Luka
11 Sasa wakati alipokuwa mahali fulani akisali, alipoacha, mmoja wa wanafunzi wake akamwambia: “Bwana, tufundishe jinsi ya kusali,+ kama vile Yohana pia alivyowafundisha wanafunzi wake.”+
2 Ndipo akawaambia: “Wakati wowote mnaposali,+ semeni, ‘Baba, jina lako na litakaswe.+ Ufalme wako na uje.+ 3 Utupe mkate+ wetu kwa ajili ya siku kulingana na mahitaji ya siku hiyo. 4 Na utusamehe dhambi zetu,+ kwa maana sisi wenyewe pia humsamehe kila mtu aliye na deni letu;+ na usituingize katika jaribu.’ ”+
5 Tena akawaambia: “Ni nani kati yenu aliye na rafiki naye amwendee katikati ya usiku na kumwambia, ‘Rafiki, nikopeshe mikate mitatu, 6 kwa sababu rafiki yangu amenijia sasa hivi kutoka safarini nami sina kitu cha kuweka mbele yake’? 7 Na huyo aliye ndani ajibu na kusema, ‘Acha kunisumbua.+ Tayari mlango umefungwa, na watoto wangu wachanga wako pamoja nami kitandani; siwezi kuamka nikupe chochote.’ 8 Ninawaambia ninyi, Ijapokuwa hataamka ampe chochote kwa sababu ya kuwa rafiki yake, hakika kwa sababu ya kudumu kwake kwa ujasiri,+ ataamka na kumpa vitu anavyohitaji. 9 Basi ninawaambia ninyi, Endeleeni kuomba,+ nanyi mtapewa; endeleeni kutafuta,+ nanyi mtapata; endeleeni kupiga hodi, nanyi mtafunguliwa. 10 Kwa maana kila mtu anayeomba hupokea,+ na kila mtu anayetafuta hupata, na kila mtu anayepiga hodi hufunguliwa. 11 Kwa kweli, ni baba gani kati yenu ambaye, ikiwa mwana+ wake anaomba samaki, labda atampa nyoka badala ya samaki? 12 Au ikiwa pia anaomba yai, atampa nge? 13 Kwa hiyo, ikiwa ninyi, mjapokuwa waovu, mnajua jinsi ya kuwapa watoto+ wenu zawadi zilizo njema, je, Baba aliye mbinguni hatawapa hata zaidi roho takatifu+ wale wanaomwomba!”
14 Baadaye alikuwa akifukuza roho mwovu aliye bubu.+ Baada ya roho huyo mwovu kutoka, yule bubu akazungumza. Nao umati wakastaajabu. 15 Lakini watu fulani kati yao wakasema: “Yeye huwafukuza roho waovu kupitia Beelzebuli mtawala wa roho waovu.”+ 16 Hata hivyo, wengine, ili kumjaribu, wakaanza kutafuta kwake ishara+ kutoka mbinguni. 17 Akijua mawazo+ yao akawaambia: “Kila ufalme uliogawanyika juu yake wenyewe hufanywa ukiwa, na nyumba iliyogawanyika juu yake yenyewe huanguka.+ 18 Kwa hiyo ikiwa Shetani pia amegawanyika juu yake mwenyewe, ufalme wake utasimamaje?+ Kwa sababu ninyi mnasema mimi hufukuza roho waovu kupitia Beelzebuli. 19 Ikiwa ni kupitia Beelzebuli mimi hufukuza roho waovu, wana+ wenu huwafukuza kupitia nani? Kwa hiyo wao watakuwa waamuzi wenu. 20 Lakini ikiwa mimi huwafukuza roho waovu kupitia kidole+ cha Mungu, ufalme wa Mungu kwa kweli umewafikia.+ 21 Wakati mtu mwenye nguvu,+ mwenye silaha za kutosha, anapolinda jumba lake, mali zake hukaa kwa amani. 22 Lakini mtu fulani mwenye nguvu+ zaidi yake anapokuja juu yake na kumshinda,+ yeye huchukua silaha zake zote alizokuwa akitegemea, naye hugawanya vitu ambavyo yeye alimpora. 23 Yule ambaye hayuko upande wangu ananipinga, na yule ambaye hakusanyi pamoja nami anatawanya.+
24 “Wakati roho mchafu anapomtoka mtu, hupita katika mahali palipokauka akitafuta mahali pa kupumzika, na, baada ya kukosa, husema, ‘Nitarudi kwenye nyumba yangu niliyoihama.’+ 25 Naye anapofika huikuta ikiwa imefagiliwa ikawa safi na kupambwa. 26 Ndipo huyo huenda na kuchukua roho saba+ tofauti walio waovu kuliko yeye mwenyewe waambatane naye, na, baada ya kuingia ndani, wao hukaa humo; na hali ya mwisho ya mtu huyo huwa mbaya zaidi kuliko ile ya kwanza.”+
27 Sasa alipokuwa akisema hayo mwanamke fulani katika umati akainua sauti yake akamwambia: “Lenye furaha ni tumbo la uzazi+ lililokuchukua wewe na maziwa uliyonyonya!” 28 Lakini akasema: “Hapana, badala yake, Wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!”+
29 Umati walipokuwa wakisongamana pamoja, akaanza kusema: “Kizazi hiki ni kizazi kiovu; kinatafuta ishara.+ Lakini hakuna ishara ambayo kitapewa ila ishara ya Yona.+ 30 Kwa maana kama vile Yona+ alivyokuwa ishara kwa Waninawi, ndivyo Mwana wa binadamu atakavyokuwa pia kwa kizazi hiki. 31 Malkia+ wa kusini atasimamishwa katika hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki naye atawahukumu kuwa wenye hatia; kwa sababu yeye alikuja kutoka miisho ya dunia ili aisikie hekima ya Sulemani, lakini, tazameni! Aliye mkuu+ kuliko Sulemani yupo hapa. 32 Watu wa Ninawi watasimama katika hukumu pamoja na kizazi hiki nao watakilaumu; kwa maana walitubu kutokana na mahubiri ya Yona;+ lakini, tazameni! Aliye mkuu+ kuliko Yona yupo hapa. 33 Baada ya kuwasha taa, mtu huiweka, si katika ghala wala chini ya kikapu cha kupimia, bali juu ya kinara cha taa,+ ili wale wanaoingia ndani wapate kuiona nuru. 34 Taa ya mwili ni jicho lako. Jicho lako linapokuwa rahisi, mwili wako wote huwa mwangavu+ pia; lakini linapokuwa bovu, mwili wako huwa na giza pia. 35 Kwa hiyo, ukae macho. Labda nuru iliyo ndani yako ni giza.+ 36 Kwa hiyo, ikiwa mwili wako wote ni mwangavu bila sehemu yenye giza hata kidogo, wote utakuwa mwangavu+ kama wakati ambapo taa inakupa nuru kwa miale yake.”
37 Baada ya kusema hayo, Farisayo mmoja akamwomba ale+ pamoja naye. Kwa hiyo akaingia na kuketi mezani. 38 Hata hivyo, Farisayo huyo akashangaa kuona kwamba hakunawa+ kwanza kabla ya chakula hicho. 39 Lakini Bwana akamwambia: “Sasa ninyi Mafarisayo, husafisha upande wa nje wa kikombe na sahani, lakini upande wenu wa ndani+ umejaa uporaji na uovu.+ 40 Ninyi watu msio na akili! Yule aliyeufanya upande wa nje+ aliufanya upande wa ndani pia, sivyo? 41 Hata hivyo, vitoeni viwe kama zawadi za rehema+ vitu vilivyo ndani, na, tazama! vitu vingine vyote ni safi kuwahusu ninyi. 42 Lakini ole wenu ninyi Mafarisayo, kwa sababu ninyi hutoa sehemu ya kumi+ ya mnanaa na mchicha na ya kila mboga nyingine za majani, lakini ninyi hupuuza haki na upendo kwa Mungu! Mambo hayo mlikuwa na wajibu wa kuyafanya, na bado kutoyaacha yale mengine.+ 43 Ole wenu ninyi Mafarisayo, kwa sababu ninyi hupenda viti vya mbele katika masinagogi na salamu katika masoko!+ 44 Ole wenu, kwa sababu ninyi ni kama makaburi yasiyoonekana, hivi kwamba watu hutembea juu yake nao hawajui!”+
45 Mtu fulani kati ya wale wenye ujuzi mwingi+ wa Sheria akajibu, akamwambia: “Mwalimu, kwa kusema mambo hayo unatutusi pia.” 46 Ndipo akasema: “Ole wenu pia ninyi mlio na ujuzi mwingi wa Sheria, kwa sababu ninyi huwatwika watu mizigo iliyo mizito kubebwa, lakini ninyi wenyewe hamwigusi mizigo hiyo kwa kimoja cha vidole vyenu!+
47 “Ole wenu ninyi, kwa sababu ninyi huyajenga makaburi ya manabii, lakini mababu zenu waliwaua!+ 48 Hakika ninyi ni mashahidi wa matendo ya mababu zenu na bado ninyi mnawapa kibali,+ kwa sababu hao waliwaua+ manabii lakini ninyi mnayajenga makaburi yao. 49 Kwa ajili ya hili hekima+ ya Mungu ilisema pia, ‘Nitatuma kwao manabii na mitume, nao watawaua na kuwatesa baadhi yao, 50 ili damu ya manabii+ wote iliyomwagwa tangu kuwekwa msingi wa ulimwengu ipate kudaiwa kutoka kwa kizazi+ hiki, 51 tangu damu ya Abeli+ mpaka damu ya Zekaria,+ aliyeuawa katikati ya madhabahu na ile nyumba.’+ Ndiyo, ninawaambia ninyi, itadaiwa kutoka kwa kizazi hiki.
52 “Ole wenu ninyi wenye ujuzi mwingi wa Sheria, kwa sababu mliuondoa ufunguo wa ujuzi;+ ninyi wenyewe hamkuingia, na wale wanaoingia mliwazuia!”+
53 Basi alipotoka hapo waandishi na Mafarisayo wakaanza kumsonga sana na kumuuliza maswali juu ya mambo zaidi, 54 wakimtega,+ ili wapate+ kitu fulani kutoka kinywani mwake.