Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • cf sura 12 kur. 138-149
  • “Hakuwa Akizungumza Nao Bila Mfano”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Hakuwa Akizungumza Nao Bila Mfano”
  • ‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kwa Nini Yesu Alitumia Mifano Alipofundisha?
  • Kulinganisha Mambo kwa Njia Rahisi
  • Mifano Inayohusu Mambo ya Kawaida Maishani
  • Mifano Inayohusu Uumbaji
  • Mifano Inayohusu Mambo Yanayojulikana
  • “Bila Kielezi Hakuwa Akisema Nao”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Mifano Inayofundisha
    Boresha Uwezo Wako wa Kusoma na Kufundisha
  • Mwige Mwalimu Mkuu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Mifano Kuhusu Ufalme
    Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
Pata Habari Zaidi
‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
cf sura 12 kur. 138-149

SURA YA KUMI NA MBILI

“Hakuwa Akizungumza Nao Bila Mfano”

1-3. (a) Wanafunzi wanaosafiri na Yesu wana pendeleo gani la pekee, naye anafanya nini ili iwe rahisi kwao kukumbuka mambo anayofundisha? (b) Kwa nini mifano yenye matokeo inakumbukwa kwa urahisi?

WANAFUNZI wanaosafiri pamoja na Yesu wana pendeleo la pekee. Wanajifunza moja kwa moja kutoka kwa Mwalimu Mkuu. Wanaisikia sauti yake anapowafafanulia Neno la Mungu na kuwafundisha kweli zenye kusisimua. Kwa sasa, lazima wakumbuke maneno hayo yenye thamani katika akili na mioyo yao kwa sababu wakati wa maneno yake kuandikwa katika vitabu bado haujafika.a Hata hivyo, Yesu anafanya iwe rahisi kwao kukumbuka mambo anayofundisha. Jinsi gani? Kupitia njia yake ya kufundisha, na hasa ustadi wake wa kutumia mifano.

2 Kwa kweli, mifano yenye matokeo haisahauliki upesi. Mwandikaji mmoja alisema kwamba mifano “hugeuza masikio kuwa macho” na kwamba “huwawezesha wasikilizaji kupiga picha akilini.” Kwa kuwa tunafahamu mambo vizuri zaidi tunapopiga picha akilini, mifano inaweza kufanya iwe rahisi zaidi kuelewa hata mambo yasiyoonekana kwa macho. Mifano inaweza kutusaidia kuwazia mambo yanayozungumziwa na kufanya mafundisho hayo kubaki akilini.

3 Hakuna mwalimu yeyote duniani ambaye amewahi kutumia mifano kwa ustadi kuliko Yesu Kristo. Mifano yake inakumbukwa kwa urahisi hadi leo. Kwa nini Yesu alitumia sana njia hiyo ya kufundisha? Ni nini kilichofanya mifano yake iwe na matokeo sana? Tunawezaje kujifunza kutumia njia hiyo ya kufundisha?

Kwa Nini Yesu Alitumia Mifano Alipofundisha?

4, 5. Kwa nini Yesu alitumia mifano?

4 Biblia inaonyesha sababu mbili kuu zilizomfanya Yesu atumie mifano. Kwanza, kwa kufanya hivyo alitimiza unabii. Tunasoma hivi katika Mathayo 13:34, 35: “Yesu alizungumza . . . na umati kwa kutumia mifano. Kwa kweli, hakuwa akizungumza nao bila mfano, ili kutimiza maneno haya yaliyosemwa kupitia nabii: ‘Nitafungua kinywa changu kwa mifano.’” Nabii aliyetajwa na Mathayo ni mwandikaji wa Zaburi 78:2. Mtunga zaburi huyo aliongozwa na roho ya Mungu kuandika maneno hayo mamia ya miaka kabla ya Yesu kuzaliwa. Fikiria jambo hilo. Miaka mingi mapema, Yehova alitabiri kwamba Masihi angefundisha kwa mifano. Hivyo basi, ni lazima Yehova anathamini njia hii ya kufundisha.

5 Pili, Yesu alisema kwamba alitumia mifano kutenganisha watu ambao mioyo yao “imekuwa migumu.” (Mathayo 13:10-15; Isaya 6:9, 10) Mifano ya Yesu ilifunua nia za watu jinsi gani? Katika visa fulani, alitaka wasikilizaji wake wamwombe awafafanulie mifano ili waelewe maana kamili ya maneno yake. Watu wanyenyekevu walikuwa tayari kuuliza maswali lakini wenye kiburi au wasiopendezwa hawakutaka. (Mathayo 13:36; Marko 4:34) Basi, mifano ya Yesu iliwafunulia kweli wale ambao walitamani kutoka moyoni kuzijua; na wakati huohuo mifano yake iliwaficha wenye kiburi ile kweli.

6. Mifano ya Yesu ilikuwa na matokeo gani?

6 Kuna sababu nyingine zilizofanya mifano ya Yesu iwe na matokeo. Iliamsha upendezi kwa kuwachochea watu kusikiliza. Iliwasaidia kupiga picha akilini na kuzielewa kwa urahisi. Kama ilivyotajwa mwanzoni, mifano ya Yesu iliwasaidia wasikilizaji wake kukumbuka maneno yake. Mahubiri ya Mlimani, yaliyo katika Mathayo 5:3–7:27, ni mfano mzuri unaoonyesha jinsi Yesu alivyotumia mifano mingi. Hesabu moja ilionyesha kwamba kuna mifano zaidi ya 50 katika mahubiri hayo. Kumbuka kwamba mahubiri hayo yanaweza kusomwa kwa sauti kwa dakika 20 hivi. Hilo linamaanisha kwamba Yesu alitumia mfano karibu kila baada ya sekunde 20! Ni wazi kwamba Yesu aliona umuhimu wa kutumia mifano!

7. Kwa nini tuige jinsi Yesu alivyotumia mifano?

7 Tukiwa wafuasi wa Kristo, tunataka kuiga njia yake ya kufundisha, kutia ndani kutumia mifano. Kama vile viungo vinavyoongeza ladha ya chakula, mifano yenye matokeo inaweza kufanya ufundishaji wetu uvutie zaidi. Pia, mifano iliyofikiriwa vizuri inaweza kufanya kweli nzito zieleweke kwa urahisi. Acheni sasa tuchunguze baadhi ya mambo yaliyofanya mifano ya Yesu iwe na matokeo sana. Kisha, tutaona jinsi tunavyoweza kutumia njia hiyo nzuri ya kufundisha.

Kulinganisha Mambo kwa Njia Rahisi

Korongo wawili wakipaa angani na ua.

Yesu alitumiaje ndege na maua kuonyesha kwamba Mungu anatujali?

8, 9. Yesu alilinganishaje mambo kwa njia rahisi, na ni nini kilichofanya ulinganifu aliotoa uwe na matokeo sana?

8 Yesu alipofundisha, mara nyingi alilinganisha mambo kwa njia rahisi akitumia maneno machache tu. Hata hivyo, maneno hayo rahisi yaliwasaidia wasikilizaji kupiga picha akilini na kufundisha kweli muhimu za kiroho waziwazi. Kwa mfano, alipowahimiza wanafunzi wake wasihangaikie mahitaji yao ya kila siku, alilinganisha hali yao na “ndege wa angani” na “mayungiyungi ya shambani.” Ndege hawapandi wala kuvuna, na mayungiyungi hayasokoti wala kufuma. Lakini Mungu anawatunza ndege hao na maua hayo. Ni wazi kwamba ikiwa Mungu anatunza ndege na maua, bila shaka atawatunza wanadamu ‘wanaoendelea kuutafuta kwanza Ufalme.’​—Mathayo 6:26, 28-33.

9 Yesu pia alitumia sana sitiari, ambayo ni njia ya kulinganisha mambo iliyo na matokeo hata zaidi. Sitiari huzungumzia kitu fulani kana kwamba ni kingine. Alipotumia sitiari, Yesu alilinganisha mambo kwa njia rahisi. Pindi moja, aliwaambia wanafunzi wake: “Ninyi ndio nuru ya ulimwengu.” Haikuwa vigumu kwa wanafunzi kuelewa waziwazi maana ya sitiari hiyo kwamba kupitia maneno na matendo yao, wangeangaza nuru ya kweli ya kiroho na kuwasaidia wengine wamtukuze Mungu. (Mathayo 5:14-16) Ona sitiari nyingine ambazo Yesu alitumia: “Ninyi ndio chumvi ya dunia” na “Mimi ndiye mzabibu, nanyi ndio matawi.” (Mathayo 5:13; Yohana 15:5) Mifano hiyo ina matokeo sana na ni rahisi kueleweka.

10. Eleza jinsi unavyoweza kutumia mifano unapofundisha.

10 Unawezaje kutumia mifano unapofundisha? Si lazima utunge hadithi ndefu zenye mambo mengi. Jaribu tu kufikiria mambo yanayoweza kueleweka kwa urahisi yanapolinganishwa. Wazia kwamba unazungumza kuhusu ufufuo na unataka kutoa mfano unaoonyesha kwamba si vigumu kwa Yehova kuwafufua wafu. Utatumia ulinganifu gani? Biblia inalinganisha kifo na usingizi. Unaweza kusema, “Mungu anaweza kuwafufua wafu kwa urahisi kama vile tunavyoweza kumwamsha mtu aliyelala usingizi.” (Yohana 11:11-14) Tuseme unatoa mfano kuonyesha kwamba watoto wanahitaji kupendwa ili wakue vizuri. Unaweza kutumia mfano gani? Biblia inatumia ulinganifu huu: Watoto ni “kama machipukizi ya mzeituni.” (Zaburi 128:3) Unaweza kusema, “Mtoto anahitaji upendo kama vile mti unavyohitaji mwangaza wa jua na maji.” Kadiri ulinganifu ulivyo rahisi, ndivyo wasikilizaji wako watakavyoelewa kwa urahisi zaidi mambo unayozungumzia.

Mifano Inayohusu Mambo ya Kawaida Maishani

11. Taja mifano ya mambo ya kawaida ambayo Yesu aliona alipokuwa akikua huko Galilaya na baadaye akayatumia katika mifano yake alipofundisha.

11 Yesu alikuwa stadi wa kutumia mifano iliyohusu maisha ya watu. Mifano yake mingi ilihusu hali ambazo inaelekea aliziona alipokuwa akikua huko Galilaya. Fikiria maisha yake ya utotoni. Ni mara ngapi alimwona mama yake akisaga nafaka ziwe unga, akiongeza chachu kwenye unga uliokandwa, akiwasha taa, au kufagia nyumba? (Mathayo 13:33; 24:41; Luka 15:8) Ni mara ngapi aliwaona wavuvi wakishusha nyavu zao katika Bahari ya Galilaya? (Mathayo 13:47) Ni mara ngapi aliwaona watoto wakicheza sokoni? (Mathayo 11:16) Bila shaka, Yesu aliona vitu vingine vya kawaida na kuvitumia katika mifano yake, kama vile mbegu zikipandwa, sherehe za ndoa zenye furaha, na mashamba yenye nafaka zilizokomaa.​—Mathayo 13:3-8; 25:1-12; Marko 4:26-29.

12, 13. Katika mfano wa Msamaria mwema, kwa nini Yesu alizungumzia barabara ‘inayotoka Yerusalemu kwenda Yeriko’ ili kukazia hoja yake?

12 Katika mifano yake, Yesu alitaja mambo ambayo wasikilizaji wake waliyajua vizuri. Kwa mfano, alianza simulizi la Msamaria mwema kwa kusema: “Mtu fulani alikuwa akishuka kutoka Yerusalemu kwenda Yeriko akavamiwa na wezi, wakamvua nguo, wakampiga, kisha wakamwacha akiwa karibu kufa.” (Luka 10:30) Yesu alitaja barabara ‘inayotoka Yerusalemu kwenda Yeriko’ alipokuwa akikazia hoja yake. Yesu alisimulia mfano huo akiwa Yudea, karibu na Yerusalemu; hivyo inaelekea wasikilizaji wake waliijua barabara hiyo. Barabara hiyo ilijulikana kuwa hatari hasa kwa mtu aliyekuwa akisafiri peke yake. Kwa kuwa haikutumiwa na watu wengi, na ilikuwa na kona nyingi, kulikuwa na sehemu nyingi ambazo wezi wangejificha.

13 Yesu alitaja mambo mengine yanayojulikana kuhusu barabara ‘inayotoka Yerusalemu kwenda Yeriko.’ Kulingana na mfano huo, kuhani ndiye aliyepita kwanza katika barabara hiyo kisha Mlawi akafuata, lakini hakuna yeyote kati yao aliyesimama ili kumsaidia mtu huyo aliyejeruhiwa. (Luka 10:31, 32) Makuhani walitumikia hekaluni huko Yerusalemu, nao walisaidiwa na Walawi. Makuhani na Walawi wengi waliishi Yeriko wakati ambapo hawakuwa wakifanya kazi hekaluni, kwa kuwa Yeriko lilikuwa umbali wa kilometa 23 tu kutoka Yerusalemu. Hivyo, walitumia barabara hiyo waliposafiri. Pia, ona kwamba Yesu alisema msafiri huyo alikuwa “akishuka,” bali hakuwa akipanda kwenye barabara ‘inayotoka Yerusalemu.’ Wasikilizaji wake walielewa jambo hilo. Yerusalemu lilikuwa juu kuliko Yeriko. Hivyo, safari ya “kutoka Yerusalemu” ilikuwa ya ‘kushuka.’b Ni wazi kwamba Yesu aliwafikiria wasikilizaji wake.

14. Tunapotumia mifano, tunawezaje kuwafikiria wasikilizaji wetu?

14 Tunapotumia mifano, sisi pia tunahitaji kuwafikiria wasikilizaji wetu. Ni baadhi ya mambo gani kuhusu wasikilizaji wetu yanayoweza kutusaidia kuamua mifano tutakayotumia? Huenda ni umri, utamaduni, malezi, na kazi. Kwa kawaida, mfano unaohusu kilimo unaweza kueleweka vizuri zaidi katika eneo la kilimo kuliko katika jiji kubwa. Ikiwa tutafikiria kuhusu maisha ya kila siku ya wasikilizaji wetu, watoto wao, nyumba zao, burudani, na chakula chao, tunaweza kupata mifano mizuri itakayowafaa.

Mifano Inayohusu Uumbaji

15. Kwa nini haishangazi kwamba Yesu alifahamu uumbaji vizuri?

15 Mifano mingi ya Yesu inaonyesha kwamba alijua mambo ya asili, kutia ndani mimea, wanyama, na hali ya hewa. (Mathayo 16:2, 3; Luka 12:24, 27) Alitoa wapi ujuzi huo? Alipokuwa akikua huko Galilaya, bila shaka alipata muda wa kutosha kuchunguza uumbaji. Isitoshe, Yesu ni “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote,” na Yehova alipoumba vitu vyote, alimtumia akiwa “mfanyakazi stadi.” (Wakolosai 1:15, 16; Methali 8:30, 31) Basi, haishangazi kwamba Yesu alifahamu uumbaji vizuri. Tuone jinsi alivyotumia ujuzi huo kwa ustadi.

16, 17. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba Yesu alijua vizuri tabia za kondoo? (b) Ni mfano gani unaoonyesha kwamba kwa kweli kondoo wanasikiliza sauti ya mchungaji wao?

16 Kumbuka kwamba Yesu alisema kuwa yeye ni “mchungaji mwema” na akawaita wafuasi wake “kondoo.” Maneno ya Yesu yanaonyesha kwamba alijua vizuri tabia za kondoo. Alijua kwamba kuna uhusiano wa pekee kati ya wachungaji na kondoo wao. Alitambua kwamba kwa kawaida kondoo hukubali kuongozwa, nao humfuata mchungaji wao kwa uaminifu. Kwa nini kondoo wanamfuata mchungaji wao? Yesu alisema ni “kwa sababu wanaijua sauti yake.” (Yohana 10:2-4, 11) Je, kweli kondoo wanaijua sauti ya mchungaji wao?

Mchungaji akiongoza kondoo wake.

17 Kutokana na mambo aliyojionea, George A. Smith aliandika hivi katika kitabu chake The Historical Geography of the Holy Land: “Mara kwa mara, tulifurahia kupumzika mchana kando ya mojawapo ya visima vya Yudea, ambapo wachungaji watatu au wanne walileta kondoo wao. Kondoo hao walichangamana, nasi tulijiuliza jinsi ambavyo kila mchungaji angewatambua kondoo wake. Lakini baada ya kondoo hao kumaliza kunywa maji na kucheza, kila mchungaji alielekea upande tofauti wa bonde, na kila mmoja akaita kwa sauti ambayo ingetambuliwa na kondoo wake; nao kondoo wa kila mchungaji wakajitenga na kumfuata mchungaji wao kwa utaratibu kama walivyokuja.” Yesu alichagua mfano unaofaa zaidi kukazia kwamba tukitambua na kutii mafundisho yake na kufuata mwongozo wake, tutatunzwa na “mchungaji mwema.”

18. Tunaweza kupata wapi habari kuhusu uumbaji wa Yehova?

18 Tunawezaje kujifunza kutumia mifano inayohusu uumbaji? Tunaweza kutumia tabia za pekee za wanyama ili kulinganisha mambo kwa njia rahisi na yenye matokeo. Tunaweza kupata wapi habari kuhusu uumbaji wa Yehova? Biblia ina habari nyingi kuhusu aina mbalimbali za wanyama, na nyakati nyingine inatumia mifano inayohusu tabia za wanyama. Katika Biblia, baadhi yao wanatajwa kuwa na kasi kama swala au chui, kujihadhari kama nyoka, na kutokuwa na hatia kama njiwa.c (1 Mambo ya Nyakati 12:8; Habakuki 1:8; Mathayo 10:16) Habari nyingine nyingi ziko katika magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, na pia makala na video kutoka katika mfululizo wenye kichwa “Je, Ni Kazi ya Ubuni?” kwenye jw.org. Unaweza kujifunza mengi kwa kuchunguza jinsi machapisho hayo yanavyolinganisha mambo kwa njia rahisi kwa kutumia mifano inayohusu maajabu ya uumbaji mwingi wa Yehova.

Mifano Inayohusu Mambo Yanayojulikana

19, 20. (a) Eleza jinsi Yesu alivyotumia kwa matokeo tukio la karibuni kupinga fundisho la uwongo. (b) Tunawezaje kutumia visa na matukio halisi tunapofundisha?

19 Mifano yenye matokeo inaweza kutia ndani visa halisi. Pindi moja, Yesu alitumia tukio la karibuni kupinga fundisho lisilo la kweli kwamba msiba huwapata watu wanaoustahili. Alisema: “Wale 18 walioangukiwa na mnara huko Siloamu wakafa, je, mnafikiri walikuwa na hatia kuliko watu wengine wote wanaoishi Yerusalemu?” (Luka 13:4) Kwa kweli, watu hao 18 hawakufa kwa sababu ya kutenda dhambi fulani iliyomkasirisha Mungu. Badala yake, walipatwa na msiba huo kwa sababu ya “wakati na matukio yasiyotarajiwa.” (Mhubiri 9:11) Kwa hiyo, Yesu alipinga fundisho la uwongo kwa kutaja kisa ambacho wasikilizaji wake walikijua vizuri.

20 Tunawezaje kutumia visa na matukio halisi tunapofundisha? Wazia unazungumza kuhusu utimizo wa unabii wa Yesu wa ishara ya kuwapo kwake. (Mathayo 24:3-14) Unaweza kutaja habari za karibuni kuhusu vita, njaa, au matetemeko ya ardhi ili kuonyesha kwamba mambo hususa yanayotajwa katika ishara hiyo yanatimia. Au wazia unataka kutumia jambo lililoonwa kuonyesha mabadiliko yanayohusika katika kuvaa utu mpya. (Waefeso 4:20-24) Unaweza kupata wapi jambo lililoonwa? Unaweza kufikiria malezi mbalimbali ya waamini wenzako, au unaweza kutumia jambo lililoonwa ambalo limechapishwa katika chapisho fulani la Mashahidi wa Yehova. Pia, unaweza kupata mambo yaliyoonwa kwenye mfululizo wenye kichwa: “Biblia Inabadili Maisha” kwenye jw.org.

21. Ni thawabu gani zinazotokana na kuwa mwalimu mwenye matokeo wa Neno la Mungu?

21 Kwa kweli, Yesu alikuwa Mwalimu Mkuu! Kama tulivyoona katika sehemu hii, kazi yake kuu maishani ilikuwa ‘kufundisha na kuhubiri habari njema.’ (Mathayo 4:23) Hiyo ndiyo kazi yetu kuu maishani pia. Thawabu ya kuwa mwalimu mwenye matokeo ni kubwa. Kuwafundisha wengine ni njia moja ya kutoa, na tunapotoa kwa njia hiyo tunapata furaha. (Matendo 20:35) Furaha hiyo ni shangwe ya kujua kwamba tunawapa wengine kitu chema na chenye thamani, yaani, kweli kumhusu Yehova. Tunaweza pia kuridhika kwa kujua kwamba tunafuata mfano wa Yesu, Mwalimu mkuu zaidi aliyewahi kuishi duniani.

a Inaonekana kwamba Injili ya Mathayo ndiyo maandishi ya kwanza yaliyoongozwa na roho kuhusu maisha ya Yesu duniani. Iliandikwa karibu miaka nane baada ya kifo cha Yesu.

b Pia, Yesu alisema kwamba kuhani na Mlawi huyo walikuwa wakija “kutoka Yerusalemu,” hivyo, walikuwa wakitoka hekaluni. Kwa hiyo, hakuna yeyote ambaye angeweza kusingizia kwamba walimwepuka mtu huyo aliyekuwa katika hali mahututi kwa sababu hawakutaka kuwa najisi kwa muda na hivyo washindwe kutumikia hekaluni.​—Mambo ya Walawi 21:1; Hesabu 19:16.

c Ili upate orodha kamili ya mifano ya wanyama katika Biblia, ona kitabu Insight on the Scriptures, Buku la 1, ukurasa wa 268, 270-271, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Unawezaje Kumfuata Yesu?

  • Ni mambo gani kuhusu uumbaji ambayo Yesu alitumia katika mifano yake, nawe unawezaje kutumia mifano kama hiyo?​—Mathayo 13:24-32.

  • Yesu alitumiaje mifano rahisi kukazia hoja nzito, nawe unaweza kujifunza nini kutoka kwake?​—Mathayo 18:12-14.

  • Ni mambo gani kuhusu maisha ya kila siku ambayo Yesu alitumia katika mifano yake, na hilo linawezaje kukusaidia unapochagua mifano?​—Luka 11:5-8; 12:6.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki