Waroma
10 Akina ndugu, nia njema ya moyo wangu na dua yangu kwa Mungu kwa ajili yao, kwa kweli, ni kwa ajili ya wokovu wao. 2 Kwa maana nawatolea wao ushahidi kwamba wana bidii kwa ajili ya Mungu; lakini si kulingana na ujuzi sahihi; 3 kwa maana, kwa sababu ya kutojua uadilifu wa Mungu bali wakitafuta sana kusimamisha ulio wao wenyewe, hawakujitiisha wenyewe kwa uadilifu wa Mungu. 4 Kwa maana Kristo ndiye mwisho wa Sheria, ili kila mtu anayedhihirisha imani awe na uadilifu.
5 Kwa maana Musa aandika kwamba mtu ambaye amefanya uadilifu wa Sheria ataishi kwa hiyo. 6 Lakini uadilifu unaotokana na imani husema kwa namna hii: “Usiseme moyoni mwako, ‘Ni nani atakayepaa kuingia mbinguni?’ yaani, kumleta Kristo chini; 7 au, ‘Ni nani atakayeshuka kuingia katika abiso?’ yaani, kumleta Kristo juu kutoka kwa wafu.” 8 Lakini lasema nini? “Lile neno liko karibu nawe, katika kinywa chako mwenyewe na katika moyo wako mwenyewe”; yaani, “neno” la imani, ambalo sisi tunahubiri. 9 Kwa maana ukitangaza hadharani lile ‘neno katika kinywa chako mwenyewe,’ kwamba Yesu ni Bwana, na kudhihirisha imani moyoni mwako kwamba Mungu alimfufua kutoka kwa wafu, utaokolewa. 10 Kwa maana kwa moyo mtu hudhihirisha imani kwa ajili ya uadilifu, lakini kwa kinywa mtu hufanya tangazo la hadharani kwa ajili ya wokovu.
11 Kwa maana Andiko lasema: “Hakuna yeyote awekaye imani yake juu ya yeye atakayekatishwa tamaa.” 12 Kwa maana hakuna tofauti yoyote kati ya Myahudi na Mgiriki, kwa maana kuna Bwana yuleyule juu ya wote, aliye tajiri kwa wote wale wanaomwita. 13 Kwa maana “kila mtu aitiaye jina la Yehova ataokolewa.” 14 Hata hivyo, watamwitiaje ambaye hawajaweka imani katika yeye? Nao watawekaje imani katika yeye ambaye hawajasikia? Nao watasikiaje bila mtu fulani kuhubiri? 15 Nao watahubirije isipokuwa wawe wametumwa? Kama vile imeandikwa: “Jinsi ilivyo yenye kupendeza miguu ya wale watangazao habari njema ya mambo mema!”
16 Hata hivyo, si wote waliotii habari njema. Kwa maana Isaya asema: “Yehova, ni nani aliyeweka imani katika jambo lililosikiwa kutoka kwetu?” 17 Kwa hiyo imani hufuata jambo lisikiwalo. Nalo jambo lisikiwalo ni kupitia neno juu ya Kristo. 18 Hata hivyo nauliza, Wao hawakukosa kusikia, sivyo? Kwani, kwa kweli, “mvumo wao ulitoka ukaenda kuingia katika dunia yote, na matamko yao hadi ncha za mwisho za dunia inayokaliwa.” 19 Hata hivyo, nauliza, Israeli hawakukosa kujua, sivyo? Kwanza Musa asema: “Hakika mimi nitawachochea nyinyi watu kwenye wivu kupitia lile ambalo si taifa; hakika nitawachochea nyinyi kwenye hasira kali kupitia taifa pumbavu.” 20 Lakini Isaya awa mjasiri sana na kusema: “Nilipatikana na wale ambao hawakuwa wakinitafuta sana; nikawa dhahiri kwa wale ambao hawakuwa wakiuliza juu yangu.” 21 Lakini kwa habari ya Israeli yeye asema: “Mchana kutwa mimi nimekunjua mikono yangu kuelekea watu wasiotii na wajibuo kwa ujeuri.”