Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • cl sura 17 kur. 202-213
  • “Lo! Jinsi kilivyo kina cha . . . Hekima ya Mungu!”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Lo! Jinsi kilivyo kina cha . . . Hekima ya Mungu!”
  • Mkaribie Yehova
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Hekima ya Kweli Ni Nini?
  • Uthibitisho wa Hekima ya Mungu
  • Hekima ya Vitu Visivyo Duniani
  • Yehova “Peke Yake Ndiye Mwenye Hekima”
  • “Heri Mtu Yule Aonaye Hekima”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Hekima ya Kweli Inapaza Sauti Kubwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
  • Je, “Hekima Inayotoka Juu” Inafanya Kazi Maishani Mwako?
    Mkaribie Yehova
  • “Hazina Zote za Hekima”
    ‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
Pata Habari Zaidi
Mkaribie Yehova
cl sura 17 kur. 202-213
Kundi la bata-bukini wakipaa.

SURA YA 17

‘Lo! Kina cha Hekima ya Mungu!’

1, 2. Yehova alikuwa amekusudia kufanya nini katika siku ya saba, na hekima Yake isiyo na mipaka ilijaribiwa jinsi gani mwanzoni mwa siku hiyo?

YEHOVA Mungu aliwaumba wanadamu katika siku ya sita. Mwishoni mwa siku hiyo alitangaza kwamba “kila kitu alichoumba,” kutia ndani wanadamu, kilikuwa “chema sana.” (Mwanzo 1:31) Lakini mwanzoni mwa siku ya saba, Adamu na Hawa waliamua kumsikiliza Shetani na wakamwasi Yehova. Hivyo, uumbaji bora zaidi wa Yehova hapa duniani, yaani, wanadamu, ukatumbukia katika dhambi, kutokamilika, na kifo. Inasikitisha sana!”

2 Huenda ilionekana kwamba kile ambacho Yehova alikuwa amekusudia kutimiza katika siku ya saba kisingeweza kutimia kamwe. Siku hiyo, ingekuwa na urefu wa maelfu ya miaka, kama siku sita zilizotangulia zilivyokuwa. Yehova alikuwa ameitangaza siku hiyo kuwa takatifu na kufikia mwisho wa siku hiyo, dunia yote ingekuwa paradiso iliyojaa wanadamu wakamilifu. (Mwanzo 1:28; 2:3) Lakini kusudi hilo lingetimizwaje baada ya Adamu na Hawa kumwasi Mungu? Mungu angechukua hatua gani? Yehova angethibitisha ukuu wa hekima yake kwa njia yenye kustaajabisha.

3, 4. (a) Kwa nini hatua ambayo Yehova alichukua baada ya uasi katika Edeni inaonyesha hekima yake yenye kustaajabisha? (b) Sifa ya unyenyekevu inaweza kutusaidia kukumbuka nini tunapojifunza kuhusu hekima ya Yehova?

3 Yehova alichukua hatua mara moja. Aliwahukumu waasi hao huko Edeni, na wakati huohuo, akatangaza habari njema kwamba angekomesha matatizo yote waliyoanzisha. (Mwanzo 3:15) Kusudi hilo lingetimizwa hatua kwa hatua kwa kipindi kirefu cha wakati hadi wakati ambapo madhara yote yaliyosababishwa na uasi yatakapoondolewa. Kusudi hilo ni rahisi lakini ni lenye hekima sana hivi kwamba msomaji wa Biblia anaweza kufurahia kujifunza kuhusu kusudi hilo na kutafakari kulihusu maisha yake yote. Bila shaka, kusudi la Yehova litafanikiwa. Litakomesha kabisa uovu, dhambi, na kifo. Kupitia kusudi hilo Mungu atawafanya wanadamu waaminifu wawe wakamilifu. Mambo hayo yote yatatukia kabla ya siku ya saba kwisha. Hivyo basi, Yehova atakuwa ametimiza kusudi lake kuhusu dunia na wanadamu kwa wakati unaofaa!

4 Tunastaajabishwa sana na hekima ambayo Yehova ameonyesha, sivyo? Mtume Paulo alichochewa kuandika hivi: ‘Lo! Jinsi kilivyo kina cha hekima ya Mungu!’ (Waroma 11:33) Tunapojifunza mengi zaidi kuhusu hekima ya Yehova, kwa unyenyekevu tunapaswa kukumbuka kwamba hata tujifunze kadiri gani—hatuwezi kamwe kufahamu kikamili hekima ya Yehova yenye kina sana. (Ayubu 26:14) Kwanza, acheni tufafanue sifa hii yenye kustaajabisha.

Hekima ya Kweli Ni Nini?

5, 6. Kuna uhusiano gani kati ya ujuzi na hekima, na ujuzi wa Yehova ni mwingi kadiri gani?

5 Hekima si sawa na ujuzi. Kompyuta zinaweza kuhifadhi ujuzi mwingi sana, lakini hakuna mtu anayeweza kusema kwamba mashine hizo ni zenye hekima. Hata hivyo, kuna uhusiano kati ya ujuzi na hekima. (Methali 10:14) Kwa mfano, ikiwa wewe ni mgonjwa sana na unahitaji ushauri wenye hekima ili kutibu ugonjwa huo, je, ungemwomba ushauri mtu ambaye ana ujuzi mdogo au hana ujuzi wowote kuhusu tiba? Bila shaka, usingefanya hivyo! Kwa hiyo, ujuzi sahihi ni muhimu ili kuwa na hekima ya kweli.

6 Yehova ana ujuzi usio na kikomo. Akiwa “Mfalme wa umilele,” yeye peke yake ndiye ambaye ameishi milele. (Ufunuo 15:3) Na anajua mambo yote yaliyotukia kwa miaka hiyo yote. Biblia inasema hivi: “Hakuna kiumbe kilichofichwa machoni pake, bali vitu vyote viko uchi navyo vimefunuliwa wazi machoni pa yule ambaye tunapaswa kutoa hesabu kwake.” (Waebrania 4:13; Methali 15:3) Kwa kuwa Yehova ndiye Muumba, anajua kila kitu kuhusu uumbaji wake. Naye ameona utendaji wote wa wanadamu tangu mwanzo. Yeye huchunguza moyo wa kila mwanadamu, na anaona kila jambo. (1 Mambo ya Nyakati 28:9) Yehova alituumba tukiwa na uhuru wa kuchagua na anafurahi sana anapoona tukifanya maamuzi ya hekima maishani. Akiwa “Msikiaji wa sala,” yeye husikiliza sala nyingi sana kwa wakati mmoja! (Zaburi 65:2) Na bila shaka, Yehova ana kumbukumbu kamilifu.

7, 8. Yehova anaonyeshaje ufahamu, utambuzi, na hekima?

7 Mbali na ujuzi, Yehova ana sifa nyingine. Anaona jinsi mambo mbalimbali yanavyohusiana, na anatambua matokeo kamili ya mambo yote. Anachanganua mambo na kufanya maamuzi, anatofautisha mema na mabaya, pia mambo muhimu na yasiyo muhimu. Zaidi ya hayo, haangalii tu jinsi watu wanavyoonekana kwa nje bali anachunguza moyo. (1 Samweli 16:7) Kwa hiyo, Yehova ana uelewaji na utambuzi, sifa ambazo ni bora zaidi kuliko ujuzi. Lakini hekima ni bora zaidi kuliko sifa hizo zote.

8 Hekima ni kutumia ujuzi, utambuzi, na ufahamu ili kutekeleza jambo fulani. Baadhi ya maneno ya awali ya Biblia yaliyotafsiriwa “hekima” kihalisi yanamaanisha “kufanya kazi kwa matokeo” au “hekima inayotumika.” Kwa hiyo, hekima ya Yehova si ya kuwaziwa tu, bali inafanya kazi na ina matokeo. Sikuzote Yehova hufanya maamuzi bora kabisa kwa kutumia hekima na uelewaji wake usio na mipaka, na anatekeleza maamuzi hayo kwa njia bora kabisa. Hiyo ni hekima ya kweli! Yehova anaonyesha ukweli wa maneno haya ya Yesu: “Hekima huthibitishwa kuwa yenye uadilifu kupitia kazi zake.” (Mathayo 11:19) Uumbaji wote wa Yehova unaonyesha waziwazi kwamba ana hekima.

Uthibitisho wa Hekima ya Mungu

9, 10. (a) Yehova ana hekima ya aina gani, naye ameionyeshaje? (b) Chembe huthibitishaje hekima ya Yehova?

9 Je, umewahi kustaajabishwa na ustadi wa fundi anayetengeneza vifaa maridadi vinavyofanya kazi vizuri? Inapendeza sana. (Kutoka 31:1-3) Yehova ndiye Chanzo cha hekima hiyo. Mfalme Daudi alisema hivi kumhusu Yehova: “Ninakusifu kwa sababu nimeumbwa kwa njia inayoogopesha na kustaajabisha. Kazi zako zinastaajabisha, ninajua vizuri sana jambo hilo.” (Zaburi 139:14) Kwa kweli, kadiri tunavyojifunza kuhusu mwili wa mwanadamu, ndivyo tunavyozidi kustaajabishwa na hekima ya Yehova.

10 Kwa mfano: Uhai wako ulianza ukiwa chembe moja—chembe moja ya yai ya mama yako iliungana na mbegu ya baba yako. Baada ya muda, chembe hiyo ilianza kugawanyika na kutokeza chembe nyingi zaidi. Mwishowe, mwili wako ukawa na chembe ndogo sana zaidi ya trilioni 100 hivi. Chembe 10,000 hivi zenye ukubwa wa wastani zinaweza kutoshea kwenye kichwa cha pini. Lakini, kila chembe ina umbo tata sana. Chembe moja ni tata sana kuliko kiwanda au mashine yoyote iliyotengenezwa na mwanadamu. Wanasayansi wanasema kwamba chembe moja ni kama jiji lililozingirwa na ukuta—lenye malango yanayolindwa, lenye mfumo wa usafirishaji, mfumo wa mawasiliano, mitambo ya kutokeza nishati, viwanda, mifumo ya kuondoa na kusafisha maji machafu, walinzi, na hata aina fulani ya makao makuu ya serikali katika kiini chake. Zaidi ya hilo, chembe hiyo inaweza kujigawanya na kutokeza chembe nyingine inayofanana nayo ndani ya saa chache tu!

11, 12. (a) Ni nini kinachofanya chembe za kiini-tete kinachokua zigawanyike, na hilo linapatanaje na Zaburi 139:16? (b) Ubongo wa mwanadamu unaonyeshaje kwamba ‘tumeumbwa kwa njia ya ajabu’?

11 Bila shaka, si chembe zote zinazofanana. Kadiri chembe za kiini-tete zinavyoendelea kugawanyika, ndivyo chembe mpya zinavyofanya kazi mbalimbali. Baadhi ya chembe hizo zitakuwa chembe za neva; nyingine zitakuwa chembe za mifupa, misuli, damu, au za macho. Utaratibu huo wa kugawanyika kwa chembe umehifadhiwa kiasili katika “maktaba” yenye ramani za chembe za urithi, yaani, DNA. Daudi aliongozwa na roho takatifu kusema hivi: “Macho yako hata yaliniona nikiwa kiinitete; sehemu zake zote ziliandikwa katika kitabu chako.”​—Zaburi 139:16.

12 Sehemu fulani za mwili ni tata sana. Kwa mfano, fikiria ubongo wa mwanadamu. Baadhi ya watu wamesema kwamba ubongo ndicho kitu tata zaidi katika ulimwengu wote. Una chembe za neva bilioni 100 hivi—huenda idadi hiyo inakaribia idadi ya nyota katika kundi letu la nyota. Kila moja ya chembe hizo inaungana na maelfu ya chembe nyingine. Wanasayansi wanasema kwamba ubongo wa mwanadamu unaweza kuhifadhi habari zilizo katika maktaba zote ulimwenguni na kwamba uwezo wake ni mkubwa sana. Licha ya kuuchunguza ubongo ‘ulioumbwa kwa njia ya ajabu,’ kwa miaka mingi sana, wanasayansi wanakubali kwamba huenda wasifaulu kamwe kufahamu kikamili jinsi unavyofanya kazi.

13, 14. (a) Chungu na viumbe wengine wanaonyeshaje kwamba wana “akili nyingi sana,” na hilo linatufundisha nini kumhusu Muumba? (b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba vitu vilivyoumbwa kama vile utando wa buibui vimefanywa “kwa hekima”?

13 Wanadamu ni sehemu ya uumbaji inayoonyesha hekima ya Yehova. Zaburi 104:24 inasema hivi: “Jinsi kazi zako zilivyo nyingi sana, Ee Yehova! Umezifanya zote kwa hekima. Dunia imejaa vitu ulivyoumba.” Kila kiumbe kinafunua hekima ya Yehova. Kwa mfano, chungu ana “hekima ya kisilika.” (Methali 30:24) Kwa kweli, makundi ya chungu yana utaratibu wa hali ya juu sana. Makundi fulani ya chungu hufuga aina fulani ya wadudu kana kwamba ni mifugo, wanawatunza na kupata chakula kutoka kwao. Chungu wengine ni kama wakulima, wanapanda chakula chao, yaani, kuvu. Viumbe wengine wengi wanafanya mambo yenye kustaajabisha kwa kutumia hekima ya kisilika. Nzi wa kawaida huruka kwa njia zenye kustaajabisha sana ambazo ndege bora ya kisasa iliyobuniwa na mwanadamu haiwezi. Ndege wanaohama huongozwa na nyota, nguvu za sumaku za dunia, au aina fulani ya ramani iliyo akilini mwao. Wanabiolojia hujifunza kwa miaka mingi tabia tata za kisilika za viumbe hao. Bila shaka, Yule aliyewapa viumbe hao uwezo huo ana hekima ya hali ya juu sana!

14 Wanasayansi wamejifunza mengi kutokana na hekima ya Yehova ya uumbaji. Mara nyingi, wanajaribu kuiga ubuni wanaoona katika uumbaji wa Mungu wanapotengeneza vitu. Kwa mfano, huenda umewahi kustaajabishwa na umaridadi wa utando wa buibui. Lakini jambo linalomvutia mhandisi ni jinsi utando huo ulivyobuniwa kwa njia ya pekee. Huenda tando fulani ni nyembamba, lakini zinaweza kuwa imara kuliko chuma, ni ngumu kuliko nyuzi za mavazi yanayozuia risasi. Ni ngumu kadiri gani? Hebu wazia utando wa buibui ulifanywa kuwa mkubwa, kufikia ukubwa wa wavu unaovutwa na mashua ya uvuvi. Utando wa aina hiyo ungeweza kusimamisha ndege ya abiria inayosafiri kwa kasi angani! Kwa kweli, Yehova amefanya vitu hivyo vyote “kwa hekima.”

Mkusanyo wa picha: Hekima ya Yehova ya uumbaji. 1. Utando wa buibui. 2. Chungu wanasafiri wakiwa wamebeba majani. 3. Kundi la bata-bukini wakipaa.

Ni nani aliyeumba viumbe hawa ambao wana “hekima ya kisilika”?

Hekima ya Vitu Visivyo Duniani

15, 16. (a) Nyota zinatoa uthibitisho gani kuhusu hekima ya Yehova? (b) Cheo cha Yehova akiwa Amiri-jeshi Mkuu wa malaika wengi sana kinaonyesha nini kuhusu hekima yake akiwa Msimamizi?

15 Hekima ya Yehova inaonekana waziwazi katika kazi zake ulimwenguni pote. Nyota ambazo tulizungumzia kwa undani katika Sura ya 5, hazijatapakaa angani bila mpangilio. Yehova amepanga nyota kwa njia maridadi sana katika makundi ya nyota, kwa kutumia hekima yake ya “sheria zinazoongoza mbingu.” Makundi hayo ya nyota yamepangwa katika makundi makubwa, ambayo huungana na kufanyiza makundi mengine makubwa hata zaidi. (Ayubu 38:33) Hivyo, tunaweza kuelewa kwa nini Yehova anasema kwamba nyota zilizo mbinguni ni kama “jeshi”! (Isaya 40:26) Hata hivyo, kuna jeshi lingine ambalo linaonyesha wazi zaidi hekima ya Yehova.

16 Kama tulivyoona katika Sura ya 4, Mungu anaitwa “Yehova wa majeshi” kwa sababu ya cheo chake akiwa Amiri-jeshi Mkuu wa jeshi la mamia ya mamilioni ya viumbe wa roho. Hilo linathibitisha nguvu za Yehova. Hata hivyo, hekima yake inahusikaje? Fikiria hili: Yehova na Yesu wanafanya kazi sikuzote. (Yohana 5:17) Basi, inapatana na akili kuamini kwamba hata malaika wanaomtumikia Mwenye Enzi Kuu wanafanya kazi sikuzote. Na kumbuka kwamba malaika wana uwezo, akili, na nguvu nyingi kuliko wanadamu. (Waebrania 1:7; 2:7) Lakini Yehova amewapa malaika hao wote kazi ya kutosha, na wamekuwa ‘wakitekeleza neno lake’ na ‘kufanya mapenzi yake’​—kwa mabilioni ya miaka wakiwa na shangwe. (Zaburi 103:20, 21) Hatuna shaka kwamba Msimamizi huyo ana hekima nyingi sana.

Yehova “Peke Yake Ndiye Mwenye Hekima”

17, 18. Kwa nini Biblia inasema kwamba Yehova “peke yake ndiye mwenye hekima,” na kwa nini tunastaajabishwa na hekima yake?

17 Mambo tuliyozungumzia yanatusaidia kuelewa kwa nini Biblia inamsifu Yehova kwa sababu ya hekima yake nyingi. Kwa mfano, inasema kwamba Yehova “peke yake ndiye mwenye hekima.” (Waroma 16:27) Yehova peke yake ndiye aliye na hekima kamili. Yeye ndiye Chanzo cha hekima yote ya kweli. (Methali 2:6) Hiyo ndiyo sababu, ingawa Yesu ana hekima nyingi kuliko viumbe wote wa Yehova, hakutegemea hekima yake mwenyewe bali alisema yale aliyoongozwa na Baba yake kusema.​—Yohana 12:48-50.

18 Mtume Paulo alifafanua jinsi hekima ya Yehova ilivyo ya pekee aliposema: “Lo! Jinsi kilivyo kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi! Jinsi hukumu zake zisivyochunguzika na njia zake zisivyotafutika!” (Waroma 11:33) Neno la mshangao, “Lo!” ambalo Paulo alitaja mwanzoni mwa mstari huo, lilionyesha hisia yenye nguvu—alistaajabishwa sana. Neno la Kigiriki ambalo alitumia kurejelea “kina” linahusiana sana na neno “shimo refu lisilo na mwisho.” Kwa hiyo, maneno yake yanatokeza picha iliyo wazi akilini. Tunapotafakari hekima ya Yehova, ni kana kwamba tunatazama katika shimo kubwa sana lisilo na mwisho, shimo lenye kina kirefu sana hivi kwamba hatuwezi kamwe kufahamu ukubwa wake, pia, hatuwezi kujua mambo yote ambayo Yehova anajua. (Zaburi 92:5) Wazo hilo linatunyenyekeza, sivyo?

19, 20. (a) Kwa nini tai ni mfano unaofaa wa kuonyesha hekima ya Mungu? (b) Yehova ameonyeshaje kwamba ana uwezo wa kuona matukio ya wakati ujao?

19 Yehova “peke yake ndiye mwenye hekima” kwa njia nyingine: Ni yeye tu anayeweza kujua matukio ya wakati ujao. Kumbuka kwamba Yehova hutumia tai mwenye uwezo wa kuona mbali, kama mfano wa hekima yake. Tai mkubwa anaweza kuwa na uzito wa kilogramu tano tu, lakini macho yake ni makubwa kuliko macho ya mtu mzima. Tai ana uwezo bora sana wa kuona. Ndege huyo anaweza kuona mnyama mdogo sana kutoka umbali wa mamia ya mita angani, au hata mamia ya kilomita! Yehova alisema hivi kumhusu tai: “Macho yake hutazama mbali sana.” (Ayubu 39:29) Vivyo hivyo, Yehova anaweza kuona ‘mbali’ sana, yaani, wakati ujao!

20 Biblia ina uthibitisho mwingi kwamba hilo ni kweli. Ina mamia ya unabii na masimulizi ya matukio ambayo yaliandikwa kabla hayajatokea. Biblia ilitabiri matokeo ya vita, kutokea na kuanguka kwa serikali kuu za ulimwengu, na hata mbinu za kivita ambazo zingetumiwa na makamanda wa jeshi. Nyakati nyingine ilitabiri matokeo hayo mamia ya miaka kabla hayajatukia.​—Isaya 44:25–45:4; Danieli 8:2-8, 20-22.

21, 22. (a) Kwa nini haifai kuamini kwamba Yehova ameamua mapema kuhusu mambo yote ambayo tutafanya maishani? Toa mfano. (b) Tunajuaje kwamba Yehova anatumia hekima yake kwa njia ya upendo?

21 Je, hilo linamaanisha kwamba Mungu anajua mapema maamuzi ambayo utafanya maishani? Baadhi ya watu wanafundisha kwamba maisha yetu yamepangwa mapema. Hata hivyo, fundisho hilo kwa kweli linadharau hekima ya Yehova, kwa kuwa linamaanisha kwamba hawezi kudhibiti uwezo wake wa kujua matukio ya wakati ujao. Kwa mfano: Kama ungekuwa mwimbaji mwenye sauti nzuri sana, je, ungeimba tu kila wakati? Bila shaka la! Vivyo hivyo, Yehova ana uwezo wa kujua matukio ya wakati ujao, lakini hatumii uwezo huo kila wakati. Akifanya hivyo huenda akaingilia uhuru wetu wa kuchagua. Uhuru huo ni zawadi yenye thamani ambayo Yehova hawezi kutunyang’anya kamwe.​—Kumbukumbu la Torati 30:19, 20.

22 Kuamini kwamba Yehova amepanga mapema mambo yote yanayotokea, kunamaanisha kwamba tunamlaumu kwa mambo mabaya yanayotokea na kufikiri kwamba anatumia hekima yake kwa njia isiyo na upendo. Lakini hilo si kweli hata kidogo! Biblia inafundisha kwamba Yehova ni “mwenye hekima moyoni.” (Ayubu 9:4) Yehova hana moyo kama wa mwanadamu, lakini mara nyingi Biblia hutumia neno hilo kumaanisha utu wa ndani kabisa, kutia ndani nia ya mtu na hisia zake kama vile upendo. Kwa hiyo, kama zilivyo sifa nyingine, hekima ya Yehova inaongozwa na upendo.​—1 Yohana 4:8.

23. Hekima ya Yehova iliyo bora sana inapaswa kutuchochea kufanya nini?

23 Ni wazi kwamba hekima ya Yehova ni kamilifu na tunaweza kuitumaini. Hekima hiyo ni bora kuliko yetu, ndiyo sababu Biblia inatuhimiza hivi: “Mtumaini Yehova kwa moyo wako wote, wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Katika njia zako zote mtambue yeye, naye atavinyoosha vijia vyako.” (Methali 3:5, 6) Acheni tujifunze mengi zaidi kuhusu hekima ya Yehova ili tuweze kumkaribia zaidi Mungu wetu mwenye hekima.

Maswali ya Kutafakari

  • Ayubu 28:11-28 Hekima ya Mungu ni yenye thamani kubwa kadiri gani, na tutafaidikaje tukiitafakari?

  • Zaburi 104:1-25 Uumbaji unaonyeshaje hekima ya Yehova, na unahisije kuhusu hilo?

  • Methali 3:19-26 Tukitafakari na kutumia hekima ya Yehova huenda tukapata matokeo gani maishani mwetu?

  • Danieli 2:19-28 Kwa nini Yehova anaitwa Mfunuaji wa siri, na tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu hekima ya kinabii inayopatikana katika Neno lake?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki