasikilizaji wake.
18, 19. Tunawezaje kusababu na mtu anayedai kwamba hamwamini Mungu asiyeweza kumwona?
18 Tunapohubiri, tungependa kutumia hoja zenye kusadikisha kupinga mafundisho ya uwongo. Pia, tungependa kusababu na watu tunapowafundisha kweli kumhusu Yehova. (Matendo 19:8; 28:23, 24) Je, hilo linamaanisha kwamba tunahitaji kutumia maneno mengi yasiyoeleweka? Sivyo hata kidogo. Jambo tunalojifunza kutoka kwa Yesu ni kwamba kufafanua mambo kwa njia rahisi kunaweza kuwa na matokeo makubwa.
19 Kwa mfano, tunaweza kumjibu jinsi gani mtu anayesema kwamba hamwamini Mungu asiyeweza kumwona? Tunaweza kujadiliana naye kwa kutumia sheria ya asili ya chanzo na matokeo. Tunapoona matokeo, tunajua kwamba lazima kuwe na chanzo. Tunaweza kusema: “Ikiwa ungekuwa jangwani na uone nyumba ambayo imejengwa vizuri iliyo na chakula kingi (matokeo), je, hungekubali kwamba lazima kuna mtu (chanzo) aliyeijenga? Hivyo basi, tunapoona majengo yaliyobuniwa na chakula kingi kilichohifadhiwa kwenye maghala (matokeo), je, haipatani na akili kufikia mkataa kwamba Mtu Fulani (Chanzo) ndiye aliyeumba vitu hivyo vyote? Biblia yenyewe inasema hivi: ‘Kila nyumba hujengwa na mtu fulani, lakini yule aliyevijenga vitu vyote ni Mungu.’” (Waebrania 3:4) Ni kweli kwamba hata tukitoa hoja zenye kusadikisha kadiri gani, si kila mtu atakayeukubali ujumbe wetu.—2 Wathesalonike 3:2.
Tumia hoja zitakazofikia moyo wa mtu huyo
20, 21. (a) Tunawezaje kutumia maneno “hata zaidi” ili kukazia sifa na njia za Yehova? (b) Tutazungumzia nini katika sura inayofuata?
20 Tunapofundisha iwe katika huduma ya shambani au kutanikoni, sisi pia tunaweza kulinganisha mambo kwa kutumia maneno “hata zaidi” ili kukazia sifa na njia za Yehova. Kwa mfano, tunapoonyesha kwamba fundisho la moto wa mateso linamvunjia Yehova heshima, tunaweza kusema: “Ni baba gani mwenye upendo anayeweza kumwadhibu mtoto wake kwa kuushika mkono wa mtoto wake na kuuweka motoni? Basi, wazo la moto wa mateso linamchukiza hata zaidi Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo!” (Yeremia 7:31) Ili tumhakikishie mwamini mwenzetu aliyeshuka moyo kwamba Yehova anampenda, tunaweza kusema: “Ikiwa Yehova anamwona shore mdogo kuwa mwenye thamani, basi anamjali na kumpenda hata zaidi kila mmoja wa waabudu wake walio duniani, kutia ndani wewe!” (Mathayo 10:29-31) Kusababu kwa njia hiyo kunaweza kutusaidia kufikia mioyo ya wengine.
21 Baada ya kuchunguza njia hizo tatu ambazo Yesu alitumia kufundisha, tunaweza kuona kwa urahisi kwamba maofisa hao walioshindwa kumkamata hawakuwa wakitia chumvi waliposema: “Hakuna mtu mwingine yeyote ambaye amewahi kuzungumza hivyo.” Katika sura inayofuata, tutazungumzia njia ambayo Yesu alitumia sana alipofundisha, yaani, kutumia mifano.
a Huenda maofisa hao walikuwa watumishi wa Sanhedrini waliokuwa chini ya mamlaka ya wakuu wa makuhani.
b Maneno hayo ya mwisho yanayopatikana kwenye Matendo 20:35 yananukuliwa tu na mtume Paulo. Huenda alisimuliwa maneno hayo (na mtu aliyemsikia Yesu akiyasema au alisimuliwa na Yesu aliyefufuliwa) au aliyapokea kupitia ufunuo kutoka kwa Mungu.
c Kila mwaka, Wayahudi walipaswa kulipa kodi ya hekalu ya drakma mbili, zinazolingana na mshahara wa kazi ya siku mbili. Kitabu kimoja cha marejeo kinasema hivi: “Kodi hiyo ilitumiwa kulipia gharama za toleo la kuteketezwa la kila siku na za dhabihu zote zilizotolewa kwa ajili ya watu.”
d Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.