Viziwi Wamsifu Yehova
KWA miaka mingi ilikuwa vigumu kwa Mashahidi wa Yehova katika Nigeria kufundisha viziwi Biblia. Hiyo ni kwa sababu ya uhaba wa Mashahidi ambao walifahamu lugha ya ishara. Lakini hali hiyo inabadilika. Mashahidi wengi zaidi wamejifunza lugha ya ishara nao wanawafikia viziwi. Kwa habari hiyo, maendeleo makubwa yalifanywa katika mkusanyiko wa wilaya wa Mashahidi wa Yehova uliofanywa Nigeria zaidi ya mwaka mmoja uliopita.
“Ungeweza kuhisi msisimko,” akasema mhudhuriaji mmoja katika mkusanyiko huo uliofanywa Ota, Nigeria. “Kulikuwa na hisi ya kicho sana, hisia ya ajabu,” akasema mwingine. Ni nini kilichochochea maneno hayo? Kwa mara ya kwanza katika Nigeria, programu nzima ilitafsiriwa katika lugha ya ishara. Huo ulikuwa mkusanyiko wa pekee kati ya mikusanyiko 96 iliyofanywa kotekote Nigeria katika mwaka huo ambapo programu yote ilitafsiriwa katika lugha ya ishara.
Miongoni mwa maelfu waliohudhuria mlikuwa wajumbe viziwi 43, ambao waliketi upande wa kushoto wa jukwaa, katika sehemu ya mbele. Juu yao kulikuwa na kibao kikubwa cheupe chenye maandishi mekundu yaliyosema, “Lugha ya Ishara.” Wajumbe viziwi walisisimka kuwapo hapo. Mmoja wao aliandika hivi: “Ni kwa shangwe nyingi sana na macho yenye machozi ninaandika. Ni ‘majuzi’ tu tulipovunjika moyo tulipojua juu ya maandalizi ya kiroho yaliyofanywa kwa ajili ya Wakristo viziwi wenzetu katika nchi nyinginezo. Hatukujua kwamba baraka hizo zilikuwa zinatujia hapa pia.”
Ni Nani Waliohudhuria?
Viziwi walikuja kutoka sehemu zote za Nigeria. Shahidi mmoja ambaye ni kiziwi alileta wanafunzi wake watatu wa Biblia. Kikundi kingine cha viziwi, ambacho kilikuwa kimesafiri kilometa 700 kuja na nyingine 700 kurudi, kilikuwa kimeweka akiba ya nauli kwa kipindi cha miezi saba. Hata hivyo, wakati ulipowadia wa kusafiri, walishindwa kukodi gari la serikali kwa sababu huo ulikuwa wakati wa sikukuu. Serikali ilipojua ugumu waliokabili, iliwapa naira 13,000 (dola 152 za Marekani) ili kuwasaidia kutafuta njia nyingine ya usafiri!
Familia zenye watoto viziwi zilisafiri kuhudhuria mkusanyiko huo wa kipekee. Mwanamke mmoja kutoka eneo fulani la mashambani alisikia juu ya mkusanyiko huo naye akaja na mwana wake aliye kiziwi. Wote wawili hawakufahamu lugha ya ishara. Wakiwa wameguswa hadi kutoa machozi kwa yale waliyoyaona, sasa wameazimia kujifunza lugha ya ishara.
Kati ya wale maelfu waliohudhuria, wengine walikuwa wametoka umbali wa mamia ya kilometa ili tu kuona jinsi viziwi “wangesikia” programu. Hudhurio siku ya Jumapili lilikuwa 13,936—idadi kubwa zaidi kushinda mkusanyiko wowote kati ya ile 96 iliyofanywa Nigeria. Wajumbe viziwi walifurahi kuwa sehemu ya umati huo.
Watazamaji Wavutiwa
Wengi wa viziwi walikuwa “wakisikia” habari njema katika lugha ya ishara kwa mara ya kwanza. Na wale wasio viziwi walikuwa wakiona lugha ya ishara kwa mara ya kwanza. Mhudhuriaji mmoja alisema kwamba alishangaa kuona kila kitu katika programu kikitafsiriwa—nyimbo, sala, matangazo, na hata drama! “Imekuwa yenye kuvutia sana,” akasema mwingine.
Shangwe ya wahudhuriaji viziwi ilidhihirika kwa jinsi walivyoimba. Kwa idili, walitumia mikono yao kumsifu Yehova. Kwa wasio viziwi, kutazama viziwi “wakiimba” kuligusa moyo sana. Kuliwafanya wengi watoe machozi. Mhudhuriaji mmoja alisikika akipaaza sauti, “Eh Yehova!” kwa uthamini wenye kicho sana. Wakati mmoja, baada ya wimbo kumalizika, wale walioketi karibu na sehemu ya lugha ya ishara walipiga makofi kwa nguvu.
Baada ya hotuba ya ubatizo, waliotaka kubatizwa waliposimama, kijana mmoja katika sehemu ya lugha ya ishara alisimama. Minong’ono ya uthamini ikajaa miongoni mwa wahudhuriaji aliposema “Ndiyo” katika lugha ya ishara kwa kujibu maswali mawili yaliyoulizwa na msemaji.
Ilikuwa shangwe kama nini kwa wahudhuriaji viziwi kukutana na ndugu na dada zao wa kiroho kutoka sehemu nyinginezo nchini! Mikono na vidole viliashiria kwa msisimko wakati ambapo viziwi walikuwa wakifahamiana. Kulikuwa na kusalimiana kwingi na kupeana anwani.
Watafsiri tisa (wa lugha ya ishara) walitoka sehemu mbalimbali za nchi. Ilipendeza kutazama mikono yao ikitafsiri kwa madaha katika lugha ya ishara hotuba zote na nyimbo zote. Kwa jitihada zao, walithawabishwa kwa kukumbatiwa, kusalimiwa, na kupongezwa. Wao pia waliulizwa maswali mengi: Ulijifunzaje? Naweza kujifunzaje? Je, kuna vitabu vinavyofundisha lugha ya ishara?
Eneo Jipya Lafunguka
Kwa viziwi, jambo kuu katika mkusanyiko huo lilikuwa kutolewa kwa ukanda wa vidio wa lugha ya ishara wa kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Wengi zaidi walihimizwa kujifunza lugha ya ishara na, kwa msaada wa vidio hiyo yenye kufundisha, wafikie viziwi kotekote Nigeria. Mkusanyiko uliwafanya wengi waazimie kufanya vivyo hivyo.
“Zamani tulipokutana na kiziwi katika utumishi wa shambani, tulienda tu kwenye nyumba iliyofuata,” akasema dada mmoja. “Sasa twajua jambo la kufanya.” Kukiwa na Wanigeria viziwi wapatao milioni tano, kwa kweli kuna uwezekano mkubwa sana wa ukuzi. Ndugu mmoja alisema: “Huu ni mwanzo. Sasa twahitaji kusitawisha shamba hili la kipekee.”
Katika miezi iliyofuata mkusanyiko, hilo ndilo jambo ambalo limetendeka hasa. Jitihada zenye bidii zinafanywa ili kufundisha kweli za Neno la Mungu kwa mamilioni ya Wanigeria ambao ni viziwi. Wao pia wahitaji kujifunza kuhusu habari njema ya ulimwengu mpya unaokuja chini ya Ufalme wa Mungu, kwa kuwa huko kutakuwa na uponyaji wa kimuujiza na “masikio ya viziwi yatazibuliwa.”—Isaya 35:5.